Nav bar

Jumatano, 6 Machi 2024

MRADI WA BOTI NA VIZIMBA UTALETA MAPINDUZI YA KWELI UCHUMI WA BULUU: WADAU

 

Na. Mbaraka Kambona, Mwanza

Wadau wa sekta ya uvuvi kutoka Kanda ya Ziwa Victoria wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwaletea mradi adhimu wa mkopo wa masharti nafuu wa maboti na vizimba wakiamini kuwa mradi huo ndio umebeba mustakabali mwema wa sekta ya uvuvi hapa nchini.

Wamesema mradi huo ambao ni wa kwanza kutekelezwa hapa nchini na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais, Dkt. Samia  Suluhu Hassan unaleta matumaini makubwa kwao kwani sasa wataweza kufanya shughuli zao za uvuvi kisasa na kusaidia kuboresha mnyororo mzima wa mazao ya uvuvi.

Sehemu ya wadau hao wa uvuvi kutoka Kanda ya Ziwa Viktoria wakiongea kwa nyakati tofauti wakiwa mkoani Mwanza hivi karibuni wameeleza hisia zao na maoni mbalimbali juu ya hatua hiyo ya Rais samia kuwakopesha boti na vizimba.

Mwenyekiti wa Chama Cha Ushirika Cha Wauza Samaki Mwaloni (USAMWA),Mwanza,  Bw. Erasto Barosha amempongeza Rais, Dkt. Samia kwa kuwaletea mradi huo wa kuwakopesha wavuvi vizimba na maboti akisema kuwa unakwenda moja kwa moja kuwagusa na kuwainua wananchi wa hali ya chini.

Ameongeza kwa kusema kuwa kwa muda mrefu ziwa hilo hawakuwa wakilitumia vizuri lakini kupitia mpango huo wa Rais Samia sasa wanakwenda kutumia ziwa hilo vizuri huku akiamini kuwa mradi huo unakwenda kuleta mapinduzi makubwa kwenye uchumi wa buluu.

Katibu wa Ushirika wa Wachakata Samaki (UWASA), Bw. Shabani Hamisi amemshukuru Rais Samia kwa kupata wahyi wa kuwainua watu wa chini kwa kuwaletea zana bora za uvuvi.

“Hapa Rais wetu ametumia falsafa; mtu usimpe samaki, mpe ndoano akavue…sasa hapa ameamua kutukabidhi ndoano tukavue ili tutoke katika hali ya chini na kuinua kipato chetu”, amesema

“Nimuahidi Rais wetu, hatutamuangusha, tutafanya vizuri zaidi ili hata kama ana kingine cha kutupa asisite kutuletea”, ameongeza

Naye, Katibu wa Chama Cha Ushiriki Cha Wauza Samaki Tushirikiane (WASATU), Bw. Luka Katabalo amempongeza Mhe. Rais  kwa niaba ya wanachama wa (WASATU) mkoani Mwanza huku akisema kuwa mradi huo utasaidia kutoa ajira nyingi zaidi na kuinua kipato cha wanaushirika na taifa kwa ujumla.

Aidha, ametumia fursa hiyo pia kumshukuru Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega kwa kusimamia vizuri sekta na kuwajali vyama vya ushirika.

“Mhe. Ulega wakati wote amekuwa akitusikiliza katika shughuli zetu hizi na tunamuomba asituchoke aendelee kutuunga mkono ili sekta hii ya uvuvi iendelee kuleta tija zaidi hapa nchini”, amesema

Mfanyabiashara wa Mazao ya Samaki katika Mwalo wa Kilumba jijini Mwanza, Bw. Jonas Luvanga amesema kuwa mradi huo umekuja wakati muafaka kwani wavuvi wengi wanachangamoto ya mitaji hivyo mradi huo wa mkopo wa maboti kwa wavuvi unaleta suluhisho la changamoto hiyo.

“Kwa kutupatia maboti ya uvuvi yatatusaidia kuboresha uchumi wetu sisi kama wananchi na taifa kwa ujumla, Ahsante sana Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan”,  alibainisha

Kwa Upande wake, Mvuvi wa Ziwa Victoria, Bw. Gerald Mayala amesema mradi huo utakuwa na faida kubwa kwao. Mradi huu utatusaidia kuondokana na uvuvi wa mazoea na utasaidia sana kupunguza uvuvi haramu kupitia ufugaji wa vizimba

Mfanyabiashara wa Samaki katika Mwalo wa Kilumba, Bw. William Clemence amesema kuwa anaamini mradi huo wa maboti na vizimba utawasaidia kupata mazao mengi ya uvuvi ambayo wataweza kuuza nje ya nchi kama vile Kongo na kuweza kukuza kipato chao na nchi kwa ujumla wake.

Januari 30, 2024, Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kugawa maboti 55 na Vizimba 222 kwa wavuvi wa Kanda ya Ziwa Viktoria tukio ambalo litafanyika katika uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza ambapo pia ataongea na Wananchi kupitia tukio hilo.


Wafanyabiashara wa samaki katika soko la Kirumba, jijini Mwanza wakipima samaki aina ya sangara katika mzani kabla ya kuwachakata na kuwauza katika masoko mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.

Mmoja wa Wafanyabiashara wa Samaki katika Soko la Kirumba, jijini Mwanza akionesha samaki aina ya Sangara wanaopatikana katika ziwa victoria ambao wanawakausha na kuwauza nje ya nchi ikiwemo Kongo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni