Nav bar

Jumapili, 6 Machi 2022

SERIKALI YADHAMIRIA KUWAINUA WAVUVI WADOGO


Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Emmanuel Bulayi amesema Serikali imedhamiria  kuboresha Sekta ya Uvuvi  kwa kuwawezesha wavuvi wadogo wakiwemo wanawake ili waweze kunufaika na rasilimali za uvuvi zilizopo nchini.

Aliyasema hayo wakati wa hafla ya mashindano ya mbio za kuendesha mitumbwi kwa wavuvi wanawake kutoka mikoa ya Kanda ya ziwa iliyofanyika jijini Mwanza Machi 6, 2022.

“ Tumedhamiria kuwainua wavuvi wadogo na ndio maana tumeandaa mwongozo wa hiari na mpango mkakati kwa ajili ya kuendeleza uvuvi, rasilimali na mazao yake hapa nchini,” alisema Bulayi

Alisema lengo la Serikali la kuandaa Mwongozo huo kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Kilimo na Chakula Duniani (FAO) ni kukuza mchango wa sekta ya uvuvi mdogo kwa maslahi mapana ya wananchi kiuchumi, kijamii na kimazingira.

Aliongeza kwa kusema kuwa mwongozo huo ambao umekubaliwa na Jumuiya ya Kimataifa, unaamsha   misingi ya kusimamia na kuendeleza uvuvi mdogo kwa sababu asilimia 85 ya shughuli za uvuvi hapa nchini zinafanywa na wananchi wenye kipato cha chini.

Alifafanua kwamba Serikali inataka kuwainua wavuvi wadogo kwa kuwawezesha mikopo na  kuwapatia  mafunzo ili waweze kufanya uvuvi wenye tija kupitia vikundi vyao vya uvuvi na ushirika.

Kwa upande wake mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO), Bw. Charles Tulahi aliishukuru Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) kwa kuwapa fursa ya kushiriki kwenye maandalizi ya mwongozo wa hiari wa kitaifa wa kutambua na kuendeleza  rasilimali za Uvuvi na kwamba hatua hiyo itasaidia katika kuboresha lishe na  ajira kwa jamii.

"Ni Imani yetu kuwa mpango kabambe huo wa Uvuvi utaleta mabadiliko makubwa katika Sekta ya Uvuvi Nchini hasa kwa wavuvi wadogo wanawake ", alisema

"Tumeshirikiana na Serikali ya Tanzania kuhakikisha mazingira ya mvuvi mdogo wa Tanzania yanakuwa bora zaidi kwa ajili ya kupata kipato lakini pia ustawi wa maisha yao" aliongeza

Alifafanua kuwa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) limeipatia Tanzania kiasi cha shilingi milioni 450 zilizotumika kuandaa mwongozo na shughuli za utawala katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

 

Naye, Mkurugenzi wa Shirika lisilo la kiserikali la EMEDO, Bi. Editrudith Lukanga alisema mchango wa mwanamke katika uvuvi ni mkubwa lakini bado mchango huo haujatambuliwa kikamilifu.

Aidha, aliishukuru Serikali kwa kuandaa Mwongozo huo ambao utawasaidia wanawake wavuvi kutambuliwa kwenye shughuli zao za uvuvi kwa kufanya uvuvi wenye tija utakaowaongezea kipato, ajira na lishe.


Washiriki wanawake wakiwa kwenye zoezi la kushindana kuendesha mitumbwi  ziwa victoria Jijini Mwanza. Machi 06, 2022. lengo likiwa ni pamoja na kuamasisha wanawake kushiriki katika zoezi la Uvuvi.

Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Emmanuel Bulayi (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa mashindano ya wanawake ya  kuendesha mitumbwi na maafisa kutoka Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO), EMEDO na maafisa kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi mara baada ya mashindano hayo yaliyofanyika ziwa victoria  kamanga Jijini Mwanza. Machi 06, 2022. 

Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Emmanuel Bulayi (wa pili kutoka kushoto) akikabidhi zawadi ya fedha kiasi cha shilingi laki saba kwa washindi wa kwanza wa mashindano ya kupiga kasia kwa wanawake mara baada ya mashindano hayo yaliyofanyika  ziwa Victoria kamanga Mkoani mwanza Machi 06, 2022. 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni