Nav bar

Jumatano, 2 Machi 2022

NZUNDA ASISITIZA WATALAAM WA MIFUGO KUFANYA KAZI KWA WELEDI


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw.Tixon Nzunda amesisitiza watalaam wa Mifugo kufanya kazi zao kwa Weledi ili kusaidia Sekta ya Mifugo kusonga mbele.

Hayo ameyasema leo 23 feb 2022 alipokuwa akifungua kikao cha Watalaam wa Mifugo na Uvuvi kanda za nyanda za juu kusini na kusini Magharibi, mkoni Katavi.

"Watalaam fanyeni kazi zenu kwa Weledi ili wafugaji hawa wafaidike na huduma zenu, kila mtalaam awe na Register, ili mwisho wa siku aulizwe amehudumia wafugaji wangapi katika halmashauri yake, kata au kijiji.Lakini kama hiyo haitoshi kwa mwaka fedha 2023/2024 tutakuwa na mkataba wa utendaji kazi ili kupima utendaji kazi wa watalaam wetu" Alisema Nzunda.

Aidha, Nzunda amesema kuwa  Tanzania ni nchi iliyobarikiwa kuwa na Mifugo mingi, asilimia 1.4 ya ng'ombe wote wako Tanzania na nchi yetu  ni ya pili barani Africa kwa uwingi wa Mifugo ikitanguliwa na Ethiopia, lakini bado tija hiyo ya kuwa na mifugo mingi kiasi hicho haionekani.

"Pamoja na kuwa Tanzania tuna ng'ombe 33 Milioni lakini bado inachangia kiasi kidogo sana katika pato la taifa, ni asilimia 7.1tu, tunazidiwa na Botswana yenye mifugo Milioni mbili lakini inachangia pato la taifa  zaidi ya asilimia 20."Alisema Nzunda.

Katibu Mkuu Mifugo amesema kuwa, sasa ni wakati mwafaka wa  kufanya mageuzi katika Sekta ya Mifugo kwa kila Mkoa wenye Mifugo/Halmashauri na kata kuandaa Mpango mkakati wa Sekta ya mifugo ili kuutekeleza Mpango huo ili Sekta iweze kusonga mbele na kuleta matokeo chanya na yenye tija kwa Taifa.

Pia, Bw. Nzunda amesisitiza kuwa suala la Uogeshaji Mifugo, Uchanjaji, Utambuzi na ufuatiliaji, ulimaji wa malisho sio suala la hiari tena,ni lazima kama tunataka mabadiliko katika Sekta, wafugaji wabadilike na waanze kufuga kwa tija.

Katika hatua nyingine katibu Mkuu mifugo ameweka jiwe la Msingi katika Ujenzi wa kiwanda cha usindikaji Maziwa cha MSS-Nsimbo Mkoani Katavi.

Mmiliki wa kiwanda hicho cha MSS-Nsimbo Bw. Marick Salum amesema kuwa kiwanda hicho kikikamilika kitakuwa na uwezo wa kusindika Maziwa lita elfu mbili kwa saa. Pia amemwambia katibu Mkuu Mifugo kuwa mkoa wa Katavi una ng'ombe zaidi ya elfu moja hivyo upatikanaji wa Maziwa sio tatizo, pia uanzishwaji wa kiwanda hicho ni muhimu kwa sababu wafugaji watapata soko la kuuzia maziwa yao.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw.Tixon Nzunda akihutubia Watalaam wa Sekta ya Mifugo na Uvuvi(Hawapo pichani) wa kanda ya nyanda za juu kusini na kusini Magharibi leo tarehe 23/02/2022 Mkoani Katavi.Lengo la kikao hicho ni kubadilishana uzoefu katika utendaji kazi.Kulia ni Dkt.Samora Mshang'a,Daktari wa Mifugo kutoka mkoa wa Mbeya,kushoto ni Dkt.Anneth Kitambi, Mkurugnzi Msaidizi huduma za ukaguzi-Ustawi wa wanyama na utambuzi wa Mifugo.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Bw.Tixon Nzunda (Kushoto) akiweka jiwe la Msingi katika Ujenzi wa Kiwanda cha kusindika Maziwa cha MSS-Nsimbo Mkoani Katavi leo tarehe 23/02/2022.Kulia ni Bw.Marick Salum,Mmiliki wa Kiwanda cha MSS-Nsimbo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni