Nav bar

Jumatano, 15 Julai 2020

WADAU WAFANYA TATHMINI YA HALI YA TASNIA YA NGOZI


Wadau wa Mfuko wa maendeleo ya Mifugo (LDF) wakutana kujadili hatma ya tasnia ya ngozi hasa baada ya kuisha kwa ugonjwa wa Corona.

Kikao hicho kimefanyika jana katika ofisi ndogo za Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilizopo jengo la NBC jijini Dodoma ambapo wadau hao kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda na Biashara, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Taasisi ya Teknolojia Dar-es-salaama tawi la Mwanza na wengine walishiriki.

Akifungua kikao kazi hicho, Mkurugenzi wa Masoko na Uzalishaji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Felix Nandonde alibainisha kuwa tasnia ya ngozi iliathiriwa na janga la Corona lililosababisha hivi sasa ngozi inayozalishwa hapa nchini kutouzwa tena nje ya nchi hata ikiwa katika nusu hatua ya usindikaji.

“Lakini katika kikao hiki mbali na kujadili matumizi ya fedha pia kitumike kujadili mbinu za kuikwamua tasnia hii ya ngozi kutoka kwenye hali iliyopo kwa sababu mpaka hivi sasa nchi yetu inaagiza zaidi ya pea milioni 52 huku uwezo wetu wa kuzalisha viatu ukiwa ni milioni 1.2 tu kwa mwaka” Alisisitiza Dkt. Nandonde.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar-es-salaam (DIT) Tawi la Mwanza Dkt. Albert Mmari alisema kuwa taasisi yake ilishaanza kuchukua hatua kadhaa za kuongeza thamani kwenye tasnia ya ngozi ikiwemo kuongeza mashine za mafunzo ya kutengenezea viatu ambapo mpaka sasa zipo 50 ukilinganisha na 25 zilizokuwepo hapo awali.

Dkt. Mmari amesema kuwa DIT kupitia benki ya dunia imepata zaidi ya shilingi bilioni 37 ambazo zitatumika kwenye mradi wa miaka mitano ya kuboresha miundombinu ya chuo ikiwemo kununua mashine za kisasa za kufundishia, studio za kubuni mitindo mipya ya viatu na bidhaa nyingine zitokanazo na ngozi, kujenga madarasa ambapo mara baada ya kukamilika kwa madarasa hayo yatakuwa na uwezo wa kubeba wanafunzi zaidi ya 1000.

Akielezea hatua zilizochukuliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika kuhakikisha inaongeza thamani ya ngozi, Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa chakula na lishe Bw. Gabriel Bura alisema kuwa mpaka sasa Wizara imeshatoa mafunzo kwa zaidi ya wachunaji 735 katika mikoa ya Kilimanjaro, Manyara, Arusha, Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Morogoro na Kagera na tayari mchakato wa kutoa leseni kwenye mikoa hiyo umeshaanza.

Vilevile wizara imeanza kugawa visu vinavyotakiwa kitaalam kwa ajili ya kazi ya uchunaji katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara na mchakato wa kuhakikisha vinafika katika kanda zote tulizotoa mafunzo unaendelea.

Bw. Bura alisema kuwa hatua iliyopo hivi sasa ni kusubiri tu nyaraka za uteuzi wa wakaguzi wa Ngozi waliopatikana kutoka kwenye Halmashauri 113 ambao tayari wameshapitishwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kusainiwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Baada ya taratibu kukamilika wataalam hao watakuwa na jukumu la kuhakikisha wanasimamia ubora wa ngozi kama ulivyoainishwa kwenye sheria namba 18 ya masuala ya Ngozi.

Katika kikao hicho pia wadau walifanya tathmini ya utekelezaji wa mpango kazi wa mwaka wa fedha 2019/2020 na kujadili changamoto zilizosababisha kutotekelezwa baadhi ya vipengele vya mpango kazi huo.



Mkurugenzi wa Masoko na Uzalishaji Dkt. Felix Nandonde akifungua kikao cha wadau wa Mfuko wa Maendeleo ya Mifugo (LDF) kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilizopo katika jengo la NBC, Dodoma. Lengo la kikao hicho ni kujadili hatma ya tasnia ya ngozi nchini. (14.07.2020)



Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe, Bw. Gabriel Bura akizungumzia namna Wizara ilivyotekeleza shughuli mbalimbali kwa lengo la kuinua tasnia ya ngozi nchini katika kikao kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilizopo katika jengo la NBC, Dodoma. (14.07.2020)


Mkurugenzi wa taasisi ya Teknolojia Dar-es-salaam (DIT) tawi la Mwanza, Dkt. Albert Mmari akielezea namna taasisi yake ilivyotekeleza mpango wa kuinua tasnia ya ngozi nchini wakati wa kikao cha wadau wa Mfuko wa Maendeleo ya Mifugo (LDF) kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilizopo katika jengo la NBC, Dodoma. (14.07.2020)

Sehemu wa wadau wa Mfuko wa Maendeleo ya Mifugo (LDF) wakifuatilia mjadala wa hatma ya tasnia ya ngozi nchini wakati wa kikao kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilizopo katika jengo la NBC, Dodoma. (14.07.2020)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni