Nav bar

Alhamisi, 13 Agosti 2020

WAZIRI LUKUVI ATAKA MAONESHO YA NANENANE KUTUMIKA KUONGEZA UZALISHAJI WENYE TIJA.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. William Lukuvi amewataka wadau wa Maonesho ya Nanenane kubadilishana teknolojia mbalimbali hususani za kilimo, ufugaji na uvuvi.

Waziri Lukuvi ameyasema hayo wakati akifungua maonesho ya 28 ya Kilimo – Nanenane 2020 katika viwanja vya John Mwakangale mkoani Mbeya.

Maonesho haya hutoa fursa kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na wadau wengine kukutana pamoja na kuweza kubadilishana uzoefu, kupeana elimu, kuona technolojia mbalimbali ambazo zinasaidia katika uzalishaji na uongezaji thamani wa mazao ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Pia amesema kwa upande wa maendeleo ya sekta ya Kilimo, serikali inaendelea na adhma yake ya upimaji wa afya ya udongo ili kuhakikisha kunakuwepo na kilimo chenye tija katika kanda husika kwa wakulima kulima mazao sahihi kulingana na kanda zao hii ni pamoja na kilimo cha malisho ya Mifugo na vyakula vya samaki.

Vilevile amezitaka kampuni na wadau wanaozalisha mbegu na kutengeneza teknolojia, kuhakikisha wanazifikisha kwa wakulima, wafugaji na uvuvi ili waweze kuzitumia na kuweza kuongeza tija katika shughuli zao. Hii ni pamoja na usambazaji wa taarifa za kiutafiti ambazo zimekamilika.

Aidha, Waziri Lukuvi amezitaka halmashauri zote nchini kuhakikisha wanafanya vizuri zaidi katika Halmashauri zao kwa kuboresha uzalishaji wa wakulima, wafugaji na wavuvi kabla ya kuja kwenye maonyesho hayo.

"Haina maana mkurugenzi wa Halmashauri yangu ninayotoka Iringa ukaja kuotesha mimea kwenye viwanja vya nanenane kabeji kubwa sana, lakini hakuna kijiji hata kimoja Iringa ambacho wananchi wake umewafundisha na wanalima kabeji hizo, hivyo huu unakuwa ni mchezo wa kuigiza" alisema Waziri Lukuvi

Aidha, akizungumzia kauli mbiu ya Maonesho ya Nanenane mwaka huu inayosema "Kwa Maendelo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Chagua Viongozi Bora 2020" amewataka wananchi kuwa makini kuelekea uchaguzi mkuu kwa kuhakikisha wanashiriki kuanzia wakati wa kampeni mpaka kwenye uchaguzi utakaofanyika October, 2020.

Naye Mkuu wa mkoa Albarty Chalamira aliongezea na kutoa changamoto mbalimbali unaokumba mkoa wa Mbeya ikiwa ni pamoja na ukosefu wa usafiri wa ndege na kupelekea kushindwa kusafirisha mazao yatokanayo na sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi katika maeneo mengine.

 

Mgeni Rasmi Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi William Lukuvi (aliyevaa suti nyeusi) akiwangalia vijana wa kikundi cha SUMA JKT wakitumbuiza kwa kuimba kwaya katika ufunguzi wa maadhimisho ya maonyesho ya nanenane kwenye viwanja vya John Mwakangale mkoani Mbeya  tarehe 01/08/2020. 




Mkuu wa mkoa wa Mbeya, Albarty Chalamira akitoa neno la shukrani kwa Mgeni Rasmi katika ufunguzi wa maadhimisho ya maonyesho ya nanenane Mbeya kwenye viwanja vya John Mwakangale  tarehe 01/08/2020. 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni