Nav bar

Ijumaa, 9 Oktoba 2020

TAKWIMU SAHIHI ZA UVUVI, CHANZO KIKUU CHA KUTUNGA SERA NA MIPANGO YA MAENDELEO NCHINI

Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Idara ya Maendeleo ya Uvuvi imesema ni muhimu kuwa na watu wenye uelewa wa kukusanya takwimu za uvuvi ili kuhakikisha watunga sera wanakuwa na vigezo mbalimbali vya kutunga sera na mipango ya maendeleo nchini.

 

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo (08.10.2020) katika mafunzo ya siku mbili ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani yanayohusisha maafisa uvuvi na viongozi kutoka Vikundi vya Kusimamia Rasilimali ya Uvuvi Mwaloni (BMU), kutoka Mikoa ya Dar es Salaam katika Wilaya za Kinondoni, Kigamboni na Ilala pamoja na Mkoa wa Pwani ukihusisha Wilaya za Bagamoyo na Chalinze, Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Upendo Hamidu amesema kusipokuwa na takwimu sahihi za uvuvi ni vigumu kutunga sera pamoja na kuweka mipango ya maendeleo.

 

“Ili kuhakikisha kwamba takwimu za uvuvi zinakusanywa na zinatoa yale matunda ambayo yanategemewa na wizara inayatimiza, katika suala la takwimu kama hauna watu wenye uelewa wa kuzikusanya maana yake hauwezi kuzipata takwimu, lakini kama pia hakuna vifaa vya kukusanyia takwimu bado hauwezi kukusanya takwimu kwa ufasaha, mafunzo haya yamelenga katika uelewa wa kukusanya takwimu.” Amefafanua Bi. Hamidu.

 

Aidha, amesema mafunzo hayo yamelenga kujenga uelewa wa ukusanyaji takwimu lakini pia kupitia mafunzo hayo washiriki watapata fursa ya kupatiwa vifaa vitakavyowasaidia kukusanya takwimu halisi.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Uratibu wa Sekta kutoka Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Bw. Yusuf Semuguruka, amesema siku za nyuma takwimu hazikuwa sahihi kutokana na utaratibu wa ukusanyaji wa taarifa na kutaka kuwepo na uhalisia katika ukusanyaji wa takwimu za uvuvi kwa kutumia vifaa sahihi.

 

Bw. Semuguruka amesema ofisi yake ina wajibu wa kuwasimamia viongozi wa serikali za mitaa wakiwemo viongozi wa ngazi za chini BMU’s, ambapo amefafanua wakati wa kutunga sera ni muhimu kuwa na takwimu sahihi na zisizo za kufikiria bali zinazofanana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ili kuwezesha taifa kuwa na taarifa sahihi kwa kutumia vifaa vinavyokubalika katika ukusanyaji wa taarifa.

 

Kwa upande wao baadhi ya washiriki wa mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani, ambao wamekuwa wakituma taarifa za takwimu kwa kutumia mfumo maalum wa njia ya simu ya mkononi katika Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI), wamesema mafunzo yamekuwa na umuhimu mkubwa katika kuhakikisha wanaboresha njia mbalimbali za ukusanyaji wa taarifa.

 

Mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani yanafanyika katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Tanga na baadaye yatafanyika katika Mkoa wa Mtwara kwa maafisa uvuvi na Vikundi vya Kusimamia Rasilimali ya Uvuvi Mwaloni (BMU), ambao wamekuwa wakikusanya takwimu hizo.

 

Mafunzo hayo yanahusisha ukusanyaji wa takwimu kwa kutumia sampuli za wingi wa samaki, idadi ya uchaguzi wa aina ya vyombo na zana za uvuvi, njia za ukusanyaji takwimu ikiwemo ya kutumia mfumo wa simu ya mkononi, namna ya kupata wastani wa uzito wa samaki pamoja na kufahamishwa umuhimu wa takwimu za uvuvi nchini.

 

Mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani yameandaliwa kupitia mradi wa usimamizi wa samaki wanaopatikana katika tabaka la maji la juu na kati unaotekelezwa kwa ushirikiano na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO).

Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Upendo Hamidu akifafanua umuhimu wa takwimu za uvuvi kwa washiriki wa mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani yanayofanyika kwa siku mbili jijini Dar es Salaam. (08.10.2020)

Mkurugenzi wa Uratibu wa Sekta kutoka Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Bw. Yusuf Semuguruka, akiwaeleza washiriki wa mafunzo (hawapo pichani) namna TAMISEMI inavyowasimamia viongozi wa serikali za mitaa na wale wa BMU’s ili kuhakikisha wanakusanya takwimu sahihi. Mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani yanafanyika kwa siku mbili jijini Dar es Salaam. (08.10.2020)

Washiriki wa mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani, wakiwemo maafisa uvuvi na viongozi kutoka Vikundi vya Kusimamia Rasilimali ya Uvuvi Mwaloni (BMU), katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani wakifuatilia mada mbalimbali juu ya ukusanyaji takwimu na umuhimu wa takwimu za uvuvi nchini. (08.10.2020)

Mchambuzi wa mifumo ya kompyuta kutoka Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI), Bw. Innocent Sailale akiwaelezea washiriki wa mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani, namna taasisi hiyo inavyokusanya taarifa za takwimu kupitia mfumo wa kompyuta kutoka katika simu za mkononi. (08.10.2020)





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni