Nav bar

Alhamisi, 8 Oktoba 2020

MAAFISA UGANI WA SINGIDA NA DODOMA WAPATIWA MAFUNZO REJEA KUHUSU UFUGAJI WENYE TIJA.

Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetoa mafunzo rejea kwa maafisa ugani kutoka mikoa ya Singida na Dodoma ili kuwawezesha wagani hao kwenda kutoa elimu kwa wafugaji.

 

Akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani, Dkt. Angello Mwilawa amesema wizara imekua ikitekeleza mikakati muhimu katika sekta ya mifugo ili kuweza kumsaidia mfugaji kufuga kisasa na kibiashara.

 

Mikakati hiyo ni pamoja na Uboreshaji wa Koosafu za mifugo nchini, Udhibiti wa magonjwa, Upatikanaji wa uhakika wa malisho na maji katika maeneo yaliyo na mifugo, Kuboresha uzalishaji ulio wa kibiashara na ustawishaji wa ndege wafugwao, Kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa migogoro ya ardhi, Kuhamasisha na kuanzisha vyama vya ushirika vya wafugaji na Kudhibiti upotevu wa mapato yatokanayo na mifugo pamoja na mazao yake.

 

Dkt. Mwilawa amesema katika kutekeleza mikakati hiyo wizara imekua ikipata changamoto nyingi ambazo ni ukosefu wa maarifa kwa wafugaji na ndio maana wizara imeamua kutoa mafunzo rejea kwa maafisa ugani ili waweze kwenda kuwaelimisha wafugaji walioko katika mikoa yao.

 

Katika kutekeleza mikakati hiyo maafisa ugani wametakiwa kwenda kushirikiana na sekta na wadau wengine waliopo katika maeneo yao ili kuhakikisha wafugaji wanapata elimu hii na kuweza kufuga kwa tija.

 

Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo na  Mshauri wa mifugo kutoka sekretarieti ya mkoa wa Singida, Dkt. David Mluma  ameishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kutoa mafunzo  rejea kwa kuwapatia ujuzi katika sekta ya mifugo.

 

Dkt. Mluma amesema mafunzo haya yamekuja muda mzuri kwani serikali kwa sasa inaendelea kuhamasisha wafugaji kuboresha koosafu za mifugo ili wafugaji waweze kuzalisha kwa tija. Lakini pia wamekumbushwa suala la udhibiti wa magonjwa ambalo usimamizi wake unasaidia mazao ya mifugo kuuzwa ndani na nje ya nchi.

 

Afisa Mifugo kutoka Halmashauri ya Kondoa Mji, Semeni Mwakasege amesema mafunzo haya yamemsaidia kutambua sheria mbalimbali ambazo hapo awali hakudhani kama zinawahusu, hivyo ameahidi kwenda kuwaelimisha wataalamu wenzake pamoja na viongozi wa halmashauri ili wote kwa pamoja waweze kuzisimamia.

 

Pia ametoa wito kwa washiriki wenzake kuhakikisha kila mmoja anakwenda kutoa elimu waliyoipata kwa wataalam wenzao na wafugaji. Vilevile ameiomba wizara ya Mifugo na Uvuvi na Ofisi ya Rais – TAMISEMI kuongeza wigo wa mafunzo haya ili wataalam wengi wa mifugo waweze kupata mafunzo haya ambayo yatasaidia kusambaza elimu hii kwa wafugaji wengi zaidi.

 

Mafunzo haya yametolewa kwa maafisa ugani 20 kutoka mikoa ya Singida na Dodoma na yamefanyika katika ukumbi wa chuo cha Mipango jijini Dodoma. Katika mafunzo hayo washiriki wameweza kupitishwa katika mada za Sheria Kanuni na Miongozo ya sekta ya mifugo, Udhibiti wa Magonjwa na matumizi ya dawa na viwatilifu, Sumukuvu, Madhara na namna ya kudhibiti, Mashamba darasa ya malisho na ustawishaji wa matunzo ya nyanda za malisho pamoja na uboreshaji wa koosafu za mifugo kwa ufugaji endelevu na tija.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni