Nav bar

Jumanne, 23 Juni 2020

MAGUFULI APONGEZA MAFANIKIO YALIYOPATIKANA SEKTA YA MIFUGO NA UVUVI



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Magufuli ameipongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa jitihada kubwa ilizozichukua katika kipindi cha miaka mitano ya Uongozi wake ambazo zimesaidia kuboresha na kukuza uchumi wa nchi.

Akizungumza wakati akitoa hotuba yake ya kulifunga Bunge la kumi na moja (11) la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Juni 16, 2020 jijini Dodoma, Rais Magufuli alisema kuwa katika kipindi hiki cha miaka mitano ya uongozi wake Wizara ya mifugo imechukua hatua kadhaa ambazo zimesaidia nchi kufikia mafanikio makubwa.

Rais Magufuli akitaja baadhi ya maeneo ambayo Wizara imeyashughulikia na kupata mafanikio, alisema kuwa katika kipindi hicho serikali iliongeza eneo la ufugaji kutoka hekta milioni 1.4 mwaka 2005 hadi kufikia hekta milioni 5 mwaka 2020. Jambo ambalo amelitaja kuwa limechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza migogoro kati ya Wakulima na Wafugaji.

Kwa mujibu wa Rais Magufuli, Serikali kupitia Wizara imejenga mabwawa mapya ya kuogeshea ng’ombe 104, imesambaza chanjo na dawa za Mifugo nchi nzima, huku idadi ya ng’ombe waliohimilishwa imeongezeka kutoka laki moja na elfu tano (105,000) mwaka 2015 hadi kufikia laki tano kumi na nne elfu na mia saba (514,700).

Aliongeza kuwa serikali imeimarisha ulinzi na usimamizi wa rasilimali za uvuvi, kwa kuanzisha kanda kuu tatu (3) za Ziwa Victoria, Tanganyika na Pwani ikiwa ni pamoja na kudhibiti zana haramu za uvuvi.

“Nakumbuka kuna wakati nilimuona Mhe. Mpina alikuwa anatembea na rula kwenye Migahawa kupima urefu wa Samaki, hiyo ilikuwa ni katika hatua za kuhakikisha tunapata mafanikio haya ambayo tumeyapata”, alisema Rais Magufuli.

Aliendelea kusema kuwa Wizara imehamasisha na kufanikiwa kuongeza idadi ya Wafugaji wa Samaki kutoka laki moja themanini elfu na mia nane arobaini na tatu (180,843) mwaka 2015 hadi kufikia laki mbili sitini elfu mia nne sabini na nne (260,474) mwaka 2020.

“Katika kipindi hiki tumeongeza idadi ya Mabwawa kutoka 220,545 hadi kufikia 260,445 na kuongeza vizimba vya samaki kutoka 109 hadi 431, na uzalishaji wa Vifaranga vya Samaki vimeongezeka kutoka milioni nane na tisini elfu (8,090,000) hadi Vifaranga milioni kumi na nne laki tano thelathini na moja elfu mia nne themanini na saba (14,531,487)”, aliongeza Rais Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli alisema kuwa sambamba na mafanikio hayo serikali imeongezea mtaji kwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) kiasi cha Shilingi Bilioni Mia Mbili na nane kupitia Mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika. Pia serikali imeipatia TADB Dola za Kimarekani Milioni 25 sawa na Shilingi Bilioni 57.8 ili kuendesha Mfuko wa dhamana.

“Hii ina maana kuwa kwa miaka mitano iliyopita Serikali imeipa TADB Shilingi Bilioni 324.8 kuiwezesha Benki hiyo kutoa mikopo ya moja kwa moja kwa wakulima, wafugaji na wavuvi yenye thamani ya kiasi cha shilingi bilioni 166.9 kwa Riba nafuu”, aliongeza Rais Magufuli

Kutokana na hatua hizo, Rais Magufuli alisema kuwa mafanikio makubwa yamepatikana ambapo Sangara kwenye ziwa Victoria wameongezeka kutoka tani 417,936 mwaka 2016 hadi kufikia tani 816,964 mwaka 2020.

“Kufuatia hatua hizo, urefu wa Sangara umeongezeka kutoka wastani wa sentimeta 16 hadi kufikia sentimeta 25.2 jambo ambalo limefanya samaki wetu kuanza kuhitajika kwa kiasi kikubwa katika soko la Ulaya na nyinyi ni mashahidi Waheshimiwa Wabunge ndege zimeanza kuja Mwanza na kubeba Samaki wetu kwa ajili ya kupeleka nje ya nchi”, alisisitiza Rais Magufuli.

 “Kwa kuzingatia hilo mauzo ya samaki nje ya nchi yameongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 379 mwaka 2015 hadi bilioni 692 mwaka 2019”, alieleza Rais Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli alisisitiza kuwa mafanikio hayo sio mambo madogo ni hatua muhimu katika kukuza uchumi wa nchi ambao kwa sasa upo katika hatua nzuri ya kufikia uchumi wa kati ifikipo mwaka 2025.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Magufuli Akizungumza wakati akitoa hotuba yake ya kulifunga Bunge la kumi na moja (11) la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Juni 16, 2020 jijini Dodoma.








Hakuna maoni:

Chapisha Maoni