Nav bar

Jumanne, 23 Januari 2024

ULEGA AKABIDHI CHANJO KWA WAHANGA WA MAFURIKO HANANG


 Na. Stanley Brayton

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amekabidhi chanjo ya ugonjwa wa kimeta kwa waathirika wa mafuriko ya Hanang yaliyotokea mwishoni mwa mwaka uliopita mkoani Manyara zilizokabidhiwa kwa niaba yake na Mkurugenzi Msaidizi Uendelezaji wa Maeneo ya Malisho, Bw. Gabriel Bura Januari 04, 2023.

Bw. Bura amekabidhi chanjo hizo kwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga ambaye ameishukuru Wizara kwa kuwapatia msaada wa chanjo hiyo itakayokuwa msaada kwa Mifugo iliyoathiriwa na maporomoko ya tope yaliyotokea mkoani humo.

"Tumeleta Chanjo ya Ugonjwa wa Kimeta (Anthrax), Dozi 20,000 kwa ajili ya Mifugo ya wakazi wa Hanang waliopatwa na janga la maporomoko ya matope kama Mheshimiwa Waziri Ulega alivyohaidi na kama sote tunavyofahamu kupitia wadau mbalimbali, Wizara imeshatoa misaada ya ng'ombe, mayai, maziwa na fedha taslimu hivyo kinachofuata sasa katika kurejesha hali kwa waathirika, ni kuhakikisha ile Mifugo iliyonusurika inakuwa salama na haitopata madhara" Alisema Bura.

Akizungumza mara baada ya kupokea chanjo hizo, Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga ameishukuru Wizara kwa msaada huo ambapo ametoa maelekezo kwa wahusika kuzielekeza kwenye maeneo yaliyoathirika.

"Ninaishukuru sana  Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa sababu hii sio mara ya kwanza mnakuja kutoa misaada hapa Hanang tangu janga hili litokee hivyo ninaagiza idara husika itafute maeneo ambayo mifugo imeathirika ili kuzuia ugonjwa huu wa Kimeta usienee" alisema Mhe. Sendiga

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Bi. Rose Kamili, ameishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa niaba ya wananchi wa Hanang na kuahidi kuzielekeza chanjo hizo kwenye maeneo yote yaliyoathirika.

"Tunawaahidi kusimamia, chanjo hizo katika vijiji vyetu vyote, ambavyo vinahitaji uchanjaji wa Mifugo ili kuweza kuzuia magonjwa kuliko kusubiri kutibu" Alisema Bi. Rose

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Bw. Francis Namaumbo amesema kuwa mbali na chanjo hizo kuisaidia mifugo iliyoathiriwa na mafuriko zitawasaidia kulinda afya ya walaji ambao wangeathirika kutokana na matumizi ya nyama inayotokana na mifugo yenye ugonjwa huo.

Na vilevile, anaishukuru Wizara kwa kuleta pikipiki 10, kwa ajili ya maafisa ugani ili kuweza kutoa huduma.

Naye mkazi wa Kata ya Ganana, ambae pia ni mfugaji, Bw. Fabiano Sule mbali na kuishukuru Serikali kwa msaada huo, ameiomba kuendelea kuwapatia chanjo za magonjwa ya ngozi kwa ng'ombe yaliyotokana na mifugo hiyo kunywa maji au kula udongo karibu na maeneo yalioathiriwa.

 

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga (katikati), akipokea msaada wa chanjo ya ugonjwa wa kimeta (Anthrax) kwa ajili ya kuchanja Mifugo, kutoka kwa mwakilishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi Uendelezaji wa Maeneo ya Malisho, Bw. Gabriel Bura, misaada hiyo imekabidhiwa katika Ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Mkoani Manyara, Januari 04, 2024.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga (katikati), akishukuru baada ya kupokea msaada wa chanjo ya ugonjwa wa kimeta (Anthrax) kwa ajili ya kuchanja Mifugo, kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Januari 04, 2024.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni