Nav bar

Jumamosi, 4 Machi 2023

ULEGA KUENDELEZA UTEKELEZAJI WA MIKAKATI YA KUKUZA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amemuhakikishia Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hasani kuwa Sekta za Mifugo na Uvuvi zinakwenda kuongeza uzalishaji, kutoa ajira na kuleta tija kwa taifa.

 

Waziri Ulega ameyasema hayo leo (28.02.2023) mara baada ya kukabidhiwa ofisi na Waziri aliyemaliza muda wake Mhe. Mashimba Ndaki kwenye Ofisi za Wizara zilizopo kwenye Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.

 

Amesema kuwa zipo fursa nyingi kupitia Sekta za Mifugo na Uvuvi ambazo zikitumiwa vizuri na vijana zinaweza kuleta mabadiliko makubwa kwa kutoa ajira na kuongeza mchango wa sekta hizo kwenye pato la taifa. Hivyo amewasihi watumishi kufanya kazi kwa uweledi, ubunifu, uaminifu na kuongeza kasi katika  utendaji.

 

Aidha, amewashukuru viongozi waliomaliza muda wao kwa ushirikiano ambao walimpatia wakati wote aliohudumu kama Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi ambapo pia amewasihi watumishi kuendelea kutoa ushirikiano kwa viongozi ili mikakati iliyowekwa ya kuendeleza sekta hizo.

 

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. David Silinde ameishukuru Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwa ushirikiano waliompatia wakati akitekeleza majukumu yake lakini amewasihi watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kushirikiana na viongozi wote wapya ili kuhakikisha maendeleo kwenye sekta yanakua.

 

Mhe. Silinde amesema wameletwa kwenye Wizara kwa ajili ya kuhakikisha inatangazwa kutokana na kazi mbalimbali zinazofanywa ili wadau waweze kutumia fursa zilizopo kwenye Sekta za Mifugo na Uvuvi.

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe amewasihi watumishi kutoa ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku. Amewasihi watumishi kutoa ushauri utakao saidia kuzifanya sekta za mifugo na uvuvi zinaendelea kukua na kuzalisha kwa tija. Pia amewasihi watumishi watumishi kufanya kazi kwa uadilifu, uaminifu na upendo.

 

Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Sekta ya Mifugo, Dkt. Daniel Mushi amesema kuwa kazi waliyonayo ni kuhakikisha wanaendelea kusimamia utekelezaji wa mpango wa mabadiliko wa sekta ili kuhakikisha uzalishaji wa mifugo na mazao yake unaleta tija kwa wafugaji na taifa kwa ujumla. Pia amesema kuwa Wizara itaendelea na jitihada ya kuimarisha taasisi zilizo chini yake ili kuhakikisha zinaendelea kutimiza wajibu wake katika kuleta maendeleo yanayotarajiwa.

 

 

Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Sekta ya Uvuvi, Bi. Agness Meena amesema kuwa matarajio yake ni kuhakikisha kwanza wanasimamia utekelezaji wa mikakati ambayo tayari imeshawekwa na viongozi waliotangulia katika kuhakikisha Sekta ya Uvuvi inakua.

 

Waziri aliyemaliza muda wake, Mhe. Mashimba Ndaki amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia kwa kumpatia nafasi ya kusimamia Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Vilevile amewashukuru watumishi wote kwa ushirikiano waliompatia wakati wa utekelezaji wa majukumu n ani Imani yake kuwa ushirikiano huo utaendelea kutolewa kwa viongozi wapya.

 

Mhe. Ndaki amewasihi viongozi kushirikiana na watumishi katika kutekeleza majukumu yao ili sekta za mifugo na uvuvi ziweze kukua na kuongeza mchango wake kwa wafugaji, wavuvi na pato la taifa kwa ujumla. Vilevile amewaeleza kuwa Mhe. Dkt. Samia ameendelea kusisitiza kuwa Sekta za uzalishaji ikiwemo Mifugo na Uvuvi zihakikishe zinazalisha ajira kwa vijana na wanawake hivyo bado kuna kazi kubwa inayotakiwa kufanyika.

 

Naye Katibu Mkuu Mstaafu aliyekuwa anasimamia Sekta ya Mifugo amewashukuru viongozi na watumishi kwa ushirikiano waliompatia katika utekelezaji wa majukumu. Pia amewasihi watumishi kuendelea kutoa ushirikiano kwa viongozi wapya walioteuliwa ili kuhakikisha sekta ya mifugo inaendelea kukua.

 

Dkt. Rashid Tamatamah ambaye alikuwa Katibu Mkuu anayesimamia Sekta ya Uvuvi licha ya kuwashukuru watumishi kwa ushirikiano waliompatia amewaasa viongozi kuendelea kusimamia maslai ya watumishi ili waweze kutimiza majukumu yao kwa ufanisi.

 

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya watumishi, Afisa Uvuvi Mkuu, Bi. Upendo Hamidu amewashukuru viongozi waliomaliza muda wao kwa ushirikiano walioutoa katika kutekeleza majukumu ya Wizara na ameahidi kuwa watumishi wataendelea kutekeleza majukumu yao ili kuhakikisha Sekta za Mifugo na Uvuvi zinakuwa ni kimbilio kwenye kutoa ajira kwa vijana na wanawake.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni