Nav bar

Ijumaa, 9 Aprili 2021

WACHUNAJI WATAKIWA MBINU BORA NA VIFAA STAHIKI

Wachunaji wa ngozi katika machinjio ya Manispaa ya Tabora wametakiwa kutumia mbinu bora na vifaa stahiki wakati wa uchunaji wa ngozi.

 

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe kutoka WMUV, Bw. Gabriel Bura leo (08.04.2021) wakati akifungua mafunzo kwa wachunaji hao yaliyofanyika katika eneo la Machinjio hiyo.

 

Bura amesema kumekuwa na uharibifu mkubwa wa ngozi unaotokana na kukosekana kwa matumizi ya mbinu bora, vifaa stahiki na umakini katika uchunaji ambapo ngozi kuchunwa vibaya na nyingine na hivyo kupoteza ubora unaotakiwa katika viwanda.

 

"Ngozi ni moja kati ya mazao ya mifugo yanayoliingizia taifa fedha nyingi lakini kutokana na uchunaji mbovu mnasababisha ngozi nyingi kutofaa kwa matumizi ya viwanda wakati mahitaji ya viwanda ni makubwa," alisema Bura.

 

Aidha, Bura aliwaeleza kuwa baada ya mafunzo hayo ya kupeana mbinu bora za uchunaji na matumizi ya vifaa stahiki, watatakiwa kujaza fomu kwa ajili ya kupatiwa leseni na endapo mchunaji hatakuwa na leseni hataruhusiwa kuingia machinjioni kufanya shughuli za uchunaji. Na ni matarajio ya wizara na wenye viwanda kuwa kuanzia sasa watakuwa wakichuna ngozi kwa kufuata maelekezo waliyopatiwa.

 

Vilevile amesema katika kuikagua machinjio hiyo amebaini ubovu wa sakafu ambao kama usiporekebishwa nao ni chanzo cha uharibifu wa ngozi hasa pale ng'ombe anapovutwa baada ya kuchinjwa.

 

Naye mwakilishi wa Mkurugenzi wa manispaa ya Tabora ambaye pia ni Afisa Mifugo, Neema Kapesa amesema mafunzo hayo ni muhimu sana kwao kama wataalam wa halmashauri na kwa wachunaji.

 

Bi. Kapesa amesema sasa watahakikisha taratibu zinazotakiwa zinafuatwa na wachunaji katika kuchuna ngozi na endapo mchunaji ataharibi ngozi watamchukulia hatua. Lakini pia ameahidi kumfikishia Mkurugenzi wa Manispaa hiyo tatizo la miundombinu hasa kwenye sakafu ili aone namna ya kulitatua kwani haitakuwa vizuri Manispaa ikawa ndio chanzo cha uharibifu wa ngozi kutokana na ubovu wa sakafu.

 

Afisa Masoko na Mahusiano kutoka Kiwanda cha Ngozi cha Kilimanjaro, Fredrick Njoka amesema wameamua kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Mifugo) kutoa elimu kuhusu mbinu bora za uchunaji ngozi na matumizi ya vifaa stahiki kwa kuanza na wachunaji kwa kuwa imebainika asilimia kubwa ya ngozi huaribika machinjioni.

 

Njoka amesema mahitaji ya ngozi katika viwanda ni makubwa na ili wazalishe bidhaa bora ni lazima wapate ngozi bora. Hivyo elimu hii wataendelea kushirikiana na wizara kuitoa katika mikoa mbalimbali.

Wataalam na Wachinaji wa Ngozi katika machinjio ya Manispaa ya Tabora wakisikiliza mafunzo kuhusu mbinu bora za uchunaji ngozi na matumizi ya vifaa stahiki. (08.04.2021)


Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo Usalama wa Chakula na Lishe kutoka WMUV, Bw. Gabriel Bura (kushoto) akizungumzia kuhusu mafunzo ambayo yangetolewa kwa wachunaji wa ngozi kuhusu mbinu bora za uchunaji ngozi na matumizi ya vifaa stahiki wakati alipokutana na Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora, Bosco Ndunguru (katikati) ofisini kwake muda mchache kabla ya mafunzo hayo kufanyika. Kulia ni Afisa Mifugo wa Manispaa ya Tabora, Neema Kapesa. (08.04.2021)
Mkaguzi wa Ngozi na Nyama, Bw. Elia Sandael (kushoto) akifafanua jambo kwa Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo Usalama wa Chakula na Lishe kutoka WMUV, Bw. Gabriel Bura (kulia) alipokuwa akiikagua machinjio ya Manispaa ya Tabora wakati alipofika hapo kwa ajili ya kutoa mafunzo kuhusu mbinu bora za uchunaji ngozi na matumizi ya vifaa stahiki. (08.04.2021)
Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo Usalama wa Chakula na Lishe kutoka WMUV, Bw. Gabriel Bura akikagua ngozi ambazo zimeanikwa nje ya machinjio ya Manispaa ya Tabora. Kulia ni mnunuzi wa ngozi, Bw. Kidanka Ntandu na kushoto ni Mkaguzi wa Ngozi na Nyama, Bw. Elia Sandael. (08.04.2021)
Picha ya pamoja kati ya wataalam na wachunaji wa ngozi wa machinjio ya manispaa ya Tabora mara baada ya kumalizika kwa mafunzo kuhusu mbinu bora za uchunaji ngozi na matumizi ya vifaa stahiki. (08.08.2021)




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni