Nav bar

Jumatano, 24 Januari 2024

WAKANDARASI WALIOSHINDA ZABUNI ZA MIRADI MBALIMBALI YA UJENZI WAPEWA MIKATABA

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe  (kushoto) akiongea na sehemu ya wakandarasi walioshinda zabuni za miradi mbalimbali ya ujenzi ikiwemo ya minada na  majengo  kwenye  kampasi za LITA  (hawapo pichani) ambapo  amewasisitiza wakandarasi hao kutekeleza miradi  kwa wakati, kuwasiliana kwa haraka pindi inapobidi na ushirikishwaji wa karibu wa viongozi wa kisiasa kwenye maeneo ya miradi, kikao hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma  (24.1.2024) kulia ni Naibu katibu Mkuu (Mifugo) Prof. Daniel Mushi.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe (katikati) akisaini mkataba wa makubaliano ya ujenzi wa soko la upili lililopo kishapu mkoani Shinyanga,  Handeni mkoani Tanga na Nzega mkoani Tabora na mwakilishi wa kampuni ya MACEA Construction Ltd, Bw. Godlove Gandye (kushoto) kulia ni Naibu Katibu Mkuu (Mifugo) Prof. Daniel Mushi (24.01.2024)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe akikabidhi mkataba wa makubaliano ya ujenzi wa soko la upili la Luaguza lililopo Lushoto mkoani Tanga kwa  Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Maruu RPK Group Ltd , Bw. Rhodes Kimambo wakati wa kikao kifupi cha makabidhiano kilichofanyika kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma (24.1.2024)

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA), Dkt. Pius Mwambene (kushoto) akikabidhi mkataba wa makubaliano ya ujenzi wa ukumbi mmoja wa miadhara wenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 100 na ujenzi wa hostel moja yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 150 kwa Arch. Eliah Mpembeni kutoka kampuni ya KADIVA, Mkataba huo umesainiwa kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma (24.01.2024)


 Sehemu ya washiriki wa kikao cha makabidhiano ya mkataba wa makubaliano wa   ujenzi miradi ya maendeleo kilichofanyika kwenye ukumbi wa NBC Jijini Dodoma  (24.1.2024)

Jumanne, 23 Januari 2024

ULEGA: TANGAZENI VITALU KWA AJILI YA UWEKEZAJI


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amewaagiza Naibu Katibu Mkuu, Sekta ya Mifugo, Prof. Daniel Mushi na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera kuhakikisha kuwa maeneo yote yaliyopo katika Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) mkoani Kagera ambayo hayana mgogoro yatangazwe kwa ajili ya uwekezaji.

Ulega ametoa maelekezo hayo wakati wa kikao chake na Viongozi mbalimbali wa  Mkoa wa Kagera kilichofanyika leo Januari 22, 2024 chenye lengo la kumaliza migogoro iliyopo baina ya wananchi na Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO).

Amesema maeneo ambayo yameshapimwa na ambayo hayana mgogoro yatangazwe ili wawekezaji wenye uwezo waweze kupewa kwa ajili ya kufanya ufugaji wenye tija.

Sambamba na hayo amewataka Wataalamu kurejea upya kwenye maeneo yote ambayo yameonekana yana migogoro ili kutatua changamoto zilizopo na kuwezesha maeneo hayo yaweze kuendelezwa na wawekezaji wenye uwezo.



Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega(kulia) akiteta jambo na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Mhe. Erasto Sima wakati wa kikao chake na Viongozi mbalimbali wa  Mkoa wa Kagera kilichofanyika leo Januari 22, 2024 chenye lengo la kumaliza migogoro iliyopo baina ya wananchi na Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO).


WAZIRI ULEGA AKUTANA NA WAWEKEZAJI KUTOKA POLAND


Leo Januari 18, 2024, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amekutana na Wawekezaji kutoka Kampuni ya Uwekezaji ya Contractus ya nchini Poland ambao wameonesha nia ya kufanya uwekezaji kwenye tasnia ya Maziwa hapa nchini.

Wawekezaji hao ambao ni Makamu Mwenyekiti wa Kampuni Contractus, Bw. Witold Karczewski na Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara ya Poland ambaye pia ni Meneja Mauzo wa Kampuni, Bw. Adam Borawski wameonesha nia ya kuingia ubia na Serikali ya Tanzania Kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuleta telnolojia ya kisasa ya kupoza maziwa katika vituo mbalimbali vya kukusanyia maziwa nchini.

Nia yao kuanzia mwaka 2024/ 2025 kuanza uwekezaji huo ambapo wataanza na vituo 500 nchi nzima vyenye uwezo wa kukusanya kati ya lita 2000 hadi 6000 kwa siku. Uwekezaji huo unatarajiwa  kuongeza ukusanyaji wa lita takribani milioni moja za maziwa kwa siku hapa nchini.

Aidha, mpango huo unaotarajiwa kuwa wa miaka 2 unakadiriwa kugharimu TZS. Bilioni 175, na inakusudiwa kupata ufadhili kutoka kwa Wadau na Serikali ya Poland.

Kwa upande wake, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amewahakikishia wawekezaji hao ushirikiano wa kutosha ili mradi huo uweze kuanza haraka ili tasnia ya maziwa iweze kuwa na tija zaidi kwa taifa.

Kampuni hiyo ya Contractus inatengeneza na kuuza Machine/Vifaa vya Kukusanyia maziwa ambazo zinatumia umeme wa jua na wana uzoefu wa kufanya kazi katika Tasnia ya Maziwa hususan usambazaji wa mashine na vifaa vya kukusanyia na kusindika maziwa kwa miaka 35 katika nchi mbalimbali ikiwemo nchi za Ulaya, Asia, na Afrika.  Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe na Msajili wa Bodi ya Maziwa, Prof. George Msalya.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (katikati) akimsikiliza Makamu Mwenyekiti wa Kampuni ya Contractus, Bw. Witold Karczewski wakati wa mazungumzo yao kuhusu uwekezaji katika sekta ya maziwa yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya waziri huyo jijini Dar es Salaam mapema leo Januari 18, 2024. Kulia kwake ni Katibu Mkuu, Prof. Riziki Shemdoe na kushoto kwake ni Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara ya Poland ambaye pia ni Meneja Mauzo wa Kampuni, Bw. Adam Borawski.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Makamu Mwenyekiti wa Kampuni Contractus, Bw. Witold Karczewski (wapili kulia) muda mfupi baada ya kumaliza mazungumzo yao kuhusu uwekezaji katika tasnia ya maziwa yaliyofanyika katika ofisi ndogo ya waziri huyo jijini Dar es Salaam mapema leo Januari 18, 2024. Wapili kushoto ni Katibu Mkuu, Prof. Riziki Shemdoe. Wa kwanza kushoto ni Msajili wa Bodi ya Maziwa, Prof. George Msalya na wa kwanza kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara ya Poland ambaye pia ni Meneja Mauzo wa Kampuni ya Contractus, Bw. Adam Borawski.


DC NGUBIAGAI ASISITIZA MAPAMBANO DHIDI YA UVUVI HARAMU


Aipa Kongole Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia zoezi la Uhakiki wa Vikundi vya Wavuvi, Wakuzaji viumbe maji.

Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Mhe. Christopher Ngubiagai ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuziongezea nguvu timu za Doria baharini zilizopo wilayani humo ili ziweze kuendelea kupambana na Uvuvi haramu.

Mhe. Ngubiagai amesema hayo baada ya kupokea timu ya wataalam kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi iliyofika Wilayani hapo kwa ajili ya zoezi la uhakiki wa taarifa za vikundi vya Wavuvi na wakuzaji viumbe maji Januari 17, 2023.

" Jitihada hizi kubwa za kuwawezesha Wavuvi zitakuwa na maana kubwa zaidi kama tutahakikisha rasilimali za bahari zinapatikana kwa wingi na hili litawezekana kama tuweka mkazo na nguvu kwenye kupambana na uvuvi haramu ukanda huu wa bahari" Amesema Mhe. Ngubiagai.

Mhe. Ngubiagai amedokeza kuwa licha ya Wilaya yake kuendelea na doria ya kupambana na changamoto hiyo ikiwa ni pamoja na kukagua nyenzo zinazotumiwa na wavuvi hao bado nguvu waliyonayo haitoshi kupambana na eneo kubwa la bahari linaloizunguka Wilaya hiyo.

"Tunazo jumuiya za Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) ambazo kwa kweli zinatusaidia sana kwenye hili ila bahati mbaya hata wenyewe hawana vifaa vya kisasa vya kuweza kudhibiti hali hiyo kwa hiyo bado nguvu kubwa inahitajika" Amesisitiza Mhe. Ngubiagai.

Aidha Mhe. Ngubiagai ameipongeza Wizara kwa utekelezaji wa programu ya "Jenga Kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na vijana" (BBT-LIFE) ambapo amesema kuwa tayari wilaya yake imeshatenga maeneo ambayo yanaweza kutumika kwa ajili ya shughuli za ufugaji wa samaki na kilimo cha zao la Mwani.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe maji baharini Dkt. Hamis Nikuli amesema kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatarajia kutekeleza miradi mbalimbali Wilayani Kilwa ikiwa ni pamoja na Kujenga chanja za kisasa za kukaushia Mwani na Ghala kubwa la kuhifadhi zao hilo.

"Lakini pia tayari kuna hatua za kudhibiti uvuvi haramu zimeshaanza kuchukuliwa upande wa Dar-es-salaam ambapo zinatarajiwa kufika kwenye maeneo yote yanayopitiwa na bahari" Ameongeza Dkt. Nikuli.

Timu ya Wataalam kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea na zoezi la uhakiki wa vikundi vya Wavuvi na Wakuzaji Viumbe Maji kupitia ujazwaji wa dodoso maalum lenye taarifa zote za Msingi lengo likiwa ni kuiwezesha Serikali kuelekeza rasilimali kwa mujibu wa mahitaji ya vikundi hivyo.


Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji baharini Dkt. Hamis Nikuli (kulia) akimueleza Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Mhe. Christopher Ngubiagai (katikati) namna yeye na timu yake watakavyoendesha zoezi la Uhakiki wa vikundi vya Wavuvi na Wakuzaji viumbe maji waliopo Wilayani humo Januari 17, 2024. Kushoto ni Katibu Tawala wa Wilaya hiyo Bw. Yusuph Mwinyi.

Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji baharini Dkt. Hamis Nikuli (kulia mbele) akimueleza Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilwa Bw. Shija Lyela (katikati) namna yeye na timu yake watakavyoendesha zoezi la Uhakiki wa vikundi vya Wavuvi na Wakuzaji viumbe maji waliopo Wilayani humo Januari 17, 2024.


PWANI IPO TAYARI KUTEKELEZA BBT-LIFE-MCHATTA

Katibu Tawala Mkoa wa Pwani Bw. Rashid Mchatta amekutana na ujumbe kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi upande wa sekta ya Mifugo Januari 15, 2024 na kufanya nao mazungumzo  kuhusu  namna ya kutekeleza mradi wa "Jenga kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na Vijana (BBT-LIFE) kwa Mkoani humo.

Akiongoza kikao hicho Bw. Mchatta ameipongeza na kuishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kupeleka programu hiyo mkoani kwake ambapo ameahidi kutoa ushirikiano wa kutosha wakati wote wa utekelezaji wake.

"Tunatambua tija kubwa watakayoipata vijana hawa na wanawake watakaofanikiwa kuchaguliwa kuingia kwenye programu hii hivyo niwashukuru sana kwa kuuleta mpango huu hapa Pwani" Amesema Bw. Mchatta.

Akizungumza wakati wa kikao hicho  Mkurugenzi msaidizi  wa utafiti na Mafunzo kutoka Wizara ya mifugo na Uvuvi (Mifugo) Dkt Hassan Mrutu  amesema kuwa  utekelezaji huo umewalenga vijana na wanawake katika  suala zima la Ufugaji wa kibiashara ambapo jumla ya vijana 30 watakaochaguliwa wanatarajiwa kunufaika na mpango huo utakaotekelezwa kwa siku 90.

Mazungumzo hayo baina ya pande hizo yamefanyika kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo ambapo mbali na watalaam hao kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi pia yalihudhuriwa na wataalam kutoka Sekretariet ya Mkoa. 


Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti na Mafunzo (Mifugo) kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Hassan Mrutu (mbele kushoto) akimuelezea Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Bw. Rashid Mchatta (kulia) namna wizara inavyotarajia kutekeleza mradi wa "Jenga kesho iliyo bora" (BBT-LIFE) kwa upande wa sekta ya Mifugo mkoani humo muda mfupi baada ya kufika ofisini kwake Januari 15, 2024.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Bw. Rashid Mchatta (katikati mbele) akiongoza kikao baina ya timu ya wataalam wa mkoa huo na wale wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kinachohusu utekelezaji wa programu ya "Jenga kesho iliyo bora" BBT-LIFE kwa upande wa sekta ya Mifugo mkoani humo Januari 15, 2024.


MNYETI: “MAAFISA MIFUGO NENDENI KWA WAFUGAJI, ACHENI KUWA WAKUSANYA MAPATO.”


 Na. Edward Kondela

Maafisa mifugo nchini wametakiwa kufanya kazi za udaktari wa mifugo walizosomea na kuwatembelea wafugaji badala ya kuwa wakusanya mapato wa halmashauri.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti amebainisha hayo (15.01.2024) mjini Dodoma wakati akizindua Baraza la Veterinari Tanzania awamu ya sita baada ya baraza hilo kupata wajumbe.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa baraza hilo Mhe. Mnyeti amesema baadhi ya maafisa mifugo wamekuwa wakijikita zaidi kwenye kukusanya mapato ya halmashauri minadani badala ya kuwatembelea wafugaji ili kujua matatizo yao.

“Maafisa mifugo kwenye halmashauri wanajifanya watumishi wa halmashauri kwa ajili ya kukusanya mapato kwenye minada kukusanya ushuru wa ng’ombe badala ya kufanya kazi za udaktari na kuwatembelea wafugaji.” Amesema Mhe. Mnyeti

Aidha, amelitaka Baraza la Veterinari Tanzania kuhakikisha linachukua hatua zaidi kwa maafisa mifugo ambao wamekuwa wakifanya kazi kinyume na maadili pamoja na kuwapatia semina mara kwa mara ili kuwakumbusha wajibu wao kwa wananchi.

Amesema pia ifike wakati maafisa mifugo ambao wanakiuka maadili wafukuzwe kazi pamoja na kufutiwa leseni zao ili kazi hiyo ifanywe na watu ambao watafuata taratibu na maadili ya kazi.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mifuo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe amesema ana imani maafisa mifugo ambao walikuwa wakituma maombi kwa ajili ya kusajiliwa kwenye Baraza la Veterinari Tanzania sasa wataanza kusajiliwa rasmi kwa kuwa baraza hilo tayari limezinduliwa.

Amefafanua kuwa amekuwa akipata ujumbe kwa njia ya simu kutoka kwa baadhi ya maafisa mifugo ambao wamekuwa wakihitaji kusajiliwa lakini hawakuweza kusajiliwa kwa kuwa baraza halikuwa na wajumbe.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Veterinari Tanzania Prof. Lughano Kusiluka amesema baraza limekuwa likisimamia sheria za veterinari kwa kuhakikisha wataalamu wanaohusika na kutoa huduma za afya za wanyama wafugwao na wasiofugwa wanafanya kazi kwa kufuata sheria na maadili.

Ameongeza kuwa kazi kubwa ya baraza ni kuwaandikisha na kuwaingiza kwenye daftari la baraza hilo na kufuatilia kiwango na huduma wanazotoa, kusimamia elimu ya wanyama inayotolewa na taasisi mbalimbali na kufuatilia kwa ukaribu wadau wapate huduma inayotakiwa.

Baraza la Veterinari Tanzania awamu ya sita lililozinduliwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti litadumu kwa miaka mitatu.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti akizungumza baada ya kuzindua Baraza la Veterinari Tanzania awamu ya sita jijini Dodoma ambapo amewataka maafisa mifugo nchini kufanya kazi za udaktari wa mifugo walizosomea na kuwatembelea wafugaji badala ya kuwa wakusanya mapato wa halmashauri. (15.01.2024)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifuo na Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe amebainisha kuwa ana imani maafisa mifugo ambao walikuwa wakituma maombi kwa ajili ya kusajiliwa kwenye Baraza la Veterinari Tanzania sasa wataanza kusajiliwa rasmi kwa kuwa baraza hilo tayari limezinduliwa. Prof. Shemdoe amesema hayo wakati wa uzinduzi wa baraza hilo awamu ya sita. (15.01.2024)

Picha ya pamoja ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti akiwa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Prof. Riziki Shemdoe, Mwenyekiti wa Baraza la Veterinari Tanzania Prof. Lughano Kusiluka, Msajili wa baraza hilo Dkt. Amani Kilemile pamoja na wajumbe wa baraza hilo baada ya kuzinduliwa rasmi jijini Dodoma. (15.01.2024)


MAJONGOO BAHARI, MWANI, KAA NI BIASHARA KUBWA”


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amewahimiza wananchi wanaoishi Mtwara na maeneo mengine ya ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi kuchangamkia fursa ya ufugaji  wa Majongoo Bahari, Kaa, Kambakochi pamoja na kufanya kilimo cha Mwani kwa sababu mazao hayo yanahitajika sana katika nchi za Asia hususan China.

Waziri Ulega ametoa rai hiyo wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji cha Ruvula kinachojengwa Msimbati, mkoani Mtwara Januari 14, 2024.

“Mahitahi ya Majongoo Bahari, Kaa, Mwani, Kambakochi na Mwatiko ni makubwa katika nchi za Asia hasa china, hivyo ni lazima tucheze na fursa tulizonazo ili tuweze kufanikiwa na ndio maana serikali inatoa elimu kuwawezesha wananchi hususan vijana na kinamama kufanya shughuli hizo ili wauze nje ya nchi wajipatie kipato”, alisema Ulega

Halikadhalika, aliwahimiza wananchi kujipanga vyema ikiwemo kuunda vikundi ili serikali iweze kuwatambua na kuwapatia mikopo ya vifaa vya kisasa kwa ajili ya kuwawezesha kufanya shughuli zao kwa ufanisi mkubwa.

Aidha, Waziri Ulega alionesha kuridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho cha ukuzaji viumbe maji cha Ruvula huku akiamini kuwa kitakamilika kwa wakati ili kianze kufanya kazi.

Awali, Mhandisi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. George Kwandu alimweleza Waziri Ulega kuwa ujenzi wa kituo hicho umefikia asilimia 90 na kwamba mpaka itakapofika Januari 30, 2024 mradi huo utakuwa tayari umekamilika.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (katikati)akikagua maendeleo ya ujenzi wa kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji kinachojengwa Msimbati, Ruvula, mkoani Mtwara alipofanya ziara ya kukagua kituo hicho Januari 14, 2024. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Ahmed Abbas. Kulia ni Mhandisi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. George Kwandu.

Pichani ni muonekano wa jengo la kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji linalojengwa Msimbati, Ruvula, mkoani Mtwara alipofanya ziara ya kukagua kituo hicho Januari 14, 2024.




TANZANIA, RWANDA KUSHIRIKIANA KUKUZA TASNIA YA MAZIWA


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega na Waziri wa Kilimo, Maliasili, na Mifugo wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. James Kabarebe wamesaini hati ya makubaliano ya kushirikiana kuendeleza tasnia ya maziwa baina ya nchi hizo mbili.

Tukio hilo la utiaji saini limefanyika Visiwani Zanzibar  Januari 12, 2024 sambamba na Sherehe za Kutimiza Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Akizungumza katika tukio hilo, Waziri Ulega alisema kuwa ushirikiano huo ambao umekusudia kuendeleza viwanda vya usindikaji wa maziwa utasaidia kuongeza uzalishaji wa maziwa wa nchi hizo mbili jambo ambalo litapelekea kupatikana kwa ajira, usalama wa chakula na kukuza uchumi wa kaya na mtu mmoja mmoja kupitia mnyororo wa thamani wa maziwa.

Alisema kuwa mpaka sasa bado nchi inaagiza maziwa mengi kutoka nje ya nchi, lakini kupitia ushirikiano huo ana uhakika uzalishaji wa maziwa nchini utaongezeka na kuchechemua biashara baina ya nchi hizo mbili. “Tanzania na Rwanda tumeamua kushirikiana katika mambo mbalimbali ya Maendeleo ya Tasnia ya Maziwa, Niwahakikishie ndugu zangu wa Rwanda na Tanzania kuwa nitawapa ushirikiano, nitasimamia utekelezaji wa makubaliano haya tuweze kufikia malengo tuliyoyakusudia”, alisema Ulega

Aidha, Waziri Ulega alimshukuru Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kufungua milango ya ushirikiano baina ya Tanzania na nchi nyingine akiongeza kuwa ushirikiano huo ni moja ya hatua zake za kuhakikisha Watanzania wanaendelea kunufaika kupitia rasilimali zao.

Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo, Maliasili, na Mifugo wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. James Kabarebe alisema amefarijika na hatua hiyo iliyofikiwa kwani waliisubiri muda mrefu na ni imani yake kuwa tija kubwa itapatikana katika tasnia hiyo ya maziwa kupitia ushirikiano huo.


 Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (kulia) na Waziri wa Kilimo, Maliasili, na Mifugo wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. James Kabarebe wakisaini hati ya makubaliano ya kushirikiana kuendeleza tasnia ya maziwa baina ya hizo katika hafla iliyofanyika Visiwani Zanzibar  Januari 12, 2024 sambamba na Sherehe za Kutimiza Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (kulia) na Waziri wa Kilimo, Maliasili, na Mifugo wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. James Kabarebe wakipeana mikono punde baada ya kusaini hati ya makubaliano ya kushirikiana kuendeleza tasnia ya maziwa baina ya nchi hizo mbili katika hafla iliyofanyika Visiwani Zanzibar  Januari 12, 2024 sambamba na Sherehe za Kutimiza Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (wa tatu kutoka kushoto) na Waziri wa Kilimo, Maliasili, na Mifugo wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. James Kabarebe (wa pili kutoka kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali punde baada ya tukio la kusaini hati ya makubaliano ya kushirikiana kuendeleza tasnia ya maziwa baina ya nchi hizo mbili katika hafla iliyofanyika Visiwani Zanzibar  Januari 12, 2024 sambamba na Sherehe za Kutimiza Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Wa nne kutoka kulia ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba.



WAFUGAJI JONGOO BAHARI MTWARA WAASWA KUFUATA TARATIBU

 

Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji upande wa mazao ya bahari Dkt. Hamis Nikuli amewataka wafugaji jongoo bahari mkoani Mtwara kufuata sheria na taratibu za ufugaji wa zao hilo.

Dkt. Nikuli ameyasema hayo wakati wa zoezi la ujazaji wa dodoso linalohusu taarifa za wavuvi na wakuzaji viumbe maji  lililofanyika Januari 12, 2024 kwenye kampasi ya Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) iliyopo eneo la Mikindani mkoani humo.

"Tunahamasisha sana ufugaji wa jongoo bahari kwa sababu wale waliopo kwenye maji ya asili kwa huku Tanzania bara hawaruhusiwi kuvuliwa kwa sasa lakini ni lazima kila mtu au kikundi kifuate taratibu zilizopo kwenye kibali chake na isitokee mmoja wenu akatumia kibali cha mwenzie kuvuna jongoo hao" Amesema Dkt. Nikuli.

Dkt. Nikuli ameongeza kuwa ni lazima wafugaji jongoo bahari wote waliopo mkoani humo kuhakikisha wanatoa taarifa sahihi za idadi ya jongoo bahari wanaowafuga na kuwa waaminifu pindi wanapopewa kibali cha kuvuna ili wavune idadi waliyoidhinishiwa kwenye vibali hivyo.

Akizungumzia kuhusu madodoso ya taarifa za wavuvi na wakuzaji viumbe maji waliopo mkoani humo, Dkt. Nikuli amesema kuwa hatua hiyo imetokana na kutopatikana kwa haraka na usahihi wa taarifa za mvuvi mmoja mmoja, kikundi au kampuni inayojihusisha na uvuvi au ukuzaji viumbe maji pindi zinapohitajika kwa ajili ya madhumuni mbalimbali ikiwemo mikopo inayotolewa na Taasisi za kifedha na wadau wa maendeleo.

" Hadi sasa Mkoa wa Mtwara una vikundi 97 vinavyofuga na vinavyotarajia kufuga jongoo bahari na kwa ujumla dodoso hili limegusia taarifa za watu binafsi, kikundi na kampuni zinazojishughulisha na Uvuvi au Ukuzaji viumbe maji na kwa kuwa nyie mnajishughulisha na ufugaji jongoo bahari, taarifa mnazojaza zitaturahisishia kuelekeza rasilimali tunazopata kutoka kwa wadau wetu wa sekta kwa mujibu wa mahitaji mliyonayo" Amesisitiza Dkt. Nikuli.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Vikundi vya wafugaji wa jongoo bahari eneo la Mtwara Mikindani Bw. Ramadhan Banda amefurahishwa na hatua hiyo ya Wizara kukusanya taarifa zao huku akiweka wazi kuwa wamepata somo kubwa la namna bora ya kudhibiti soko la jongoo bahari ikiwa ni pamoja na kuwadhibiti wauzaji wa zao hilo kiholela.

"Nimefurahi pia kusikia hakuna mtu anayeruhusiwa kuvuna jongoo bahari bila kibali kutoka kwenu (wizarani) kwa sababu hatua hiyo itamaliza changamoto ya wizi wa zao hilo ambapo wengi wamekuwa wakiibuka sokoni na jongoo waliyowaiba kwenye vizimba vya wenzao" Ameongeza Bw. Banda.

Timu ya Wataalam kutoka Wizara ya mifugo na Uvuvi inaendesha zoezi la ujazaji madodoso ya Taarifa za Wavuvi na wakuzaji viumbe maji Mkoani kwenye mikoa ya Mtwara na Lindi kwa lengo la kuwa na taarifa sahihi za makundi hayo pindi wanapohitaji  kuwawezesha nyenzo mbalimbali za uendeshaji wa shughuli zao.


Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Viumbe Maji (Bahari) Dkt. Hamis Nikuli akizungumza na vikundi vya Ufugaji jongoo bahari wa eneo la Mtwara Mikindani (hawapo pichani)  wakati wa zoezi la Ujazaji wa dodoso linalohusu taarifa za Wavuvi na wakuzaji viumbe maji waliopo mkoani Mtwara lililofanyika Januari 12, 2024, Kulia kwake ni Mwenyekiti wa vikundi hivyo Bw. Ramadhan Banda na kushoto kwake ni Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Janeth Rukanda.

Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi  Kresensia Mtweve (kulia) akiweka taarifa za mmoja wa wafugaji jongoo bahari  kwenye dodoso wakati wa zoezi la ujazaji wa taarifa hilo lililofanyika Januari 12, 2024,  Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya  Mikindani mkoani Mtwara.

Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi Janeth Rukanda (kushoto) akifafanua jambo wakati wa zoezi la ujazaji wa dodoso la wavuvi na wakuzaji viumbe maji lililofanyika Januari 12, 2024,  Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya  Mikindani mkoani Mtwara.


UTEKELEZAJI WA UFUGAJI SAMAKI KWA VIZIMBA WAANZA ZIWA TANGANYIKA


Na, Edward Kondela

Serikali imeanza utekelezaji wa ufugaji samaki kwa njia ya vizimba katika Ziwa Tanganyika baada ya mpango huo kuonesha mafanikio makubwa katika Ziwa Victoria.

Akizungumza (11.01.2024) katika Mwalo wa Kasanga uliopo Wilaya ya Kalambo Mkoani Rukwa, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti amesema tayari wizara imeanza kutoa elimu kwa wavuvi wa ukanda wa Ziwa Tanganyika kabla ya kufikisha vizimba hivyo na mbegu bora za samaki.

Mhe.Mnyeti ameongeza kuwa kwa sasa serikali imetenga Shilingi Bilioni 20 kwa ajili uwekaji vizimba katika Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika kwa sababu ufugaji wa samaki unakua kwa kasi maeneo mbalimbali duniani kutokana na upungufu wa samaki waliopo kwenye maji ya asili yakiwemo mabonde, maziwa, mito na bahari kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ya uharibifu wa mazingira, ongezeko la watu na uharibifu wa mazalia ya samaki.

Ameongeza kuwa ili kunusuru upungufu wa samaki katika masoko ya ndani na nje ya nchi serikali imeamua kuanza kusambaza vizimba kwa wavuvi wa Ziwa Tanganyika ambavyo vitatolewa kwa mkopo nafuu usio na riba.

Awali akiwa katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Rukwa alipokutana na mkuu wa mkoa huo Mhe. Charles Makongoro Nyerere alimueleza azma ya serikali ya kulipumzisha Ziwa Tanganyika katika shughuli zozote za uvuvi kwa kipindi cha miezi mitatu kila mwaka kwa miaka mitatu mfululizo ambapo kwa mwaka huu litafungwa kuanzia tarahe 15 mwezi Mei hadi 15 mwezi Agosti 2024 ili kupisha samaki waweze kuzaliana.

Amesema kupumzishwa kwa shughuli za uvuvi katika ziwa hilo ni utekelezaji wa Mkataba wa Kikanda wa Usimamizi wa Uvuvi endelevu katika ziwa hilo na bonde lake ambapo nchi wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika kwa maana ya Burundi, Jamhuri ya Kidemokeasia ya Kongo, Tanzania  na Zambia zilitia saini mkataba huo Tarehe 9 Mwezi Desemba Mwaka 2021 kwenye mkutano wa 9 wa mawaziri wa nchi hizo.

Amebainisha kuwa kupumzishwa kwa ziwa hilo kutatoa fursa kwa wavuvi kujifunza namna bora ya kufuga samaki pamoja na kuwa na njia nyingine za kujipatia kipato zikiwemo za kufuga mifugo na kilimo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Charles Makongoro amesema mpango wa serikali kuhamasisha kufuga samaki kwa njia ya vizimba ni mzuri kwa kuwa wavuvi watapata fursa ya kujifunza namna nyingine ya kuendeleza biashara ya samaki na kwamba  mkoa utasimamia utekelezaji huo ili wananchi waendelee kunufaika na mazao ya uvuvi.

Baadhi wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi katika Ziwa Tanganyika wakiwa kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti katika Kata ya Kasanga, wamepongeza juhudi za serikali kwa kuwatafutia njia mbadala ya kuendeleza Sekta ya Uvuvi na kuiomba serikali kuzidi kutoa elimu zaidi juu ya ufugaji kwa njia ya vizimba.

Aidha, wamekiri kwamba kwa sasa mazao ya samaki yamepungua kwa kiasi kikubwa katika ziwa hilo na samaki wanaopatikana ni wadogo ambao wanahitaji kubakia ziwani ili kukua.

Naibu Waziri Mnyeti amepata pia fursa ya kushuhudia maendeleo ya ujenzi wa soko la samaki katika Kata ya Kasanga linalogharimu Shilingi Bilioni 1.4 na kuwataka wananchi hao mara soko litakapokamilika ni vyema wakaliendesha wao wenyewe na kulifanya la kisasa zaidi. 


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti akizungumza na wadau wa uvuvi kwenye mkutano wa hadhara katika Kata ya Kasanga Wilaya ya Kalambo Mkoani Rukwa, akibainisha juu ya utekelezaji wa ufugaji samaki kwa njia ya vizimba katika Ziwa Tanganyika baada ya mpango huko kufanya vizuri Ziwa Victoria. Serikali imetenga Shilingi Bilioni 20 kwa ajili uwekaji vizimba katika Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika. (11.01.2024)

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti (katikati) akikagua maendeleo ya ujenzi wa soko la samaki katika Kata ya Kasanga Wilaya ya Kalambo Mkoani Rukwa alipofanya ziara ya kkazi ya siku moja kukagua maendeleo ya Sekta ya Uvuvi na kutaka mara soko likikamilika wananchi wa eneo hilo waliendeshe kisasa ili liwe na tija kwako. Soko hilo linagharimu Shilingi Bilioni 1.4 (11.01.2024)

Mkurugenzi Msaidizi wa Undelezaji Rasilimali za Uvuvi Bi. Merisia Mparazo akizungumza na wananchi wakati akimwakilisha Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), kwenye mkutano wa hadhara katika Mwalo wa Kasanga Wilaya ya Kalambo Mkoani Rukwa akiwakumbusha juu ya shughuli za uvuvi zinazofuata sheria. (11.01.2024)


RAS MWANZA AIPONGEZA WIZARA KWA KUWA NA MKAKATI WENYE TIJA KWA KUWAJENGEA VIJANA KUJIAJIRI


Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Bw. Balandya Elikana ameipongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuweka mkakati wenye tija kwa vijana kwa kuwajengea kuweza kujiajiri kwa kutoa mikopo isiyo na riba ya pembejeo za vizimba, chakula cha samaki na vifaranga vya samaki kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo TADB.

Balandya ameyasema hayo ofisini kwake mara baada ya kupokea ugeni  kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi ukiongozwa na Afisa Uvuvi Mkuu Bi. Mkomanile Mahundi na kusema ufugaji kwenye vizimba utasaidia sana katika uzalishaji wa samaki.

Katika mazungumzo pia alitoa ushauri mpango huo wa ufugaji kwa njia ya vizimba ufanyike kwa awamu kutokana na wingi wa vikundi husika kutoka mikoa ya kanda ya ziwa.

"Serikali inayoongozwa na Mhe. Rais Samia imedhamiria kuwainua kundi la vijana kimaendeleo, mpango huu wa ufugaji wa kisasa wa samaki wataalamu kutoka wizarani ukiwawekea mazingira mazuri ya kazi utazidi kuwa na tija kwao kiuchumi", amefafanua Mtendaji huyo wa Mkoa wakati wa mazungumzo hayo.

Ameiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuweka ushirikiano na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ili kuhakikisha miradi hiyo inafanyiwa ufuatiliaji na kuwa endelevu na mwishowe inafikisha ndoto ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuona inawakomboa kiuchumi Wananchi hususani Vijana na wakinamama.

Kwa upande wake Afisa Uvuvi Mkuu Bi. Mkomanile Mahundi amesema lengo la kuja Mwanza ni kuainisha wanufaika wa mikopo ya pembejeo za ufugaji Samaki kwa Vizimba na kuwawezesha kukidhi vigezo vya mkopo wenye  masharti nafu na kushauri pale zitakapo bainika changamoto ili zoezi hilo liwe limekamilika kabla ya Januari 29 2024.

"Tutapita maeneo yote Mikoa ya Kanda ya Ziwa ambayo mradi huu wa ufugaji wa samaki kisasa kwa njia ya vizimba unafanyika ili tujiridhishe kwa kila hatua kabla ya kuwakabidhi wahusika wote waliokidhi vigezo vya mradi huu",amesisitiza Bi.Mahundi

Mkoa wa Mwanza una jumla ya vikundi 79 wakiwemo watu binafsi 11, kampuni 6, vijana 13 na vikundi 49.


Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Bw. Balandya Elikana akiongea jambo na wataalamu wa Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi mara baada ya kifika ofisini kwake kwa lengo la kujitambulisha kwa ajili ya zoezi la kuainisha wanufaika wa Mikopo ya pembejeo za ufugaji samaki kwa Vizimba katika Mkoa wa huo, Januari 11.2024, Afisa Uvuvi mkuu Bi. Mkomanile Mahundi (kushoto) na Afisa uvuvi Mkuu Bw. Fredrick Mussa (kulia). Wakimsikiliza katibu huyo, Mkoani Mwanza.

Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi,  Bw. Fredrick Mussa akitoa elimu na kuelezea faida ya kuomba mikopo ya pembejeo za vizimba kwa wanufaika (hawapo pichani) wa mkopo wa vizimba na pembejeo zake kwa vyama vya Ushirika, Vikundi na watu binafsi kwenye  Halmashauri ya Wilaya ya Nyamagana Mkoani  Mwanza, Januari 11.2024.

Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Bw. Balandya Elikana (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na maafisa Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Mkoa wa Mwanza mara baada ya kikao kifupi kilichofanyika ofisini kwake,  lengo likiwa ni pamoja na kueleza nia ya Wizara hiyo kwa kushirikiana  na benki ya maendeleo ya kilimo (TADB) ya kutoa mkopo wenye masharti  nafuu isiyo na riba kwa vikundi, vyama vya ushirika na watu binafsi ikijumuisha  Pembejeo za  vizimba, Chakula cha Samaki  Mkoani Mwanza Januari 11.2024.


ZIWA TANGANYIKA KUPUMZISHWA, SERIKALI YAPIGIA CHAPUO UVUVI WA VIZIMBA

 

Na. Edward Kondela

Serikali yaazimia kupumzisha shughuli za uvuvi katika Ziwa Tanganyika kwa kipindi cha miezi mitatu kwa miaka mitatu mfululizo ili kuongeza mazalia ya samaki na kuhamasisha ufugaji samaki kwa njia ya vizimba katika ziwa hilo.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti amebainisha hayo (10.01.2024) kwa nyakati tofauti wakati alipokuwa akiongea na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Katavi na wadau wa uvuvi katika mkoa huo wakiwemo wanaojishughulisha na shughuli za uvuvi katika Mwalo wa Ikola uliopo katika Wilaya ya Tanganyika.

Naibu Waziri Mnyeti amesema serikali imeazimia kupumzisha shughuli za uvuvi katika Ziwa Tanganyika kuanzia tarehe 15 Mei hadi tarehe 15 Agosti Mwaka 2024 ikiwa ni utekelezaji wa Mkataba wa Kikanda wa Usimamizi wa Uvuvi endelevu katika ziwa hilo na bonde lake ambapo nchi wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika kwa maana ya Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Tanzania  na Zambia zilitia saini mkataba huo Tarehe 9 Mwezi Desemba Mwaka 2021 kwenye mkutano wa 9 wa mawaziri wa nchi hizo.

Mhe. Mnyeti amebainisha kuwa lengo la mkataba huo kwa nchi hizo ni kutoa muda kwa samaki kuzaliana ambapo kutokana na tafiti zilizofanywa na Tasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) katika kipindi cha Mwezi Mei na Agosti samaki huwa wanazaliana kwa wingi.

“Tunapumzisha ziwa hili kwa sababu samaki wanaenda kuisha ziwani ili tupishe wazaliane baada ya muda wa miezi mitatu tutaendelea na shughuli za uvuvi na jambo hili litakuwa la kila mwaka ili kuruhusu mazalia ya samaki ni mkataba wa nchi zinazozunguka Ziwa Tanganyika.” Amesema Mhe. Mnyeti

Aidha, ametaka wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi katika ziwa hilo kupatiwa elimu ya kutosha na pia serikali itaweka nguvu kwa wananchi hao kujikita katika ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba kwenye ziwa hilo huku wakiacha samaki wa asili waliopo ziwani kuzaliana.

Ameongeza kuwa serikali itafanya tathmini ya kupumzisha shughuli za uvuvi katika maziwa mengine kila baada ya muda kwa kipindi ambacho itaona inafaa ili samaki waweze kuzaliana kwa wingi ambapo kwa sasa inaanza na Ziwa Tanganyika.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko amesema uongozi wa mkoa huo uko tayari kusimamia utekelezaji huo ambao tayari umeanza kutekelezwa kwa mara ya kwanza Mwaka 2023 na nchi wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika ambapo Tanzania itatekeleza kwa mara ya kwanza mwaka huu. 

Mhe. Mrindoko amewataka wakazi wa mkoa huo kutoa ushirikiano kwa kuwa ni kwa manufaa yao na kwamba matarajio ni baada ya kufungwa Ziwa Tanganyika kwa miezi mitatu kutakuwa na ongezeko la samaki na katika kipindi cha miaka mitatu serikali itaweza kupata tathmini ya ongezeko la samaki.

Nao baadhi ya wananchi katika Mwalo wa Ikola Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi wamepokea taarifa hiyo na kuahidi kushirikiana na serikali wakati wote wa miezi mitatu ambapo shughuli za uvuvi zitakapokuwa hazifanywi katika Ziwa Tanganyika ili kupisha samaki kuzaliana kwa wingi.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kiwango cha samaki katika Ziwa Tanganyika kimekuwa kikipungua kila mwaka huku baadhi ya wavuvi wakitoa ushuhuda wa kupotea kabisa baadhi ya samaki katika ziwa hilo.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti akizungumza na wananchi wanaojishughulisha na uvuvi katika Mwalo wa Ikola uliopo Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi juu ya maamuzi ya serikali kulipumzisha Ziwa Tanganyika kwa shughuli za uvuvi kwa miezi mitatu kuanzia tarehe 15 Mwezi Mei hadi tarehe 15 Mwezi Agosti Mwaka 2024. (10.01.2024)

Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Ambakisye Simtoe akifafanua hoja mbalimbali kwa wananchi wa Mwalo wa Ikola uliopo Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi, baada ya wananchi hao kupatiwa taarifa juu ya upumzishwaji wa Ziwa Tanganyika kwa shughuli za uvuvi ili kuacha samaki wazaliane. (10.01.2024)


Mkurugenzi Msaidizi wa Undelezaji Rasilimali za Uvuvi Bi. Merisia Mparazo akizungumza na wananchi wakati akimwakilisha Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwenye mkutano wa hadhara katika Mwalo wa Ikola juu ya upumzishaji wa shughuli za uvuvi katika Ziwa Tanganyika kwa miezi mitatu. (10.01.2024)


ZIWA TANGANYIKA KUPUMZISHWA ILI KUWEZESHA SAMAKI KUZALIANA


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega ametangaza mpango wa Serikali wa kupumzisha  shughuli za uvuvi katika ziwa Tanganyika kwa miezi mitatu ili kuwezesha samaki kuzaliana na kuongeza tija kwa wavuvi wanaofanya shughuli zao ziwani humo.

Waziri Ulega  ametoa kauli ya serikali kwa nyakati tofauti ambapo awali alitoa kauli hiyo akizungumza na wadau wa uvuvi kwenye ofisi ya Mkuu wa mkoa Kigoma na baadaye kuzungumza na wananchi na wadau wanaofanya shughuli za uvuvi kwenye Mwalo wa Katonga Manispaa ya Kigoma Januari 9, 2024.

Akiwa kwenye kikao cha ndani na wadau wa uvuvi Waziri Ulega alisema kuwa utekelezaji wa mpango huo utaanza rasmi Mei 15 hadi Agosti 15 mwaka huu na hiyo ikiwa ni Utekelezaji wa Mkataba wa Kikanda wa Nchi Wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika unaoweka hatua na taratibu za usimamizi endelevu wa shughuli za uvuvi katika ziwa hilo.

Akieleza sababu ya maamuzi hayo alisema ni kutokana na utafiti kubainisha kuwa kumekuwepo na upungufu mkubwa wa samaki na dagaa katika ziwa Tanganyika kunakotokana na ongezeko kubwa la uvuvi usio endelevu uliopelekea uharibifu wa mazalia ya samaki.

"Pamoja na kufunga shughuli za uvuvi katika ziwa Tanganyika, Serikali ya Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imeanza kutekeleza njia mbadala za kuwawezesha wananchi kujiendeleza kiuchumi katika ziwa Tanganyika ikiwemo kukopesha vikundi maboti na vizimba kwa ajili ya miradi ya ufugaji wa samaki na tayari imetenga shilingi milioni 200 kupitia Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi (TAFIRI) kubainisha maeneo yanayofaa kwa ufugaji huo,' alisema Waziri Ulega

Aliongeza kuwa Mhe. Rais, Dkt. Samia ametoa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuanzisha kituo cha uzalishaji wa vifaranga vya samaki bora mkoani humo kwa ajili ya kuwawezesha wafugaji wa samaki kwa njia ya vizimba kuwa na uhakika wa kupata vifaranga bora wakati wote.

Halikadhalika alifafanua kuwa hatua hiyo ya kupumzisha ziwa sio jambo geni kwa sababu linafanyika katika Mikoa ya ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi ambapo wanafunga miamba kwa ajili ya uvuvi wa pweza na matokeo yameonesha kuwa wakati wa kufungua tani takriban 100 zimekuwa zikipatikana.

Aidha, alitumia nafasi hiyo pia kuwahimiza wananchi mkoani humo kuchangamkia fursa hiyo ya mikopo ya vizimba na maboti ili waweze kujikwamua kiuchumi katika nyakati hizo za upumzishaji wa shughuli za uvuvi katika ziwa hilo.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti alisema kuwa mpango huo una manufaa makubwa kwa wananchi na taifa kwa ujumla na ni muhimu kuharakisha utekelezaji wake ili kunusuru ziwa hilo ambalo uzalishaji wake umeshuka sana.

Mnyeti alisema kuwa zipo nchi duniani zimetekeleza mpango huo na faida kubwa imeonekana kwa kuongeza mazao ya uvuvi, kuongeza mapato kwa wavuvi na serikali kwa kiwango kikubwa.

Awali Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uvuvi Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ambakisye Simtoe akiwasilisha hali ya uvuvi na wingi wa samaki ziwa Tanganyika alisema kuwa umepungua na kwa sasa hali sio nzuri.

Ambakisye alisema kuwa mwaka 1995 takwimu zilikuwa zikionyesha kuwepo kwa wingi wa samaki tani 197,493 zinazoweza kuvuliwa kwa mwaka ambapo kiwango hicho kimeshuka na kufikia tani 144,690. Pia, uvuvi umeshuka kutoka tani 104,178 mwaka 2020 na kufikia tani 85,180.

Naye Mkurugenzi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais- Mazingira, Paul Deogratius alisema kuwa mkataba mdogo wa nchi zinazozunguka ziwa Tanganyika ibara ya saba wa mwaka 2021 unaitaka Tanzania kutekeleza ulinzi na utunzaji wa rasilimali za ziwa Tanganyika ikiwemo shughuli za uvuvi.

Deogratius alisema kuwa nchi za Burundi,Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Zambia zilitekeleza mkataba huo mwaka jana isipokuwa Tanzania jambo ambalo halileti picha nzuri kwenye uhusiano na ushirikiano wa kimataifa.

Wabunge wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Kilumbe Ng'enda wa Kigoma Mjini na Mhe. Josephine Genzabuke wakizungumza kwenye mkutano wa hadhara wa Waziri Ulega uliofanyika katika mwalo wa Katonga wameunga mkono mpango huo wa serikali na kusema utaleta faida kubwa kwa sekta ya uvuvi.

Miongoni mwa Nchi Wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika sambamba na Tanzania ni pamoja na Zambia, Burundi na Jamhuri ya Demokrasia ya Congo ambao wao walishaanza kutekeleza zoezi hilo la upumzishaji wa ziwa Mwaka jana (2023).


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akizungumza na wananchi (hawapo pichani) wanaofanya shughuli za uvuvi kwenye Ziwa Tanganyika alipokutana nao katika Mwalo wa Katonga Manispaa ya Kigoma Januari 9, 2024.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akisalimiana na baadhi ya kina mama wanaojishughulisha na uvuvi wakati wa mkutano uliofanyika kwenye Mwalo wa Katonga Manispaa ya Kigoma Januari 9, 2024.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Watendaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi muda mfupi baada ya kumaliza kikao na wadau wa uvuvi (hawapo pichani) kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Januari 9, 2024. Kushoto kwake ni Naibu Waziri was Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti. Wa kwanza kulia ni Naibu Katibu Mkuu, Sekta ya Uvuvi, Bi. Agnes Meena.