Nav bar

Jumatatu, 31 Mei 2021

MATEMBEZI YA HIARI NA UPANDAJI MITI ILIYOFANYIKA KATIKA ENEO LA MEDELI TAREHE 29.05.2021

*Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wakiwa kwenye Matembezi ya Hiari - Mazingira Walk kuanzia viwanja vya Bunge kuelekea eneo la Medeli kwa ajili ya zoezi la Upandaji Miti lililoongozwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mh.Selemani Jafo leo tarehe (29.05.2021) Jiji Dodoma *


* Katibu Mkuu Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah (mwenye T-shirt nyeupe) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Sekta ya Uvuvi kabla ya kuanza zoezi la Upandaji miti katika eneo la Medeli lillozinduliwa leo tarehe (29.05.2021)Jiji Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mh. Selemani Jafo. Wengine ni Afisa Uvuvi Bw. Makorwa Hamadi (wa kwanza kushoto), Mkuu wa kitengo cha Mazingira (Uvuvi) Bw.Melton Kalinga (wa kwanza kulia) akifutiwa  na Afisa Uvuvi Mkuu Bi. Magreth Dominick


Gg
























Jumatatu, 24 Mei 2021

TUTAENDELEA KUBORESHA MASHAMBA YA SERIKALI – ULEGA.

Naibu Waziri wa mifugo na uvuvi Mhe. Abdalla Ulega amesema Wizara hiyo ina mkakati wa miaka mitatu (2020/2021 – 2022/2023) ambao umelenga kuendeleza mashamba kwa kuongeza ng’ombe wazazi na kuimarisha huduma za uhimilishaji ili kupata ngombe bora na wenye tija.

Ulega aliyasema hayo  bungeni Mei 24, 2021 wakati akijibu swali la Mbunge wa Makete, Mhe. Festo Sanga ambaye alitaka kufahamu mkakati wa Serikali wa kuendeleza Shamba la Mifugo la Kitulo.

Mhe. Ulega alisema kuwa katika kutekeleza Mkakati huo Wizara kupitia bajeti ya mwaka 2021/2022 imenunua madume matano (5) ya ng’ombe wazazi kutoka shamba la Shafa Farm lililopo mkoani Iringa, kilo 400 za mbegu za malisho kutoka Marekani na nyingine 100 kutoka Kenya kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa malisho.  

Alisema, shughuli nyingine ni uhimilishaji ambapo ng’ombe 135 wamehimilishwa na ununuzi wa tenki la kupoozea maziwa lenye ujazo wa lita 3,000 ambapo utaratibu wa manunuzi unakamilishwa.

“Shamba la Kitulo linahitaji uwekezaji wa kiasi cha shilingi bil. 6.6 ili kufikia kiwango cha juu cha uzalishaji, na uwekezaji huu utaendela kufanywa na Serikali kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo.” Alisema Ulega

Aidha akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Makete, Mhe. Festo Sanga aliyetaka kufahamu iwapo Wizara ya Mifugo na Uvuvi ipo tayari kushirikiana na benki ya maendeleo ya kilimo (TADB) ili kuendesha shamba ilo kwa tija zaidi na kujua siku ambayo maslahi ya wafanyakazi yatalipwa na vifaa kununuliwa, Mhe. Ulega alisema juu ya uwekezaji wapo tayari na milango yetu ipo wazi, karibuni tuweze kujadili jambo hilo, na jambo la kuboresha maslahi na kununua vifaa ni sehemu ya pesa zilizopangwa kutumika kwenye bajeti hii, hivyo hilo tunalielekea pia.

Kwa upande wake Mbunge wa Chalinze Mhe. Ridhiwani Kikwete   alitaka kufahamu siku Serikali itapima eneo la mifugo la Ruvu na kulikabidhi kwa Halmashauri ya Chalinze ambapo Mhe. Ulega alisema Serikali imeshapima na kutoa kipande cha ardhi chenye ukubwa wa hekta 2,208 kutoka Ranchi ya Ruvu kwa ajili ya matumizi ya wananchi. 

Aliongeza kuwa, Halmashauri  ya Wilaya ya  Chalinze ilikatiwa hekta 1,488  kwa ajili ya  vijiji sita ambavyo ni; kijiji cha Ruvu Darajani hekta 200; kijiji cha  Kidogozero hekta 200; kijiji cha Kitonga hekta 480; kijiji cha Magulumatali hekta 200; kijiji cha Vigwaza hekta 8 na kijiji cha  Milo-Kitongoji cha Kengeni hekta 400. 

Aidha, Serikali imepima na kutoa kipande cha ardhi chenye ukubwa wa hekta 120 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo kwa ajili ya vijiji vitatu vya Kidomole hekta 40; Fukayosi hekta 40 na Mkenge hekta 40. Pia, Serikali imepima na kutoa ardhi yenye ukubwa wa hekta 600 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha vijijini kwa ajili ya kijiji cha Mperamumbi Kitongoji cha Waya.

Ijumaa, 21 Mei 2021

SERIKALI YASISITIZA UPATIKANAJI WA TAARIFA SAHIHI ZA UVUVI MDOGO

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imesisitiza upatikanaji wa taarifa sahihi za uvuvi mdogo nchini  kwa kuangaza taarifa za wavuvi wadogo zilizofichika ili ziweze kutumika kwa mipango ya maendeleo endelevu kwa lengo la kukuza Uchumi.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Uvuvi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwenye hotuba yake ya ufunguzi wa warsha ya wadau wa sekta ya uvuvi ya kupitia matokeo ya utafiti wa mchango wa Uvuvi mdogo iliyosomwa kwa niaba yake na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani (DRTE) Dkt. Erastus Mosha mjini Morogoro (21.5.2021).

Akisoma hotuba hiyo, Mkurugenzi amewakumbusha wadau kuwa Uvuvi ni sayansi, hivyo usimamizi wa rasilimali hiyo ni muhimu na unahitaji taarifa za kutosha za kitafiti ili kufikia malengo ya kuwa na Uvuvi endelevu nchini.

Alizitaja baadhi ya changamoto zinazoikabili sekta ya Uvuvi kwa muda mrefu kuwa ni kukosekana kwa taarifa sahihi za mavuvi, zana haramu, idadi ya wavuvi, vyombo vya Uvuvi na nyinginezo.

Pia alisema ana matumaini makubwa kuwa matokeo ya utafiti huo wa kuangaza taarifa za uvuvi zilizofichika yatasaidia kuboresha mipango ya sekta ya Uvuvi nchini kuendana na kasi ya maendeleo ya viwanda na kuongeza mchango wa sekta kwenye pato la Taifa kutoka asilimia 1.7 hadi asilimia 3.5 ifikapo mwaka 2025.

Aidha katika hotuba yake mgeni rasmi aliwafahamisha wadau kuwa,mwaka 2016 Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi iliingia makubaliano na Shirika la Kilimo na Chakula (FAO) ili kutekeleza mradi wa kuwezesha utekelezaji wa Mwongozo wa Hiari wa Kuhakikisha Uvuvi Mdogo unakuwa Endelevu katika Muktadha wa Uhakika wa Chakula na Kuondoa umasikini.

Aliongeza kuwa matokeo mazuri yanayoendelea kutokea yanatokana na Mradi wa kutekeleza Mwongozo wa Wavuvi Wadogo (SSF Guidelines),ambapo Wizara kwa mara nyingine tena ilisaini makubaliano ya  kutekeleza Mradi huo wa kuimarisha mchango wa Uvuvi Mdogo kwa usalama wa Chakula na Maisha Endelevu.

Kwa upande wake kiongozi wa timu ya utafiti Dkt. Paul Onyango kutoka Chuo Kikuu cha Dar  es salaam anasema utafiti huo uliofadhiliwa na FAO ulianza Mwaka 2018, na umefanyika kwenye takribani nchi 40 Duniani.

Akigusia matokeo ya utafiti huo, Dkt. Onyango anasema kuwa kuna taarifa nyingi zilizofichika ambazo zinasababisha thamani ya mchango wa uvuvi mdogo kiuchumi kuonekana ndogo sana tofauti na uhalisia wenyewe.

Dkt. Onyango anabainisha mapendekezo ya kukabiliana na changamoto hiyo kuwa ni vyema Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) kuwa na bajeti maalum ya ukusanyaji takwimu za wavuvi wadogo, kuongeza wakusanya takwimu wenye weledi wa kazi hiyo na pia kutoa elimu kwa wavuvi kuhusu umuhimu wa kutoa taarifa sahihi kwa Serikali.

Mvuvi mdogo Bw. Peter Sumuni kutoka ziwa Nyasa akizungumzia sababu ya wao wavuvi kutokutoa takwimu sahihi kwa maafisa Uvuvi wa maeneo yao, anasema kuwa hawana elimu ya kutosha ya umuhimu wa takwimu hizo pia ushirikiano wao na maafisa Uvuvi hauridhishi.

Aidha Bi.Sijali Hemedi kutoka Kilwa ambaye ni mkusanya takwimu ameelezea kuwa changamoto ni uchache wa wakusanyaji wa takwimu pamoja na uwezeshwaji wa rasilimali Fedha kwa ajili ya kazi hiyo.

Ili kufanikisha lengo la kuwa na Uvuvi Endelevu kwa ajili ya kukuza uchumi, Bw. Yusuph Semuguruka kutoka ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anasisitiza ushirikiano kati ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi na TAMISEMI ikiwa ni pamoja na kufuata taratibu za kupeana taarifa katika utekelezaji wa shighuli mbalimbali za sekta ya Uvuvi nchini.


Mgeni rasmi,Kaimu Mkurugenzi, idara ya utafiti, Mafunzo na Ugani (DRTE) Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Erastus Mosha akisoma hotuba ya ufunguzi wa warsha ya wadau wa sekta ya uvuvi ya uwasilishwaji wa matokeo ya utafiti wa mchango wa uvuvi mdogo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi.Warsha hiyo inayofanyika (20-21.5.2021) kwenye hoteli ya Edema mjini Morogoro imehusisha wadau mbalimbali wakiwemo wavuvi, wakusanya takwimu, watafiti na watumishi kutoka sekta ya Uvuvi. 


Mwenyekiti wa Kikosi Kazi cha Kitaifa cha Maandalizi ya Mpango wa Utekelezaji wa Mwongozo wa Hiari wa Kuendeleza Sekta ya Uvuvi Mdogo nchini, Alhaj Yahya Mgawe akitoa maelezo ya awali kuhusu suala la Uvuvi mdogo nchini kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufungua warsha ya  wadau wa sekta ya uvuvi ya uwasilishwaji wa matokeo ya utafiti wa mchango wa uvuvi mdogo inayofanyika kwenye Hoteli ya Edema iliyopo mjini Morogoro (20-21.5.2021).Utafiti huo umefanywa na Chuo Kikuu cha Dar es salaam kwa ufadhili wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO). 


Bw. Yusuph Semuguruka kutoka Idara ya Uratibu wa Sekta Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) akitoa salamu za ofisi hiyo kabla ya kukaribishwa kwa Mgeni rasmi kufungua warsha ya wadau wa sekta ya uvuvi ya uwasilishwaji wa matokeo ya utafiti wa mchango wa uvuvi mdogo inayofanyika kwenye Hoteli ya Edema iliyopo mjini Morogoro (20-21.5.2021) ambapo alisisitiza ushirikiano kati ya Wizara na TAMISEMI katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Uvuvi nchini.Utafiti huo umefanywa na Chuo Kikuu cha Dar es salaam kwa ufadhili wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO). 


Baadhi ya watafiti Dkt. Paul Onyango kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaam (kulia) ambaye ndio kiongozi wa timu ya watafiti na Bi. Fatma Sobbo wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi (hayupo pichani) wakati wa ufunguzi wa warsha ya wadau wa sekta ya uvuvi ya uwasilishwaji wa matokeo ya utafiti wa mchango wa uvuvi mdogo inayofanyika kwenye Hoteli ya Edema iliyopo mjini Morogoro (20-21.5.2021). Utafiti huo umefanywa na Chuo Kikuu cha Dar es salaam kwa ufadhili wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO). 


Mgeni rasmi, Kaimu Mkurugenzi, idara ya utafiti, Mafunzo na Ugani (DRTE) Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Erastus Mosha kwenye picha ya pamoja (waliokaa,katikati) mara baada ya ufunguzi wa warsha ya wadau wa sekta ya uvuvi ya uwasilishwaji wa matokeo ya utafiti wa mchango wa uvuvi mdogo inayofanyika kwenye Hoteli ya Edema iliyopo mjini Morogoro (20-21.5.2021). Utafiti huo umefanywa na Chuo Kikuu cha Dar es salaam kwa ufadhili wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) ambapo utafiti huo umependekeza serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) kuwa na bajeti maalum ya utafiti, kuwa na wakusanya takwimu wenye weledi pamoja na utoaji wa elimu kwa wavuvi ikilenga kuwaelimisha umuhimu wa kutoa takwimu sahihi.


Alhamisi, 20 Mei 2021

WASAMBAZAJI NA WAUZAJI WA DAWA ZA MIFUGO WATAKIWA KUZINGATIA UTARATIBU ULIOWEKWA NA SERIKALI

Wauzaji na wasambazaji wa madawa ya mifugo wametakiwa kuzingatia utaratibu ambao umewekwa na Serikali kupitia Baraza la Veterinari Tanzania ili kutoa huduma stahiki kwa wafugaji.

Hayo yalisemwa na Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania, Dkt. Bedan Masuruli  wakati wa kikao na wauzaji na wasambazaji wa dawa kilichojadili kuhusu changamoto zinazohusu tasnia ya Mifugo kwenye uuzaji na udhibiti wa madawa  kilichofanyika  Jijini Dar es Salaam Mei 19, 2021.

Dkt. Masuruli alisema kuwa bado lipo tatizo kwa baadhi ya wauzaji na wasambazaji wa madawa hayo kutozingatia taratibu ambazo zimewekwa na hivyo kusababisha madhara kwa wafugaji kwa kutopata huduma stahiki.

Aliongeza kuwa wauzaji na wasambazaji wa madawa hayo wanatakiwa kufuata na kuzingatia utaratibu uliowekwa kwa kuhakikisha madawa yote ya mifugo yanauzwa sehemu ambayo ni sahihi na imesajiliwa na kutambulika na Baraza la Veterinari Tanzania.

Aidha, Dkt. Masuruli aliwahimiza wamiliki hao kuwatumia wataalam wa mifugo katika kutoa huduma hizo kwani kwa kutofanya hivyo kunaweza kusababisha madhara makubwa kwa wafugaji na hatua zitachukuliwa kwa yeyote atakayekiuka sheria na taratibu zilizowekwa.

Dkt. Masuruli aliendelea kusema kuwa Baraza litaendelea kuwaelimisha wauzaji na wasambazaji wa madawa ya mifugo ili waweze kujua sheria, kanuni na taratibu ili waweze kutoa tiba stahiki kwa wafugaji pale wanapohitaji huduma hiyo.

Katika kikao hicho wauzaji na wasambazaji wamekubaliana kwa pamoja kudhibiti uingizwaji na usambazaji wa madawa feki ambayo yamekuwa yakitumiwa na wafugaji kwa kutokujua na kusababisha mifugo yao kutopona na mfugaji kudhoofika kiuchumu.

Naye Mwenyekiti wa kikao hicho ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya MULTIVET, Dkt. Henry Ruhinguka alisema lipo tatizo la dawa hizo kuuzwa maeneo ya wazi kama minadani ambayo sio sahihi kisheria.

Dkt. Ruhinguka alitumia fursa hiyo kuwahimiza wauzaji na wasambazaji wa madawa hapa nchini kushirikiana na serikali kuhakikisha wanadhibiti tatizo la madawa kuuzwa bila utaratibu unaotakiwa na kuhakikisha wanawadhibiti watu wanaoingiza madawa feki yanayokuja kuleta matatizo kwa wafugaji na kuwarudisha nyuma kiuchumi.


Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania, Dkt. Bedan Masuruli akisisitiza jambo wakati wa kikao kilichojadili kuhusu changamoto zinazohusu tasnia ya Mifugo kwenye uuzaji na udhibiti wa madawa. Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Baraza la Veterinari Temeke Mkoani Dar es Salaam. (19.05.2021)* 

 



Baadhi ya wajumbe wa kikao kilichoitishwa na Baraza la Veterinari kilichojadili kuhusu changamoto zinazohusu tasnia ya Mifugo kwenye uuzaji na udhibiti wa dawa feki wakisikiliza hoja mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa zinazohusu tasnia ya Mifugo kwenye uuzaji na udhibiti wa madawa. Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Baraza la Veterinari Temeke Mkoani Dar. es Salaam. (19.05.2021)

 

SERIKALI KUWEKA UTARATIBU WA KUVUA KAMBAMITI*

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeweka utaratibu wa kuvua kambamiti kwa wavuvi wakubwa na wadogo ili kufanya kambamiti waweze kuzaliana na kukua.

Hayo yamebainishwa leo bungeni na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (Mb) wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Kibiti Mhe. Twaha Ally Mpembenwe, ambaye alitaka kufahamu ni lini serikali itatoa uamuzi wa kuwaruhusu wavuvi wa kambamiti kuvua kuanzia mwezi Desemba hadi Julai kila Mwaka.

Alisema, utaratibu huo wa kuvua kambamiti umewekwa kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo unaruhusiwa kufanyika kuanzia mwezi Machi hadi Septemba kila mwaka kwa ukanda wa Kaskazini unaohusisha Wilaya za Bagamoyo, Pangani na Chalinze na kuanzia mwezi Aprili hadi Agosti kila mwaka kwa Ukanda wa Kusini unaohusisha Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Kilwa.

Aliongezea kuwa, kipindi kilichobaki kimeachwa ili kambamiti waweze kuzaliana na kukua.

Maamuzi haya yamefanyika baada ya taarifa za utafiti wa kisayansi na kuzingatia uendelevu wa Rasilimali hii.

“Kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya Mwaka 2003 pamoja na Kanuni zake za Mwaka 2009 na Marekebisho yake ya mwaka 2020; Serikali haijawahi kuzuia uvuvi wa kambamiti” Alisema Mhe. Ulega

Akijibu swali la nyongeza la Mhe. Twaha Mpembenwe, ambaye alitaka kufahamu siku serikali itaruhusu uvuvi wa kambamiti kuanzia mwezi Desemba hadi Mei kila mwaka, Mhe. Ulega alisema serikali inatambua kuwa shughuli kuu ya wananchi katika baadhi ya maeneo ya Kibiti na Mkuranga wanatengemea uvuvi hasa wa kambamiti.

Alisema, katika kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa suala hili Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Taasisi ya Utafiti ya Uvuvi Tanzania (TAFIRI) na Idara ya Uvuvi kwa kushirikiana na wavuvi  itafanya tena utafiti katika maeneo ya uvuvi kwa kambamiti ili kupata mwafaka wa pamoja wa suala hili. 

“Serikali imejipanga kuwezesha wavuvi kuweza kunufaika na rasilimali za uvuvi katika maeneo yao, samaki wanakulia maeneo ya kibiti na baadhi kuelekea maeneo ya Bahari Kuu ambako wavuvi wengi wanashindwa kufika kwa ajili ya kuvua “ Alisema Mhe. Ulega.

Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Ilala, Mhe. Mussa Zungu aliyetaka kufahamu ni kwa nini wavuvi katika soko la feri jijini Dar es Salaam wanashindwa kusajili vyombo vya uvuvi hasa katika zone na. 8 kunakosababishwa na kuwepo kwa vitendo vya rushwa, Mhe. Ulega alisema kuwa mwenye mamlaka ya kutoa leseni kwa vyombo vya uvuvi katika wilaya ni Mkurugenzi wa Halmashauri kupitia Idara yake ya uvuvi ama afisa mwingine aliyeidhinishwa.

“Mhe. Mwenyekiti ikiwa kama feri, soko ambalo linamilikiwa na Manispaa ya Ilala kuna vitendo visivyokuwa vya nidhamu vya uvunjifu wa sheria, kama ulivyosema watu wanatoa rushwa natoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala na mamlaka zote pale ilala zishughulikie jambo hili na hao wanaofanya vitendo hivi tumepata taarifa za awali na vyombo vyetu vya dola vinafanyia kazi, hiyo ni kinyume cha sheria, vyombo vyetu vitachukua hatua stahiki na jambo hilo liachwe mara moja.” Alisema Mhe. Ulega 

Mhe. Ulega alihitimisha majibu yake kwa kujibu swali la nyongeza la Mbunge wa Jimbo la Mtama Mhe. Nape Nnauye aliyetaka kufahamu ni lini serikali itatekeleza ahadi ya kuwasaidia wavuvi ukanda wa Pwani kupata injini za boti ambapo amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi itapeleka mashine za boti kwa wavuvi katika jimbo la Lindi mjini na Mtama kama ilivyoahidi.



Jumatatu, 17 Mei 2021

WAWEKEZAJI WATAKIWA KUGEUKIA FURSA YA KILIMO CHA MBEGU ZA MALISHO YA MIFUGO

Serikali imewataka wadau wa uwekezaji nchini kugeukia Sekta ya Mifugo hasa katika kutumia fursa ya changamoto ya uhaba wa mbegu za malisho ambayo mahitaji yake ni zaidi ya tani milioni 7 kulinganisha uzalishaji wa sasa wa tani 127 pekee.

Rai hiyo ilitolewa na Katibu Mkuu  wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Elisante Ole Gabriel wakati akifungua warsha maalum ya wadau wa uzalishaji mbegu za malisho hapa nchini  Mkoani Morogoro 12, Mei 2021.

Alisema kuwa takwimu zinaonyesha kiwango cha uzalishaji wa mbegu ni mdogo ukilinganisha na mahitaji yake na kwamba kama wawekezaji wakigeuza changamoto hiyo kuwa fursa inasadia kwa kiasi kikubwa kuongeza uzalishaji.

“Mahitaji ya mbegu za malisho Tanzania ni tani milioni 7 lakini kiwango cha  mbegu kilichozalishwa kwa mwaka 2019/20 ni tani 127 maana yake ni kwamba kuna uhaba mkubwa sana ivyo changamoto hiyo tuichukulie kama fursa ya uwekezaji katika sekta hiyo” alisema Prof Gabriel.

Kadharika alisema Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi  itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo, makampuni na watu binafsi wenye nia ya kuzalisha mbegu bora za malisho, kufanya kazi hii kibiashara kwa kuwapa mwongozo unaostahili.

Alibainisha kuwa lengo ni kufanikisha juhudi hizi za Serikali hasa kujiletea faida za kiuchumi kupitia uwepo wa fursa ya wingi wa mifugo nchini na hata kuuza malisho katika mataifa mengine.

“Hii si tu kwamba itainua uchumi wa mtu binafsi bali italipatia Taifa fedha za kigeni, hasa tukizingatia kuwa wananchi wanaweza kutumia fursa ya ardhi iliyopo kuzalisha malisho kibiashara kama wanavyo zalisha mazao ya chakula”. alisema Prof. Gabriel

Kwa upande wake Mkurugenzi Idara ya Utafiti Mafunzo na huduma za Ugani, Dkt. Angello Mwilawa alisema lengo la warsha hiyo ni kuhakikisha tafiti zilizofanyika kubaini mbegu bora za malisho zinawafikia wafugaji wadogo kwenye mashamba yao.

Alisema zipo mbegu ambazo zimekuwa rahisi kuwafikia wafugaji kama mbegu aina ya Nyasi, mikunde inayotaambaa na mikunde jamii ya miti malisho ambazo zipo katika makundu tofauti ambazo pia mahitaji ya msingi katika mashamba ya malisho.

“Tunaona kuna fursa kubwa ya uzalishaji wa mbegu endelevu na hapa tunazungumzia mbegu mafungu matatu ambazo hizo tunaangalia ni namna gani tunaongeza uzalishaji hapa nchini” alisema Dkt. Mwilawa.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akifungua warsha ya wadau wa uzalishaji wa mbegu za malisho kwenye ukumbi wa Cate hotel Mkoani Morogoro (12.05.2021)

 


Mkurugenzi wa Utafiti Mafunzo na Ugani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Angello Mwilawa akimkaribisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani), kufungua warsha ya uzalishaji wa mbegu za malisho kwenye ukumbi wa Cate hotel Mkoani Morogoro. (12.05.2021)


Mhadhiri mstaafu chuo kikuu cha Sokoine na Mwenyekiti mstaafu wa chama cha nyanda za malisho Tanzania, Prof. Ephraim Mtengeti akimshukuru Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani) kwa kuweza kushiriki nao na kufungua warsha ya uzalishaji wa mbegu za malisho kwenye ukumbi wa Cate hotel Mkoani Morogoro 12.05.2021


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (waliokaa katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau walioudhuria warsha ya uzalishaji wa mbegu za malisho mara baada ya kufungua warsha hiyo kwenye ukumbi wa Cate hotel Mkoani Morogoro.  (12.05.2021)

Jumapili, 16 Mei 2021

KIKAO CHA MAKATIBU WAKUU WA NCHI ZA JUMUIYA YA MAENDELEO YA NCHI ZA KUSINI MWA AFRIKA (SADC) WENYE DHAMANA YA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Rashid Tamatamah (katikati) akiongoza ujumbe wa Tanzania katika kikao cha makatibu wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wenye dhamana ya  kilimo, mifugo na uvuvi. Kulia kwake ni Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Andrew Massawe na Katibu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel wakiwa kwenye maandalizi ya mkutano wa mawaziri wa SADC utakaofanyika Tarehe 07 Mei 2021. Mkutano huo umefanyika kwenye ukumbi wa Ofisi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Mkutano huo unafanyika kwa njia ya video na kuhudhuriwa na nchi wanachama wa SADC. (05.05.2021)

Wajumbe kutoka Tanzania wakiwa katika kikao cha makatibu wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wenye dhamana ya  kilimo, mifugo na uvuvi, kwa ajili ya maandalizi ya mkutano wa mawaziri wa SADC utakaofanyika Tarehe 07 Mei 2021. Ujumbe wa Tanzania umehudhuria mkutano huo kwenye ukumbi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Mkutano huo unafanyika kwa njia ya video na kuhudhuriwa na nchi wanachama wa SADC. (05.05.2021)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Rashid Tamatamah (kushoto) ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania katika kikao cha makatibu wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wenye dhamana ya  kilimo, mifugo na uvuvi, akibadilishana mawazo na Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Andrew Massawe (katikati) na Katibu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel kwa ajili ya maandalizi ya mkutano wa mawaziri wa SADC utakaofanyika Tarehe 07 Mei 2021. Ujumbe wa Tanzania umehudhuria mkutano huo kwenye ukumbi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Mkutano huo unafanyika kwa njia ya video na kuhudhuriwa na nchi wanachama wa SADC. (05.05.2021)

Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Sera na Mipango kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Bw. Adam Mwaigoga (katikati), Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Didas Mtambalike (kulia) na Mkurugezi wa Idara ya Sera na Mipango kutoka Wizara ya Kilimo Bw. Obadiah Nyagiru wakibadilishana mawazo kabla ya kuanza kwa kikao cha maandalizi ya mkutano wa mawaziri wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wenye dhamana ya  kilimo, mifugo na uvuvi, utakaofanyika Tarehe 07 Mei 2021. Ujumbe wa Tanzania umehudhuria mkutano huo kwenye ukumbi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Mkutano huo unafanyika kwa njia ya video na kuhudhuriwa na nchi wanachama wa SADC. (05.05.2021)


Ijumaa, 7 Mei 2021

WAVUVI WAHIMIZWA KUJIUNGA KWENYE VYAMA VYA USHIRIKA

Serikali imeendelea kuhamasisha uanzishwaji na uimarishaji wa vikundi na vyama vya ushirika vya msingi vya  wavuvi  wadogo kwa lengo la kuwapatia mtaji, ujuzi, vifaa pamoja na dhana za uvuvi katika maeneo ya mwambao wa bahari ya hindi , maziwa, mabwawa na mito ili kuzalisha ajira na kipato. 

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), bungeni leo wakati akijibu swali la Mbunge wa Nyasa, Mhe. Eng. Stella Manyanya   ambaye alitaka kufahamu mikakati ya Serikali katika kuhakikisha mikopo inatolewa kwa mtu mmoja mmoja aliye tayari, kuliko kutoa kupitia vikundi jambo ambalo linachelewesha ukuaji wa sekta ya uvuvi.

Mhe. Ulega alisema kuwa katika kutekeleza ilani  kwa mwaka wa fedha 2020/2021 serikali iliadhimia kuhamasisha wavuvi na wakuzaji viumbe maji kujiunga kwenye vyama vya ushirika ili kuwa na sauti ya pamoja ikiwa ni rahisi kutatua changamoto zinazowakabili kwa pamoja na kuwa na usimamizi endelevu wa rasilimali za uvuvi.

Aidha Serikali iliwezesha vyama vya ushirika kwa kuvipatia elimu, dhana na vifaa bora vya uvuvi kama vile injini za boti, pamoja na kuviunganisha na taasisi za fedha ili kupata mikopo yenye riba na masharti nafuu kwa lengo la kufanya shughuli zao kwa tija.

"Mhe. Naibu Spika kutokana na ilani ya chama cha mapinduzi Serikali itaendelea kuvihamasisha na kuviendeleza vyama vya ushirika, aidha mtu mmoja mmoja anayo fursa ya kuomba injini za boti kupitia taasisi za kifedha nchini.” Alisema Mhe. Ulega

Ulega aliongezea kuwa Serikali imejipanga vyema katika kuhakikisha wavuvi wote nchini wanapata suluhu ya changamoto zinazo wakabili wakiwemo wavuvi wa ziwa Nyasa na ndio maana imejipanga pia kwenda kuhakikisha inajenga soko la kisasa katika eneo la mwambao wa ziwa Nyasa.

Akijibu swali la nyongeza la Mhe. Mwamtum Zodo, ambaye alitaka kufahamu mkakati wa Serikali wa kuwakwamua wavuvi wa pembezoni mwa bahari ya hindi, kwa mikoa ya Tanga, Dar- es- salaam, Pwani, Lindi na Mtwara katika kushiriki kwenye uchumi wa bluu, Mhe. Ulega alisema Serikali ya awamu ya sita inayo ongozwa  Mhe. Samia Suluhu Hassan, inayo mkakati madhubuti ya kuhakikisha inawasaidia wavuvi wa ukanda wa Pwani hasa kuendana na uchumi wa bluu kwa kuongeza uzalishaji kwa wavuvi kwa kuweka miamba ya kuvutia samaki na kutengeneza katika ukanda wote wa pwani

“Tutahakikisha kwamba tunatengeneza vichanja vya kukaushia samaki ili kusaidia kutopoteza mazao ya uvuvi wanayo zalisha, kwa kuoza na kuaribika, tunataka tuhakikishe samaki wote wanaozalishwa kwenye ukanda wa pwani hawaaribiki kwa sababu tutawaongezea thamani kwa kuwakausha lakini vilevile tutakwenda kuongeza uzalishaji wa barafu na kuwa na “cold rooms” za kutosha katika ukanda mzima wa pwani ili kuweza kuutumia vyema uchumi wa bluu na kuongeza kipato cha mvuvi mmoja mmoja na hatimae kuongeza kipato cha Serikali yetu. Alisema Ulega.

Hata hivyo ametoa wito kwa wabunge wote kuhimiza wavuvi na wakuzaji viumbe maji wa maeneo yao kujiunga kwenye vyama vya ushirika vya wavuvi kama chachu ya kuwaletea maendeleo.

WAKAGUZI WA NGOZI WATAKIWA KUHAKIKISHA UZALISHAJI WA NGOZI BORA*

  

Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetoa mafunzo na kuwakabidhi majukumu wakaguzi wa ngozi 33, kutoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa Victoria ili kuhakikisha ngozi inayozalishwa nchini inakuwa bora.

Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe, kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw.  Gabriel Bura, aliyasema hayo wakati wa kufunga mafunzo ya kuwajengea uwezo wakaguzi wa ngozi yaliyofanyika jijini Mwanza Mei 5, 2021.

Alisema, wakaguzi wa ngozi waliopatiwa mafunzo kutoka mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu wanatakiwa kuongeza usimamizi wa sheria ya biashara ya ngozi.

“Hii ni kutokana  na kati ya  asilimia 100 ya ngozi zinazopelekwa viwandani,  asilimia 10  ndizo zinafaa kusindikwa  na kutengenezea bidhaa huku asilimia 90 hazifai kutokana na kukosa ubora unaotakiwa, ambapo jambo hilo limekuwa likisababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara na wenye viwanda.” Alisema

Aliongeza kuwa watahakikisha uzalishaji wa ngozi unakuwa bora kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya viwanda, kwani kumekuwa na changamoto ya ubora hafifu wa ngozi zinazozalishwa hapa nchini hasa kwenye maeneo ya machinjio, wakati wa usafirishaji na mfugaji mwenyewe.

Bw. Bura alisema ili kukabiliana na changamoto hiyo Wizara ya Mifugo na Uvuvi iliamua kuteua wakaguzi na kuwakabidhi majukumu ili waweze kusimamia ngozi kwenye machinjio, inazalishwa  kwa kuhakikisha hazitobolewi na zinahifadhiwa vizuri kwa njia ile inayokubalika ya kutumia chumvi na zinaposafirishwa vibali vitolewe na zifike kwenye viwanda vilivyopo na vinavyofanya kazi ili kuepusha changamoto ya ngozi kutokufika kiwandani.

"Kuwepo kwa wakaguzi kutasaidia kujua ngozi imetolewa lini na kwa kiasi gani na zinatarajiwa kufika wapi, ndiyo sababu ya mafunzo haya,  tunatarajia baada ya mafunzo ubora wa ngozi utaongezeka.

"Mwanzo viwanda vilikuwa vinapata asilimia 10 pekee ya ngozi bora lakini tunaamini ubora wa ngozi utaongezeka kutoka asilimia 10 sasa hadi kufikia asilimia 80 mwaka 2022, kuwa zikifika kiwandani zinaweza kusindikwa na kutengenezea bidhaa," Alisema Bw. Bura.

Sambamba na hayo alisema ubora wa ngozi unachangiwa na afya ya mnyama mwenyewe na kama ameathiriwa na magonjwa hata ngozi itakuwa haina ubora unaotakiwa kwa hiyo kwa kutoa chanjo watakuwa wamedhibiti magonjwa ambapo kwa kumuogesha mnyama watakuwa wamesaidia asishambuliwe na wadudu  mfano ng'ombe akiwa ameshambuliwa na kupe katika kusindika ngozi alama za kupe au michirizi itaonekana kwenye ile bidhaa itakayokuwa imezalishwa hivyo bidhaa hiyo haitauzwa kwa bei inayotakiwa.

Kwa upande wake afisa wa ngozi mstaafu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, mkufunzi wa mafunzo hayo Bw. Emmanuel Muyinga alisema, moja ya maeneo ambayo amewasisitiza wakaguzi wa ngozi ni kusimamia wachunaji wa ngozi katika machinjio kwa sababu ndipo ngozi zinapozalishwa katika changamoto yote ya mnyororo wa thamani tatizo la uharibifu wa ngozi katika machinjio linachangia kwa kiwango kikubwa sana.

Bw. Muyinga alisema, ngozi ikishatobolewa inapunguza thamani, hivyo amesisitiza namna ya kuhifadhi ngozi baada ya kuchuna ambapo ngozi inatakiwa isikae zaidi ya saa nne katika machinjio baada ya kuchunwa ili iweze kufika katika mkondo wa biashara kabla ya kuanza kuoza.

Hata hivyo amewasisitiza Wakaguzi hao wakasimamie madaraja ya ngozi hali itakayosaidia kila mmoja katika eneo lake pindi wanapofanya uchambuzi wa madaraja kuzingatia na kuona ni madhara gani yanaathiri ngozi hivyo watatayarisha mpango kazi wa kuweza kutatua changamoto katika eneo husika linalokabili uzalishaji wa ngozi.

Naye Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Emmily Kasagala, amewaasa washiriki wa mafunzo hayo kujiepusha na vitendo vya ukosefu wa maadili na uonevu na badala yake wajenge mazingira rafiki kwa wadau kufanya biashara.


Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo Usalama wa Chakula na Lishe kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Gabriel Bura akiongea na wakaguzi wa ngozi (hawapo pichani) walioudhuria mafunzo ya kuwajengea uwezo wakaguzi hao kutoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa yaliyofanyika Mkoani Mwanza. 05.05.2021)


Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Bw. Emmily Kasagala akizungumza kwenye mafunzo ya kuwajengea uwezo wakaguzi wa ngozi kutoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa yaliyofanyika Mkoani Mwanza. (05.05.2021)


Mkufunzi wa mafunzo, Bw. Emmanuel Muyinga akitoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wakaguzi wa ngozi (hawapo pichani) kutoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa yaliyofanyika Mkoani Mwanza. (05.05.2021)



Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Gabriel Bura (waliokaa katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo ya ngozi mara baada ya mafunzo hayo yaliyofanyika Mkoani Mwanza. (05.05.2021)

Jumamosi, 1 Mei 2021

SIKU YA WAFANYAKAZI DUNIANI


 

WATUMISHI WA UMMA WATAKIWA KUPIMA AFYA ZAO MARA KWA MARA

 Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo),  Prof. Hezron Nonga, ametoa wito kwa  watumishi wa umma kupima afya zao mara kwa mara ili kutambua afya zao kama ambavyo muongozo wa kudhibiti virusi vya ukimwi (VVU), Ukimwi na magonjwa sugu yasiyo ambukiza mahala pa kazi unavyowataka.

 

Prof. Nonga, aliyasema hayo  wakati akifungua mafunzo pamoja na upimaji wa afya kwa watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi yaliyofanyika Jijini Dodoma Aprili 30, 2021.

 

Alisema kuwa upimaji wa afya kwa watumishi wa umma kwa mujibu wa muongozo huo wa mwaka 2014 ni jambo la lazima siyo hiyari.

 

“Kupima afya ni jambo la lazima na muhimu sana kwa mtumishi kwani itasaidia hata kuongeza tija katika taasisi baada ya kutambua afya yake” amesema Prof.Nonga.

 

Aidha amesema kuwa kwa kutambua afya za wafanyakazi kutamwezesha  mwajiri kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa jukumu mbalimbali.

 

“Kama mtumishi atakuwa na afya njema basi atasaidia kuongeza uzalishaji katika taasisi hivyo wafanyakazi wanatakiwa kupima afya zao kwa mujibu wa muongozo huo wa kudhibiti vvu, ukimwi, pamoja na magonjwa sugu yasiyoambukiza” alisisitiza Prof. Nonga.

 

Aliongeza  kuwa, kwa mtumishi ambaye atabainika mara baada ya vipimo kuwa ana maambukizi ya virusi vya ukimwi taratibu zinamtaka mwajiri wake kumpatia kiasi cha Sh. 100,000 kila mwezi.

 

Alisema kuwa mafunzo hayo kwa wafanyakazi, watapatiwa mada mbalimbali kutoka kwa watalaam wa masula ya afya.

 

“Wafanyakazi wanatakiwa pia kufanya mazoezi ili kuondokana na tatizo la uzito uliopitiliza pamoja na msongo wa mawazo” alisema.

 

Kwa upande wake mtoa mada katika mafunzo hayo Daktari Bingwa kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Dkt. Garvin Kweka, amesema lengo la mafunzo hayo ni kuongea na watumishi ili kuwasaidia kujenga tabia ya kutambua afya zao mara kwa mara.

 

“Leo nimekuja kuzungumza na watumishi hawa kwani tumekuwa tukipoteza nguvu kazi nyingi kutokana na magonjwa, asilimia 60 ya watumishi inaonyesha wana tatizo la uzito kupindukia pamoja na msongo wa mawazo kwa hiyo mafunzo haya yatawasaidia kutambua nini wafanye na kipi wasifanye ili kuwa na afya njema, ili kuendelea kuleta tija katika maeneo yao ya kazi”alisema Dk.Kweka.

 

Naye Mratibu wa Ukimwi, Vvu na magonjwa sungu yasiyoambukiza mahala pa kazi Sekta ya Mifugo Rachel Maliselo, amesema kuwa lengo la zoezi hilo ni kutoa fursa kwa wafanyakazi kupima afya zao kwa mujibu wa muongozo huo.

 

Alisema wafanyakazi wamefurahi sana kupata fursa hii kwani inawapa nafasi ya kutambua afya zao na kufanya kazi  kwa bidii na kuongeza tija katika maeneo yao ya  kazi.

Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Hezron Nonga akizungumza na watumishi wa Wizara hiyo (hawapo pichani) wakati akifungua mafunzo pamoja na upimaji wa afya yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Wizara hiyo Mtumba jijini Dodoma Aprili 30, 2021.


Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ( Mifugo) walioshiriki mafunzo pamoja na upimaji  afya yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Wizara hiyo Mtumba jijini Dodoma. Aprili 30, 2021.


Kaimu Mkurugenzi Idara ya Utawala na Rasilimali watu, Bw. Fraksed Mushi, akimkaribisha Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Hezron Nonga (hayupo pichani) kufungua mafunzo pamoja na upimaji wa afya yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Wizara hiyo Mtumba jijini Dodoma 31.04.2021.


Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Hezron Nonga akiongoza watumishi wa Wizara hiyo (hawapo pichani) kwenye zoezi la upimaji afya mtumba jijini Dodoma Aprili 30, 2021.


Daktari Bingwa wa magonjwa yasiyo ambukiza kutoka hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Garvin Kweka akieleza lengo la kutoa mafunzo  ikiwa ni pamoja na kuwasaidia watumishi  kujenga tabia  ya  kupima na kutambua afya zao mara kwa mara mtumba jijini Dodoma. Aprili 30, 2021.