Nav bar

Jumanne, 17 Agosti 2021

TADB YAOMBWA KUENDELEA KUWASAIDIA WAVUVI NCHINI

Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeiomba Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kuwasaidia wavuvi  katika mambo matatu ikiwemo kuwaondoa wavuvi  kutoka kwenye uvuvi wa  maji ya ndani na kuwapeleka kuvua kwenye maji ya Kitaifa kwa kutumia maboti ya kisasa badala ya mitumbwi na ngalawa.

Ombi hilo lilitolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Rashid Tamatamah alipokuwa akiongea na ujumbe kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania  (TADB) wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Bw. Frank Mugeta,  alisema uvuvi wa samaki katika ukanda wa bahari unaweza kuongezeka iwapo wataweza kuwasaidia wavuvi katika mambo mbalimbali.

Pia, kuwaondoa wavuvi wadogo wadogo kutoka kwenye uvuvi wa  maji ya ndani na kuwapeleka kuvua kwenye maji ya Kitaifa kwa kutumia maboti ya kisasa badala ya mitumbwi na ngalawa ambazo wengi wao bado wanazitumia.

“Sasa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na sekta binafsi imeanza kutekeleza baadhi ya mikakati kuwawezesha wafugaji samaki wadogo kwenye maji ya asili kukabilina na changamoto za uwekezaji mdogo  katika maeneo yao lakini hapo bado tuna changamoto,”alisema.

Alisema mafanikio katika utekelezaji wa mikakati yanategemea  kwa kiasi kikubwa  ushiriki wa Taasisi za kifedha za ndani pamoja na nje.

Alisema Wizara imeanzisha dawati la sekta binafsi ili kuratibu upatikanaji wa mikopo kwa vyama vya ushirika kwa kuyafanyia marekebisho maandiko yao ili yakidhi matakwa ya Kibenki.

“Kufikia Februari 2021, dawati limewezesha  kupokelewa  kwa maombi ya mikopo  ya uvuvi katika Benki ya TADB yenye thamani  ya shilingi bilioni 51.4 lakini kiasi kilichotolewa hadi sasa ni shilingi bilioni 1.2 kwa vyama vya ushirika vitatu  katika Wilaya ya Ukerewe, Buchosa na Chato,”alisema.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Mugeta amesema mara baada ya kikao hicho wataenda kuangalia namna ya kuisaidia sekta hiyo ambayo inaajiri watanzania wengi.

Alisema wataisaidia sekta hiyo kutokana na kufanyika kwa  tafiti nyingi ambazo zitawaongoza wao wasaidie sehemu zipi ili kuhakikisha Mtanzania anaweza kujikwamua kimaisha.

“Niahidi wataalam wetu watakaa,  hili ni eneo la kusapoti kwa nguvu zetu zote nimeteuliwa nina siku 10 bado nina nguvu hivyo tutapata majawabu ya haraka  ili tuone tunaanzia wapi.Tunataka kuhakikisha sekta ya uvuvi inaajiri watu wengi nafikiri ni eneo ambalo tutaliangalia kwa kina zaidi,”alisema.

Awali akitoa wasilisho kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mkurugenzi wa Ukuzaji viumbe maji kutoka Wizara hiyo, Dkt. Nazael Madalla alisema uvuvi ni miongoni mwa sekta zinazoajiri watu wengi wa kipato cha chini ambapo moja kwa moja takribani wavuvi na wakuzaji viumbe maji  wapatao 225,435.

Alisema zaidi ya watanzania milioni 4.5 wameendelea kupata kipato cha kila siku kutokana na shughuli zinazohusiana na sekta ya uvuvi ikiwemo kuunda na kutengeneza boti, kuuza na kushona nyavu kutengeneza na kuuza  barafu, biashara ya samaki na mazao yake.

Mkurugenzi huyo alisema sekta hiyo inachangia katika lishe na usalama wa chakula ambapo takribani asilimia 30 ya protein itokanayo na wanyama inachangiwa na samaki.

Alisema kwa upande wa kipato na fedha za kigeni katika mwaka 2020-2021 tani 483,756.4 zilivunwa na kuingiza kipato cha shilingi trilioni 2.42 kati ya mavuno hayo tani 41,319.00 na samaki hai wa mapambo 165,413 wenye thamani ya shilingi bilioni 18.91.

Mkurugenzi huyo amesema sekta hiyo ni muhimu kwani  inachangia pato la Taifa kwa asilimia 1.7

Alisema kwa sasa kiasi cha rasilimali za samaki  kwenye maji ni zaidi ya tani nne ambapo amedai kiasi kinachoweza kuvunwa  bila kuathiri mazingira ni tani 750,000.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah akieleza lengo la kufanya kikao na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Bw. Frank Mugeta (hayupo pichani) ikiwa ni pamoja na kuomba kuwasaidia wavuvi kupata mikopo Ili kuweza kutatua changamoto zao katika masuala ya Uvuvi  kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma. Agosti 16, 2021.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Bw. Frank Mugeta akielezea namna watakavyoweza kuiendeleza Sekta ya Uvuvi kwa kuwapatia wavuvi mkopo Ili waweze kujiendesha kwenye shughuli zao za Uvuvi  kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma. Agosti 16, 2021.

Mkurugenzi wa Ukuzaji viumbe maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt Nazael Madalla, akiwasilisha mada wakati wa kikao na wajumbe kutoka Benki ya maendeleo ya kilimo Tanzania (TADB) kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma. Agosti 16, 2021.

Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi Dkt. Rashid Tamatama, (waliokaa kulia) akiwa kwenye  picha ya pamoja mara baada ya kukutana na wajumbe kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) lengo likiwa ni  kuwasaidia Wavuvi kukabiliana na changamoto za uwekezaji mdogo katika maeneo yao pamoja kuvipatia vyama vya ushirika vya uvuvi mikopo ili viweze kujiendesha kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma.


 

Ijumaa, 13 Agosti 2021

WAKAGUZI WATAKIWA KISIMAMIA UBORA WA VYAKULA VYA MIFUGO

Serikali imewataka wakaguzi wa maeneo ya malisho na rasilimali za vyakula vya mifugo kuhakikisha mifugo inapatiwa vyakula vyenye ubora na stahiki ili kuondokana na madhara ya sumukuvu yanayoweza kuwaathiri walaji wa nyama, mayai, maziwa na bidhaa nyingine za mazao ya mifugo.

Rai hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bw. Peter Nyakigera wakati akifungua mafunzo ya wakaguzi wa maeneo ya malisho na rasilimali za vyakula vya mifugo yaliyofanyika leo Agosti 12, 2021 katika ukumbi wa siasa ni kilimo Mkoani Iringa.

Nyakigera alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu sana kwa wakaguzi walio kwenye mamlaka za serikali za mitaa kwa vile yatasaidia kutatua changamoto ya ubora na viwango hafifu vya vyakula vya mifugo vinavyotumiwa na wafugaji walio wengi ambapo hata vifo vya baadhi ya mifugo vimesabishwa na kutumia baadhi ya rasilimali za vyakula vyenye sumukuvu.

“Tanzania ni nchi ya pili kwa kuwa na idadi kubwa ya mifugo Afrika ikiwa na ng’ombe milioni 33.4, mbuzi milioni 21.29, kondoo milioni 5.65, kuku milioni 83.28 ambapo kwa mwaka 2019/2020 zilizalishwa hadi lita bilioni 3.01 za maziwa, tani 701,679 za nyama na mayai bilioni 4.05 hivyo uzalisaji wa mazao haya kwa kiasi kikubwa unategemea upatikanaji wa uhakika wa rasilimali za vyakula vya mifugo vyenye ubora na viwango stahiki” alisema Bw. Nyakigera.

Nyakigera alisema kuwa wakaguzi hao wanawajibu mkubwa wa kulinda afya za walaji na mifugo yenyewe kwa kusimamia sheria na kanuni ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya kutosha kwa wadau kwenye mnyororo wa thamani kwenye tasnia ya vyakula vya mifugo.

Aliongeza  kuwa elimu ya ufugaji wenye tija inayoendelea kutolewa imeongeza hamasa kwa wafugaji  hivyo ni  muhimu kupatikana kwa vyakula vyenye ubora na viwango  hususani kwa ng’ombe na kuku.

“Kuwepo kwa vyakula vyenye ubora kutapuguza malalamiko ya ukuaji hafifu uliobainika kwa kuwa wafugaji hutumia takribani asilimia 60 ya gharama zote za uzalishaji kwenye vyakula, hivyo uzalishaji wenye tija hutegemea sana uwepo wa viini lishe vyote muhimu kwenye vyakula hivyo” amemalizia Nyakigera.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Rasilimali za vyakula vya mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Rogers Shengoto alisema mafunzo hayo ni moja ya utekelezaji wa majukumu yaliyopangwa na Idara hiyo lengo likiwa ni kuhakikisha changamoto za ubora wa vyakula vya mifugo vinavyozalishwa na vinavyotumiwa na wafugaji nchini vinakuwa vimezingatia kanuni bora, sheria na taratibu zote ambazo zinatakiwa.

"Tunataka kuhakikisha changamoto za ubora kwa malalamiko ya ukuaji wa wanyama na uzalishaji hafifu unapungua kwa wazalishaji wa Mifugo. Amesema Bw. Shengoto.

Naye Mkaguzi wa maeneo ya malisho na Rasilimali za vyakula vya mifugo kutoka Mkoa wa Babati, Bw. Mayanzi Bubinza ameishukuru Serikali kwa kuendelea kutoa mafunzo kwa wafugaji na wataalam nchini.


Kaimu Mkurugenzi wa Rasilimali za vyakula vya mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Rogers Shengoto (wa pili kutoka kulia) akimueleza machache Kaimu Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya uchumi na uzalishaji Mkoa wa Iringa Bw. Peter Nyakigera (kushoto) kabla ya ufunguzi wa mafunzo kwa wakaguzi wa maeneo ya malisho na Rasilimali za vyakula vya mifugo nje ya ukumbi wa siasa ni kilimo halmashauri ya wilaya ya Iringa Mkoani  Iringa  Agust 12, 2021.

Kaimu Mkurugenzi wa  Rasilimali za vyakula vya mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi , Bw. Rogers Shengoto,  akimkaribisha mgeni rasmi (hayupo pichani) Ili kuweza kufungua mafunzo ya wakaguzi wa maeneo ya malisho na Rasilimali za vyakula vya mifugo kwenye ukumbi wa siasa ni Kilimo halmashauri ya wilaya ya Iringa Mkoani Iringa  Agosti 12, 2021.

Baadhi ya wataalam wakitoa wafunzo kwa wakaguzi wa maeneo ya malisho na Rasilimali za vyakula vya mifugo kwenye ukumbi wa siasa ni kilimo Mkoani Iringa Agosti 12, 2021.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya wakaguzi wa maeneo ya malisho na Rasilimali za vyakula vya mifugo yaliyofanyika  Agosti 12, 2021 kwenye ukumbi wa Siasa ni kilimo Mkoani Iringa.

 


Kaimu Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya uchumi na uzalishaji (wa tatu kutoka kulia), Bw. Peter Nyakigera akiwa kwenye picha ya pamoja na  wataalam wa Mifugo na wakaguzi kutoka ngazi za Wizara na Mikoa mara baada ya ufunguzi wa mafunzo ya wakaguzi wa maeneo ya malisho na Rasilimali za vyakula vya mifugo  kwenye ukumbi wa Siasa ni kilimo  Mkoani Iringa. (12/08/2021.)


Jumamosi, 7 Agosti 2021

TANZANIA KUUZA NYAMA NCHINI SAUDIA ARABIA

 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel amekutana na Ujumbe kutoka nchini Saudi Arabia kwa lengo la kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara ya nyama na nchi hiyo.

Prof. Ole Gabriel alikutana na Ujumbe huo kutoka Saudi Arabia ulioongozwa na Mkaguzi,  Mamlaka ya Dawa na Chakula, Saudi Arabia, Ahmed Alhajouj jijini Dar es Salaam Agosti 7, 2021.

Kwa mujibu wa Prof. Gabriel kabla ya kukutana nao, ujumbe huo ulipata fursa ya kukagua maeneo mbalimbali yanayohusika na uchakataji wa mazao ya mifugo ikiwemo Machinjio, Maabara na Shirika la Viwango Tanzania(TBS) ambapo kote wamejirisha na kutoa mapendekezo kadhaa ya kuboresha ili biashara hiyo iweze kufanyika kwa viwango vinavyohitajika na nchi hiyo. 

Alisema kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ameielekeza Wizara hiyo kutafuta masoko nje ya nchi hivyo Wizara inaendelea kufanya jitihada ikiwemo hatua hiyo ya kutafuta soko katika nchi Saudi Arabia.

"Haya masoko ya nje ya nchi ni mazuri kwa sababu yanatupatia fedha za kigeni lakini pia yanawahakikishia wafugaji wetu soko la uhakika kwa mazao ya mifugo yao," alisema Prof. Ole Gabriel

Aidha, Prof. Gabriel alitoa rai kwa Wafugaji nchini kuchukulia hatua hiyo kama ni fursa kubwa na hivyo wahakikishe wanaboresha ufugaji wao kuwa wa kisasa zaidi ili kukidhi soko hilo la kimataifa.

"Serikali ni rahisi kutafuta masoko lakini je, mifugo iliyopo inakidhi soko hilo? hivyo niwaombe wafugaji na Wafanyabiashara watumie fursa hii vizuri ili kuboresha uchumi wao na wa Taifa pia," aliongeza Prof. Ole Gabriel

Alisema Sekta ya Mifugo kwa sasa inachangia katika pato la Taifa kwa asilimia 7.4 lakini lengo la Wizara ni kufikia asilimia 15 ifikapo mwaka 2025 na hilo linawezekana kama milango ya masoko nje ya nchi  ikianza kufunguka kwa uhakika.

Prof. Ole Gabriel aliongeza kuwa wao kama wizara watatoa ushirikiano kwa kila mdau anayechangia katika mnyororo wa thamani wa mazao ya mifugo kuhakikisha kunakuwa na mazao bora kwa ajili ya soko la ndani na la nje.

Naye, Msajili wa Bodi ya Nyama, Dkt. Daniel Mushi alisema anaishukuru Serikali kwa jitihada mbalimbali inazozifanya kwa kushirikiana na wadau kufungua masoko mengine nje ya nchi ili kuuza nyama katika masoko yanayolipa bei nzuri.

Aliongeza kuwa ujio wa ujumbe huo umewapa changamoto kwani kuna mambo wanapaswa kufanya ili nyama ya Tanzania iweze kukubalika katika masoko ya nje.

Aliendelea kusema kuwa ili waweze kufikia masoko hayo ni lazima kuboresha lishe ya mifugo ili wanyama waweze kukua kwa haraka na ambao watakuwa na nyama nyingi yenye ubora.

Itakumbukwa hivi karibuni, Rais Samia alikutana na Mtoto wa Mfalme wa Saudi Arabia ambapo miongoni mwa maeneo yaliyoangaliwa ni pamoja na Sekta ya Mifugo na aliielekeza Wizara kutafuta masoko nje ya nchi ikiwemo nchi ya Saudi Arabia.

 


Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiongea na Ujumbe kutoka nchini Saudi Arabia alipokutana nao jijini Dar es Salaam leo Agosti 7, 2021. Kushoto kwake ni Mkaguzi, Mamlaka ya Dawa na Chakula, Saudi Arabia, Ahmed Alhajouj.



Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati- mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe kutoka nchi ya Saudi Arabia uliokuja nchini kwa lengo la kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara ya Nyama na Tanzania. Wa pili kutoka kulia ni Mkaguzi, Mamlaka ya Dawa na Chakula, Saudia Arabia, Ahmed Alhajouj. Ujumbe huo ulikutana na Prof. Ole Gabriel jijini Dar es Salaam leo Agosti 7, 2021. Wengine katika picha ni Maafisa waliombatana na Mkaguzi huyo pamoja na  Viongozi mbalimbali kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi.


Ijumaa, 6 Agosti 2021

TUSISUBIRI KUSUKUMWA, TUFANYE KAZI-Prof. Ole Gabriel*

Katibu Mkuu wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka watumishi wote wa Sekta yake kutosubiri kushinikizwa ili watimize wajibu wao.

Prof. Ole Gabriel ameyasema hayo leo (06.08.2021) alipokutana na watumishi hao kwa lengo la kutathmini mipango na malengo mbalimbali yanayotarajiwa kutekelezwa na sekta hiyo kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

“Tusisubiri kusukumwa, wakurugenzi na wakuu wa vitengo simamieni hilo na kuhakikisha watu wenu wa chini wanatimiza wajibu wao ipasavyo” amesema Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabriel amewaahidi watumishi hao kuwa katika mwaka huu wa fedha Sekta yake itaendelea kuboresha mazingira yao ya kazi na kuwaongezea morali ya kufanya kazi.

“Watu wengi sana wanahamia kwenye Sekta yetu kwa hivi sasa na tunawakaribisha sana na wale wanaotaka kuhama walete maombi yao nami ntapitisha haraka sana ila nawakumbusha kuwa pindi wakitaka kurejea mchakato huo hautakuwa mwepesi” Amesisitiza Prof. Ole Gabriel.

Katika hatua nyingine Prof. Ole Gabriel amewataka watendaji na watumishi wote wa sekta yake kuchukua tahadhari ya kutosha ili kujikinga na maambukizi ya wimbi la tatu la virusi vya Uviko 19.

“Hofu haitakufikisha popote na ukishaanza kuwa na hofu hata kinga za mwili wako zitapungua hivyo msijenge hofu na wala msibaguane” Ameongeza Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabriel amewataka watumishi hao kupuuza taarifa zinazotolewa na vyanzo visivyo rasmi na kutafuta ukweli wa masuala yote yanayohusiana na maambuzi ya virusi hivyo kupitia vyanzo rasmi vilivyofanya utafiti kuhusiana na jambo hilo.

“Hatobaguliwa mtumishi yoyote aliyechanja au ambaye hajachanja kwa sababu suala la chanjo ni la hiyari na hatolazimishwa yoyote kufanya hivyo lakini ni vizuri uwe na sababu za msingi za kutochanja” Amesema Prof. Ole Gabriel

Kikao hicho baina ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel na watumishi wa sekta hiyo ni sehemu ya utamaduni wa Viongozi mbalimbali wa Wizara hiyo kukutana na watendaji na watumishi waliopo chini yao ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya Wizara hiyo.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel, (Pichani juu) akiongea na watumishi wa sekta ya Mifugo wa makao makuu Dodoma kwenye kikao cha kujadili na kutathmini utekelezaji wa mipango na malengo kwa upande wa sekta ya Mifugo kwa mwaka huu wa fedha wa 2021/2022, Kikao hicho kimefanyika katika Ukumbi wa Halmashauri ya jiji la Dodoma, leo tarehe 06.08.2021.*

SERIKALI YAOMBWA KUSITISHA UCHINJAJI WA PUNDA SHINYANGA.

Serikali imeombwa kusitisha uchinjaji na uuzaji wa ngozi na malighafi zitokanazo na punda katika machinjio ya Shinyanga na kuwachukulia hatua watu wote waliobainika kukiuka haki za wanyama.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Shirika la Ulinzi na Utetezi wa haki na Ustawi wa Wanyama Arusha (ASPA) Bw. Livingstone Masija leo Agosti 6, 2021 Jijini Dodoma mbele ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel baada ya ukaguzi uliofanyika juni 20 mwaka huu na kubaini ukiukwaji mkubwa wa haki za mnyama punda kwa kuwafanyiwa mateso makubwa.

Alisema, miongoni wa vitendo vinavyofanyika ni pamoja na kuwakosesha malisho kwa muda mrefu, kuchinja punda walio na mimba, kuchinja punda wakati wengine wanawaangalia na kuwapiga na vitu vizito kichwani pindi mashine zimeharibika na kukaa na majeraha bila ya kutibiwa.

“kwa sababu watu wako pale wameaminiwa na Serikali lakini namna ya utekelezaji wao wa majukumu ni shida, wameambiwa wasimamie punda wachinjwe 20 kwa siku  lakini wao wako pale sijajua wanakuwa hawaoni au hawako kazini basi unakuta punda wanachinjwa zaidi ya walioambiwa wasimamie, tunaomba pia wachukuliwa hatua za kinidhamu” alisema Masija

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel alisema kuwa serikali imepokea wasilisho hilo na italifanyia kazi haraka iwezekanavyo kwa mujibu wa sheria kwa sababu lengo la Wizara ni kuona kuwa wanyama kazi wanaendelea kulindwa.

Alisema mpaka juni 30, 2020 idadi ya punda ilikuwa  ni 657,380 kwa hiyo endapo wangefata utaratibu wa kuchinja punda 20 kwa siku kama maelekezo ya Serikali yalivyo Punda hao  wangeishi kwa miaka 50 kama wazaliaji. 

“nimesema tuna taratibu zetu sasa za kisheria ambazo ndani ya Wizara  tutazitumia ili kuhakikisha tunasonga mbele nanyi mtaendelea kupewa taarifa kupitia Ofisi ya Mkurugenzi wa  huduma za Mifugo kwamba nini kinaendelea”. Alisema.

Aliongeza kuwa lengo la serikali si kufanya punda waishe bali kuongezeka lakini pia swala la punda kutoka nje ya nchi ni jambo lingine ambalo ni kosa kisheria kwa sababu serikali inapoteza mapato, kwa hiyo suala hilo litaangaliwa kwa umakini.

Naye Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania, Dkt. Bedan Masuruli amemshukuru Katibu Mkuu kwa kutenga muda wake na kuja kuwasikiliza wadau wa ustawi wa wanyama na wamekusikia vizuri na kwamba Wizara imelichukua.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akiongea na wadau (hawapo pichani) kwenye kikao cha mapendekezo ya usitishaji wa shughuli za uchinjaji punda uuzaji wa ngozi na malighafi nyinginezo zinazotokana na punda leo Agosti 6, 2021 Jijini Dodoma.* 

 


Mkurugenzi wa Shirika la Ulinzi na Utetezi wa Haki na Ustawi wa Wanyama Arusha (ASPA), Bw. Livingstone Masija akionyesha nyundo kama moja ya dhana inayotumiwa katika kupiga punda kichwani pale mashine zinapoharibika ambacho ni ukiukwaji wa haki za wanyama kwenye ukumbi wa Ofisi za Tume ya vyama vya ushirika makao makuu Jijini Dodoma leo Agosti 6, 2021.*
 


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto), akiangalia video pamoja na wadau  ya namna haki za punda zinavyokiukwa kwenye kampuni ya Fang Huo Investment Co. Ltd leo Agosti 6, 2021  Jijini Dodoma. 


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (Waliokaa katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wawakilishi kutoka Shirika la Ulinzi na Utetezi wa Haki na Ustawi wa Wanyama Arusha (ASPA) pamoja na watumishi wa Wizara hiyo mara baada ya kikao cha mapendekezo ya usitishaji wa shughuli za uchinjaji punda, uuzaji wa ngozi na malighafi nyinginezo zinazotokana na punda katika machinjio ya Shinyanga leo Agosti 6, 2021 Jijini Dodoma.* 

 

Alhamisi, 5 Agosti 2021

WAFUGAJI KUNUFAIKA NA MBEGU BORA ZA MIFUGO YA ASILI*

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki ametoa wito kwa wafugaji wa mifugo ya asili kuunga mkono mkakati wa uboreshaji kosaafu za mifugo  nchini ili kupata tija zaidi kwa taifa kwa kuwa koo za mifugo zinazopatikana hapa nchini ni nzuri.

Waziri Ndaki amebainisha hayo leo (03.08.2021) jijini Dodoma wakati akizindua mpango mkakati wa uboreshaji kosaafu za mifugo nchini wenye lengo la kuhakikisha kosaafu hizo zinazopatikana katika Bara la Afrika na maeneo mengine duniani zinahifadhiwa na kudumishwa kwa ajili ya maendeleo ya nchi na raia wake.

“Ilikuwa lazima mkakati uzinduliwe leo kuhakikisha yale yaliyosemwa kwenye Sera ya Mifugo mwaka 2006, sasa yanakamilishwa kwa sababu tunaweza kuboresha kosaafu ya mifugo lakini hatukuwa na mikakati ya namna sera hiyo inaweza kuboresha kosaafu ya mifugo yetu ya asili.” Amesema Mhe. Ndaki

Aidha Waziri Ndaki amesema hapa nchini kuna mifugo ya aina nyingi na hizo zote ni kosaafu za mifugo ambazo zinatakiwa kulindwa kuhifadhiwa na kuendelezwa kwa njia ya ubora zaidi ili kunufaisha watu wake hivyo mkakati huo utasaidia kuona namna gani ya kuboresha ili ziweze kuwanufaisha zaidi wafugaji.

Kwa upande wake Mratibu wa Kosaafu za Mifugo hapa nchini kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Hassan Mruttu amesema tayari kulishakuwa na rasimu na kuanza utekelezaji kwa ufadhili wa Shirika la Umoja wa Afrika la Rasilimali za Mifugo (AU-IBAR) kwa kuanzisha kikundi cha wafugaji wa mbuzi weupe wa kipare na kuwezesha kupata mbegu ya ng’ombe aina ya sahiwal ambayo inakuwa na nyama na maziwa mengi pamoja na kusaidia uhifadhi wa mbegu hizo.

Pia amesema wamefurahishwa na kitendo cha Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki kulipa kipaumbele suala hilo kwa ajili ya uzinduzi na kwamba utekelezaji ni muhimu zaidi kwa kuwa watahakikisha wizara inatekeleza kwa umakini ili kila kilichopangwa kitekelezwe na mafanikio yaonekane.

Akizungumza kuhusu mkakati huo mmoja wa wafugaji wa ng’ombe wa asili Bw. Elinami Mshao amesema matarajio yao ni kupata faida kwa kupata mbegu bora za mifugo na kwa bei nafuu ambapo serikali itawafikishia kwa kuwa baadhi ya aina ya ng’ombe wakiwemo waliopo nchini jirani wanauzwa bei ghali na wamekuwa na matokeo mazuri kwa wafugaji.

Ameongeza kuwa wao kama wafugaji uchumi wao mkubwa unategemea mifugo hivyo ikiboreshwa itakuwa na tija kwao kwa kuwa watapata mbegu bora ya mifugo ya asili.

Uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Uboreshaji Kosaafu za Mifugo nchini, umehudhuriwa na washiriki kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Shirika la Umoja wa Afrika la Rasilimali za Mifugo (AU-IBAR) Nairobi-Kenya, Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC) na Umoja wa Afrika (AU).


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizindua Mpango Mkakati wa Uboreshaji Kosaafu za Mifugo nchini, katika hafla fupi iliyofanyika jijini Dodoma na kutaka mpango huo uwawezeshe wafugaji wa asili kuboresha mifugo yao na iwe na tija zaidi kwa taifa. (03.08.2021) 

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na washiriki wakati wa uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Uboreshaji Kosaafu za Mifugo nchini, katika hafla fupi iliyofanyika jijini Dodoma na kubainisha kuwa kosaafu za mifugo zilizopo nchini ni nzuri hivyo zinapaswa kuboreshwa ili zitoe matokeo mazuri zaidi. (03.08.2021) 

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) ambaye pia ni Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania Dkt. Bedan Masuruli akifafanua jambo wakati wa uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Uboreshaji Kosaafu za Mifugo nchini, katika hafla fupi iliyofanyika jijini Dodoma. (03.08.2021) 

 

Picha ya pamoja ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (aliyesimama katikati mstari wa mbele) akiwa na washiriki wa mkutano baada ya kuzindua Mpango Mkakati wa Uboreshaji Kosaafu za Mifugo nchini, katika hafla fupi iliyofanyika jijini Dodoma. (03.08.2021) 

 


KATIBU MKUU, WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI, (MIFUGO) PROF. ELISANTE OLE GABRIEL VISIWANI ZANZIBAR.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akiongea na  Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo (Zanzibar), Dkt. Soud Hassan alipomtembelea Waziri huyo Ofisini kwake. Prof. Ole Gabriel alifanya ziara  Visiwani Zanzibar Agosti 2, 2021 kwa ajili ya kuimarisha ushirikiano baina ya Sekta ya Mifugo, Tanzania bara na Sekta ya Mifugo,  Zanzibar, pia kufanya uhamasishaji wa ufugaji wa kisasa Visiwani humo. 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akikagua moja kati ya aina mbalimbali za malisho ya mifugo zinazofanyiwa Utafiti  na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo, Zanzibar (ZALIRI) alipotembelea taasisi hiyo iliyopo Visiwani Zanzibar Agosti 2, 2021. 

 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kushoto) akiongea na Viongozi wa Kiwanda cha kuzalisha maziwa cha Azam Kilichopo Fumba, Visiwani Zanzibar. Prof. Ole Gabriel alifanya ziara katika Kiwanda  hicho Agosti 2, 2021 kwa lengo la  kukagua maendeleo yake ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka kuendelee kuzalisha maziwa kwa kiwango kilichokusudiwa  huku akiwaeleza kuwa Serikali ipo pamoja nao. Katikati ni Meneja wa Kiwanda hicho, Adilson Fagundes na wa kwanza kulia ni Mkuu wa Udhibiti Ubora wa bidhaa katika Kiwanda hicho, Tumaini Fredrick. 

 


 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (watatu kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo, Zanzibar, Dkt. Soud Hassan (katikati). Prof. Ole Gabriel alimtembelea Waziri huyo Ofisini kwake, Visiwani Zanzibar Agosti 2, 2021. 

SERIKALI YAANZA KUSAKA MATOKEO CHANYA YA ZAO LA MWANI*

 

Serikali imesema itaendelea kuwawezesha wakulima wa zao la mwani kwa vifaa pamoja na utaalamu ili waweze kuzalisha kwa wingi na ubora unaohitajika sokoni.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema hayo (01.08.2021) akiwa katika Kijiji cha Zingibari kilichopo Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga, wakati akitoa vifaa vyenye thamani ya Shilingi Milioni Nne kwa ajili ya kilimo cha mwani kwa vikundi vitatu vya wakulima wa zao hilo na kufafanua kuwa serikali itaendelea kutoa bure vifaa hivyo kwa wakulima wa mwani katika mwambao wa pwani ya Bahari ya Hindi ili kuhakikisha zao hilo linalimwa kwa wingi nchini.

Akiwa katika ziara ya kikazi ya siku moja Mkoani Tanga, Mhe. Ndaki amesema kutokana na zao la mwani kuwa la kiuchumi kwa wananchi wa mwambao wa pwani ya Bahari ya Hindi, serikali imeanza kuweka mazingira mazuri ya uwezeshaji na kutafuta masoko ya uhakika ili wakulima waweze kunufaika kiuchumi.

"Huu msaada wa vifaa kwa ajili ya kilimo utafika katika maeneo yote yenye uzalishaji na msisitizo tumeanza kuweka kwenye elimu ya namna ya kulima zao la mwani kwa ajili ya tija zaidi." amesema Waziri Ndaki

Aidha, Waziri Ndaki akiwa katika Kata ya Kipumbwi Wilaya ya Pangani Mkoani Tanga, amesema serikali inatarajia kutumia Shilingi Bilioni 1.2 kwa ajili ya ujenzi wa soko la kimataifa katika kata hiyo kwa ajili ya kuuza dagaa ndani na nje ya nchi.

Mhe. Ndaki amesema wanunuzi wa dagaa wanaotoka nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Zambia, Malawi, Rwanda na Burundi wataenda kununua dagaa kutoka Kipumbwi hivyo wafanyabiashara wa kata hiyo hawatapata shida ya kutafuta soko la dagaa.

“Niwaambie serikali imesikia na inakusudia kujenga kujenga soko la kimataifa la kuuza dagaa, msipate shida kuuza dagaa wenu.” Amesema Waziri Ndaki.

Amesema kwa kipindi kirefu wakazi wa Kata ya Kipumbwi wamekuwa wakilalamikia ukosefu wa masoko ya dagaa wanaopatikana katika eneo hilo na kwamba wamekuwa wakivua dagaa kwa wingi.

Kuhusu uvuvi haramu Waziri Ndaki amesema serikali itavunja Vikundi vya Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) ambavyo vitabainika kujihusisha na uvuvi haramu na kuhakikisha viongozi wa vikundi hivyo wanafikishwa Katika vyombo vya sheria.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema imebainika baadhi ya viongozi wa BMU wanajihusisha na wavuvi kushiriki vitendo vya uvuvi haramu katika maziwa pamoja na Bahari ya Hindi.

“Baadhi ya BMU zimeshindwa kutekeleza wajibu wake na kushirikiana na wavuvi haramu acheni mara moja kabla hamjakumbana na mkono wa sheria, yeyote atakayematwa anajihusisha na uvuvi haramu atachukuliwa hatua kali za kisheria.” Amesema Mhe. Ndaki

Katika ziara hiyo ya kikazi ya siku moja Mkoani Tanga, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amekagua pia majengo ya Vikundi vya Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) katika Wilaya za Mkinga na Pangani, yaliyojengwa kupitia mradi wa Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi Kusini Magharibi mwa Bahari ya Hindi (SWIOFISH).

Katika sekta ya mifugo, Waziri Ndaki pia ametembelea mnada wa mpakani wa Horohoro kujionea miundombinu mbalimbali inayowekwa kabla ya kuanza rasmi kwa mnada huo ambao anasema utakuwa na matokeo chanya pindi utakapokamilika.

“Licha ya kusaidia kupunguza utoroshaji wa mifugo mnada utasaidia kuongeza kipato kwa wananchi na hivyo kuinua uchumi wao, kwa sababu wakipeleka ng’ombe nje ya nchi wanauza bei ya juu lakini pia tunataka tuwapunguzie wananchi adha ya kuvuka mipaka kwani jambo hili wakati mwingine linasababisha kuuza mifugo yao kwa bei ya chini.” Amesema

Hata hivyo Waziri Ndaki amesema wameamua kuondoa shida hizo kwa kuwa na minada ya mipakani ili wafugaji waweze kuuza mifugo yao maeneo rasmi na serikali iweze kupata mapato yao.

Akizungumza katika nyakati tofauti kwenye ziara hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah amesema wizara ina malengo ya kuhakikisha wananchi wanaohusika na sekta ya uvuvi wananufaika kupitia rasilimali zinazopatikana katika Bahari ya Hindi pamoja na maziwa yaliyopo nchini huku kwa kuwa serikali itaendelea kuwasaidia kwa kila hali likiwemo suala la vifaa pamoja na marekibisho ya sheria na tozo mbalimbali.

Nao baadhi ya wananchi wamesema wamefurahishwa na ziara ya kikazi ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki kwa kuwa imeendelea kujibu changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo katika sekta ya uvuvi pamoja na kuwatafutia fursa zilizopo kupitia sekta hiyo.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na wakazi wa Kata ya Kipumbwi iliyopo Wilaya ya Pangani Mkoani Tanga, wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja mkoani humo na kusisitiza kuwa serikali inatarajia kujenga soko la kimataifa la samaki aina ya dagaa katika kata hiyo na kutoa onyo kwa watu wanaohusika na uvuvi haramu nchini kuwa watachukuliwa hatua kali za kisheria. (01.08.2021) 

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah akizungumza na wakazi wa Kata ya Kipumbwi iliyopo Wilaya ya Pangani Mkoani Tanga, na kuwafahamisha mikakati ya serikali katika kuhakikisha sekta ya uvuvi inawanufaisha wananchi ikiwemo ya kufanya marekebisho ya sheria na tozo mbalimbali, wakati wa ziara ya kikazi ya siku moja ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki Mkoani Tanga. (01.08.2021) 

 


 

Jumanne, 3 Agosti 2021

BODI YA NYAMA YATAKIWA KUANZISHA MFUMO WA KUWATAMBUA WANENEPESHAJI MIFUGO

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi mheshimiwa Abdallah Ulega ameiagiza Bodi ya Nyama nchini kuanzisha mfumo utakaosaidia wafugaji kunenepesha mifugo yao ili waweze kunufaika zaidi na fulsa za masoko ya ndani na nje ya nchi kwani mahitaji ya nyama ni makubwa.

 

Amesema hayo wakati akizungumza katika mkutano maalumu na wafugaji wa kienyeji, wafugaji wa kisasa pamoja na taasisi wezeshi za wafugaji wafuge kibiashara ili waweze kutoshereza soko la ndani na soko kubwa la nje ya nchi katika ukumbi wa Mvuvi house jijini Dar es salaam.

 

Mheshimiwa Ulega alisema elimu ya kutosha iendelee kutolewa ili kuwajengea uwezo wa kunenepesha mifugo yao hata wafugaji wa kienyeji katika ng’ombe, mbuzi na kondoo wao wa asili maana taifa limepata fulsa kubwa huko katika nchi za uarabuni hivyo mahitaji ya nyama ni makubwa.

 

Alisema katika halmashauri zote nchini wafugaji wa fundishwe namna moja ya kunenepesha na kuzalisha kwa wingi mifugo yao huku wakijua soko la ndani na nje ya nchi linachotaka ili kupata nyama yenye ubora na yenye thamani ya kimataifa itakayompa mfugaji faida kubwa.

 

Akizungumzia wafugaji kukopesheka kwenye mabenki ya mifugo nchini Mheshimiwa Ulega alisema Wafugaji waingie mikataba na wenye viwanda vya kuchakata nyama kwa namna wanavyowasambazia mifugo yao ili wapate thamani ya kuweza kukubalika na kuaminiwa kupata fulsa za fedha katika mabanki hayo.

 

“Mikataba watakayopata itakuwa sehemu ya wao kukubalika Wafugaji wapate fedha kwenye mabanki wanenepeshe mifugo yao wauze kimataifa wapate pesa maana biashara ni nzuri sana” alisema Mheshimiwa Ulega.

 

 Alisema lengo kubwa likiwa ni kuwajengea uwezo wafugaji  kuzalisha kiwango kikubwa cha nyama kitakachoweza kutoshereza mahitaji ya soko la ndani na soko la nje ya nchi katika ubora wa nyama iliyoandaliwa vyema.

 

“Ukiandaa vizuri nyama yako mteja akiiona ni nzuri na yenye ubora utafanya biashara maana soko lipo” alifafanua.

 

Hatahivyo Naibu Waziri huyo alisema hadi sasa viwanda vya kuchakata nyama za ng’ombe, mbuzi na kondoo nchini bado vinazalisha chini ya viwango vya idadi iliyohitajika kuzalisha katika viwanda hivyo kutokana na kukosekana kwa idadi kubwa ya mifugo hiyo hivyo aliwataka watanzania kutumia vyema fulsa hiyo kwa kufuga kwa wingi ilikuweza kutoshereza soko.

 

Aidha Mheshimiwa aliitaka pia bodi hiyo ya nyama kutafuta namna ya kufundisha wafugaji wa asili wabadilike kwa kufuga kisasa zaidi hata kuachana na ufugaji wa kuzurulisha mifugo bali uwe ni ufugaji katika ubora na viwango vya kimataifa katika mashamba yao ya ufugaji.

 

Naye Afisa manunuzi wa Tanchoice cha kibaha mkoani Pwani Jabil Mohamed alisema kiwanda chao kinauwezo wa kuchinja mbuzi 4500 kwa siku na ng’ombe 1000 kwa siku lakini mpaka sasa wanapata idadi ya mifugo chini ya idadi wanayohitaji kulingana na uwezo wa kiwanda ambapo wanachinja mbuzi hadi 2000 kwa siku na ng’ombe 150

 

“Jambo ambalo uzalishaji wetu bado ni kiwango kidogo sana sawa na asilimia 20 cha kiwanda chetu hivyo kiwanda hicho ni fulsa kwa wafugaji kwani inaweza kuwatoa kwenye umasikini hadi mafanikio ya utajiri” alisema Jabil.

 

Jabil alisema kiwanda hicho mpaka sasa kina vibali vya kupeleka nyama katika nchi tano duniani.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akizungumza na wadau wa bodi ya nyama kwenye kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa Uvuvi house jijini Dar es Salaam ambapo amewataka wadau hao kutumi fursa ya biashara ya Mifugo iliyopo huku akiitaka Bodi ya Nyama Tanzania kuhakikisha inawatambua wadau wake. (02.08.2021)


Jumatatu, 2 Agosti 2021

KATIBU MKUU SEKTA YA UVUVI DKT. RASHID TAMATAMAH AFANYA MAZUNGUMZO NA WASHAURI KUTOKA AGRONOMOS SIN FRONTERAS FOUNDATION.


 Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi ( Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na washauri kutoka Agronomos Sin Fronteras Foundation, wa pili kutoka kulia ni Dkt. Miguel Salvo Mendivil, wa  pili kutoka kushoto ni Bw. Klaus Poppe na watumishi wa Sekta ya Uvuvi  mara baada ya kufanya mazungumzo ofisini kwake leo 02/08/2021 Mtumba Jijini Dodoma, lengo likiwa ni kusaidia kuweza kupata  msaada kutoka  Serikali ya Spain kupitia mfuko wao unaojulikana kama COVID - 19 Recovery Fund, Aidha miradi iliyopendekezwa kuwasilishwa kwa ajili ya msaada huo  ni pamoja na ujenzi wa kiwanda cha kuchakata Mazao ya Uvuvi kupitia Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO), kuangalia uwingi  wa samaki katika ukanda wa uchumi wa Bahari kuu, kufanya ubia na makampuni ya Spain katika Uvuvi wa Bahari kuu kupitia TAFICO na kuingiza masuala ya ufugaji viumbe maji katika mradi wa Kilimo unaotarajiwa kuanzishwa Mkoani Iringa.