Nav bar

Jumatano, 9 Oktoba 2024

DKT. MPANGO AZIPONGEZA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI KWA UTEKELEZAJI MZURI WA SHUGHULI ZAKE

Na. Stanley Brayton

Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango, amezipongeza Sekta za Mifugo na Uvuvi kwa utekelezaji mzuri wa shughuli zake ambazo zimelenga kukuza shughuli za ufugaji na uvuvi kwa kuendana na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika kuhudumia wananchi na kuwapa maisha Bora.

Akizungumza, Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango leo Oktoba 8, 2024 katika Ziara yake wilayani Igunga, Mkoani Tabora, Dkt. Mpango amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi inafanya vizuri katika kuhakikisha mifugo bora inapatikana kwa wananchi kwa kutoa pembejeo bora kwa wafugaji na wavuvi, vilevile kutoa mikopo kwa wafugaji na wavuvi pamoja na kuwapatia mbegu bora za vifaranga vya samaki pamoja na madume Bora ya ng'ombe.

Kwa Upande wake, Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti amesema Serikali kupitia Wizara ya Mifugo imefanya mambo mengi sana kwa watanzania na ata katika Wilaya ya Igunga ikiwa ni kutoa elimu kwa wafugaji na wavuvi.

“tuna fursa ya ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba, na ya utengenezaji wa mabwawa ya kufugia samaki pamoja na kutoa madume Bora ya ng'ombe kama mbegu”, amesema Mhe. Mnyeti

Aidha, Mhe. Mnyeti amesema, Madume Bora ya ng'ombe yalishagawiwa katika baadhi ya wilaya, ikiwemo Wilaya ya Bahi, Serengeti na Bunda.

Vilevile, Mhe. Mnyeti amesema mpango huo ni endelevu hapa nchini, na Wizara inampango wa kusambaza madume hayo Bora ya ng'ombe katika wilaya zote nchini Tanzania ila yaweze kupanda ng'ombe wa kienyeji na kupata ng'ombe wengine walio Bora.


Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango, akimuuliza swali Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti (hayupo pichani), ni lini Wizara italeta Madume Bora ya ng'ombe Wilayani Igunga, ni katika Ziara yake ya kikazi Mkoani Tabora, Oktoba 8, 2024, Igunga - Tabora


Naibu Waziri Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti, akijibu swali la Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpangoni (hayupo pichani), kuwa Wizara italeta Madume Bora ya ng'ombe 20 Wilayani Igunga baada ya wiki tatu, ni katika Ziara ya kikazi Mkoani Tabora, Oktoba 8, 2024, Igunga - Tabora


Picha ni wananchi wakimsikiliza Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango, katika Ziara yake ya kikazi Mkoani Tabora ya Oktoba 8, 2024, Igunga - Tabora


Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango, akizungumza na wananchi wa kijiji cha Bukene kuhusu umuhimu wa kuzingatia lishe Bora kwa watoto na mama wajawazito ili waweze pata Protini ya kutosha itakayowasaidia kukuza ufikiri wa mtoto na kusisitiza Maafisa kutoa elimu kuhusu lishe Bora ili jamii zielewe nini maana ya lishe bora na umuhimu wake, ni katika Ziara yake ya kikazi Mkoani Tabora, Oktoba 8, 2024, Nzega - Tabora


Naibu Waziri Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti, akisalimia wanakijiji wa Bukene na kutoa Salamu za Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ni katika Ziara ya kikazi Mkoani Tabora ya Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango, Oktoba 8, 2024, Nzega - Tabora



 Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango (aliyeshika bomba la maji), akifungua maji kama Ishara ya Uzinduzi  na Upanuzi wa Mradi wa Maji kutoka ziwa Viktoria kwenda Bukene, ni katika Ziara yake ya kikazi Mkoani Tabora, Oktoba 8, 2024, Nzega - Tabora, Wa tatu kulia ni Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti


Picha ni Washiriki mbalimbali wakiwemo wakazi wa Bukene na Maafisa mbalimbali na Viongozi wa Serikali wakiwa katika Ziara ya kikazi Mkoani Tabora ya Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdor Mpango, Oktoba 8, 2024, Nzega - Tabora





Jumanne, 1 Oktoba 2024

DKT. MHINA AIPA HEKO MRADI WA AgResults KWA UTEKELEZAJI MZURI

Na. Stanley Brayton

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Dkt. Charles Mhina amepongeza utekelezaji wa Mradi wa Utatuzi wa Changamoto za Uzalishaji wa Maziwa (AgResults Tanzania Dairy Productivity Challenge) kwa utekelezaji mzuri wa kukuza Sekta ya Mifugo, ususani katika kuboresha mahusiano mazuri kati ya wafugaji na maafisa wa malisho pamoja na maafisa Mifugo, na kutoa pembejeo kwa wafugaji na utoaji wa huduma za Ugani ili kukuza Sekta hii ya Mifugo. 

Akizungumza, katika Kikao cha kufunga Mradi wa Utatuzi wa Changamoto za Uzalishaji wa Maziwa,  kilichofanyika katika Ofisi za Wizara ya Mifugo na Uvuvi - Mtumba, Octoba 01, 2024, mkoani Dodoma, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Dkt. Mhina amesema anawapongeza maafisa wa Mradi wa AgResults kwani wametumia namna mbalimbali ili kuweza kuwafikia wafugaji wadogo na kuweza kuwapatia huduma mbalimbali za ugani, ikiwa ni pamoja na kutoa pembejeo za Mifugo.

“mradi huu umefika mpaka kwa wafugaji mbaimbali maeneo ya vijijini kiasi kwamba umetoa huduma kwa wafugaji na mifugo yako kwa kuboresha malisho pamoja utoaji chanjo”, amesema Dkt. Mhina

Aidha, Dkt. Mhina amesema ni wajibu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuhakikisha huduma zinawafikia wafugaji hadi vijijini, ikiwa ni pamoja na utoaji chanjo za mifugo na tiba kwa mifugo pamoja na pembejeo ili kuweza kuwapa huduma mbalimbali zitakazosaidia kuboresha mifugo na maisha ya wafugaji.

Vilevile, Dkt. Mhina amesema Wizara iangalie ni namna gani inaweza kuwafikia wafugaji Tanzania nzima ili kuhamasisha na kutoa mbegu Bora za madume ya ng'ombe kwa wafugaji na kuhakikisha matibabu ya mifugo yanapatikana kwa wakati.

Dkt. Mhina ametoa rai kwa maafisa wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuendelea kushirikiana na Sekta binafsi katika kuboresha huduma za mifugo, na kuhakikisha maziwa salama yanapatikana kwani asilimia kubwa ya watanzania hawanywi maziwa salama, na hii inatokana na maziwa mengi kuuzwa kienyeji, na mashirikiano hayo yatasaidia katika kuboresha usindikaji na utunzaji maziwa kwa njia ya usalama zaidi kiasi cha kutanua masoko nchini hadi nchi za nje.


Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambaye ni Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Dkt. Charles Mhina na ndiye Mgeni Rasmi, akitoa Hotuba fupi, katika Kikao cha kufunga Mradi wa Utatuzi wa Changamoto za Uzalishaji wa Maziwa, uliyofanyika katika Ofisi za Wizara ya Mifugo na Uvuvi - Mtumba, Octoba 01, 2024, Dodoma


Msimamizi wa Mradi wa Utatuzi wa Changamoto za Uzalishaji wa Maziwa (AgResults Tanzania Dairy Productivity Challenge Project), Bi. Neema Mrema, akitoa Ripoti ya Utekelezaji wa Mradi wa AgResults, ni katika Kikao cha kufunga Mradi wa Utatuzi wa Changamoto za Uzalishaji wa Maziwa, uliyofanyika katika Ofisi za Wizara ya Mifugo na Uvuvi - Mtumba, Octoba 01, 2024, Dodoma


Mkurugenzi wa Uzalishaji na Maendeleo ya Masoko Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Stephen Michael, akitoa neno la Ukaribisho kwa washiriki, ni katika Kikao cha kufunga Mradi wa Utatuzi wa Changamoto za Uzalishaji wa Maziwa, uliyofanyika katika Ofisi za Wizara ya Mifugo na Uvuvi - Mtumba, Octoba 01, 2024, Dodoma






Jumatatu, 30 Septemba 2024

WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI YATOA ELIMU YA KICHAA CHA MBWA KWA WANANCHI

Na.  Martha Mbena

Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetaoa elimu kwa wananchi juu ya kichaa cha Mbwa Wilayani Misungwi Mkoani Mwanza ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya kichaa cha mbwa duniani ambayo yanatarajiwa kufanyika Septemba 28.2024.

Akiongea na wakazi wa kitongoji cha Ng'walo gwa magole kata ya Bulemeji Wilayani hapo Leo (27.09.2024) Mkurugenzi Msaidizi wa afya ya jamii ya Veterinari kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Stanford Ndibalema amewataka wananchi kuzingatia chanjo ya kichaa cha Mbwa ili kuepusha madhara yanayoweza kutokea.

"Huu ugonjwa unaweza kuzuilika iwapo tutaamua kuwachanja Mbwa wetu, hivyo kila mmoja wetu anaemiliki Mbwa anapaswa kumlinda Mbwa huyo dhidi ya ugonjwa huu", Amesema Dkt. Ndibalema.

Aidha, Dkt. Ndibalema amesisitiza umuhimu wa kuwaona wataalam wa Mifugo kwa ajili ya chanjo badala ya kusubiri chanjo ya bure inayotolewa na Serikali 

Baadhi ya wazazi na wanafunzi waliofikiwa Na elimu ya kichaa cha Mmbwa wanasema  elimu  imewasaidia kutambua dalili za Mbwa mwenye kichaa na matibabu ya mtu aliyeng'atwa na Mbwa.

Elimu hiyo imetolewa katika maeneo mbali mbali ya Wilaya ya Misungwi zikiwemo Shule za msingi na sekondari pamoja na wataalam kutoka sekta ya Mifugo.








SERIKALI KUFANYA UTARATIBU WA KUWEZESHA UPATIKANAJI WA CHANJO ZA KICHAA CHA MBWA ZA KUTOSHA NCHINI

Na. Martha Mbena

Serikali kwa kushirikiana na mashirika ya Kimataifa tayari imeanza kufanya utaratibu wa kuwezesha upatikanaji wa chanjo za kutosha ili Mbwa na paka wengi wapate Chanjo dhidi ya kichaa Cha Mbwa.

Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia sekta ya Mifugo  Ndug. Abdul Mhinte alipokuwa anafunga kilele Cha maadhimisho ya siku ya Kichaa Cha Mbwa Duniani yaliyofanyika Kitaifa Katika Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza Septemba 28.2024.

Mhinte amesema katika jitihada za kutokomeza ugonjwa huo Serikali inaratibu upatikanaji wa chanjo za kutosha kwa ajili ya kuchanja Mbwa na paka ambapo kwa kuchanja zaidi ya idadi ya 70% ya Mbwa na Paka kwa miaka mitano mfululizo tunaweza kutokomeza kabisa ugonjwa huo Nchini.

"Pamoja na hatari kubwa ya ugonjwa huu, ni kwamba unaweza kuzuilika kwa asilimia mia Moja na tunaweza kutokomeza iwapo tutaweza kuwachanja Mbwa na Paka wetu na kuwatunza vizuri", amesema Mhinte. 

 Aidha, Septemba 28 kila mwaka ni siku ya kichaa cha Mbwa duniani ambapo kutokana na takwimu za Wizara ya Afya Tanzania, watu 1,500 hufariki kwa ugonjwa wa kichaa cha Mbwa kila mwaka huku watu 60,000 hufariki kila mwaka kwa ugonjwa huo duniani. 

Pia Mhinte amesema lengo la siku hiyo ni kuongeza ufahamu kwa wananchi juu ya ugonjwa huo na kujua namna ya kujikinga.

"Tunajua Mbwa na Paka ni wanyama muhimu katika maisha yetu lakini wanyama hawa kama hawatatunzwa vizuri pamoja na kuwakinga dhidi ya magonjwa wanageuka kuwa hatari kwa mwanadamu",amesema Mhinte.

 Pia, amesema mwanadamu anaweza kupata ugonjwa huo kwa kung'atwa na Mbwa au Paka na kwa njia ya mate ya mnyama alieathirika na ugonjwa huo na kuweza kuambukizwa kwa mwanadamu.

Mh. Naibu katibu Mkuu amesema lengo la umoja wa mataifa ni kuhakikisha ugonjwa unatokomezwa duniani kote ifikapo 2030 kwa kutumia kauli mbiu ya "Breaking Rabies Boundaries" kama hamasa ya kutokomeza kabisa ugonjwa wa kichaa cha mbwa duniani.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Mhe. Johari Samizi ameishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuchagua kufanya maadhimisho hayo Wilayani hapo.

Mhe. Samizi amesema ni jukumu la kila mmiliki wa Mbwa kumtunza Mbwa wake kwa kumpatia chakula, dawa na Chanjo zote na kumpenda Mbwa huyo ili kuhakikisha Mbwa  wahazuruli mitaani.

Kauli mbiu ya kutokomeza kichaa cha mbwa inakuja na jitihada za kuondoa vikwazo vya kuwezesha mbinu za kutokomeza ugonjwa huo zikiwemo matumizi ya teknologia katika kutokomeza ugonjwa, kuongeza uelewa kwa wananchi kupitia kampeni mbalimbali na kuunganisha wadau.





Ijumaa, 27 Septemba 2024

MNYETI AGAWA MADUME BORA YA NG’OMBE 40 KWA WAFUGAJI SERENGETI NA BUNDA

Na. Stanley Brayton

Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti amekabidhi madume bora 20 ya ng’ombe wa nyama kwa vikundi vya wafugaji wa kijiji cha Nyichoka Wilayani Serengeti na madume Bora 20 kwa vikundi vya wafugaji wa kijiji cha Mariwanda Wilayani Bunda, ili iwasaidie kuzalisha kizazi chenye uwezo wa kutoa nyama nyingi zaidi ya wale wa asili waliopo hapa nchini. 

Akikabidhi, madume hayo Bora ya Ng'ombe kwa vikundi vya wafugaji katika hafla fupi zilizofanyika leo Septemba 27, 2024 Wilayani Serengeti na Bunda mkoani Mara, Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mnyeti amesema kuanzia mwaka wa fedha 2022/2023 Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikitekeleza mpango wake wa kuleta mabadiliko katika Sekta ya Mifugo, ambapo mpango huo umegusa nyanja mbalimbali za uzalishaji wa mifugo ili kuhakikisha ukuaji wa uhakika wa uzalishaji wa mifugo na mazao yake ili kukidhi ongezeko la soko la ndani na nje ya nchi.

“mpango huu unahusisha kuboresha mbari za mifugo, upatikanaji wa maji na malisho kwa ajili ya mifugo na kuhakikisha afya ya mifugo kwa kuwapatia wafugaji dawa za kuogeshea na kampeni ya chanjo”, amesema Mhe. Mnyeti

Aidha, Mhe. Mnyeti amesema hatua zingine zinazochukuliwa ni pamoja na kuboresha huduma za ugani kwa kuwapatia maafisa ugani mafunzo rejea na vitendea kazi vikiwemo pikipiki kwa ajili ya usafiri wa kuwafikia wafugaji, kuongeza fedha kwa ajili ya utafiti pamoja na kujenga na kuboresha masoko ya mifugo.

Vilevile, Mhe. Mnyeti amesema asilimia 97 ya ng’ombe walioko hapa nchini ni wale wa asili, ila ng’ombe hawa wa madume Bora ni wavumilivu kwenye masuala ya magonjwa pamoja na uhaba wa malisho na maji, na uzalishaji wake wa nyama ni wa juu ukilinganisha na ng’ombe wengine wa asili, kwani wameboreshwa kwa kuingiza vinasaba vya mbegu yenye uzalishaji mkubwa kwa kuchanganya mbegu za ng’ombe wa asili na wale wenye uzalishaji wa juu kunazalisha ndama mwenye sifa zaidi ya wazazi wake kwani anakuwa na uzalishaji mkubwa kuliko yule wa asili na kwa upande mwingine anakuwa na uwezo wa kuvumilia mazingira magumu kuliko yule mwenye uzalishaji mkubwa asiye wa asili.

Mhe. Mnyeti ameongezea kwa kusema, Wizara imefanya hivyo kwa vikundi kadhaa vya wafugaji kwenye Halmashauri mbalimbali hapa nchini kwa lengo la kutoa hamasa kwa wafugaji ili kubadilika na kufuga kibiashara kwa kuwa na ng’ombe wenye tija.

Kwa Upande wake, Mkurugenzi Msaidizi  Uzalishaji Mifugo, Bw. Simon Lyimo amesema Wizara ya Mifugo imejipanga vyema katika kutatua changamoto mbalimbali za wafugaji pamoja na mifugo.

“tumechukua hatua mbalimbali za kuiboresha mifugo ili wafugaji waweze kupata mifugo bora na kufuga kwa tija”, amesema Bw. Lyimo

Naye, Kiongozi wa wafugaji Kanda ya Nyanza ambayo inajumuisha Mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga, Bw. Kikuri Mnikokostantine ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani, Dkt. Samia Suluhu Hassani kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya Mhe. Abdallah Ulege (Mb), kwa kuwapatia madume Bora ya ng'ombe na kuomba kuongezewa tena kama ikimpendeza Mheshimiwa Rais na Waziri mwenye dhamana.

Naibu Waziri Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti (aliyeshika nyaraka ya Buluu), akikabidhi mdume bora 20 ya ng'ombe kwa wafugaji wa kijiji cha Nyichoka, ni katika Hafla fupi iliyofanyika Septemba 27, 2024, Serengeti - Mara


Picha ni madume Bora 20 ya ng'ombe, yaliokabidhiwa kwa vikundi vya wafugaji wa kijiji cha Nyichoka na Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti, Septemba 27, 2024, Serengeti - Mara


Naibu Waziri Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti, akizungumza na wanavikundi wa ufugaji ng'ombe (hawapo pichani), ni katika Hafla fupi ya kukabidhi Madume Bora 20 ya ng'ombe kwa vikundi vya wafugaji katika kijiji cha Nyichoka, Septemba 27, 2024, Serengeti - Mara






Jumatano, 25 Septemba 2024

PROF. SHEMDOE ASHIRIKI UVUNAJI SAMAKI MRADI WA KISOKO

Na. Stanley Brayton

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe, ameshiriki shughuli za uvunaji wa samaki aina ya Sato katika Vizimba vilivyopo eneo la Kisoko ili kushuhudia  hali ya Samaki hao ikiwemo ukubwa wake na shughuli za uuzaji wa Samaki hao ulivyofanyika katika eneo hilo.

Akizungumza, leo Septemba 25, 2024 mkoani Mwanza alipotembelea eneo hilo la Mradi wa Ukuzaji Samaki kwa njia ya Vizimba, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Shemdoe amesema samaki hawa walikuwa wadogo sana, ila leo hii wanavunwa wakiwa wakubwa kiasi cha kwamba wanafaa kuingia sokoni na kuliwa.

"hii mbegu ya samaki ilikuwa ndogo sana na haishikiki, ila leo hii tunavuna ikiwa kitu ambacho tunakiona hapa kwa mara ya kwanza, na hii yote ni Shukrani kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kutoa fedha ili ziweze kutumiwa na Vijana hawa wa Jenga Kesho Iliyo Bora - BBT katika uzalishaji huu wa bidhaa za uvuvi" amesema Prof. Shemdoe

Aidha, Prof. Shemdoe alisema Tarehe 30 Januari mwaka huu Mhe. Rais alizindua Mradi huu ambao ulikuwa na vizimba 222 na Boti 160 ambazo zimekopeshwa katika maeneo ya ziwa Viktoria na Bahari ya Hindi, na kutokana na mkopo huo, leo hii kinaonekana kilichopatikana ambacho ni uwepo wa Samaki wengi na wakubwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Imani Kapinga, amesema lengo la Mradi huu ilikuwa ni kufikisha gramu 300, ila ni habari njema kuwa kuna samaki wenye gramu 400 hadi 500, kiasi kwamba malengo yamevukwa.

Vilevile Dkt. Kapinga amesema, mvuno wa leo ni wa Kikundi kimoja kati ya vikundi 12 vilivyopo hapa eneo la Kisoko, ila vikundi vingine vitaendelea kuvuna kuanzia mwezi wa kumi na moja hadi wa tatu mwakani. 

Naye, Afisa Maendeleo ya Biashara Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TAD, Bw. Samson Siyengo amesema Mkoa wa Mwanza umenufaika kwa kiasi kikubwa kwani zaidi ya Bilioni 4 zimetolewa kwa Vijana wa Jenga Kesho Iliyo Bora waliopo Mwanza.

Mnufaika wa Vizimba ambaye pia ni Katibu wa Kikundi kilichovuna samaki leo, Kikundi cha Vijana Nguvu Kazi, Bw. Pius Mtenya ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassani kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya  Mheshimiwa Abdallah Ulega kwa kuwapa Mkopo husio na Riba ili waweze kufanya shughuli za ukuzaji viumbe maji ili waweze kujipatia kipato.

Vilevile, Bw. Mtenya Amesema katika uvunaji wa leo wanataraji kupata jumla ya tani 19.8, katika vizimba 6, ikimaanisha kila kizimba kitatoa tani 3.3, na hii inaonyesha ni jinsi gani watakavyopata faida kutokana na Mradi huu.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe (wa kwanza kushoto), akiwa ameshikiria Samaki aina ya Sato waliovunwa kwenye Vizimba, ni mara baada ya kushiriki shughuli za uvunaji Samaki hao, uliyofanyika eneo la Mradi wa Kisoko, Septemba 25, 2024, Mwanza








Alhamisi, 19 Septemba 2024

TANGA YAJIPANGA KUONGEZA UZALISHAJI WA SAMAKI

Na Edward Kondela

Mkoa wa Tanga unajikita kuongeza kiwango cha uzalishaji wa samaki na mazao mengine ya baharini, ili kuzinufaisha jamii zake kupitia shughuli hizo zinazohusiana na Uchumi wa Buluu.

Mkuu wa Mkoa huo, Mhe Balozi Dkt. Batilda Burian, ameyasema hayo (18.09.2024) kwenye mkutano ulioandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwa ajili ya kujadili masuala ya uhifadhi wa bahari kwa vizazi na maendeleo ya sekta hiyo Mkoani Tanga.

Amesema uvuvi ni moja ya sekta muhimu mkoani humo, hususan kwenye wilaya za Tanga, Pangani, Mkinga na Muheza ambapo takwimu zinaonesha kuwepo jumla ya wavuvi 13,336 na vyombo vya uvuvi vilivyosajiliwa 1,922. 

Mhe Balozi Dkt. Burian ametoa mfano kuwa, mwaka 2023/2024 samaki waliouzwa mkoani humo walikuwa na thamani ya Shilingi Bilioni 47.208, zilizowezesha ukusanyaji ushuru uliofikia takriban Shilingi Milioni 951.7 huku wakulima wa mwani wakifikia 5,300.

Ameongeza kuwa uzalishaji wa zao hilo la baharini umefikia tani 3,000 kwa thamani ya takribani Shilingi bilioni 5, kiasi kinachotarajiwa kuongezeka kufikia tani tani 5,000.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia uvuvi, Dkt. Edwin Mhede, amemtaja Mhe Balozi Dkt. Batilda Burian kuwa ni ‘Champion’ wa ulinzi wa rasilimali za bahari na mazao yake, kutokana na jitihada mbalimbali anazozifanya katika sekta hiyo Mkoani Tanga.

Amebainisha kuwa mkuu huyo wa mkoa amekuwa akifanya kampeni mbalimbali za kuhakikisha rasilimali za bahari hususan samaki wanazaliana kwa wingi kwa kupiga marufuku na kusimamia matukio ambayo yanaashiria uvunjifu wa sheria katika Sekta ya Uvuvi.

Aidha, amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi itaendelea kutoa elimu na kuhakikisha wadau wa sekta hiyo wanaendelea kufanya shughuli kwa misingi ya sheria, kanuni na taratibu za nchi lengo likiwa kuhakikisha ukuaji wa pato la taifa kupitia Sekta ya Uvuvi.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Mohamed Sheikh ametoa wito kwa Sekretarieti za Mikoa kusimamia halmashauri kutekeleza sheria, kanuni na miongozo ya uvuvi, kupitia sera, sheria na kanuni za uvuvi, kuandaa miongozo ya usimamizi wa rasilimali za uvuvi na mazingira yake, kupanga na kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya uvuvi.

Amesema endapo hayo yatasimamiwa vyema rasilimali za uvuvi zitakuwa na tija kwa mwananchi mmoja mmoja na taifa kwa ujumla na kuifanya Sekta ya Uvuvi kuwa endelevu na kubadili mtazamo juu ya jamii ya wavuvi na wote wanaojishughulisha na mazao ya uvuvi.

Baadhi ya washiriki wa mkutano huo wametoa maoni yao juu ya kuendeleza rasilimali za uvuvi wakitaka elimu zaidi kutolewa kwa wadau wa uvuvi ya namna ya kutunza rasilimali za uvuvi na mazao ya uvuvi kwa ujumla na kuendelezwa kwa kampeni mbalimbali za kudhibiti uvuvi haramu.


Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede (kulia kwake) na baadhi ya viongozi kutoka katika wizara hiyo na ofisi ya mkuu wa mkoa huo, baada ya Mhe. Balozi Dkt. Burian kutembelewa ofisini kwake na Naibu Katibu Mkuu Dkt. Mhede, kabla ya kushiriki mkutano wakujadili namna ya kukuza rasilimali za uvuvi na kudhibiti uvuvi haramu, kilichohusisha baadhi ya viongozi na wadau wa Sekta ya Uvuvi Mkoa wa Tanga. (18.09.2024)











RASILIMALI ZA BAHARI ZATAJWA KUWA ONGEZEKO PATO LA TAIFA

Na. Edward Kondela

Katibu Tawala Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Toba Nguvila amesema Sekta ya Uvuvi ikisimamiwa vyema kupitia rasilimali za Bahari ya Hindi, sekta hiyo itaweza kuimarisha pato la taifa kupitia kupitia mnyororo wa thamani.

Dkt. Nguvila amesema hayo leo (19.09.2024) jijini Dar es Salaam wakati akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Bw. Albert Chalamila, kwenye ufunguzi wa mkutano uliohusisha kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa pamoja na viongozi wa wilaya za Ilala, Kigamboni, Temeke na Kinondoni zenye maeneo yenye bahari.

Amesema kuwa mnyoyoro huo wa thamani unaohusisha wadau wa Sekta ya Uvuvi wakiwemo wavuvi wenyewe, kwenye masoko na wachakataji wa mazao ya uvuvi utakuwa na tija kwa kuhakikisha ulinzi wa rasilimali za uvuvi unazingatiwa ili kupata fedha nyingi kupitia biashara ya mazao hayo.

“Samaki wanaovuliwa wakiwa wadogo kwenye soko hawaingii hivyo hauwezi kupata hesabu yao kwenye pato la taifa, hii inamaanisha ni uvuvi haramu lakini tukilinda rasimali za uvuvi vyema watavuliwa samaki wanaohitajika na pato la taifa litakuwa kubwa.” Amesema Dkt. Nguvila.

Aidha, ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kufanya tafiti zaidi ili vizimba vya kufugia samaki viweze kutumika pia katika upande wa bahari kuu kwa kuwa yapo maeneo ambayo yanaweza kufaa kwa ajili ya uwekaji wa vizimba.

Amesema ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba kwa bahari kuu utasaidia kuwawezesha wadau wa Sekta ya Uvuvi kupatiwa mikopo na kufuga samaki kwa tija na kutoa fursa ya kupatiwa elimu ya ufugaji huo na kuondokana na dhana ya uvuvi haramu.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayesimamia Sekta ya Uvuvi Dkt Edwin Mhede, amesema wizara imepewa mamlaka ya kuhakikisha kunakuwa na uvuvi endelevu kama moja ya mbinu ya kulinda rasilimali za uvuvi hazipotei na zinavuliwa kwa kufuata sheria, kanuni na miongozo.

Dkt. Mhede amesema mkutano huo unalenga kukumbushana majukumu na umuhimu wa kuongeza ufanisi ili ulinzi wa rasilmali za uvuvi unaotakiwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uweze kutekelezwa na kwamba itaendelea kusimamia hilo.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohamed Sheikh amesema lengo la mikutano ya kukutana na kamati za ulinzi na usalama za mikoa ni kuwa na mikakati mbalimbali ya kuhakikisha rasilimali za uvuvi katika maji yote ya asili zinalindwa ili kuwa na tija katika pato la taifa.

Ameongeza kuwa kumewekwa mikakati mbalimbali ya muda mrefu, mfupi na kati kwa kushirikisha wadau ili kuwa na makubaliano ya pamoja ya namna ya kulinda rasilimali za uvuvi na kuhakikisha rasilimali hizo zinazidi kuzaliana kwa wingi na kuongeza uhitaji katika masoko.

Nao baadhi ya washiriki wamesema mkutano huo umekuja muda muafaka katika kuelimishana na kuwa na mawazo ya pamoja ya kuhakikisha rasilimali za uvuvi zinazidi kulindwa na kuwa na tija kwa taifa.


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede, akielezea mamlaka iliyopewa wizara kuhakikisha kunakuwa na uvuvi endelevu kama moja ya mbinu ya kulinda rasilimali za uvuvi hazipotei na zinavuliwa kwa kufuata sheria, kanuni na miongozo. Dkt. Mhede ameelezea hayo wakati wa mkutano ulioandaliwa na wizara hiyo uliofanyika jijini Dar es Salaam kwa kuhusisha kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa pamoja na viongozi wa wilaya za Ilala, Kigamboni, Temeke na Kinondoni zenye maeneo yenye bahari wenye lengo la kuimarisha rasilimali za uvuvi na kudhibiti uvuvi haramu. (19.09.2024)






Jumatano, 4 Septemba 2024

WATAALAMU KUANDAA MFUMO WA UFUATILIAJI WA TAARIFA ZA MASOKO YA MIFUGO

Wataalamu Wizara ya Mifugo na Uvuvi wamekutana kwa ajili ya kujadili Mifumo inayopendekezwa katika kuanzisha Kitengo cha Ufuatiliaji wa Taarifa za Masoko ya Mifugo na Mazao yake ikiwa ni njia mojawapo ya kuwasaidia wafugaji na wafanyabiashara wa mifugo kujua nini kinatokea katika masoko, pamoja na kuisaidia serikali kufanya maamuzi kuhusiana na masoko ya mifugo.

Akizungumza, leo Septemba 04, 2024, mkoani Morogoro katika kikao cha kujadili Mifumo inayopendekezwa katika kuanzisha Kitengo cha Ufuatiliaji wa Taarifa za Masoko ya Mifugo na Mazao yake, Mkurugenzi Msaidizi Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe, Dkt. Nyamizi Bundala, amesema mafunzo haya yana lengo la kujengeana uwezo kuhusu taarifa za masoko ya mifugo na mazao yake ikiwemo, upatikanaji, uchakataji na uwasilishawaji wa taarifa hizo sambamba na uanzishwaji wa dawati/kitengo mahususi kitakacho shughulikia taarifa za masoko ya mifugo na mazao yake.

"Mafunzo haya yamekuja wakati muafaka na yanaendana na dhamira ya dhati ya Serikali katika kuhakikisha Sekta zetu za uzalishaji, hususani sekta za mifugo na uvuvi, zinachangia ipasavyo katika kuinua kipato cha wananchi katika mnyororo wa thamani, kuchangia katika Pato la Taifa, kuongeza pato la fedha za kigeni, na kuimarisha uhakika na usalama wa chakula na lishe nchini. Aidha, katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, Serikali imefanya uwekezaji mkubwa katika miundombinu masoko na kuweka mazingira wezeshi ambayo yamechangia ongezeko la biashara la mifugo hai na mazao yake " amesema Dkt. BundalaAidha, 

Dkt. Bundala amesema, katika kipindi cha miaka mitatu (2021/22-2023/24), Serikali imejenga minada 51 ya kisasa ya mifugo  yenye thamani ya shilingi bilioni 17.5. Minada hii imewezesha ongezeko la biashara ya mifugo nchini ambapo, thamani ya mifugo iliyouzwa katika minada imeongezeka kutoka shilingi trilioni 1.5 mwaka 2021/22 hadi trilioni 3.4 mwaka 2023/24, na hii imeleta ongezeko la mauzo ya nyama nje ya nchi kutoka tani 1,774 mwaka hadi kufikia tani 14,701 mwaka. Hivyo kufanya jumla ya tani 40,635.48 zenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 164.8 zilizouzwa nje ya nchi katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Dkt. Bundala amesema kuwa, suala la kuweka mifumo ya upatikanaji wa taarifa za masoko si geni, hapa nchini kwani lilianza zamani, katika miaka ya 90, Wizara ya iliyokuwa kuwa ikisimamia mifugo kupitia mradi wa TLMP ilianzisha mfumo wa LINKS (Livestock Information Network and Knowledge System) ambayo ilikuwa ikiratibu taarifa za masoko. 

Vilevile, Dkt. Bundala alisema kwa kuzingatia maendeleo ya teknolojia yaliyopo, mageuzi ya uchumi, kukua kwa masoko ya ndani, kikanda na kimataifa na uwepo wa soko huria la biashara ya bidhaa mbalimbali duniani, upatikanaji wa taarifa za masoko ya hususani ya mifugo na mazao yake kwa wakati ni suala la muhimu, ili kuwawezesha wadau kutambua fursa za masoko na biashara zilizopo, kupenyeza katika masoko mapya, kuongeza wigo wa masoko na kufanya maamuzi sahihi ya kupanga bei, kuuza au kununua bidhaa hizo kulingana na ushahidi wa taarifa.

Naye, Mwakilishi wa Shirika la ASPIRES Tanzania, Bw. Emmanuel Domonko, amesema suala la kuandaa kitengo cha  Ufuatiliaji wa Taarifa za Masoko ya Mifugo ni muhimu sana kwa wafugaji, wafanyabiashara na serikali kwa ujumla kwani kitasaidia kuongeza tija katika ufugaji, na faida kwa wafugaji na wafanyabiashara na mapato kwa taifa. Pamoja na hayo, taarifa za wakati za masoko zitasaidia Wizara kufanya maamuzi sahihi na kwa wakati.

Pia, Bw. Domonko amesema wao kama ASPIRES wapo katika kusaidia kuboresha mifumo ikiwemo pamoja na maboresho ya Sera za kilimo pamoja na mifugo ili kuleta mabadiliko chanya katika Sekta ya Mifugo na Uvuvi.

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uzalishaji na Maendeleo ya Masoko, ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe, Dkt. Nyamizi Bundala, akitoa hotuba kwa washiriki wa kikao cha kujadili Mifumo inayopendekezwa katika kuanzisha Kitengo cha Ufuatiliaji wa Taarifa za Masoko ya Mifugo na Mazao yake, kilichofanyika katika Ukumbi wa Edema, Septemba 04, 2024, Morogoro