Nav bar

Jumanne, 3 Oktoba 2023

WADAU WAHIMIZWA KUWEKEZA KWENYE SEKTA YA MIFUGO NA UVUVI WILAYANI PANGANI

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti amewasihi wadau kuwekeza kupitia Sekta za Mifugo na Uvuvi wilayani pangani ili kuongeza uzalishaji na tija.

 

Naibu Waziri Mnyeti ameyasema hay oleo (03.10.2023) wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Wilaya ya Pangani Mkoani Tanga ambapo aliwaeleza washiriki kuwa zipo fursa nyingi kupitia sekta za mifugo na uvuvi.

 

Wadau wamehimizwa kutumia fursa zilizopo katika ufugaji wa mifugo na samaki kwa kuhakikisha wanaongeza uzalishaji na uongezaji wa thamani wa mazao ya mifugo na uvuvi ili kuongeza ajira, kipato na mchango wa sekta hizo kwenye pato la taifa.

 

“Niwaombe wadau kuja kuwekeza hapa pangani kupitia sekta hizi za mifugo na uvuvi kwa kuwa fursa zipo kuanzia kwenye kuongeza uzalishaji na uongezaji wa thamani wa mazao ya mifugo na uvuvi, hivyo kupitia kongamano hili ni vema tukazitumia fursa hizi kwa ajili ya kuleta maendeleo yetu, ya wanapangani na taifa kwa ujumla,’ alisema

 

Naibu Waziri Mnyeti pia amewasihi wafugaji kufuga mifugo iliyobora ambayo inakuwa na thamani kubwa badala ya kuwa na ng’ombe wengi ambao tija yake ni ndogo na hivyo kusababisha migogoro ya ardhi. Amewashauri wafugaji kuanza kubadilisha mifugo yao kwa kutumia njia ya uhimilishaji pamoja na kupunguza ng’ombe wengi ambao tija yake ni ndogo na kununua ng’ombe ambao ni wakubwa na wanauwezo wa kutoa maziwa mengi.

 

Aidha, amewasihi wadau kutumia fursa ya uwepo wa bandari wilayani Pangani kwa shughuli za uvuvi kwa kuzingatia sheria kwani bila hivyo serikali itaendelea kuchukua hatua kwa wale wanaokiuka. Naibu Waziri Mnyeti amesema kwa sasa serikali imejipanga kuwashughulikia wauzaji wa nyavu zisizokidhi vigezo kwa kuwa wao ndio wanaowauzia wavuvi.

 

Naye Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kihale amesema serikali imeweka mazingira wezeshi ya kuhakikisha wadau hawakwamishwi pale wanapokuwa na lengo la kuwekeza hapa nchini. Hivyo amewasihi wadau kupitia kongamano hilo kwenda kuwekeza wilayani pangani kwa kuwa fursa zilizopo ni nyingi kupitia sekta mbalimbali.

 

Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Mhe. Zainab Issa amesema wilaya imejipanga kupokea wawekezaji na kwamba suala la umeme upo katika vijiji vyote, mradi wa maji unaendelea kukamilishwa kwenye maeneo ambayo yanachangamoto na kwa upande wa barabara mkandarasi anaendelea na kazi. Hivyo wawekezaji walio na nia wamekaribishwa kuwekeza wilayani Pangani. Lakini pia ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuangalia uwezekano wa kujenga bandari ya mifugo wilayani humo ili mifugo na mazao yake yawe yanasafirishwa kupitia bandari hiyo.

 

Kongamano hilo ambalo lilikuwa na lengo la kutangaza fursa mbalimbali zilizopo wilayani pangani liliwashirikisha wadau kutoka sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na wizara za kisekta na taasisi ambapo wawakilishi walipata fursa ya kuelezea nini taasisi zao zinafanya ili kuweka mazingira sahihi ya biashara na uwekezaji.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Myeti (Mb) akizungumza wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji wilayani Pangani mkoa wa Tanga lililofanyika kwenye ukumbi wa YMCA. Mhe. Mnyeti amewasihi wafugaji kufuga Mifugo michache yenye tija na kuhakikisha shughuli za Uvuvi zinafanyika kwa kuzingatia Sheria ikiwa ni pamoja na matumizi ya nyavu sahihi. (03.10.2023)


Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kigahe (Mb) akiwahutubia washiriki wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji wilayani Pangani Mkoa wa Tanga ambapo amewahakikishia kuwa serikali inaendelea kuweka mazingira sahihi kwa ajili ya biashara na uwekezaji hivyo amewasihi wadau kutumia fursa za uwekezaji zilizopo wilayani Pangani. (03.10.2023)


Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Mhe. Zainab Issa akitoa salam za wilaya wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji lililofanyika katika ukumbi wa YMCA ambapo ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuangalia uwezekano wa kujenga bandari ya Mifugo katika wilaya hiyo. (03.10.2023)


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Myeti (Mb) akifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji wilayani Pangani mkoa wa Tanga lililofanyika kwenye ukumbi wa YMCA. Kushoto kwake ni Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kigahe na kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Mhe. Zainab Issa. (03.10.2023)


Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Uvuvi Tanzania, Bw. Dennis Simba akielezea mikakati iliyopo ya ufufuaji wa shirika hilo wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji wilayani Pangani mkoa wa Tanga lililofanyika kwenye ukumbi wa YMCA. Aliyekaa ni Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Mhe. Zainab Issa. (03.10.2023)


Mtaalam wa Ukuzaji Viumbe Maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Omary Masomaso (wa kwanza kulia) akitoa maelezo mafupi kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya Uvuvi wilayani Pangani wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji wilayani Pangani mkoa wa Tanga lililofanyika kwenye ukumbi wa YMCA. (03.10.2023)


Baadhi ya wadau na wananchi wa Pangani wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa wakati wa Kongamano la Biashara na Uwekezaji wilayani Pangani mkoa wa Tanga lililofanyika kwenye ukumbi wa YMCA. (03.10.2023)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni