Nav bar

Ijumaa, 2 Oktoba 2020

WADAU WA TAFICO WATAKIWA KUTOKA NA MAPENDEKEZO YA AINA YA VIFAA VYA MELI YA UVUVI.

 Wadau wa TAFICO wametakiwa kujadili na kutoka na mapendekezo ya aina ya vifaa vya uvuvi hususani vitakavyotumika katika ujenzi wa meli ya uvuvi itakayomilikiwa na shirika hilo kwa niaba ya serikali.

 

Hayo yamesemwa na Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Bw. Emmanuel Bulayi leo tarehe 01/10/2020 wakati akifungua kikao cha wadau hao kilichowahusisha washiriki kutoka kampuni za uvuvi, TDB, THA, DMI, FETA, TAFIRI, TASAC, Menejimenti ya TAFICO, Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu na wawakilishi wa Idara ya Uvuvi.

 

Bw. Bulayi amesema serikali ilishatiliana saini na serikali ya Japan mkataba wa kuanza utekelezaji wa Programu ya Uchumi na Maendeleo ya Jamii utakaosaidia ununuaji wa vifaa vya uvuvi ikiwa ni pamoja na meli moja ya uvuvi.

 

“Kwa kuwa taratibu za awali zilishakamilika ambapo tayari mkandarasi kwa ajili ya kununua vifaa hivyo ameshapatikana CROWN AGENT kutoka Japan, kinachosubiriwa ni sisi kutoka na mapendekezo ya aina ya vifaa vya uvuvi tunavyotaka vinunuliwe na mkandarasi huyo,” alisema Bw. Bulayi.

 

“Serikali katika suala hili imeona ni vema wadau wakashirikishwa ili na wao waweze kutoa ushauri wao kutokana na uzoefu walionao ili vifaa hivyo vitakapoagizwa viweze kukidhi mahitaji kama ilivyokusudiwa hivyo ni muhimu majadiliano haya yatakapokamilika, orodha ya vifaa hivyo iweze kujulikana,” aliongeza Bw. Bulayi.

 

Naye Kaimu Meneja Mkuu TAFICO, Bi. Esther J. Mulyila amesema lengo la kikao hicho ni kujadili aina ya vifaa vya uvuvi vitakavyonunuliwa kwa ajili ya meli ya uvuvi, majokofu kwa ajili ya kuhifadhia samaki na mtambo wa kuzalishia barafu.

 

Bi. Mulyila amesema TAFICO kwa sasa itatekeleza majukumu yake pamoja na miradi 10 yenye thamani ya bilioni 89.8 itakayokuwa inatekelezwa kwa awamu, ambayo itashirikisha wadau.

 

Miradi hii imegawanyika katika maeneo matatu, kwanza ni miradi ya uvuvi kwa kutumia meli za aina 3 za uvuvi (kwa ajili ya uvuvi wa maeneo matatu ya bahari), mradi wa mtambo wa kuzalisha barafu, mradi wa majokofu ya kuhifadhia samaki, mradi wa viwanda vya uchakataji samaki, miradi ya ukuzaji viumbe maji (uzalishaji wa vifaranga vya samaki, uzalishaji wa vyakula vya samaki, ufugaji wa samaki kwenye vizimba na ufugaji wa samaki kwenye mabwawa).

 

Serikali inaendelea na mchakato wa ufufuaji wa shirika lake la TAFICO ambapo imepata msaada kutoka serikali ya Japan wa Yen Milioni 200 takriban shilingi za kitanzania Bilioni 4.2 kupitia Programu ya Uchumi na Maendeleo ya Jamii.

 

Miongoni mwa vifaa vitakavyonunuliwa kupitia programu hiyo ni pamoja na meli moja ya uvuvi, majokofu ya kuhifadhia samaki, na mtambo wa kuzalisha barafu. Serikali ya Japan itanunua, itasafirisha, itasimika mitambo katika eneo la Ras Mkwavi na kufundisha juu ya matumizi ya mitambo hiyo.

Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Bulayi akifungua kikao (kwa niaba ya Katibu Mkuu Uvuvi) cha kujadili vigezo mbalimbali vitakavyowezesha kupatikana mapendekezo ya aina ya vifaa vya uvuvi vya TAFICO vitakavyonunuliwa kupitia ufadhili wa serikali ya Japan. Kulia kwake ni Kaimu Meneja Mkuu TAFICO, Bi. Esther J. Mulyila na kushoto kwake ni Mhadhiri Mwandamizi – UDSM, Bw. Paul Onyango akifuatiwa na Meneja Mkuu Mstaafu TAFICO, Bw. Francis R. Nkoka. (01.10.2020)

Kaimu Meneja Mkuu TAFICO, Bi. Esther Mulyila (aliyesimama) akizungumza jambo wakati wa kikao cha kujadili vigezo mbalimbali vitakavyowezesha kupatikana mapendekezo ya aina ya vifaa vya uvuvi vya TAFICO vitakavyonunuliwa kupitia ufadhili wa Japan. Kushoto kwake ni Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Bulayi akifuatiwa na Mhadhiri Mwandamizi – UDSM, Bw. Paul Onyango. (01.10.2020)

Wadau wakisikiliza mada katika kikao cha kujadili vigezo mbalimbali vitakavyowezesha kupatikana mapendekezo ya aina ya vifaa vya uvuvi vya TAFICO vitakavyonunuliwa kupitia ufadhili wa Japan. (01.10.2020)

Picha ya pamoja ya Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi, Bw. Emmanuel Bulayi na washiriki wa kikao cha kujadili vigezo mbalimbali vitakavyowezesha kupatikana mapendekezo ya aina ya vifaa vya uvuvi vya TAFICO vitakavyonunuliwa kupitia ufadhili wa Japan. (01.10.2020)





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni