Nav bar

Jumamosi, 12 Juni 2021

MENEJA MACHINJIO YA DODOMA APEWA MIEZI 3 KUBORESHA MIUNDOMBINU

Na Mbaraka Kambona, Dodoma

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega ametoa miezi mitatu (3) kwa Meneja wa Machinjio ya Dodoma, Victor Mwita kufanya maboresho ya miundombinu iliyopo katika machinjio hayo ili iweze kutoa huduma inayostahiki na kuchangia ipasavyo katika pato la taifa.

 

Waziri Ulega alitoa maelekezo hayo wakati alipofanya ziara ya kukagua machinjio hayo yaliyopo jijini Dodoma Juni 8, 2021 ambapo pamoja na mambo mengine alimtaka meneja huyo kutumia vyema mapato wanayokusanya ili kuboresha miundombinu ya machinjio hiyo.

 

“Natoa miezi mitatu (3) ya kuboresha miundombinu ya machinjio hii, na mimi nitakuwa nakuja hapa kila mwezi kuangalia ni maboresho gani mmeyafanya, madhumuni yetu machinjio hii iweze kutoa mchango unaohitajika kwa taifa,” alisema Ulega

 

Alisema kuwa lengo la Serikali ya awamu ya sita ni kuona machinjio hiyo inafanya kazi katika uwezo wake uliosimikwa ili mchango wa sekta ya mifugo katika pato la taifa uweze kuonekana.

 

Aidha, alitumia nafasi hiyo pia kuwakumbusha maafisa wanaohusika katika kukusanya mapato katika machinjio na maeneo mengine kuwa hawatamvumilia mtu yeyote asiyekusanya mapato ya Serikali.

 

“Tuko imara sana katika ukusanyaji wa mapato, afisa yeyote asiyekusanya mapato ya serikali tutamtoa mara moja, tunataka tuhakikishe watu wanakusanya kwa haki na huduma inayotolewa pia itolewe kwa haki, hili jambo tunataka kulisimamia bila muhali,” aliongeza Ulega

 

Aliendelea kusema kuwa ukusanyaji wa mapato ya Serikali yaende sambamba na uboreshaji wa mazingira mazuri ya biashara ili kumfanya anayelipa ushuru aone ni haki na ni halali kulipa, kwani kwa kufanya hivyo biashara ya mifugo itashamiri zaidi.

 

Naye, Meneja wa Machinjio hiyo, Victor Mwita alisema kuwa wamepokea maelekezo yote ya Naibu Waziri huyo na aliahidi kuyatekeleza yote ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

 

Alisema mkakati watakaoanza nao ni kuhakikisha wanabana matumizi ili waweze kutumia vizuri mapato watakayoyapata kuboresha miundo mbinu ya machinjio hayo ili iweze kuleta tija zaidi.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega (katikati) akikagua miundombinu ya Machinjio ya Dodoma alipotembelea machinjio hayo yaliyopo jijini Dodoma Juni 8, 2021. Wa kwanza kushoto ni  Meneja wa Machinjio hayo, Victor Mwita.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega akiongea na Waandishi wa Habari hawapo pichani alipofanya ziara ya kukagua Machinjio ya Dodoma yaliyopo jijini Dodoma Juni 8, 2021. Akiwa katika Machinjio hayo alishuhudia shehena ya nyama za Mbuzi zikipakiwa katika gari maalum la kubebea nyama hizo kwa ajili ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi kwa ajili ya kuuzwa.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega akiangalia Ng'ombe waliopelekwa katika Machinjio ya Dodoma kwa ajili ya kuchinjwa. Waziri Ulega alifanya ziara ya kukagua Machinjio hiyo Juni 8, 2021.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega (wa pili kutoka kushoto) akishuhudia shehena ya nyama za Mbuzi zinazopakizwa katika gari maalum la kubebea nyama hizo kwa ajili ya kusafirishwa na kuuzwa nje ya nchi alipotembelea machinjio ya Dodoma yaliyopo jijini Dodoma Juni 8, 2021. Kulia ni Mmiliki wa shehena hiyo, Muhamad Azim.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega (kulia) akiongea na Mfanyabiashara wa nyama za Mbuzi, Muhamad Azim alipokutana nae katika Machinjio ya Dodoma yaliyopo jijini Dodoma Juni 8,  2021. Waziri Ulega alifanya ziara ya kukagua Machinjio hayo na amemtaka Meneja wa machinjio hayo kufanya uboreshaji wa miundombinu ili iweze kutoa huduma stahiki.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni