Nav bar

Alhamisi, 17 Novemba 2022

WAZIRI NDAKI AWATAKA WAFUGAJI KUISHI NA WATUMIAJI WENGINE WA ARDHI KWA AMANI


 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amewataka wafugaji kuishi na watumiajiwengine wa ardhi kwa amani na sio kuleta migogoro.

 

Waziri Ndaki ameyasema hayo (02.11.2022) wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Ngunichile wilayani Nachingwea mkoani Lindi alipofika na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwa lengo la kuwasikiliza wananchi wa Kijiji hicho ambapo kuna mgogoro wa wakulima na wafugaji.

 


“Shughuli za ufugaji ni shughuli halali kama zilivyoshughuli nyingine katika jamii, lakini shughuli hizi ni lazima zifanyike kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ili ziweze kufanyika bila kuleta migogoro,” Alisema

 

Waziri Ndaki amesema vitendo vya baadhi ya wafugaji kulisha mifugo kwenye mashamba ya wakulima, kuwapiga na kuwaua ni vya kihalifu hivyo watatafutwa kama wahalifu wengine na hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.

 

Wafugaji wametakiwa kuishi kwa amani, kuwa na ushirikiano na mahusiano mazuri katika jamii wanazoishi na kuacha tabia ya kuleta vurugu au migogoro kwenye jamii hizo.

 

Naye Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mhandisi Hamad Masauni amesema kutokana na tatizo la migogoro waliloliona kwenye mkoa wa Lindi kuhusu migogoro ya wakulima na wafugaji amemuagiza Kamishna wa Operesheni na Mafunzo Tanzania kuendesha operesheni ya kuwatafuta wafugaji waliosababisha migogoro na kuchukua hatua.

 

Pia amewataka wafugaji kuzingatia mipango ya matumizi ya ardhi iliyowekwa na kuhakikisha wanafuga mifugo kwenye maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya kazi hiyo, hivyo wafugaji ambao wamevamia maeneo bila kufuata taratibu wametakiwa kutoka kwenye maeneo hayo.

 

Kamishna wa Operesheni na Mafunzo Tanzania, CP. Awadhi Juma amesema Jeshi la Polisi limezipokea changamoto zote za kiusalama zilizotolewa na wananchi, hivyo jeshi litakwenda kuendesha operesheni kali kuhakikisha amani na utulivu unarejea na wananchi kuwa huru katika kutekeleza shughuli zao za kiuchumi bila usumbufu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni