Nav bar

Jumatano, 14 Aprili 2021

MPANGO WA UNYWAJI MAZIWA KWA WATUMISHI WA UMMA WAZINDULIWA

Na Mbaraka Kambona,

 

Serikali imezindua mpango wa unywaji maziwa kwa Watumishi wa Umma kwa lengo la kuhamasisha unywaji wa maziwa yanayozalishwa ndani ya nchi lakini pia kuongeza kipato cha wafugaji.

 

Akizindua mpango huo jijini Dodoma Aprili 13, 2021, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki alisema kuwa utekelezwaji wa mpango huo utasaidia kutatua changamoto ya soko la maziwa na kuleta tija kwa wafugaji.

 

Waziri Ndaki alisema kuwa lita za maziwa zinazozalishwa na wafugaji nchini ni bilioni 3 lakini maziwa yanayochakatwa kwa mwaka ni milioni 74.3 na hivyo kufanya maziwa mengi kupotea kwa kukosa soko la uhakika jambo ambalo sio zuri kwa mustakabali wa tasnia ya maziwa.

 

" Leo tunazindua awamu ya kwanza ya unywaji wa maziwa kwenye Ofisi za Serikali na kwa awamu hii ya kwanza tumeanza na wizara kumi (10), lakini  kutakuwa na awamu nyingine ya uzinduzi zitakazohusisha  wizara, taasisi na mashirika ya umma,” alisema Ndaki

 

Alisema kuwa uzinduzi huo unakwenda sambamba na ugawaji wa majokofu ya kutunzia maziwa kwa wizara hizo huku akitumia nafasi hiyo kuwaomba Viongozi katika Wizara, Watumishi na Wananchi kwa ujumla kuunga mkono mpango huo.

 

Aliongeza kuwa unywaji wa maziwa katika ofisi za umma utainua kwa kiwango kikubwa soko la maziwa yanayozalishwa nchini na kuepuka unywaji wa maziwa kutoka nje ya nchi, na hivyo kukuza pato la wafugaji pia itachochea upatikanaji wa ajira.

 

Ndaki alisema itakua ni jambo la ajabu kuona Ofisi ya Serikali inaagiza maziwa yanayotengenezwa kutoka nje wakati Serikali imezindua mpango mahususi unaohamasisha unywaji wa maziwa yanayozalishwa nchini.

 

Kwa upande wake Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini, Dkt. George Msalya alisema ana imani kuwa kama ofisi zote za Serikali ambapo watumishi wa umma wanafika takribani Laki Tano zitaunga mkono unywaji huo wa maziwa itakua ni fursa nzuri na pana ya kukuza soko la maziwa ya ndani.

 

Wizara  ambazo zimehusishwa katika awamu hiyo ya kwanza ya uzinduzi  wa unywaji wa maziwa unaoratibiwa na Bodi ya Maziwa  ni pamoja na  Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Viwanda na Biashara, TAMISEMI, Wizara ya Mambo ya Ndani na Wizara ya Elimu.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa mmoja wa Wawakilishi wa Kampuni ya kuchakata maziwa ya ASAS kuhusu bidhaa mbalimbali wanazozalisha muda mfupi kabla ya uzinduzi wa  mpango wa unywaji maziwa kwa Watumishi wa Umma uliofanyika jijini Dodoma Aprili 13, 2021.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (wa tatu kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wawakilishi wa Makampuni ya kuchakata Maziwa yaliyoungana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Bodi ya Maziwa kuzindua mpango wa unywaji maziwa kwa Watumishi wa Umma jijini Dodoma Aprili 13, 2021. Baadhi ya Makampuni hayo yaliyoshirikiana na Wizara ni pamoja na ASAS, Milkcom, na Kilimanjaro Fresh.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na  Msajili wa Bodi ya Maziwa, Dkt. George Msalya (wa kwanza kushoto) na Watumishi wengine wa Bodi hiyo muda mfupi baada ya uzinduzi wa mpango wa unywaji wa maziwa kwa Watumishi wa Umma uliofanyika jijini Dodoma Aprili 13, 2021.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (kulia) akimkabidhi Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Bedan Masuruli (kushoto) Jokofu lenye maziwa ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa mpango wa unywaji wa maziwa kwa Watumishi wa Umma uliofanyika jijini Dodoma Aprili 13, 2021.

Msajili wa Bodi ya Maziwa, Dkt. George Msalya (kulia) akitoa maelezo mafupi kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba ndaki (wa kwanza kushoto) kuhusu Mpango wa Unywaji wa Maziwa kwa Watumishi wa Umma muda mfupi kabla kuuzindua  jijini Dodoma Aprili 13, 2021.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (katikati) akinywa maziwa kuashiria uzinduzi wa mpango wa unywaji maziwa kwa Watumishi wa Umma uliofanyika jijini Dodoma Aprili 13, 2021. Kulia ni Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Bedan Masuruli na kushoto ni Kaimu Mkurugenzi, Idara ya Uzalishaji na Masoko, Abdallah Temba.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni