Nav bar

Ijumaa, 25 Novemba 2022

​DKT. MUSSA AELEZA FAIDA ZA UNYWAJI MAZIWA

Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro, Dkt. Mussa Ali Mussa amesema kuwa maziwa ni muhimu kwa lishe ya mwanadamu kuanzia anapozaliwa.

 

Dkt. Mussa ameyasema hayo (18.11.2022) wakati akifunga kikao kazi cha kuandaa mpango wa unywaji wa maziwa shuleni kwa niaba ya Katibu Mkuu Mifugo kilichofanyika kwenye ukumbi wa hotel ya Edema Manispaa ya Morogoro ambapo alisema kuwa matumizi ya maziwa yamekuwa yakihimizwa kwa watoto hadi watu wazima kutokana na umuhimu wake katika lishe.

 

“Maziwa yakitolewa kwa watoto yatawasaidia kukua kimwili na kiakili na hivyo kusaidia kujenga taifa bora lenye watu wanaojitambua,” Alisema

 

Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Sekta ya Mifugo inakuja na mpango wa unywaji maziwa sheleni kwa watoto ili kuhakikisha watoto wanakunywa maziwa ambayo yatawasaidi katika lishe ikiwa ni pamoja na kukabiliana na njaa wawapo sheleni kwa kuwa sio shule zote zinazotoa chakula na hivyo kuwafanya watoto kuwa wasikivu wanapokuwa wanafundishwa.

 

Aidha, Dkt. Mussa ameishauri Wizara kwenye utekelezaji wa mpango huo wa unjwaji maziwa sheleni kuhakikisha wanawashirikisha viongozi mbalimbali kwenye jamii husika ili na wao waweze kusaidia kuelimisha, kuhamasisha na kusimamia kuhakikisha watoto wanapata maziwa kulingana na mpango utakavyokuwa umeelekeza.

 

Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe, Dkt. Nyamizi Bundala amesema kuwa kupitia kikao hicho wameweza kupokea ushauri na ambao utasaidia kuuboresha mpango wa ugawaji maziwa shuleni na kuufanya kuwa endelevu kwa lengo la kuboresha afya za watoto.

 

Pia amesema kuwa Wizara imepanga kununua mitamba na kuipeleka katika mashamba ya serikali ili kurahisisha upatikanaji wa mitamba bora hapa nchini bila kutegemea kuagiza kutoka nje. Vilevile Wizara imepanga kujenga vituo vya kukusanyia maziwa ambavyo vitasaidia sana katika kusimamia ubora wa maziwa yanayotolewa.

 

Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini, Dkt. George Msalya amesema kuwa mpango huu wa unjwaji maziwa shuleni utasaidia kuongeza soko la maziwa hapa nchini na kuwafanya wafugaji kuongeza uzalishaji. Vilevile amewashukuru wadau wote walioshiriki na kutoa maoni ya kuboresha mpango huo ambapo amewaomba watoe ushirikiano hata wakati wa utekelezaji wa mpango huo.


Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro, Dkt. Mussa Ali Mussa (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi na Wataalam kutoka Sekta za Umma mara baada ya kufunga kikao kazi cha kuandaa mpango wa unywaji maziwa shuleni kilichofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Edema Manispaa ya Morogoro. (18.11.2022)


Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro, Dr. Mussa Ali Mussa akifunga kikao kazi cha kuandaa Mpango wa Unywaji Maziwa Shuleni kwa niaba ya Katibu Mkuu Mifugo kilichofanyika kwenye ukumbi wa hotel ya Edema Manispaa ya Morogoro ambapo ameshauri mpango huo uwe shirikishi kwa viongozi na makundi mbalimbali katika jamii ili wasaidie kuhamasisha unywaji maziwa. (18.11.2022)


Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe, Dkt. Nyamizi Bundala akielezea kazi iliyofanyika katika kikao kazi hicho kilichowahusisha wadau mbalimbali wa maziwa ambapo wadau hao walipata fursa ya kutoa maoni yatakayosaidia mpango huo kutekelezeka ili kuboresha afya za Watoto kwa kuwa na lishe bora. Kikao kazi hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa hotel ya Edema Manispaa ya Morogoro. (18.11.2022)


Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini, Dkt. George Msalya akiwashukuru washiriki wa kikao kazi cha kuandaa mpango wa unywaji wa maziwa shuleni ambapo amewasihi kuendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali ili kuhamasisha unywaji maziwa hapa nchini. (18.11.2022)


Washiriki wa kikao kazi cha kuandaa Mpango wa Unywaji Maziwa Shuleni wakisikiliza hotuba Katibu Mkuu Mifugo ya kufunga kikao kazi hicho iliyosomwa na Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro, Dkt. Mussa Ali Mussa. Kikao kazi hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa hotel ya Edema Manispaa ya Morogoro. (18.11.2022)


Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro, Dkt. Mussa Ali Mussa (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi na Wataalam kutoka kwa Wadau wa Maendeleo mara baada ya kufunga kikao kazi cha kuandaa mpango wa unywaji maziwa shuleni kilichofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Edema Manispaa ya Morogoro. (18.11.2022)


Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro, Dkt. Mussa Ali Mussa (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi na Wataalam wa Kampuni zinazosindika maziwa mara baada ya kufunga kikao kazi cha kuandaa mpango wa unywaji maziwa shuleni kilichofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Edema Manispaa ya Morogoro. (18.11.2022)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni