Nav bar

Ijumaa, 22 Oktoba 2021

WAVUVI WAHIMIZWA KUTUNZA MAZALIA YA SAMAKI KUINUA UZALISHAJI

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amewataka wavuvi wanaofanya shughuli zao Wilayani Uvinza, Mkoani Kigoma kutunza mazalia ya Samaki ili waweze kuzaliana na kuongezeka jambo ambalo litasaidia kuongeza uzalishaji na kukuza uchumi wa buluu nchini.

Ulega alitoa wito huo wakati akiongea na wavuvi wa Vijiji vya Buhingu  na Igalula alipofanya ziara  ya kukagua shughuli za uvuvi zinazofanyika Mkoani humo Oktoba 16, 2021.

Alisema ni muhimu kutunza mazalia hayo kwani ndio kiwanda cha kuzalisha malighafi huku akiwakumbusha wananchi kuwa kwa kufanya hivyo kutapelekea samaki kuongezeka na hivyo watakuwa na uhakika wa kupata lishe bora na kukuza kipato chao.

"Wananchi ungeni mkono jitihada za Serikali na wadau wengine wa maendeleo katika kuhakikisha mazingira ya mazalia ya Samaki yanatunzwa vizuri, mkifanya hivyo mazao mengi yatapatikana na uchumi wenu hapa utainuka," alisema Ulega

Aliendelea kusema kuwa uchumi wa wananchi hao ukiinuka kupitia biashara nzuri ya samaki watakayoifanya wataweza kutoka katika uvuvi wanaofanya sasa wa kuwinda na kufanya uvuvi wa kisasa kwa sababu watakuwa na uwezo wa kupata vifaa bora vya kuwarahisishia shughuli zao hizo.

Aidha, aliupongeza Mradi wa Tuungane ambao kwa kushirikisha na Serikali wanahamasisha jamii kutunza maeneo ya mazalia samaki Wilayani Uvinza na tayari wametenga maeneo ya hifadhi katika Vijiji mbalimbali.

"Niwaombe muendelee kutanua wigo wa utunzaji wa mazalia, ongezeni mipaka ya kutunza, tunzeni na baada ya muda mvune samaki, huu ndio uchumi wa buluu anaouhamasisha Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan," aliongeza 

Waziri Ulega aliwataka wananchi wanaoishi katika Vijiji hivyo vilivyopo kandokando ya Ziwa Tanganyika kuhakikisha wanajipanga kuyalinda maeneo hayo ili waharibifu wasiweze kuingia katika maeneo hayo kuvuna samaki kiholela.

"Hakikisheni harakati zenu hizi hazirudi nyuma, muwe walinzi wa maeneo haya, Serikali ipo pamoja na nyinyi," alisistiza

Katika kuunga mkono jitihada hizo, Naibu Waziri Ulega alitoa ahadi ya kuwapatia Injini za Boti 2 kwa kikundi cha Ushirika cha Wavuvi cha Katumbi kilichopo katika  Kijiji cha Buhingu na  kingine kimoja kitakachopatikana katika Kijiji cha Igalula ili waweze kuzitumia kufanya shughuli zao za uvuvi ikiwemo kutunza mazalia ya Samaki.

Naye, Kaimu Mkurugenzi, Mradi wa Tuungane, Peter Limbu alisema kuwa kupitia mradi huo wanaweza kuunda mazalia ya samaki 10 kwenye Vijiji 10 ambayo jamii katika vijijini hivyo wanashiriki kuhifadhi na maeneo hayo yamechukua jumla ya Ekari Elfu Thelathini na Nne (34000).

"Zoezi hili la kutambua maeneo ya mazalia ya samaki tulishirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) na walitusaidia kubainisha maeneo hayo ambayo sasa tumeyahifadhi," alisema Limbu.



Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega (kushoto) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa jengo jipya lililojengwa kupitia ufadhili wa Mradi wa Tuungane kwa ajili ya kutumika na kikundi shirikishi cha ulinzi na usimamizi wa rasilimali za uvuvi katika ziwa Tanganyika (BMU) kilichopo katika Kata ya Igalula, Wilayani Uvinza, Mkoani Kigoma Oktoba 16, 2021. Kulia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Ester Mahawe. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni