Nav bar

Jumanne, 25 Januari 2022

ULEGA AELEZA FURSA ZINAZOPATIKANA KWENYE UCHUMI WA BULUU.


Serikali ya awamu ya Sita ya Mhe. Samia Suluhu Hassan kupitia programu ya kuendeleza kilimo na uvuvi (AFDP) imetenga takribani sh Bil 29 mwaka 2022/2023 kwa ajili ya kuwezesha kiuchumi shughuli za uvuvi na mikopo kwa wananchi waliopo kwenye sekta hiyo pamoja na kukuza pato la Taifa.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa mifugo na uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega Januari 24, 2022 wakati wa ufunguzi wa kikao  kazi cha mkakati na kampeni ya  kuhamasisha shughuli za ukuzaji viumbe maji bahari kwa viongozi na  wataalam katika Mamlaka za Serikali za mitaa mkoani Tanga.

Alisema kuwa sehemu ya fedha hizo takribani sh Bil. 2.1 zinakwenda kukopeshwa kwa vikundi vya wafugaji wa samaki, wakulima wa mwani,wafugaji wa majongoo bahari,  wanenepeshaji wa kamba koche na  kaa, katika ukanda wa bahari ya Hindi.

 "Tumekutana sisi wataalamu kwa ajili ya kupeana mbinu na mikakati ya kuweza kuwafikia wananchi ambao ndio walengwa wakuu wa Mradi huo ili kuona namna ambavyo tutawainua kiuchumi kupitia fursa zilizoko baharini" alisema Naibu Waziri Ulega.

Alisema kuwa kuna utajiri mkubwa kupitia fursa ya rasilimali zinazopatikana katika ukanda huu hivyo Serikali imedhamiria kuinua hali duni za wananchi waishio katika ukanda huo hivyo wataalam hao wanaweza kusaidia kuwaonyesha wananchi fursa zilizopo.

Aliongeza kuwa Benki ya kilimo kwa kushirikiana na mabenki mengine ya biashara yaweke mazingira rafiki ya kutoa mikopo  kwa vyama vya ushirika vya  vijana na wanawake Ili waweze kufanya shughuli za kunenepesha kaa, kamba koche , ufugaji wa samaki,  majongoo bahari,  na kilimo cha  mwani.

Utolewaji wa mikopo hii pia iwaguse wavuvi wadogowadogo, mmojammoja au katika vikundi kwani kwa kufanya hivyo kilio chao cha kutumia fursa hizi za bahari kitakuwa kimesikika.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Tanga Hashim Mgandilwa alisema kuwa Changamoto kubwa iliyopo kwa wavuvi  wa ukanda huo ni ukosefu wa viwanda pamoja na masoko ya uhakika wa mazao ya bahari.

Alisema kuwa kampeni hiyo itaweza kuleta chachu na maendeleo ya wananchi kwani wataweza kupata fursa nyingine ya kiuchumi katika maeneo yao kupitia kilimo cha mwani pamoja na unenepeshaji wa viumbe bahari.

Aidha mwakilishi kutoka Benki ya kilimo (TADB), Bw. Furaha Sichula amesema kwa mwaka 2021/2022 jumla ya TSH. 4.827bil zimekopeshwa kwenye Sekta ya Uvuvi ikilinganishwa na mwaka  2020/2021 ambapo kiasi cha Tsh. Bil 1.625 kilikopeshwa.

Nae Mkurugenzi wa ukuzaji viumbe maji kutoka wizara ya mifugo na uvuvi, Dkt Nazael Madalla alisema kuwa katika mwaka uliopita uzalishaji wa viumbe vya bahari ulikuwa ni asilimia 11% pekee.

Kampeni hiyo iliyoanzishwa na Serikali inakwenda kuwasaidia wananchi  kujikwamua kiuchumi kupitia fursa za bahari.

Kikao kazi hicho kimeazimia kila baada ya miezi mitatu Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega atapita kukagua utekelezaji wa mikakati iliyoandaliwa.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akiongea na viongozi pamoja na  wataalam kutoka mamlaka ya Serikali za mitaa wa  Mkoa wa Tanga (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha mkakati na kampeni na kuhamasisha shughuli za ukuzaji viumbe maji bahari. Januari 24, 2022.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na watendaji wa Serikali mara baada ya kikao kifupi  juu ya fursa za uchumi wa buluu Mkoani Tanga. Januari 24.2022


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni