Nav bar

Ijumaa, 25 Novemba 2022

WAZIRI NDAKI AWATAKA WAFUGAJI KUTUNZA MIFUGO YAO

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb), amewataka wafugaji wa Halmashauri ya Msalala kutunza Mifugo yao na kuangalia Afya ya Mifugo, ili kuweza kuboresha kosaafu za mifugo hususani Ng'ombe wa Nyama.


Waziri Ndaki ameyasema hayo (19.11.2022) akiwa kwenye ziara ya kikazi Jimbo la Msalala Wilaya ya Kahama alipokuwa akikabidhi madume ya Ng'ombe 50 kwa vikundi vya wafugaji 36, vilivyopo Halmashauri ya Jimbo hilo, kwa lengo la kuwasaidia wafugaji kuboresha mifugo yao.


Mhe. Ndaki amesema wafugaji wahakikishe wanawapeleka Mifugo yao kwenye majosho kwa kuogesha na kuwapatia tiba maana Ng'ombe ni mifugo ambayo inahitaji uangalizi wa hali ya juu.


" Niwasisitize kutunza mifugo hii ambayo leo tumewapatia, kufuga ni gharama, hakikisheni mnawapeleka kwenye majosho kwa kuogesha mifugo yetu na tuwapatie tiba," amesema Ndaki.


Ameongezea kwa kusema Wizara ya mifugo na Uvuvi ina nia ya kuendelea kuona mifugo inakuwa kwenye afya na bora zaidi na inataka wafugaji kutoka taratibu kwenye ufugaji wa zamani kwa maana ya kutaka kuona kunakuwa na ufugaji bora na wenye tija Nchini. 


Aidha, Waziri Ndaki amemshukuru Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi kiasi cha Shilingi milioni  915 kwa haya madume ya Ng'ombe ili kuweza kuboresha mifugo na kufuga kwa tija.


"Kwahiyo nilitaka tuu kuwafahamisha wafugaji wenzangu kwamba Serikali ipo pamoja na ninyi", Amesema Ndaki.


Pia, amesema serikali imetoa dawa za kuogesha Mifugo kwa kuwa mifugo inahitaji kuogeshwa ili isipatwe na kupe na kuwasababishia magonjwa, hivyo na kumtaka Afisa mifugo wa Halmashauri hiyo kusaidia kufatilia na kutoa elimu kwa wafugaji jinsi ya kutunza mifugo yao.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) akisalimiana na Viongozi wa Mkoa na Halmashauri ya Msalala mara baada ya kufika kwenye eneo la kukabidhi madume ya Ng'ombe 50 kwa vikundi vya wafugaji, Lengo ikiwa ni kuboresha kosaafu ya Mifugo hususani Ng'ombe wa Nyama, makabidhiano hayo yamefanyika katika  Kata ya Isaka Halmashauri ya Msalala Wilayani Kahama, Mkoa wa Shinyanga, Novemba 19, 2022.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (Mb) (aliyeshika fimbo) akiswaga madume ya  Ng'ombe ikiwa ni ishara ya kukabidhi madume hayo kwenye vikundi vya  wafugaji, Lengo ikiwa ni kuboresha kosaafu za Mifugo hususani Ng'ombe wa Nyama, makabidhiano hayo yamefanyika katika kata ya Isaka, Halmashauri ya Msalala Wilaya Kahama, Mkoa wa Shinyanga, 19, Novemba 2022.


Sehemu ya Madume ya Ng'ombe 50 ambayo yamekabidhiwa kwa vikundi vya wafugaji kutoka kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki, Lengo ikiwa ni kuboresha kosaafu za Mifugo hususani Ng'ombe wa Nyama, makabidhiano hayo yamefanyika katika kata ya Isaka  Halmashauri ya Msalala, Mkoa wa Shinyanga, 19 Novemba 2022.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) akiongea na wafugaji wakati wa Hafla fupi ya kuweka jiwe la Msingi kwenye ujenzi wa mnada wa awali wa Burige, uliopo Halmshauri ya Msalala, Mkoa wa Shinyanga, 19, Novemba 2022.


Mbunge wa Jimbo la Msalala Mhe. Iddi Kassimu Iddi (aliyesimama) akitoa changamoto ya Lambo na majosho ya Mifugo ya jimbo lake mbele Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki, (Mb), kwenye hafla fupi ya kuweka jiwe la msingi kwenye mnada wa awali wa Burige, Halmashauri ya Msalala, Mkoa wa Shinyanga, 19 Novemba 2022.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) (watatu kushoto) akishirikiana na Viongozi wa Mkoa na  Halmashauri kuweka jiwe la Msingi kwenye ujenzi wa mnada wa awali wa Burige, Halmashauri ya Msalala, Mkoa wa Shinyanga, 19, Novemba 2022.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni