Nav bar

Jumatano, 27 Novemba 2019

WAZIRI MPINA AZINDUA VITUO VYA UCHUNGUZI WA MAGONJWA YA MIFUGO SUMBAWANGA



WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amezindua kwa pamoja vituo viwili vya Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo (ZVC) na Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Magharibi- Sumbawanga na kutangaza msimamo wa Serikali ya awamu ya tano wa kupambana na magonjwa ya mifugo ili kuongeza uzalishaji wa mifugo na mazao yake nchini.

Hivyo Serikali inawahakikishia wananchi uhakika wa upatikanaji wa chanjo kwa bei nafuu kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanyika ikiwa ni pamoja na Taasisi ya Chanjo (TVI) kuzalisha chanjo za kimkakati 11 ifikapo Juni mwakani na kwamba Serikali iko mbioni kutangaza bei elekezi ya Chanjo ili kuwadhibiti watu wachache waliokuwa wanawaibia wananchi.

Aliongeza kuwa hivi sasa kuna ujenzi mkubwa wa Kiwanda kipya cha kuzalisha chanjo cha Hester Bioscience Africa Limited (HBAL) ambacho kitazalisha chanjo 27 ifikapo Juni na uwekezaji wake una thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 50 na kuwezesha upatikanaji wa chanjo zote kwa wafugaji wa ndani ya nchi, Afrika na Dunia.

Akizungumza mara baada ya kuzindua vituo hivyo vitakachohudumia mikoa ya Songwe, Rukwa na Katavi vyenye makao yake mjini Sumbawanga, Waziri Mpina amesema kamwe Serikali haiwezi kukubali mifugo iendelee kufa kwa magonjwa na kwamba sasa magonjwa hayo hayana nafasi tena nchini.

Hivyo Serikali imeamua kuandaa Kanuni mpya za usimamizi wa uogeshaji na uchanjaji mifugo ili kudhibiti utoaji wa chanjo kwa wananchi na kwamba itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa wote wataokwenda kinyume na kanuni hizo.

Hivyo ameziagiza halmashauri zote nchini kuhakikisha zinashirikiana kwa karibu na vituo vya uchunguzi wa magonjwa na wakala wa maabara ya magonjwa ya mifugo vilivyoko katika kanda zao ili kutoa huduma bora kwa wafugaji na kuongeza uzalishaji wa mifugo na mazao yake.

Waziri Mpina pia amemuagiza Katibu Mkuu Mifugo na Katibu Mkuu Tamisemi kufanya mgawanyo mpya wa maafisa mifugo ili kuweza kupelekwa kwenye maeneo ambayo hayana kabisa maafisa mifugo ukiwemo Mkoa wa Katavi ambao hauna kabisa Madaktari wa Mifugo.

Pia ameagiza ZVC na TVLA Kanda ya Magharibi Sumbawanga kuwa wasimamizi na walezi wazuri wa wafugaji na mifugo na kuhakikisha kuwa chanjo, uogeshaji na haki za mifugo zinasimamiwa kikamilifu.

Waziri Mpina pia ameiagiza Kanda kusimamia kikamilifu uingizaji wa chanjo, madawa, viuatilifu, chakula na mazao ya mifugo yanayoingizwa nchini bila vibali, bila kulipiwa ushuru, bila kukaguliwa na yaliyokwisha muda wa matumizi na feki.

Kufuatia mageuzi ya utoaji huduma za mifugo nchini, Waziri Mpina amemwagiza Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo kufanya ukaguzi wa maafisa wa kanda zote ili kupanga safu mpya itakayokuwa tayari kuendana na kasi ya Serikali ya awamu ya tano.

Waziri Mpina ameonya kuwa siku nyingine ikitokea hatua zikachelewa kuchukuliwa kwa maafisa wanaohujumu mifugo basi Mkurugenzi wa huduma za mifugo ataondolewa kwenye wadhifa wake.

Waziri Mpina alisema wafugaji walikuwa wakipata huduma za uchunguzi wa magonjwa kilichopo Iringa umbali wa zaidi ya kilomita 900 kutoka Sumbawanga hali ilisababisha ugumu kwa wafugaji na kusababisha vifo vingi vya mifugo

Hivyo Waziri Mpina amebanisha kuwa uanzishaji wa kanda hiyo utaongeza ufanisi wa kazi ya udhibiti wa magonjwa ya mifugo katika mikoa ya Songwe, Rukwa na Katavi na kuleta ahueni kubwa kwa wafugaji.

Mpina aliongeza kuwa hadi sasa kuna Kanda 8 za Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo na Kanda 11 za Wakala wa Maabara Tanzania (TVLA) ambapo wizara inakusudia kuanzisha kanda nyingine moja katika mwaka fedha wa 2019/ 2020 itakayohudumia mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga kituo hicho kikikamilika kitasogeza huduma ya udhibiti wa magonjwa katika mikoa hiyo.

Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo nchini, Dk Hezron Nonga amesema tangu kuanzishwa kwa kituo hicho kumewezesha kuongezeka kwa huduma za uchunguzi wa magonjwa ya mifugo na mazao yake, shughuli za uchunguzi kimaabara zimesogezwa karibu na wananchi.

Pia upatikanaji wa chanjo kwa wafugaji kwa bei nafuu umekuwa rahisi, kuongezeka kwa upatikanaji wa taarifa za magonjwa , kuongezeka kwa majosho hamasa ya wafugaji kuongeza mifugo na idadi ya lita za kuogesha mifugo.

Pia ongezeko la maduhuli ya Serikali yatokanayo na usafirishaji wa mifugo na mazao yake ndani na nje ya nchi kutoka makadirio ya sh milioni 120 kwa mikoa miwili Rukwa na Katavi hapo awali na kufikia makadirio ya sh milioni 500 kwa mwaka, kufanikiwa kudhibiti ugonjwa wa homa ya nguruwe.

Dk Nonga amesema pia kumeongezeka mahusiano kati ya wizara na Serikali za mitaa na hivyo kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za mifugo kwa wananchi tofauti na ilivyokuwa awali.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina afungua kituo cha kanda cha ufuatiliaji, utambuzi na kuzuiaiya magonjwa ya mifugo Kanda ya Kusini Magharibi Sumbawanga tarehe 30/10/2019 Mkoani Rukwa.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni