Nav bar

Jumatano, 26 Januari 2022

UCHUMI WA BULUU KUWANUFAISHA WANANCHI - MHE. ULEGA


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema kuwa kupitia kampeni ya uchumi wa buluu wanakwenda kuimarisha hali za kiuchumi za mwananchi mmoja mmoja hususan wanaoishi katika mikoa ya Pwani ya bahari ya Hindi na Taifa kwa ujumla.

Hayo aliyasema wakati wa ziara yake ya kutembelea vikundi vinavyojihusisha na shughuli za kilimo cha mwani, na unenepeshaji kaa katika Wilaya za Pangani, Tanga jiji na  Mkinga, Mkoani Tanga Januari 25, 2025.

Alisema kuwa kupitia kampeni hiyo Serikali inakwenda kufanya mapinduzi makubwa ya namna ya rasilimali za bahari zitakavyotumika kuweza kuleta mabadiliko ya kiuchumi kwa wananchi ambao wanategemea bahari kwa ajili ya shughuli za uzalishaji.

"Serikali ya Mama Samia inakwenda kuondoa hali duni za wavuvi kwa kuwaunganisha na fursa za kiuchumi zilizopo kwenye ukanda wa bahari ya hindi kwa kushiriki kwenye  fursa zilizopo badala ya kutegemea uvuvi  pekee" alisema Mhe. Ulega.

Aidha alisema wanataka watanzania kuhamasika na kuchangamkia fursa za kilimo cha mwani, kunenepesha kaa, kamba kochi kwani soko la uhakika lipo na Serikali ipo tayari kuwawezesha kwa mitaji sambamba na vifaa.

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Pangani Ghaibu Lingo alisema kuwa tayari wameshaanza kunufaika na fursa za uchumi wa buluu kwa wananchi kuweza kushiriki kwenye shughuli ya kunenepesha kaa na kufunga miamba kwa ajili ya Uvuvi wa pweza na kisha kuwauza kwa faida kubwa tofauti na hapo awali.

"Tumeanza hii mbinu ya kufunga miamba kwa ajili ya Uvuvi wa pweza katika eneo la Ushongo na matokeo tumeweza kuyaona hivyo tunaiomba Serikali kuweza kuwasaidia wavuvi wa maeneo mengine kama Kipumbwi na Mkwaja" alisema DC huyo.

Nao wananchi waliipongeza Serikali kwa kuja na fursa ya uchumi wa buluu kwani unakwenda kusaidia kubadilisha uvuvi wao wa mazoea na kuwa wa kisasa na wenye tija.

Hamis Ramadhani Mwenyekiti wa kikundi cha Jifute aliiomba serikali kuwawezesha mitaji pamoja na mashine kubwa ya kuvutia maji ili waweze kukuza mitaji yao na hivyo kupata faida kubwa.

Nae Burhan Ramadhani alisema kuwa uvuvi haramu pamoja na ukosefu wa soko imekuwa ni kikwazo kwa kilimo cha mwani kuweza kufanya vizuri katika maeneo yao hivyo aliiomba wizara kuona namna ya kuwawezesha vifaa na mitaji.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akieleza umuhimu na faida ya mwani kwa wanakijiji wa mwandosi wakati wa ziara yake Wilayani Mkinga Mkoani Tanga, Januari 25, 2022.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akimtambulisha mwakilishi kutoka Benki ya kilimo (TADB), Bw. Furaha Sichula kwa wananchi wa Tanga kueleza namna wanaweza kunufaika na mikopo kutoka Benki hiyo ya kilimo wakati wa ziara yake Mkoani humo Januari 25, 2022.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akieleza fursa zinazopatikana kutokana na unenepeshaji kaa wakati wa ziara yake Wilaya ya pangani Mkoani Tanga alipotembelea kikundi cha Jifute kinachojishughulisha na unenepeshaji huo na kukabidhi kikundi hicho kwa  Benki ya kilimo (TADB) Ili iweze kutoa mikopo itakayowasaidia  kujiendeleza na kujipatia kipato. Januari 25, 2022.

Muonekano wa mabwawa ya kienyeji ya unenepeshaji kaa yaliyotengenezwa na akina mama na  vijana kikundi cha jifute, pangani Mkoani Tanga, januari 25, 2022.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni