Nav bar

Jumanne, 24 Mei 2022

WADAU WA KUKU WATAKIWA KUPUNGUZA GHARAMA ZA UZALISHAJI, MLAJI KUNUFAIKA

Na. Edward Kondela


Wadau wa tasnia ya kuku nchini wametakiwa kutafakari namna ya kupunguza gharama za uzalishaji ili mnufaika wa mwisho ambaye ni mlaji aweze kununua kuku kwa bei nafuu na kufikia lengo la kila mtanzania kula nyama Kilogramu 50 kwa mwaka, kulingana na mwongozo wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO).


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amebainisha hayo (14.05.2022) katika viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam, wakati wa tamasha la Kuku Choma ambapo amefafanua kuwa wazalishaji wa chakula cha kuku wanatakiwa kutafakari namna ya kupunguza bei za vyakula vya kuku hali kadhalika wazalishaji wa vifaranga vya kuku kupunguza bei za vifaranga ili watu wengi wajitokeze kufuga kuku na kufanya bidhaa hiyo upatikanaji wake uwe wa wingi na bei nafuu.


Waziri Ndaki amesema endapo bei za vyakula vya kuku na vifaranga zitazidi kupanda, mnufaika wa mwisho hataweza kumudu kununua kuku ambapo amesema kwa sasa ulaji wa nyama hapa nchini kwa kila mtanzania ni takriban Kilogramu 15 kwa mwaka kulingana na utafiti uliofanywa na FAO.


“Wadau wote wa nyama kwa ujumla wake tujitahidi kwenda pamoja na walaji wanavyotaka, suala la bei, lakini suala la ubora na masuala mengine ambayo yanavutia wateja wetu ili kuweza kuinua tasnia hii ya nyama kwenye nchi yetu.” Amesema Mhe. Ndaki


Aidha Waziri Ndaki akizungumza katika tamasha hilo la Kuku Choma amewataka wadau wa tasnia ya kuku, kuangalia namna ya kuzidi kuwaongezea thamani kuku wa asili na kuzalishwa kwa wingi ili soko lake lizidi kuwa imara zaidi kama soko la kuku wa kisasa.


Kwa upande wake Msajili wa Bodi ya Nyama nchini (TMB) Dkt. Daniel Mushi akizungumzia juu ya tamasha hilo ambalo bodi yake imeliratibu, amesema lengo lake ni kuihamasisha jamii kuhusu ulaji wa nyama ambapo kwa kuanzia wameanza na kuhamasisha ulaji wa nyama ya kuku kwa sababu mfugo huo ni rahisi kufuga na kwamba hauhitaji eneo kubwa na pia ni njia mojawapo ya kumuondolea mwananchi katika umasikini.


Pia amesema lengo lingine la tamasha la Kuku Choma ni kuwakutanisha wadau wa tasnia ya kuku ili kubadilishana mawazo na kuulizana maswali ili kuboresha ufugaji wa kuku na kuiongezea thamani tasnia hiyo na hatimaye tasnia ya nyama iweze kukua.


Nao baadhi ya wadau wa tasnia ya kuku walioshiriki katika tamasha la Kuku Choma lililofanyika kwenye viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam wamesema wameridhishwa na tamasha hilo na kuomba matamasha ya namna hiyo yawe yanafanyika mara kwa mara kote nchini ili kuwakutanisha pamoja wazalishaji wa vyakula vya kuku na vifaranga vya kuku, pamoja na wafugaji na watumiaji wa mazao ya kuku ili kuiboresha zaidi tasnia ya kuku.


Wameongeza kuwa tasnia ya nyama nchini inatakiwa kuboreshwa zaidi hususan gharama za uzalishaji kupunguzwa ili wananchi wengi zaidi waweze kula nyama mara kwa mara pamoja na kuiomba serikali kusimamia sheria ili kuondokana na wazalishaji holela wa vifaranga vya kuku ambavyo vimekuwa vikiwasababishia wafugaji hasara kwa magonjwa na kufa.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiwa ameshika moja ya kuku wa asili waliofikishwa na mdau wa tasnia ya kuku katika tamasha la Kuku Choma kwenye viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam, ambapo Waziri Ndaki amewataka wadau wa kuku kuhakikisha wanaongeza uzalishaji wa kuku wa asili ili kukuza soko la kuku hao. (14.05.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili kwenye banda la Bodi ya Nyama nchini (TMB), katika viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya kushuhudia tamasha la Kuku Choma lililoratibiwa na bodi hiyo ili kuhamasisha ulaji wa nyama nchini na kukutanisha wadau mbalimbali wa tasnia ya kuku. (14.05.2022)


Msajili wa Bodi ya Nyama nchini (TMB) Dkt. Daniel Mushi (wa kwanza kushoto) akitoa maelezo kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (kushoto kwake), juu ya utendaji kazi wa bodi, mara baada ya Waziri Ndaki kufika katika banda la bodi hiyo iliyoratibu tamasha la Kuku Choma katika viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam. (14.05.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akikagua mashine ya kunyonyolea manyoya ya mifugo jamii ya ndege (kuku, bata nk), wakati akitembelea wadau wa tasnia ya kuku waliojitokeza kwenye tamasha la Kuku Choma katika viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam. (14.05.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akimsikiliza mmoja wa wadau wa tasnia ya kuku aliyeshiriki tamasha la Kuku Choma kwenye viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam, ambaye amemwarifu Mhe. Waziri Ndaki kuwa amekuwa akiongeza thamani ya biashara ya kuku kwa kufuga na kuwavuna kuku hao na kuwaandaa kwa ajili ya mlo kwenye matukio mbalimbali. Kulia kwa Mhe. Waziri Ndaki ni Msajili wa Bodi ya Nyama nchini (TMB) Dkt. Daniel Mushi ambao wameratibu tamasha hilo. (14.05.2022)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (aliyekaa katikati), akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa Bodi ya Nyama nchini (TMB), walioshiriki kwenye tamasha la Kuku Choma katika viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam, wakiongozwa na Msajili wa bodi hiyo Dkt. Daniel Mushi (kulia kwake) na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TMB Bw. Clemence Tesha (kushoto kwake). (14.05.2022)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni