Nav bar

Jumanne, 14 Mei 2019

KATIBU MKUU WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI (MIFUGO) AAHIDI KUBORESHA WIZARA KUWA YA MFANO KIUTENDAJI SERIKALINI



                                                                                                                                                               

                                                                                                                                                            
 Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo)   Prof. Elisante Ole  Gabriel amesema anataka wizara hiyo iwe ya mfano katika kumsaidia Rais Dkt. John Magufuli katika kutimiza majukumu na malengo ya nchi kwa kufanya kazi kwa bidii na ufanisi zaidi.

Prof. Gabriel amesema hayo leo (08.05.2019) ofisini kwake jijini Dodoma wakati akipokea taarifa ya ukaguzi wa utendaji kazi wa wizara hiyo katika idara ya utawala na rasilimali watu, na kupongeza utendaji kazi wa idara hiyo katika kusimamia matakwa ya mtumishi wa umma.

 "Nina dhamira ya dhati ya kuboresha wizara na mambo yote yaliyofanyiwa ukaguzi yatafanyiwa kazi na yanaendelea kufanyiwa kazi pamoja na kusaini fomu zote za likizo kwa wakati, kupandisha watumishi vyeo pamoja na kutoa elimu ya majukumu kwa waajiriwa wote." Alisema Prof. Gabriel.

Aidha Katibu Mkuu huyo akizungumza mbele ya wakaguzi kutoka katika tume hiyo wakiongozwa na bibi Kombe Shayo, ameshauri wakaguzi kutembelea taasisi zilizo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi zikiwemo TALIRI, TAFIRI, TVLA, FETA, Bodi ya Maziwa na Bozi ya Nyama kuona wanavyofanya shughuli zao, kuonyesha kiwango au hatua walizofikia tangu kuanza kwa ukaguzi.

Hali kadhalika Prof. Gabriel ameomba wakaguzi kutoa elimu ya ‘opras’ kwa watumishi wa wizara mwishoni mwa mwezi Mei au mwanzoni mwa mwezi Juni ili watumishi waelewe vizuri na  kupewa zaidi elimu ya nidhamu ya kazi pamoja na ufanyaji kazi mzuri, ulio bora na wenye tija.

Awali akiwasilisha taarifa kwa katibu mkuu huyo, Mkaguzi kutoka Tume ya Utumishi wa Umma Bibi Kombe Shayo amesema watumishi wanapaswa kupewa elimu juu ya kujaza fomu ya ‘opras’ na watu wa masijala wapate maelekezo ya jinsi ya kutunza fomu hizo pamoja na menejimenti ya wizara kuhakikisha inapandisha watumishi madaraja na kuwathibitisha kazini kwa wakati pamoja na watumishi kupata mgawanyo wa kazi.

"Watumishi wanaenda kwenye mafunzo na wanatoa taarifa pindi wakiwa masomoni na pindi wamalizapo ambalo ni jambo zuri  na pia ufadhili upo na watumishi wakasome mapema na wasisubiri umri usogee" alifafanua Bibi Shayo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Bw. Zakariyya Kera alipatiwa sifa za kipekee na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel pamoja na Mkaguzi wa Tume ya Utumishi wa Umma Bibi Kombe Shayo kwa kufanya kazi kwa umahiri mkubwa katika idara hiyo kutokana na kusimamia kwa ufanisi mkubwa mambo mbalimbali yahusuyo watumishi wa wizara hiyo.


Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Zakariyya Kera akimwagiwa sifa za utendaji na mkaguzi Bi. Kombe Shayo.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wakaguzi kutoka tume ya Utumishi wa Umma  pamoja na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu wa Wizara hiyo Bw. Zakariyya Kera (wa kwanza kushoto).


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni