Nav bar

Jumatatu, 1 Julai 2019

WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI YAPONGEZWA KWA NIA YA KUANZISHA USHIRIKA WA WAFUGAJI WA ASILI




Wizara ya Mifugo na Uvuvi imepongezwa kwa jitihada zake za kuboresha mazingira ya wafugaji nchini, baada ya kuanzisha mchakato wa uanzishwaji wa chama cha ushirika wa wafugaji wa ng’ombe wa asili.

Akifungua semina iliyowahusisha wafugaji wa ng’ombe wa asili waliopo Wilayani Tunduru, Mkoani Ruvuma katibu tawala wa wilaya hiyo Bw. Ghaibu Lingo amesema ushirika huo utakapoanzishwa itakuwa rahisi kwa uongozi wa wilaya hiyo kutatua na kuwabaini wafugaji waliopo ili waweze kusaidiwa namna ya kukua kiuchumi na kuboreshewa mazingira ya maeneo ya ufugaji.

Bw. Lingo amesema kupitia ushirikia huo pia itakuwa rahisi kwa serikali ya wilaya kufahamu idadi halisi ya ng’ombe wa asili waliopo wilayani hapo na mahitaji yanayotakiwa yakiwemo ya majosho na madawa kwa ajili ya kuwahudumia mifugo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa Ugani kutoka Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani Dkt. Pius Mwambene amesema kuanzishwa kwa chama cha ushirika wa wafugaji wa ng’ombe wa asili ni kati ya malengo saba ya wizara hiyo yanayolenga kuboresha sekta ya mifugo nchini.

Dkt. Mwambene amesema ushirika huo utaweza kuwasaidia wafugaji kujiinua kiuchumi na pia serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi itaweza kuwatambua rasmi wafugaji hao kupitia chama hicho na kuweza kuwasaidia kupitia chama chao.

Akitoa mada kuhusu malisho bora ya mifugo mara baada ya kufunguliwa kwa semina hiyo, Afisa Mifugo kutoka Idara ya Uendelezaji wa Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo Bw. Deogratius Nholope amewataka wafugaji kuwa na ufahamu juu ya malisho bora ya mifugo yao ili iweze kuwa na afya bora na kuweza kutoa mazao bora.

Bw. Nholope amesema kupitia kuanzishwa kwa chama cha ushirika cha wafugaji wa ng’ombe wa asili katika Wilaya ya Tunduru, wafugaji watapata fursa ya kufahamu namna ya kupata malisho bora na pia kupatiwa mbegu kwa ajili ya kupanda malisho.

Naye Afisa Ushirika kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Bi. Miriam Mahuwi amewafahamisha wafugaji hao umuhimu wa ushirika kwa kuwa utawajenga kiuchumi na hatimaye kuwa na ufugaji wenye mafanikio kupitia chama hicho.

Bi. Mahuwi amesema ili kuanzishwa kwa ushirika huo ni vyema wafugaji hao wakawa katika kikundi wanachoelewana na ambao wanafanya shughuli inayofanana na kujiwekea malengo na hatimaye chama hicho mara baada ya kuanzishwa kiweze kuwapatia mafanikio kiuchumi.

Semina hiyo imewahusisha wafugaji kutoka Wilaya ya Tunduru, Mkoani Ruvuma ambao wamepatiwa vitalu na Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ili waweze kulisha mifugo yao na kuondokana na tabia ya kuhamahama kutafuta malisho.



Mkurugenzi Msaidizi wa Ugani, kutoka Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani Dkt. Pius Mwambene akitoa mada kwa wafugaji juu ya umuhimu wa kuanzishwa kwa chama cha wafugaji wa ng’ombe wa asili katika Wilaya ya Tunduru, Mkoani Ruvuma. (12.06.2019)




Afisa Mifugo kutoka Idara ya Uendelezaji wa Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo Bw. Deogratius Nholope akitoa mada kwa wafugaji juu ya umuhimu wa malisho bora ya mifugo kwa wafugaji waliohudhuria semina ya uanzishwaji wa chama cha ushirika wa wafugaji wa ng’ombe wa asili katika Wilaya ya Tunduru, Mkoani Ruvuma. (12.06.2019)




Afisa Ushirika kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Bi. Miriam Mahuwi akizungumzia faida na namna ya kuanzishwa kwa ushirika kwa wafugaji waliohudhuria semina yenye lengo la kuanzishwa kwa chama cha ushirika wa wafugaji wa ng’ombe wa asili katika Wilaya ya Tunduru, Mkoani Ruvuma. (12.06.2019)






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni