Nav bar

Jumatano, 16 Machi 2022

UJENZI WA BANDARI YA UVUVI MBIONI KUANZA


Na Saja Kigumbe

Serikali imeweka wazi kuwa mradi  wa ujenzi wa bandari ya uvuvi  unatarajia kuanza muda wowote kuanzia sasa baada ya kukamilika kwa upembuzi yakinifu.

Bandari hiyo ambayo inatarajiwa kujengwa Wilayani Kilwa Masoko, Mkoani Lindi inatarajiwa kuwa chachu ya kuimarika kwa uchumi wa buluu nchini.

Hayo yalibainishwa Machi 16, 2022 Jijini Dar es salaam na Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti  na Mafunzo ya uvuvi, Dkt. Erastus Mosha wakati wa mkutano wa wadau uliolenga kupitia rasimu ya taarifa ya upembuzi yakinifu wa mradi huo wa kimkakati.

Alisema bandari hiyo itaiwezesha nchi kupata mapato kupitia  meli za uvuvi na bidhaa zinazotokana na uvuvi zitauzwa hapa ndani  na nje ya nchi.

Dkt. Mosha alisema Serikali tayari imetenga fedha za kufanikisha ujenzi huo ambao unatarajiwa kufanyika katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia sasa.

“Tanzania hatujawahi kuwa na bandari ya uvuvi na hili limesababisha tumeshindwa kunufaika vya kutosha kupitia rasilimali za uvuvi kwa maana kwamba meli kubwa zinazovua kwenye ukanda wa uchumi wa bahari kushindwa kuja kwetu kutoa mizigo yao.

“Kutokana na  mazingira hayo tumeishia kupata tozo ya leseni ya hizo meli pekee, tukiacha mizigo yote wanayopata na shughuli zote zinazohusu uvuvi na bandari zinaenda kufanyika katika nchi nyingine tungekuwa na bandari, meli zingeweza kuja kwetu,” alisema Dkt. Mosha.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Idara ya Uvuvi Bi. Merisia Mparazo alisema utekelezaji wa mradi huo utaiwezesha nchi kuvuna rasilimali zilizopo kwenye ukanda wa uchumi wa bahari hususani kwenye kina kirefu.

Alisema uwepo wa bandari hiyo utapanua wigo wa kiuchumu katika mkoa wa Lindi ambapo licha ya shughuli za bandari utawezesha kuanzishwa kwa viwanda vya kuchakata samaki watakaovuliwa, biashara ya mafuta ya meli na utengenezaji wa vyombo hivyo vya uvivu.

“Kama kuna bandari ya uvuvi lazima zitakuwepo shughuli nyingine zinazoendana na hiyo, mfano zile meli zitahitaji mafuta au marekebisho madogo madogo tunategemea huduma za aina hii zitapatikana pale.

"Kana kwamba hiyo haitoshi kama samaki hao wakubwa watakuja kwenye bandari yetu lazima uchakataji utafanyika hapa nchini hivyo kutakuwa na viwanda vya kuchakata minofu ya samaki, bado biashara ya vyakula na hoteli itachukua nafasi hivyo vyote vitazidi kuuchangamsha mkoa mzima wa Lindi,” alisema Merisia.

 

Kwa upande wake mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi ambaye ni Katibu Tawala Msaidizi, Bw. Ramadhani Hatibu amesema Mkoa huo umepokea vizuri mradi huo kutokana na kuwa na tija kwa taifa na jamii kwa ujumla.

Amesema kutokana na mradi huo kutasaidia kuvua samaki wenye ujazo mkubwa ambao utasaidia pato la Taifa.

Naye Mdau wa uvuvi Bw. Khalfan Shabani amesema ujenzi wa bandari hiyo ya Uvuvi utaleta maendeleo makubwa katika Sekta ya Uvuvi.

Aidha ameiyomba Serikali kuwakaribisha wawekezaji kwa ajili ya ujenzi wa karakana ya meli baada ya ujenzi wa bandari kukamilika.


Mkurugenzi Msaidizi Utafiti na Mafunzo ya uvuvi Sekta ya Uvuvi Dkt. Erastus Mosha (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa Sekta hiyo mara baada ya kikao kifupi kilichofanyika kwenye ukumbi wa millennium tower Jijini Dar es salaam lengo likiwa ni pamoja na kujadili taarifa ya upembuzi yakinifu ya ujenzi wa bandari ya Uvuvi Machi 16, 2022.

Mkurugenzi Msaidizi wa uendelezaji wa Uendelezaji wa Rasilimali za Uvuvi (Uvuvi), Bi. Merisia Parazo (kulia) akifungua kikao na kueleza lengo la kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa millennium tower Jijini Dar es salaam, Machi 16, 2022





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni