Nav bar

Jumatano, 2 Machi 2022

NZUNDA ASISITIZA WAWEKEZAJI KUFUATA TARATIBU NA SHERIA YA MIKATABA YAO.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw.Tixon Nzunda amesisitiza wawekezaji wa Ranchi ya Taifa ya kalambo kufuata taratibu na sheria ya mikataba waliyoingia na  Ranchi hiyo.

Hayo ameyasema  Februari 22, 2022 alipotembelea Ranchi hiyo iliyopo mkoani Rukwa na kupata fursa ya kutembelea baadhi ya Vitalu vya Kalambo Ranchi na kushuhudio ufugaji bora unaofanyika katika Ranchi hiyo. 

"Fuateni taratibu mlizokubaliana na Ranchi katika kuendesha shughuli zenu katika vitalu vyenu mlivyopangishwa, kuanzia Vitalu vya muda mrefu mpaka vile vya Muda mfupi, Mikataba yenu inaelekeza mlime malisho kwenye vitalu vyenu,mjenge majosho, mchimbe Visima, nani kati yenu ametekeleza hayo??"Aliuliza Nzunda.

Aidha, Katibu Mkuu Mifugo Bw.Tixon Nzunda amekemea vikali wawekezaji ambao hawataki kuchanja mifugo yao, kuogesha au wanachanja mifugo michache na baadhi kuiacha bila kuchanja, amesema kwa kufanya hivyo mifugo hiyo bado itaendelea kuambukizana magonjwa.

"Tunataka vitalu vyenu viwe vya mfano kwa kuwa na mikakati endelevu ya Ufugaji, ogesheni, chanjeni mifugo yenu ili maeneo haya yawe maeneo huru ya Magonjwa"

Pia, Nzunda ameelekeza wafugaji hao kulima malisho katika Vitalu vyao, Kujenga Majosho, kuchimba Malambo na Visima ili inapotokea ukame au uhaba wa Malisho wawe na malisho ya kulisha mifugo yao.

Pia Katibu Mkuu Mifugo Nzunda alipata fursa ya kutembelea  ofisi za Zonal Veterinary centre (ZVC), Tanzania Veterinary laboratory Agency (TVLA) na kiwanda cha nyama cha SAAFI kilichopo Mjini sumbawanga na kukagua baadhi ya Miundombinu ya kiwanda hicho.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Joseph Mkirikiti amesema kuwa anafarijika sana kuona sasa Viongozi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi  wanasimama kidete kusimamia na kutetea maslahi ya wafugaji ikiwemo kuhakikisha maeneo ya malisho hayachukuliwi na wakulima.

Katika hatua nyingine Meneja wa Kalambo Ranchi Bw. Noel Makawia amemweleza katibu Mkuu Mifugo kuwa Ranchi ya Kalambo inaukubwa  wa hekta 62,088.3 zenye uwezo wa kulisha ng'ombe Elfu ishirini mpaka ng'ombe Elfu ishirini na tano (20,000 -25,000)

Makawia amesema kuwa Ranchi hiyo imegawanyika katika sehemu kuu tatu ambapo ni eneo mama la Ranchi hiyo, lenye ukubwa wa hekta 13,588.3 ambalo lina jumla ya ng'ombe 1,796 Kondoo 186, Mbuzi 181 na farasi 11.

Makawia amebainisha kuwa eneo lingine ni la vitalu vya muda Mrefu ambalo linaukubwa wa Hekta 38,500 ambalo limetengwa katika vitalu 13 ambavyo vinaukubwa kati ya hekta 2,000-3,000 ambavyo vina jumla ya ng'ombe 14,036 mbuzi 1,103 kondoo 1,318 na Punda 85.

Eneo la tatu ni la vitalu vidogo vidogo lenye ukubwa wa hekta 10,000 ambalo limetengwa katika Vitalu 20 ambapo linajumla ya ng'ombe 5,700.

Makawia amemweleza katibu Mkuu Nzunda baadhi ya mipango yao ya baadaye ya kuhakikisha Ranchi hiyo inaendelea kuwa na malisho ya kutosha ikiwa ni pamoja na kulima shamba la malisho ekari 500 kutoka ekari 100 walizolima sasa, kuchimba bwawa kwa ajili ya kuvuna Maji ya Mvua na kujenga Machinjio ya kisasa.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw.Tixon Nzunda (Mwenye kaunda Suti ya Dark Blue) akikagua majengo ya ZVC pamoja na TVLA sumbawanga yaliyokarabatiwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) leo tarehe 22/02/2022. Anayemwongo Katibu Mkuu Mwenye sharti la Draft ni Dkt. Rajabu Mlekwa Meneja Mfawidhi TVLA.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw.Tixon Nzunda (wa pili kutoka kushoto) akimsikiliza Meneja wa Kiwanda cha nyama cha SAAFI Bw.James Michael (wa kwanza kushoto) akitoa maelezo mafupi juu kiwanda hicho.Wengine ni Dkt.Anneth Kitambi, Mkurugenzi Msaidizi huduma za Ukaguzi-Ustawi wa Wanyama na Utambuzi wa Mifugo, Bw.Salehe Msanda, Katibu Tawala Msaidizi Seksheni ya Uchumi na Uzalishaji kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Watumishi wengine kutoka ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Rukwa.


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni