Nav bar

Ijumaa, 22 Mei 2020

WAFANYABIASHARA WATAKIWA KUTHAMINI SOKO LA NYAMA.






Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amewataka wafanyabiashara wanaouza nyama nchini kutopandisha bei ya nyama kipindi hiki cha sikukuu ya Eid El Fitr  ili kuhakikisha kila mwananchi anapata kitoweo hicho.



Akizungumza (18.05.2020) jijini Dar es Salaam, Naibu Waziri Mhe.Ulega amemtaka pia Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Bw. Jumanne Shauri ndani ya siku saba kuhakikisha wanawapeleka wafanyabiashara wanaofanya biashara katika machinjio ya vingunguti kujionea eneo jipya lililotengewa na Manispaa ya ilala.



Mhe. Ulega amebainisha hayo wakati akikagua ujenzi wa mradi wa machinjio ya kisasa katika eneo la vingunguti katika Manispaa ya Ilala, ambapo amesisitiza wafanyabiashara wa nyama wanapaswa kuuza nyama kwa bei ya kawaida kulingana na hali ilivyo ili kuhakikisha watu wote wanapata kitoweo hicho.



Aidha amesema imekuwa ni kawaida kwa wafanyabiashara wa Nyama kupandisha bei kipindi cha sikukuu kinapofika hali inayosababisha  wananchi kutopata nyama kulingana na bei kuwa juu.



"Serikali ya awamu ya tano inatengeneza uchumi endelevu hivyo katika kuhakikisha hili wafanyabiashara wa nyama wanatakiwa kuchangamkia fursa ya sikukuu ya Eid El kuuza nyama kwa bei ya kawaida na sio ya kuwaumiza wananchi," amesema Mhe. Ulega.



Kuhusu mradi wa machinjio ya kisasa ya vingunguti ambapo hadi sasa umefikia asilimia 85 ya ukamilikaji wake, Mhe. Ulega amesema mradi huo unaogharimu kiasi cha Sh.Billioni 12.4 ambao unalengo la kuhakikisha wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam, mikoa mingine na nchi za nje kupata nyama itakayokuwa bora na yenye kuandaliwa vizuri kutokana na jengo hilo.



"Wizara yangu ndiyo inashughulikia masuala ya mifugo natoa pongezi kwa serikali kwa hatua hii ya kufikisha jengo hili katika kiwango cha juu kwani kiwanda pekee kinachotusaidia kwa sasa kipo Mwanza, Chobo Investmest hivyo kupitia kiwanda hiki naamini tutaongeza nguvu katika uuzaji wa nyama." Ameongeza Mhe. Ulega



Hata hivyo Mhe. Ulega amesema uwekezaji wa mradi huu utailipa serikali katika hatua zote ikiwemo kiuchumi na kijamii pindi shughuli za mnada zitakapoanza kufanyika katika jengo hilo.



Naibu waziri huyo amesema Tanzania bado ina fursa nyingi katika mifugo na serikali tayari ina mikakati mizuri ya kuhakikisha sekta hii inazidi kukua siku hadi siku na kutoagiza nyama nje ya nchi.



"Bado tuna fursa nyingi katika kuhakikisha nyama inapatikana kwa wingi na tutaacha ununuaji wa nje ya nchi pindi mradi huu utakapokamilika na tutahakikisha sisi ndio tunawapelekea watu wa  nchi nyingine" amesema Mhe. Ulega



Amesema eneo hilo litachinja ng'ombe takriban 1,500 na mbuzi 1000 kwa siku moja pindi itakapokamilika hivyo upandishaji holela wa bei ya nyama kwa vipindi vya sikukuu hautakuwepo tena kutokana na nyama kupatikana kwa urahisi zaidi.



Pia amesema kwa wafanyabiashara wa machinjio hayo wanaofanya biashara, tayari wamepatiwa eneo ambalo watajengewa na kufanya shughuli zao karibu na eneo hilo kama kawaida.



"Najua kuna watu wanajiuliza kuhusu wakinamama na vijana wanaofanya kazi hapa, Manispaa ya Ilala imeshawatafutia eneo na ni zuri lipo karibu na machinjio haya ya kisasa litawapa fursa ya kuendelea kufanya shughuli zenu, ninamuagiza Mkurugenzi wa Manispaa kuwapeleka wafanyabiashara na kuliona hilo eneo." amesema Ulega



Wakati huo huo Mhe. Ulega amempongeza Rais Dkt. John Magufuli kwa hotuba yake aliyotoa juzi ambapo wafugaji na wavuvi wamempongeza kwani bila kutoka kwao hawawezi kupata kipato.



Pia amesema maono ya Rais Magufuli ni ya kizalendo, Kiutu na kuwainua wananchi wake hivyo watendaji katika nyanja mbalimbali wanapaswa kutomuangusha ili kuifikisha nchi katika uchumi wa juu.



Kwa Upande wake Kaimu Msajili wa Bodi ya Nyama nchini, Bw. Imani Sichalwe amesema kupitia mradi huo wafugaji watapata masoko makubwa na kutoingiliwa na madalali ambao kwa asilimia kubwa walikuwa wanawapunja.



Amesema ni wakati wa wafugaji kujipanga na kuanza kufuga kisasa kwa kuongeza ubora na kuwaongezea thamani mifugo yao.


"Wafugaji wataunganishwa moja kwa moja na watu wa mradi hivyo hawatawatumia tena madalali, kinachotakiwa wafugaji wanenepeshe mifugo yao iwe tayari kwa kuuza," amesema Bw. Sichalwe





Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (wa pili kutoka kushoto) akisikiliza kwa makini maelekezo ya ramani ya jengo la machinjio ya Vingunguti Wilaya ya Ilala mkoani Dar es salaam. (18/05/2020) 
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (wa pili kutoka kushoto) atembelea machinjio ya Vingunguti Wilaya ya Ilala jijini dar es salaam. (18/05/2020) lengo likiwa ni pamoja na kuimiza ukamilishwaji wa mradi huo.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (kushoto) atembelea machinjio mpya inayojengwa Vingunguti Wilaya ya Ilala Mkoani Dar es salaam.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni