Nav bar

Jumatatu, 20 Februari 2023

WATAFITI NA WANASAYANSI KUTOKA NCHI 18 DUNIANI WAKUTANA JIJINI ARUSHA

WATAFITI na wanasayansi kutoka nchini 18 duniani, wamekutana jijini  Arusha kutafuta ufumbuzi wa kutokomeza ugonjwa wa  Ndorobo unaoenezwa na Mbung’o ambao umekuwa tishio kwa wanyama na binadamu kwa nchi za Afrika ikiwemo Tanzania.

Akiongea kwenye mkutano huo jana Jijini Arusha Mkurugenzi wa huduma za Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Hezron Nonga alisema watafiti hao watakuja na jibu la pamoja la namna ya kutokomeza ugonjwa huo unaotishia soko la Nyama kimataifa.

Amesisitiza kuwa uwepo wa ugonjwa wa Ndorobo, Afrika inapata hasara ya takribani dola za kimarekani bilioni 1.2 kutokana na gharama za matibabu na mifugo kukataliwa kuchinjwa .

Amesema Tanzania imefanikiwa kudhibiti ugonjwa huo kwa kiasi kikubwa ambapo hadi sasa upo chini ya asilimia 1.5, lakini jitihada zaidi zinahitajika ili kuutokomeza kutokana na mbung’o wengi kuwepo maeneo yaliyo jirani na misitu na hifadhi za wanyama pori na hivyo kusababisha mifugo mingi kukondeana na hatimaye kufa kutokana na vimelea wanavyoambukizwa na Mbung’o. 

“Ng’ombe anapougua ugonjwa huo hukondeana kwa muda mrefu, afya yake huwa mbovu na hivyo hushindwa kuzalisha na nyama yake huwa mbovu haifai kuliwa na binadamu ndio maana watafiti wamekutana ili kubadilishana uzoefu ili kupata njia bora ya kutokomeza ugonjwa huo” amesema

Prof. Nonga amesema kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikifanya jitihada kubwa ya kupambana na ugonjwa huo kupitia majosho ya uogeshaji mifugo zaidi ya 3000 yaliyopo nchi nzima ili kuua wadudu kupe na mbung’o.

“Serikali imekuwa ikinunua dawa za kuogesha mifugo na kuzitoa kwa wafugaji ili wakaogeshe mifugo yao na kutokomeza magonjwa yaenezwayo na Mbung’o, Kupe na Mbu anayesambaza ugonjwa wa homa ya bonde la ufa” amesema Prof Nonga.

Aidha amesema hapa nchini kuna viwanda vya nyama zaidi ya 10 vinavyohitaji kuzalisha nyama iliyobora ili kuuza nje ya nchi, lakini vimeshindwa kukidhi mahitaji ya soko kutokana na changamoto ya nyama kunakosababishwa na ugonjwa wa mbung’o.

Ameongeza kuwa, pamoja na mambo mengine mkutano huo utakuja na majibu juu ya ufugaji bora wenye tija utakaokuwa na manufaa kwa mfugaji kuweza kutajirika na mifugo yake. Alitoa wito kwa wafugaji kuwatumia wataalamu wa mifugo pindi wanapoona uwepo wa dalili za magonjwa hayo.

Naye Dkt. Furaha Mramba ambaye ni mtafiti kiongozi kupitia mradi wa kudhibiti ugonjwa wa Ndorobo kwa njia ya kutumia dawa Tanzania, amesema kuwa wamefanikiwa kugundua aina saba za Ndorobo wenye uwezo wa kusambaza ugonjwa kwa mifugo na binadamu.

Dkt. Mramba ambaye pia ni Mkurugenzi wa kampuni ya kuzalisha chanjo za wanyama Tanzania, amesema maeneo ya uhifadhi wa wanyama pori ndio yenye Ndorobo wengi na hivyo aliwashauri wafugaji kuhakikisha wanafuata ushauri wanaopewa na wataalam wa mifugo ikiwa ni pamoja na uogeshaji mifugo ili pale wanapolisha maeneo jirani na hifadhi za Wanyama pori mifugo isiweze kuathiriwa na magonjwa hayo.

Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Mifugo, Prof. Hezron Nonga akifungua mkutano uliowakutanisha watafiti wa mifugo Africa kujadili namna ya kudhibiti ugonjwa wa Ndorobo kwa kutumia dawa ambao umefanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Mount Meru Jijini Arusha. (14.02.2022)


Mtafiti kiongozi wa Mradi wa kudhibiti ugonjwa wa ndorobo kwa njia ya dawa Tanzania, Dkt. Furaha Mramba akitoa maelezo ya awali kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufungua mkutano uliowakutanisha watafiti wa mifugo Africa kujadili namna ya kudhibiti ugonjwa wa Ndorobo kwa kutumia dawa ambao umefanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Mount Meru Jijini Arusha. (14.02.2022)

Baadhi ya washiriki wa mkutano uliowakutanisha watafiti wa mifugon Africa kujadili namna ya kudhibiti ugonjwa wa Ndorobo kwa kutumia dawa wakifuatilia mada zilizokuwa zinawasilishwa. Mkutano huo umefanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Mount Meru Jijini Arusha. (14.02.2022)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni