Nav bar

Jumatano, 2 Machi 2022

ULEGA AZIAGIZA HALMASHAURI KUWEZESHA VIKUNDI VYA USHIRIKA


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega ameziagiza Halmashauri za  Wilaya hususan zilizopo katika Ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi kutoa asilimia 10 zinazotengwa na Serikali kwa ajili ya kuwezesha vijana na kuwapa vikundi vya ushirika vya Wafugaji jongoo bahari, kaa na Wakulima wa Mwani ili waweze kuongeza nguvu na kuendeleza shughuli zao za uzalishaji.

Ulega alitoa maelekezo hayo alipokuwa akiongea kwa nyakati tofauti na kikundi cha ufugaji jongoo bahari na kikundi cha wakulima wa mwani alipowatembelea kukagua shughuli wanazofanya Wilayani Bagamoyo, Mkoani Pwani Februari 25, 2022.

Wakati akiongea na wanavikundi hao, Naibu Waziri Ulega alitumia nafasi hiyo kufikisha ujumbe kwa Wakurugenzi wa Halmashauri kupitia Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Bagamoyo, Bw. Shauri Selenda kuwa asilimia 10 zinazotengwa na Serikali kwa ajili ya kuwezesha vijana  wapewe wanavikundi hao wanaofuga jongoo bahari, kaa na kilimo cha Mwani ili waweze kufanya uzalishaji mkubwa na wenye tija.

“Tunataka hii Pwani yetu yote kuanzia Moa kule Tanga Mpaka Msimbati itumike kwa ajili ya shughuli za uzalishaji, vijana na kina mama wawezeshwe kufanya shughuli hizi ili kuvutia watu wengine kufanya shughuli hizi na kuzalisha kwa tija zaidi”, alisisitiza Mhe. Ulega

Alisema lengo la kuwezesha vikundi hivyo ni kutaka wakue ili watoke katika uzalishaji mdogo na kuwa Kampuni na kuzalisha kwa wingi kitendo ambacho kitawaongezea kipato wao na taifa kwa ujumla.

“Haya mambo mnayofanya ya uzalishaji yameandikwa katika ilani ya Chama cha Mapinduzi, na hizo pesa tunazosema zitolewe ni utekelezaji wake chini ya maono ya Rais Samia Suluhu Hassan”, alifafanua

Aidha, Mhe. Ulega aliutaka uongozi wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kutembelea vikundi hivyo ili kujua changamoto zao na kuwaelekeza namna ya kufanya ili waweze kukopeshwa na benki hiyo.

“Lakini natoa maelekezo pia kwa watu wa benki ya kilimo, mtembelee hivi vikundi mpange vizuri na muwaongezee nguvu ili wapate mavuno ya uhakika, wewe Afisa Biashara kutoka Benki ya TADB, nakupa wiki moja urudi hapa ukutane na hawa wanavikundi, uweke nao mikakati na uwaelekeze namna ya kufanya ili waweze kupata hiyo mikopo”,alisema

Pamoja na hayo, aliwahimiza vijana kuendelea kuchangamkia fursa hizo za ufugaji wa majongoo bahari na ukulima wa mwani kwa sababu soko biashara hiyo ina manufaa makubwa na soko pana ambalo sio rahisi kulikidhi.

Katika hatua nyingine, Mhe. Ulega pia kuvipongeza vyombo vya habari kwa kazi nzuri wanayofanya ya kutangaza vyema fursa mbalimbali zinazopatikana katika uchumi wa buluu na hivyo aliendelea kuwaomba kuendelea na kazi hiyo ya kutangaza fursa hizo zinazopatikana nchini ili ziweze kuvutia wawekezaji wengi zaidi.

Lengo la ziara yake Mkoani Pwani ni kutathmini na kufanya kikao kazi cha kuweka Mikakati na kampeni ya kuhamasisha kutumia ipasavyo fursa za uchumi wa buluu huku akisisitiza  kuwa baada ya miezi 3 atarejea tena katika maeneo hayo ili kufanya ufuatiliaji wa maelekezo hayo.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akiongea na Wanakikundi wa Kilimo cha Mwani kilichopo Kijiji cha Mlingotini, Wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani Februari 25, 2022. Mhe. Ulega alitembelea kikundi hicho ikiwa Ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku mbili Mkoani Pwani ambayo lengo lake ni kutathmini na kufanya kikao kazi cha kuweka Mikakati na kampeni ya kuhamasisha kutumia ipasavyo fursa za uchumi wa buluu.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (kushoto) akiwa amemshika Jongoo Bahari alipotembelea Kikundi cha kuzalisha Majongoo Bahari cha Kaole kilichopo Wilayani Bagamoyo, Mkoani Pwani Februari 25, 2022. Mhe. Ulega alimuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo kukiwezesha Kikundi hicho ili kiweze kuzalisha kwa tija.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni