Nav bar

Ijumaa, 22 Oktoba 2021

WAVUVI WATAKIWA KUWA WALINZI WA MAZINGIRA YA BAHARI KUKABILIANA NA ASIDI

Wavuvi na watumiaji wengine wa baharini wametakiwa kuwa walinzi wa mazingira ili kukabiliana na uchafuzi wa hewa ya ukaa inayoikabili dunia kutokana na kuwepo kwa asidi nyingi baharini.

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Dkt. Ishmael Kimirei, amesema hayo (15.10.2021) wakati wa uzinduzi wa mitambo itakatayotumika kupata taarifa ya hali ya hewa katika Bahari ya Hindi kwenye mwambao wa Tanzania.

“Ripoti zinaonesha Bahari ya Hindi inaongezeka joto kwa kasi zaidi kuliko bahari zote duniani na joto limeongezeka kwa asilimia 0.88, na hii ni ripoti ya mwaka jana. Tukiondoa mifumo ya ikolojia inayosababisha dunia iwe baridi itasababisha kesho kuwa ngumu zaidi,” amefafanua Dkt. Kimirei.

Kwa upande wake Afisa Utafiti wa TAFIRI, Dkt. Baraka Sekadende alisema mbali na mradi huo wa kuangalia asidi baharini, TAFIRI imeanza kupima ongezeko la vurutubisho maji ili kuwa na samaki wenye afya ambapo kutaongeza tija kwenye mazao ya samaki na kunufaisha wavuvi

Aidha, Mwenyekiti wa Kikundi cha Ulinzi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) katika Mwalo wa Kunduchi jijini Dar es Salaam, Bw. Zedi Mwinyi Zedi aliipongeza serikali kwa mradi huo na kuahidi kuwa wataulinda maana una manufaa zaidi kwenye shughuli zao za uvuvi, hasa kupata taarifa za uvuvi wanapokuwa baharini.

Dunia inakabiliwa na uchafuzi wa mazingira kutokana na hewa ya ukaa kunakopelekea mataifa mbalimbali kutafuta njia za kukabiliana na hali hiyo ikiwepo kupanda miti na usafi wa mazingira kwa ujumla.

Mtambo huo uliofungwa na TAFIRI unathamani ya zaidi ya Shilingi Milioni 25 za kitanzania na utakuwa unakusanya taarifa kwa njia ya kidigitali kila siku na kuziwasilisha katika kituo kikuu cha utafiti TAFIRI kwa kutumia program maalum.




Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Dkt. Ishmael Kimirei (Kulia) akifunga mitambo maalum kwa ajili ya kukusanyia taarifa ya mabadiliko ya mazingira katika Bahari ya Hindi katika mwambao wa bahari hiyo jijini Dar es Salaam. (15.10.2021) 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni