Nav bar

Jumatatu, 13 Mei 2019

SERIKALI ZA TANZANIA NA DENMARK ZAJA NA MPANGO WA KULINDA RASILIMALI ZA ZIWA TANGANYIKA.




SERIKALI ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Denmark kupitia Shirika la Misaada la Kimaendeleo (DANIDA) imesema kuna haja ya kuendeleza mapinduzi makubwa katika sekta ya uvuvi nchini ili kulinda rasilimali zipatikanazo katika maziwa, bahari na mito nchini.

Akizungumza jijini Dodoma wakati wa kupokea taarifa ya utafiti uliofanywa katika Ziwa Tanganyika lililopo Mkoani Kigoma, kutazama mabadiliko ya tabia nchi katika eneo la ziwa hilo, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amesema utafiti huo umeonyesha wazi kuwa zipo athari zinazotokana na tabia nchi na sababu zingine kama idadi ya wavuvi kuongezeka na baadhi yao kutumia zana haramu za uvuvi na kuathiri mazingira ya ziwa na rasilimali zilizopo.

Mhe. Ulega amesema mambo yote ambayo yamefanyiwa utafiti yakijadiliwa vyema litatolewa tamko la Sera ambayo itakuwa ni ushauri wa kitaalam ambao utaiongoza serikali ikiwa inaendelea kufanya maboresho ya kanuni na sheria za uvuvi.

"Kitu hiki ni muhimu sana kwa sababu eneo la Ziwa Tanganyika watu wanatengemea sana kwa shughuli za kujipatia samaki na kuendesha maisha yao, ile rasilimali tusipoweza kuweka mkakati mzuri wa kuitunza na kuhakikisha kuwa inakuwa endelevu basi maana yake jamii ile kuna wakati ile rasilimali kama sasa hivi kiasi cha samaki kimepungua sio kama ilivyokuwa huko kipindi cha nyuma”. Alisema Mhe. Ulega

Amefafanua kuwa ni muhimu kuchukua hatua mbalimbali za kielimu kwa kuwaelimisha wavuvi, hatua za kusimamia kwa kutumia njia zilizo bora zaidi ili kupatikana kwa uendelevu wa rasilimali zilizopo katika Ziwa Tanganyika.

“Kinyume na hapo watu watakosa zile fursa na umasikini utajikita zaidi kwa hivyo ni muhimu kudhibiti na kuweza kuwa na mpangilio mzuri ili mradi ile rasilimali iweze kuwa endelevu”. Alifafanua Mhe. Ulega

Aidha Naibu Waziri Ulega amebainisha kuwa serikali na wananchi kwa ujumla ina jukumu la kudhibiti shughuli za   kibinadamu ziendane na utaratibu wa ulinzi wa mazingira ili kudhibiti athari za mazingira.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Rashid Tamatamah amesema matokeo hayo ya utafiti yamekuja wakati muafaka kwa sababu baadhi ya majukumu ya kisera ambayo wameyaleta yanahusiana na zoezi ambalo linaendeshwa na wizara la kuboresha Sheria ya Uvuvi ya mwaka 2003 ili iendane na hali halisi ya sasa.

“Tumekusanya maoni kwa wadau nchi nzima na sasa tunachambua yale maoni tuangalie maendeleo yanayotakiwa, kwa hiyo na hawa katika ushauri wanaokuja nao na matamko ya kisera kuna maeneo vilevile kutokana na uchunguzi waliofanya wanaona ili tuendelee vizuri katika kujenga rasilimali za uvuvi katika Ziwa Tanganyika kuna vitu tunatakiwa tubadilishe kwenye sheria hivyo wamekuja muda muafaka na tumefurahi sana”. Alisema Dkt. Tamatamah

Hali kadhalika, Bw. Ismail Aron Kimbilei ambaye ni Mkurugenzi wa Kituo cha Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Mkoa wa Kigoma amesema wamependekeza Ziwa Tanganyika kupumzishwa kwa shughuli za uvuvi kila baada ya muda fulani ili kuongeza mazalia ya samaki.

“Naamini kwamba yatafanyiwa kazi na naamini utafiti wetu utakuwa  na faida kama watawahusisha wadau kwamba wavuvi wawekwe chini na waelezwe faida za kutunza ziwa na waelezwe hasara za kufanya kinyume na matarajio halafu waangalie na waamue  kwa pamoja na wanaweza kufanya kwa mfano tuu tuanze kwa kufunga miezi mitatu tuone matokeo yake kama dagaa na migebuka itakuwa imeongezeka na baada ya hapo wataamua cha msingi ni kushirikisha wadau.” Alisema Bw. Kimbilei


Naibu Waziri wa Wizara ya MIfugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega katika picha ya pamoja na Watafiti wa kutazama mabadiliko ya tabia nchi katika eneo la Ziwa Tanganyika na wawakilishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi jijini Dodoma.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni