Nav bar

Jumatatu, 28 Oktoba 2019

WAWEKEZAJI WATAKIWA KUYAONGEZEA THAMANI MAZIWA KUFIKIA SOKO LA NJE YA NCHI



Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel amekutana na wawekezaji kutoka Jamhuri ya Ireland wenye nia ya kuwekeza katika sekta ya maziwa hapa nchini na kuwataka kuangalia zaidi mnyororo wa thamani wa namna ya kuyaongezea thamani maziwa ili kupanua zaidi soko la maziwa kutoka Tanzania kwenda nchi za nje.

Akizungumza na wawekezaji hao  (Jumatatu 30.09.2019) kutoka shirika la Sustainable Food Systems Ireland (SFSI) ofisini kwake katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma, Prof. Gabriel amesema maziwa yatakapoongezewa thamani yataiwezesha Tanzania kuingia zaidi katika masoko ya nje ya nchi yakiwemo ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Ushirikiano na Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC)

“Waangalie pia zaidi mnyororo wa thamani namna ya kuyaongezea maziwa thamani ili tuingie zaidi katika solo la Afrika Mashariki, SADC na nje ya SADC. Lengo kubwa la wizara kwa wadau kama hawa wakija kutuona inakuwa faraja kwa kuwa inagusa maisha ya mfugaji wa kawaida, pale ambapo maziwa yatachakatwa na kuongezewa thamani soko litakuwepo tungependa wafugaji wazalishe maziwa ambayo wataweza kuuza.” Amesema Prof. Gabriel

Ameongeza kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi inafanya jitihada mbalimbali kuhakikisha inatengeneza mazingira wezeshi kwa wawekezaji ili soko la maziwa liendelee kuwepo kwa kuwa kwa sasa Tanzania inazalisha maziwa lita Bilioni 2.7 kwa mwaka hivyo yanapaswa kuongezewa thamani ili kukuza zaidi soko la maziwa ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa shirika la SFSI ambalo lipo chini ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Bahari ya Jamhuri ya Ireland Bw. David Butler, amesema shirika hilo ilimekuwa likifanya kazi katika nchini mbalimbali, ambapo limekuwa likifanya vizuri katika sekta ya nyama na maziwa kwa zaidi ya miaka 40 na kuendesha programu mbalimbali za kilimo na mifugo ili kuyaongezea thamani mazao.

Bw. Butler ameambatana na Dkt. Seamus Crosse kutoka Shirika la Greenfield International la Jamhuri ya Ireland, ambapo wawekezaji hao watakutana na wataalam mbalimbali kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na taasisi zilizo chini ya wizara hiyo ili kuangalia namna ya bora ya uwekezaji katika tasnia ya maziwa nchini.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akipokea ugeni kutoka Jamhuri ya Irland waliofika ofisini kwake Mtumba jijini Dodoma kwa nia ya kuwekeza katika sekta ya maziwa Nchini. Wageni hao wanatoka katika Shirika la SUstainable Food System  Ireland (SFSI) (30.9.2019)



Mkurugenzi wa Sera na Mipango (Mifugo), Bw. Amosy Zephania akitoa utambulisho wa wageni kutoka Jamhuri ya Ireland ambao wamefika  kwenye ofisi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi jijini Dodoma na kuwa na kikao na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel  wakielezea nia yao ya kuwekeza katika sekta ya maziwa nchini. (30.9.2019)


Picha ya pamoja ya mawaziri katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi mara baada ya kusaini maazimio 42 kwa ajili ya kuboresha sekta hizo, kufuatia kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa EACC jijini Arusha. (27.09.2019)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni