Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema Serikali imeendelea na mkakati wa kukuza Soko la maziwa Nchini kwa kuimarisha na kuendeleza programu ya unywaji wa maziwa shuleni.
Mhe. Ndaki aliyasema hayo Mei 10, 2022 wakati akijibu swali la Mbunge wa Busanda Mheshimiwa Bryceson Magessa ambaye alitaka kufahamu mkakati wa Serikali katika kushughulikia Soko la ndani la maziwa kwa kuhimiza na kuhamasisha unywaji wa maziwa shuleni kabla ya kutafuta masoko ya nje.
Alisema mpango wa unywaji maziwa shuleni umeweza kuwafikia watoto 90,000 wa shule za msingi 39 katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Iringa, Mbeya na Tanga.
Aliongeza kuwa Serikali inaendelea kuhamasisha unywaji wa maziwa Nchini kwa kutoa elimu kupitia vyombo vya habari, maonyesho mbalimbali na wiki ya maziwa kitaifa inayoadhimishwa mwezi Mei kila mwaka.
Mhe. Ndaki amesema katika mwaka wa fedha 2022/23 Serikali itakutana na wadau mbalimbali wakiwemo wa tasnia ya maziwa Ili kuandaa mikakati thabiti kwa lengo la kuongeza idadi ya shule zinazotoa huduma ya unywaji maziwa.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni