Nav bar

Jumanne, 29 Desemba 2020

VIWANDA KUONDOA UMASIKINI WA WAFUGAJI NA WAVUVI

Na. Edward Kondela

 

Serikali imesema itahakikisha sekta za mifugo na uvuvi zinawaondoa wananchi katika umasikini, kupata ajira na nchi iweze kuuza bidhaa bora za mazao ya mifugo na uvuvi ndani na nje ya nchi.

 

Akizungumza jana (28.12.2020) katika siku yake ya kwanza ya ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani mwanza, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki wakati akihitimisha ziara hiyo kwenye kiwanda cha kuchinja na kuchakata nyama cha Chobo kilichopo Kata ya Usagara Wilaya ya Misungwi amesema wizara imekuwa ikichukulia kwa uzito mkubwa suala la viwanda ambalo litaweza kubadilisha fikra za wafugaji na wavuvi.

 

“Wananchi wetu waondoe umasikini, wananchi wetu wapate ajira na sisi tuuze bidhaa za mazao haya ya mifugo na uvuvi yaliyo bora hapa ndani na kule kwa wenzetu nje, sasa mimi nikikuta hali ya mkwamo kwa kitu ambacho kinatusaidia kuelekea huko napata shida.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Waziri Ndaki akifuatana na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Pauline Gekul katika ziara hiyo amefafanua kuwa haridhishwi na baadhi ya changamoto wanazokutana nazo wawekezaji ambao wamejikita katika kuyaongezea thamani mazao ya mifugo na uvuvi na kumuagiza Kaimu Msajili wa Bodi ya Nyama nchini Bw. Iman Sichalwe kumpatia taarifa ya hali ya viwanda vya nyama nchini ili apate tathmini halisi ya utendaji kazi wa viwanda hivyo, baada ya Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda cha Chobo, Bw. John Chobo kubainisha baadhi ya changamoto ambazo Waziri Ndaki amesema wizara itahakikisha inafuatilia changamoto zinazoihusu wizara hiyo ili kuzipatia majibu.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda hicho Bw. John Chobo amesema kwa sasa kiwanda chake kimesimamisha uzalishaji na kinatarajia kuanza kurejea katika shughuli zake Mwezi Januari Mwaka 2021 baada ya ugonjwa wa Covid 19 kuathiri shughuli za kiwanda hicho ambacho kimekuwa kikisambaza nyama katika nchi za falme za kiarabu.

 

Bw. Chobo amesema kutopatikana kwa taarifa sahihi za mifugo kumekuwa kukichangia kwa kiasi kikubwa soko la nyama kutoka Tanzania kwenda nje ya nchi kuwekwa katika daraja la chini kwa kuwa mifugo mingi ambayo inachakatwa viwandani haina taarifa sahihi juu ya ukuaji wake, magonjwa na chanjo mbalimbali ambazo mfugo huo umepatiwa.

 

Akiwa katika Kiwanda cha kuchakata samaki Nile Perch kilichopo eneo la viwanda katika Kata ya Nyakato Wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiambatana na Naibu Waziri Mhe. Pauline Gekul amewataka wawekezaji wa viwanda vya samaki vilivyopo Mkoani Mwanza kuhakikisha wanatumia usafiri wa ndege kutoka katika kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Mwanza kusafirisha minofu ya samaki ili kutangaza bidhaa zinazotengezwa hapa Tanzania.

 

“Tungependa kuona usafirishaji wa minofu ya samaki unafanyika hapa nchini kwetu, badala ya nchi jirani kwa kusafirisha kwa malori kwenda nchi za jirani, kuna uwekezekano kabisa wa kutoa minofu ya samaki kutoka kiwanja cha ndege cha Mwanza kwenda nje ya nchi badala ya kutumia nchi za jirani.” Amefafanua Mhe. Ndaki

 

Aidha, amewataka wawekezaji wa viwanda vya samaki kuangalia namna ya kuongeza bei ya kununulia samaki kwa wavuvi wanaopeleka samaki katika viwanda hivyo ili wavuvi hao waweze kubadilisha maisha yao na kunufaika kupitia Sekta ya Uvuvi.

 

Waziri Ndaki amebainisha hayo baada ya Meneja Mkuu wa Kiwanda cha kuchakata samaki cha Nile Perch Bw. Rupesh Mohan kumueleza Waziri Ndaki na Naibu Waziri Gekul kuwa viwanda vya samaki vimekuwa vikikosa malighafi ya kutosha kutokana na soko la ndani kukua na wakati mwingine kupata samaki kwa bei ya juu, hali iliyomlazimu Waziri Ndaki kubainisha kuwa kama bei ya soko la ndani imepanda ni dhahiri wavuvi watauza samaki katika soko hilo badala ya kupeleka viwandani ambapo wanauza kwa bei ndogo.

 

Hivyo amevitaka viwanda vya kuchakata samaki kuangalia upya bei ya samaki wanayonunua ili wavuvi nao waweze kunufaika na kuboresha maisha yao na viwanda pia viweze kupata malighafi za kutosha.

 

Pia, Waziri Ndaki ametembelea kiwanda cha kukausha mabondo ya samaki cha Hong Lin International Ltd kilichopo Wilaya ya Ilemela jijini Mwanza na kufurahishwa na kiwanda hicho kwa kutumia kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Mwanza kusafirisha bidhaa zake kwenda nchi za nje.

 

Naye Mkurugenzi wa kiwanda hicho Bi. Wang Shenghong ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji hali inayomuwezesha kufanya shughuli zake bila matatizo huku akiomba pia baadhi ya tozo zipunguzwe.

 

Katika siku ya kwanza ya ziara yake Mkoani Mwanza, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiwa na Naibu Waziri Mhe. Pauline Gekul wametembelea pia Maabara ya Taifa ya Uvuvi, Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi nchini (FETA) na Kituo cha Ulinzi wa Rasilimali za Uvuvi (FRP).

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kutoka kushoto), akiwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Pauline Gekul (anayemfuata) pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah (wa kwanza kutoka kulia), wakati Waziri Ndaki alipofanya ziara ya kikazi katika kiwanda cha kukausha mabondo ya samaki cha Hong Lin International Ltd kilichopo Wilaya ya Ilemela, jijini Mwanza. (28.12.2020)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiwa na Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Pauline Gekul walipofanya ziara ya kikazi katika kiwanda cha kuchinja na kuchakata nyama cha Chobo kilichopo Kata ya Usagara Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza, ambapo Waziri Ndaki amesema viwanda vya namna hiyo vina nafasi kubwa ya kubadilisha fikra za wafugaji kufuga kisasa. (28.12.2020)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki na Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Pauline Gekul wakiangalia mabondo ya samaki baada ya kukaushwa tayari kwa ajili ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi, wakati walipofanya ziara ya kikazi katika kiwanda cha kukausha mabondo ya samaki cha Hong Lin International Ltd kilichopo Wilaya ya Ilemela, jijini Mwanza. (28.12.2020)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Pauline Gekul wakati walipofanya ziara ya kikazi katika Maabara ya Taifa ya Uvuvi iliyopo Kata ya Nyegezi Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza na kushuhudia namna maabara hiyo inayofanya kazi kwa kufanyia uchunguzi sampuli za samaki kutoka viwandani. Wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah. (28.12.2020)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa pili kutoka kushoto), akiwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Pauline Gekul (wa pili kutoka kulia) pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah (wa kwanza kutoka kushoto), wakati Waziri Ndaki alipofanya ziara ya kikazi katika kiwanda cha kuchakata samaki cha Nile Perch kilichopo kata ya Nyakato, Wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza. (28.12.2020)




Jumamosi, 26 Desemba 2020

SALAAM ZA KRISMASI NA MWAKA MPYA

 


SALAAM ZA KRISMASI NA MWAKA MPYA


 

SALAAM ZA KRISMASI NA MWAKA MPYA

 


SERIKALI YASISITIZA MATUMIZI YA CHANJO ILI KUPATA MIFUGO BORA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema Tanzania ina chanjo za kutosha dhidi ya magonjwa ya mifugo na kuagiza wafugaji wote nchini pamoja na maeneo ambayo serikali inafuga kuhakikisha mifugo yao inachanjwa ili kuondokana na magonjwa hayo.

 

Akizungumza jana (24.12.2020) mara baada ya kutembelea Taasisi ya Chanjo Tanzania (TVI) iliyopo Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani, wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani humo, Waziri Ndaki amesema ili kuhakikisha Tanzania inakuwa na mifugo bora inayokidhi soko la kimataifa ni lazima mifugo ichanjwe dhidi ya magonjwa ili yapatikane mazao bora ya mifugo.

 

“Tunayo chanjo ya kutosha hivyo niwatake wafugaji wote ikiwa ni pamoja na sisi serikali kwenye maeneo ambayo tunafuga tuchanje mifugo yetu ili tupate mifugo iliyo bora, tunataka sasa nchi yetu iende kwenye ubora badala ya uwingi wa mifugo, ili tupate nyama bora na maziwa bora kwa maana ya mazao bora ya mifugo ili tuweze kuuza katika soko la kimataifa.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Katika ziara hiyo kwenye taasisi ya TVI, Waziri Ndaki alitaka kufahamu namna agizo alilolitoa hivi karibuni la ng’ombe waliopo kwenye ranchi 14 za taifa kuchanjwa dhidi ya ugonjwa wa homa ya mapafu kutokana na baadhi ya mifugo hiyo kuathiriwa na ugonjwa huo katika Ranchi ya Kongwa iliyopo Mkoani Dodoma, ambapo Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) ambayo inaisimamia TVI, Dkt. Stella Bitanyi amesema chanjo zimesambazwa kutokana na mahitaji ya ranchi hizo na sasa wapo katika hatua ya chanjo hizo kuwafikia majirani wa ranchi hizo ili kuweza kuchanja ng’ombe wao.

 

Aidha, Waziri Ndaki amejionea ujenzi wa kiwanda cha kuzalisha chanjo cha HESTER kilichopo Wilayani Kibaha na kupongeza hatua mbalimbali ambazo zimefikiwa katika ujenzi huo na kusema mara kiwanda hicho kitakapoanza kufanya kazi Mwezi Aprili Mwaka 2021, kitasaidia kuongeza wigo wa uwepo wa chanjo nyingi hapa nchini na kusaidia endapo magonjwa ya mifugo yatajitokeza.

 

“Hii inaonesha umuhimu wa kuwa na chanjo tayari kwa ajili ya mifugo yetu yote ili ikitokea magonjwa ya milipuko tuweze kupata mahali pa kusaidiwa kwa karibu na pengine kwa bei nafuu kwa kuwa chanjo hizi zitakuwa zinazalishwa hapa nchini.” Amefafanua Mhe. Ndaki

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amefika pia katika kiwanda cha kuchinja na kuchakata nyama cha TAN CHOICE kilichopo Wilayani Kibaha, na kubainisha kuwa umuhimu wa uwepo wa viwanda hivyo kutasaidia kubadilisha fikra za wafugaji kwa kuingia kwenye ufugaji bora.

 

Kuhusu changamoto ya vibali vya kuingiza nyama zilizochakatwa kwenye baadhi ya nchi kutoka Tanzania, Waziri Ndaki amesema wizara itawasiliana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa pamoja na Wizara ya Viwanda na Biashara ili kufahamu changamoto zinazovikabili baadhi ya viwanda kushindwa kusafirisha nyama kwenda baadhi ya nchi kutokana na kukosa vibali vya kuingiza nyama hizo kutoka Tanzania.

 

Pia, amefafanua kuwa uwepo wa viwanda vya kuchinja na kuchakata nyama nchini kunazidi kusaidia kukuza biashara ya mifugo nchini na kuongeza wigo wa soko la mifugo hivyo ni muhimu kwa wafugaji kuanza kuhakikisha wanakuwa na mifugo iliyo bora ili waweze kuuza mifugo yao kwa bei nzuri na waweze kunufaika kiuchumi na taifa pia liweze kupata mapato ya kutosha kupitia biashara ya mifugo.

 

Awali akiwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amekutana na mkuu wa mkoa huo Mhandisi Evarist Ndikilo ambapo wamezungumza mambo mbalimbali yanayohusu sekta za mifugo na uvuvi.

 

Katika mazungumzo hayo Mhandisi Ndikilo amesema kwa sasa migogoro ya wakulima na wafugaji imepungua kwa kiasi kikubwa huku akitaka juhudi zaidi zifanyike katika kuwapatia wafugaji elimu ya kuwa na mifugo michache na yenye tija badala ya kuwa na mifugo mingi ambayo haitoshi kutokana na uwepo wa maeneo ya kufugia.

 

Kwa upande wake Waziri Ndaki amesema changamoto zinazohusu wizara atahakikisha zinafanyiwa kazi ili sekta za mifugo na uvuvi ziwe endelevu na kuondokana na migogoro isiyo na tija kwa taifa.

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amemaliza ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani Pwani, ambapo katika siku ya kwanza (23.12.2020) alipata fursa ya kuzungumza na baadhi ya wafugaji Wilayani Rufiji na kuwataka kuheshimu maeneo waliyopewa na uongozi wa mkoa kwa ajili ya ufugaji na kuacha kuingia katika maeneo ya wakulima.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kushoto) akiangalia namna nyama ya mbuzi ilivyohifadhiwa katika chumba chenye baridi kali kabla ya taratibu nyingine za kusafirisha nyama hiyo kwenda nje ya nchi. Waziri Ndaki amefanya ziara ya kikazi ya siku moja katika kiwanda cha kuchinja na kuchakata nyama TAN CHOICE kilichopo Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani. (24.12.2020)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa pili kulia) akishuhudia namna kiwanda cha kuchinja na kuchakata nyama TAN CHOICE kinavyofanya kazi wakati alipofanya ziara ya kikazi katika kiwanda hicho kilichopo Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani na kuwataka wafugaji waanze kubadilisha fikra zao na kufuga kisasa kwa kuwa viwanda vya namna hiyo vinahitaji nyama bora ili kukidhi soko la kimataifa. (24.12.2020)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akishuhudia namna wataalam wa Taasisi ya Chanjo Tanzania (TVI), wakiwa kwenye moja ya hatua za kuzalisha chanjo dhidi ya magonjwa ya mifugo ambapo Waziri Ndaki ameridhishwa na utendaji kazi wa taasisi hiyo na kusisitiza kuwa chanjo zinazozalishwa katika kituo hicho zinatosheleza mahitaji ya nchi na kuwataka wafugaji kuchanja mifugo yao. (24.12.2020)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza) akikagua mitambo mbalimbali iliyofungwa katika kiwanda cha kuzalisha chanjo HESTER ambacho kinajengwa Wilayani Kibaha, Mkoani Pwani, ambapo Waziri Ndaki amesema uwepo wa viwanda vingi vya chanjo hapa nchini kutasaidia nchi kuwa tayari kukabiliana na magonjwa yoyote ya mifugo pindi mlipuko wa magonjwa ukitokea. (24.12.2020)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kulia) akishuhudia chanjo mbalimbali zinazozalishwa na Taasisi ya Chanjo Tanzania (TVI) iliyo chini ya Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA), wakati alipofanya ziara ya kikazi ya siku moja katika taasisi hiyo iliyopo Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani ili kushuhudia chanjo zinazozalishwa hapa nchini. (24.12.2020)



 

GEKUL AWAAGIZA WAKURUGENZI HALMASHAURI KUTENGA FEDHA ZA MIFUGO

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri zote nchini kutekeleza Waraka wa mwaka 2002 ambao unawataka kutenga asilimia 15 ya mapato yanayotokana na shughuli za Sekta ya Mifugo na Uvuvi na kuzirejesha kwenye sekta hizo ili kuboresha shughuli zake.

 

Gekul alitoa agizo hilo alipokuwa akiongea na Viongozi wa Wilaya ya Mwanga, Mkoani Kilimanjaro alipotembelea kukagua shughuli za Sekta ya mifugo na uvuvi zinazotekelezwa Wilayani humo Disemba 23, 2020.

 

Kwa mujibu wa Gekul, mwaka 2002 Serikali ilitoa waraka ambao unaelekeza kuwa Halmashauri zote nchini zihakikishe kuwa mapato yanayopatikana kutokana na shughuli za sekta ya mifugo na uvuvi itengwe asilimia 15 na zirudishwe kwa sekta hizo ili kuboresha huduma kwa mifugo ikiwemo ukarabati wa majosho, minada na kununua chanjo za mifugo.

“Wakurugenzi rejeeni huo waraka ambao unadumu mpaka mwaka 2025 ili mtekeleze kama ulivyoagiza na tukifanya hivyo itasaidia kuboresha huduma za mifugo yetu na tupate mazao bora yanayotokana na mifugo hiyo,” alisema Gekul

 

Aliendelea kusema kuwa miundombinu mingi ya kuhudumia mifugo imechoka akitolea mfano minada ya kuuzia ng’ombe kuwa mingi haina uzio, mifugo inauzwa katika maeneo ya wazi jambo ambalo linachangia upotevu wa mapato ya Halmashauri.

 

“Najua katika Halmashauri zetu mara nyingi fedha huwa hazitoshi lakini ni muhimu kujenga nidhamu ya matumizi ya fedha na tukifanya hivyo itakuwa rahisi kutenga hizo pesa ili kuboresha sekta za mifugo na uvuvi, hivyo naagiza baada ya kutoka hapa tukatekeleze hilo,” alisisitiza Gekul

 

Aidha, Waziri Gekul alisema kuwa muelekeo wa serikali kwa sasa ni kuhakikisha majosho yanaboreshwa, minada inakarabatiwa na chanjo zinapatikana kwa urahisi ili wananchi wasihangaike kupata huduma kwa ajili ya mifugo yao.

 

Pia, aliwataka maafisa mifugo kuhakikisha wanasimamia vyema ukusanyaji wa maduhuli ya serikali ili kuzuia upotevu wa mapato kwani makusanyo yakiwa mazuri na huduma za mifugo zitaboreshwa.

Mkurugenzi, Idara ya Uvuvi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Magese Bulayi (wapili kushoto) akitoa maelezo kwa Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (katikati) kuhusu moja ya nyavu inayotumiwa na wavuvi wanaofanya shughuli zao katika bwawa la Nyumba ya Mungu lililopo Wilayani Mwanga, Mkoani Kilimanjaro. Waziri Gekul alikwenda katika Mwalo wa bwawa hilo kukagua shughuli zinazoendelea hapo Disemba 23, 2020. Wa kwanza kulia ni Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka.

Wavuvi wa Bwawa la Nyumba ya Mungu (kushoto) wakimuonesha Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (kulia) Samaki aina ya Perege waliovuliwa kutoka katika bwawa hilo muda mfupi baada ya kumaliza kuongea na wavuvi wanaoishi kandokando mwa bwawa hilo lililopo Wilayani Mwanga, Mkoani Kilimanjaro Disemba 23, 2020.

Mkuu wa Wilaya ya Mwanga, Thomas Apson akieleza jambo katika mkutano wa Wavuvi wanaofanya shughuli zao kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (kushoto aliyekaa) uliofanyika  Wilayani Mwanga, Mkoani Kilimanjaro Disemba 23, 2020. Kulia ni Mkurugenzi, Idara ya Uvuvi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Magese Bulayi.



VIONGOZI WA KATA NA VIJIJI WAONYWA URAFIKI WAO NA WAFUGAJI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amewataka baadhi ya viongozi wa vijiji na kata wanaoshirikiana na wafugaji kuvunja sheria, taratibu na kanuni za nchi ili kuwanyanyasa wakulima katika maeneo yao kuacha mara moja kufanya hivyo kwani viongozi hao wanakuwa wanashiriki katika migogoro kwa kuchonganisha wakulima na wafugaji.

 

Akizungumza jana (22.12.2020) wilayani Liwale, kwenye kikao kilichoshirikisha wakulima na wafugaji wa Mkoa wa Lindi kwa ajili ya kutatua kero zao, Waziri Ndaki amekemea urafiki wa baadhi ya viongozi hao na wafugaji ambao umekuwa ukilenga kuwanyanyasa wakulima kutokana na wafugaji kuingiza mifugo kwenye maeneo ya wakulima hao.

 

“Wakati mwingine mnawapa tabu wakulima kwa sababu wafugaji wanashirikiana na hawa viongozi wetu wa ngazi za chini kufanya mambo yasiyotakiwa sasa tuache, watendaji wa vijiji na kata fuateni sheria, taratibu na kanuni mlizoelekezwa zinazopaswa kuwaelekeza katika kutenda kazi zenu.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Aidha, Waziri Ndaki amefafanua kuwa siku zote wakulima na wafugaji zimekuwa ni jamii zinazoelewana kwa sababu kila mmoja amekuwa akihitaji huduma kutoka kwa mwenzake, kwa maana ya mazao ya kilimo na mifugo na kutaka uhusiano huo usiharibiwe na baadhi ya viongozi wa ngazi za chini kuingia katikati yako kwa maslahi binafsi na kutaka urafiki usio na tija kwa wakulima kati ya baadhi ya viongozi hao na wafugaji ufe mara moja.

 

Pia, kuhusu sheria, taratibu na kanuni za nchi waziri huyo amesema nchi haiwezi kuendeshwa kwa sababu jamii moja ya watu wakali na wengine wapole bali lazima ifuate sheria, taratibu na kanuni zilizopo kutokana na wakulima kulalamikia vitendo vya baadhi ya wafugaji kuwa wakali wanapoingia katika maeneo yao na kulisha mifugo mazao ya wakulima.

 

“Tukifuata sheria itatusaidia sana kuishi pamoja kama nchi wakulima na wafugaji fuateni sheria, taratibu na kanuni zilizopo ili tuishi pamoja, na sheria zimewekwa na wawakilishi wenu wabunge kwamba wananchi tukiwawekea utaratibu wa namna hii tunaweza kuishi kwa amani na utaratibu.” Amefafanua Mhe. Ndaki

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki ameuarifu mkutano huo wa Mkoa wa Lindi kati ya wakulima na wafugaji kuwa ni muhimu wafugaji kushirikiana na serikali katika kujenga miundombinu ya ufugaji yakiwemo malambo ya kunyweshea mifugo yao maji kwenye maeneo ambayo wamekabidhiwa na serikali kufuga mifugo kwa kuwa mahitaji ya wafugaji ni mengi na hayawezi kukamilishwa na serikali pekee kwa mara moja.

 

“Mahitaji ya wafugaji ni mengi wanahitaji malambo, malisho, majosho na minada haya yote kwa mara moja inawezekana kabisa serikali isiweze kufanya kwa mara moja, ombi langu kwa wafugaji ninaomba tushikiriane sisi wizara tunaweza kutengeneza michoro ya aina ya malambo yanayotakiwa kuwepo ikiwemo gharama, lakini pia tunaweza kupata pesa kiasi sasa naomba tushirikiane, wizara tukipata pesa kidogo tutawachangia nanyi mtafute pesa kupitia umoja wenu ili tugharamie kwa pamoja hayo malambo kwa kufanya hivyo itawezekana kabisa lakini mkubali nyinyi ni matajiri.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Ameongeza kuwa katika kuhakikisha hilo linafanikiwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi itaangalia kuanzia bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022 kutenga kiasi cha fedha kwa ajili ya kujengea malambo katika maeneo mbalimbali nchini kwa kuanzia na baadhi ya vijiji kwa kushirikiana na halmashauri.

 

Akizungumza kwenye kikao hicho kuhusu ujenzi wa machinjio ya kisasa ya Ngongo yaliyopo halmashauri ya Manispaa ya Lindi, ambayo ameyatembelea siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi Mkoani Lindi (21.12.2020) na kushuhudia kukamilika kwa ujenzi wa jengo la machinjio hayo, ambapo inasubiri awamu ya pili ya ujenzi ya kuweka vifaa vya kuchinjia na kuchakata nyama, Waziri Ndaki amesema ataongea na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Selemani Jafo, kuingiza bajeti ya awamu ya pili ya ujenzi huo kwa mwaka wa fedha 2021/2022 badala ya 2022/2023 ambapo ujenzi huo umewekwa sasa unaokadiriwa kugharimu Shilingi Bilioni 2.5.

 

Waziri Ndaki amesema kwa kuwa jengo la machinjio limekamilika ni vyema likamilike kwa kuwekewa vifaa mapema ili machinjio hayo yaanze kufanya kazi na kuwanufaisha wafugaji kwa kuwa kwa sasa mikoa ya Kusini ukiwemo Mkoa wa Lindi na Mtwara imeanza kupokea mifugo mingi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi, hivyo hitaji la mazao ya mifugo litaongezeka na mkoa utaongeza mapato kupitia machinjio hayo.

 

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Lindi Mhe. Godfrey Zambi amesema mkoa umeweka utaratibu wa kutenga maeneo kwa ajili ya wafugaji ambao wamekuwa wakiingia katika mkoa huo, lakini wanakabiliana na gharama kubwa katika upimaji wa maeneo hali iliyolazimu mkoa kusitisha kupokea mifugo kwa sasa kwa kuwa maeneo yaliyotengwa ni machache.

 

“Tunaomba wizara ione namna gani na TAMISEMI tunaweza kuja na mpango wa kuziwezesha halmashauri ili ziweze kupima maeneo kwa kasi ambayo inaweza kusaidia kutosheleza mifugo kwa sasa hivi niseme mheshimiwa waziri na ukweli kabisa tumesema tusipokee tena mifugo kwa sababu hatuna pakuiweka, ardhi tunayo lakini hatuna sehemu tulizopima hivyo mifugo ikija inakuwa vurugu na kukaribisha ugomvi kati ya wafugaji na wakulima.” Amefafanua Mhe. Zambi

 

Mhe. Zambi pia amesema ni muhimu kuangalia namna ya kudhibiti idadi ya mifugo kutokana na wafugaji kuwa na mifugo mingi huku wakiendelea kuishi maisha duni na kutaka kuwepo na sheria ya kudhibiti idadi ya mifugo.

 

Pia amekemea matumizi ya silaha ya baadhi ya wafugaji wanaoingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima hali ambayo inatishia usalama wa wananchi wenzao na kuharibu mazao ya wakulima.

 

Nao baadhi ya wakulima na wafugaji waliozungumza katika kikao hicho wamepongeza jitihada za Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Mkoa wa Lindi kwa kuwepo kwa mkutano huo kati ya wakulima na wafugaji wenye lengo la kusikiliza kero zao na kuangalia namna ya kuzitatua.

 

Wametaka wakulima na wafugaji ambao watakiuka sheria, taratibu na kanuni zilizopo kwenye maeneo yao juu ya maeneo ya wafugaji na wakulima wachukuliwe hatua za kisheria badala ya kuadhibu kundi lote la jamii ya mtu mmoja aliyeshindwa kufuata sheria, taratibu na kanuni.

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amemaliza ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani Lindi ukiwa ni mkoa wake wa kwanza nje ya Dodoma kufanya ziara mara baada ya kushika wadhifa huo, akisaidiwa na Naibu Waziri Mhe. Pauline Gekul.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza kwenye kikao kati ya wakulima na wafugaji Mkoa wa Lindi kilichofanyika wilayani Liwale na kuwataka viongozi wa ngazi za chini kutokuwa chanzo cha migogoro kati ya jamii hizo mbili. (22.12.2020)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (wa kwanza kushoto) akipatiwa taarifa ya Mkoa wa Lindi na mkuu wa mkoa huo Mhe. Godfrey Zambi wakati Waziri Ndaki alipofika katika Wilaya ya Liwale kabla ya kuhudhuria mkutano kati ya wakulima na wafugaji ikiwa ni siku ya pili ya ziara yake ya kikazi Mkoani Lindi. (22.12.2020)


Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Uendelezaji wa Rasilimali za Vyakula vya Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Rogers Shegoto akielezea umuhimu wa kuendeleza maeneo ya malisho kwa kupanda malisho ya mifugo pamoja na kujenga miundombinu ya maji ili kudhibiti migogoro ya ardhi kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi, wakati wa kikao cha wakulima na wafugaji Mkoa wa Lindi kilichofanyika wilayani Liwale. (22.12.2020)

Muonekano wa wakulima na wafugaji waliohudhuria kikao kilichofanyika wilayani Liwale Mkoani Lindi chenye lengo la kutatua migogoro kati ya jamii hizo mbili, kikao hicho kimehudhuriwa pia na wakuu wa wilaya za Mkoa wa Lindi na viongozi wengine wa serikali ya mkoa wakiongozwa na mkuu wa mkoa huo Mhe. Godfrey Zambi ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki. (22.12.2020)




Jumatano, 23 Desemba 2020

ZECO YAPEWA SIKU 14 KUKAMILISHA UKARABATI WA BWAWA LA KIMOKUWA

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel ameipa Kampuni ya ZECO yapewa siku 14 kukamilisha ukarabati wab wawa la Kimokuwa litakalotumika kwa ajili ya matumizi ya kunyweshea mifugo na matumizi ya binadamu.

 

Prof. Gabriel ametoa maelekezo hayo leo (22.12.2020) wakati alipotembelea kukagua maendeleo ya ukarabati wa mradi huo unaotekelezwa katika kijiji cha Kimokuwa, wilayani Longido, mkoani Arusha.

 

“Mwanzoni kampuni hii ilianza kazi vizuri lakini mwishoni imekuwa na matatizo kwani usimamizi wao wa mradi sio mzuri kitu ambacho kimesababisha umaliziaji wa mradi kuwa na mapungufu,” alisema Prof. Gabriel.

 

Pia amemtaka mkandarasi kujiridhisha kwenye kingo za bwawa hilo walizoziweka kwani ikitokea zikabomoka hatua kali zitachukuliwa dhidi ya kampuni hiyo.

 

Kutokana na mapungufu aliyoyaona amempa mkandarasi siku 14 kuhakikisha anakamilisha mradi. Kutokana na kuwepo kwa mapungufu hayo, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Pauline Gekul hataupokea mradi huo kama ilivyokuwa imepangwa hapo awali.

 

Prof. Gabriel amewasihi wakandarasi wazawa kuhakikisha wanafanya kazi zao kwa umakini ili waendelee kuheshimika na kupewa kazi na serikali kwani fedha zinazotolewa za miradi zinatoka kwa wananchi walipa kodi. Hivyo amewataka wafanye kazi kwa uadilifu na kwa kuzingatia viwango.

 

Naye Katibu Tawala wa Wilaya ya Longido, Bw. Simba amempogeza Katibu Mkuu Gabriel kwa uamuzi wake wa kukagua maendeleo ya mradi huo kabla ya kukabidhiwa kwa mapungufu yaliyopo hata uongozi wa wilaya ulishayabaini. Lakini pia amemsihi mkandarasi kuhakikisha anayafanyia kazi mapungufu yote yaliyoainishwa katika ukaguzi huo ili wafugaji na jamii kwa ujumla iweze kupata huduma hiyo ya maji.

 

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kimokuwa, Bw. Kileli Olendere amesema Katibu Mkuu yupo sahihi kuamua kutomleta Naibu Waziri kuja kukabidhiwa bwawa hilo kwani ukarabati wake bado haujakamilika hivyo ni vema mkandarasi kwanza akamilishe kazi zinazotakiwa ndipo mradi ukabidhiwe kwa viongozi pamoja na wananchi.

 

Zephania Umbuli ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya ZECO Construction amesema ameyapokea maelekeo yaliyotolewa na Katibu Mkuu Gabriel na ameahidi kuyatekeleza ndani ya siku 14 walizopewa.

 

Ukarabati wa bwawa hili la Kimokuwa unaogharimu milioni 511.9 ulitakiwa kukamilika Novemba 25. 2020 lakini mkandarasi aliomba kuongezewa muda mpaka Decemba 10. 2020. Kutokana na mapungufu yaliyoainishwa amepewa siku 14 mpaka Januari 06, 2021 kuhakikisha anakamilisha kazi vinginevyo hatua za kimkataba zitaanza kuchukuliwa.




Katibu Mkuu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa maelekezo wakati akikagua maendeleo ya mradi wa ukarabati wa bwawa la kunyweshea maji mifugo na matumizi ya binadamu la Kimokowua lililopo wilayani Longido, mkoani Arusha. (22.12.2020)

Bwawa la Kimokuwa linaloendelea kukarabatiwa na Kampuni ya ZECO Construction kwa ajili ya kunyweshea maji mifugo na matumizi ya binadamu lililopo katika Kijiji cha Kimokuwa, wilaya ya Longido, mkoani Arusha. (22.12.2020)

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akionyesha moja ya mapungufu aliyoyabaini wakati wa ukaguzi wa mradi wa ukarabati wa bwawa la Kimokowua lililopo wilayani Longido, mkoani Arusha. (22.12.2020)


Jumanne, 22 Desemba 2020

SERIKALI YAJA NA MFUMO SHIRIKISHI KUDHIBITI UVUVI HARAMU


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesema serikali itaandaa mfumo shirikishi na endelevu wa kudhibiti zaidi uvuvi haramu ambao utafanya mikoa na wilaya zishiriki kikamilifu katika kutokomeza uvuvi huo badala ya kuwa na operesheni za kutafuta wavuvi haramu.

 

Waziri Ndaki amebainisha hayo (21.12.2020) alipokuwa katika mkutano wa hadhara na wakazi wa Kijiji cha Mchinga Namba Mbili, kilichopo Wilaya ya Mchinga Mkoani Lindi wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani humo na kubainisha kuwa mfumo huo utasaidia serikali kuondokana na operesheni za za vipindi maalum na badala yake mfumo uwe unafanya kazi siku zote.

 

“Tuwe na mfumo endelevu wa kumaliza kabisa tatizo la uvuvi haramu kwa hiyo tutafanya hivyo badala ya kuwa na operesheni au zimamoto ya kutafuta wavuvi haramu tuwe na mfumo unaofanya kazi siku zote huku mikoani, wilayani na mahali pengine popote.” Amesema Mhe. Ndaki

 

Waziri Ndaki amewataka pia watu wanaojihusisha na wanaofikiria kujiingiza katika uvuvi haramu kwamba watatafutwa popote watakapokuwa na watapata adhabu kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni za nchi huku akipongeza wananchi wanaoishi Ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi, kwa kudhibiti uvuvi haramu hususan unaotumia mabomu ambao kwa mujibu wa taarifa ya Mkoa wa Lindi, uvuvi huo umedhibitiwa kwa asilimia mia moja, huku akiahidi kuyafanyia kazi mapungufu yaliyopo ndani ya wizara katika kudhibiti uvuvi haramu.  

 

Aidha, kuhusu zao la mwani Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na wakazi hao wa Kijiji cha Mchinga Namba Mbili ameyataka makampuni yanayonunua zao hilo kutumia mizani zilizo sahihi na kuacha mara moja kuwadhulumu wakulima hao na kuwataka pia wakulima kuangalia uwezekano wa kuliongezea thamani zao hilo ili kuuza kwa bei nzuri tofauti na bei ya sasa ya kilo moja kwa Shilingi Elfu Moja ambayo wakulima hao wanasema haitoshelezi.  

 

Pia, amesema wizara itaangalia utaratibu kwa kushirikiana na halmashauri kuwawezesha wakulima wa mwani kupitia vikundi vyao katika kutengeneza bidhaa zitokanazo na mwani badala ya kuuza kama malighafi ili waweze kunufaika zaidi kibiashara kwa kujiongezea mapato.

 

Awali akiwa katika Ofisi za Mkoa wa Lindi, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amesomewa taarifa ya mkoa huo na Mkuu wa Wilaya ya Lindi Bw. Shaibu Ndemanga ambaye amemwakilisha mkuu wa mkoa huo Bw. Godfrey Zambi ambapo taarifa hiyo imebainisha mkoa kwa kushirikina na wizara umedhibiti uvuvi haramu kwa asilimia mia moja na kubainisha kuwa mkoa utaendelea kuhakikisha unadhibiti kabisa vitendo hivyo.

 

“Mheshimiwa Waziri katika eneo hili tumefanya vizuri sana miaka mitano iliyopita tusingeweza kusafiri kutoka pale Mnazi mmoja hadi hapa mkoani bila kusikia bomu tuna zaidi ya miaka mitatu hadi minne hatujasikia bomu kwa hili tumedhibiti kwa asilimia mia moja.” Amesema Bw. Ndemanga

 

Akizungumza kwa niaba ya wabunge wa Mkoa wa Lindi, Mbunge wa Jimbo la Mchinga Mama Salma Kikwete amemwambia Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki wavuvi wa mkoa huo wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya vifaa vya uvuvi kwa kuwa wanatumia zana duni badala ya kutumia boti za kisasa na kuwepo kwa soko la kisasa la kuuzia mazao ya samaki, huku akitaka pia akinamama wawezeshwe katika kilimo cha mwani hususan suala la bei.

 

“Lindi tuna changamoto za vitendea kazi tunakuomba mheshimiwa waziri ulichukue suala la changamoto uende nalo ukalifanyie kazi ninaamini na ninajua baada ya muda mfupi tutapata majibu ambayo ni chanya hususan katika upatikanaji wa boti ya kisasa ya uvuvi na suala la bei ya zao la mwani.” Amefafanua Mama Kikwete.

 

Mapema akiwa njiani kuelekea Mkoani Lindi kuanza ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani humo, ikiwa ya kwanza kikazi nje ya Mkoa wa Dodoma tangu kuapishwa kushika wadhifa huo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Magufuli, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amefika katika ofisi za taasisi na wakala zilizo chini ya wizara hiyo zilizopo Kata ya Naliendele, Manispaa ya Mtwara Mikindani na kuwataka watumishi hususan wa Kituo cha Ulinzi na Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi (FRP) kufuata sheria, taratibu na kanuni zilizopo katika kudhibiti uvuvi haramu na kutowaonea watu kwa kuwabambikizia kesi.

 

Amewataka watumishi hao kuwa waaminifu kwa kuhakikisha faini zinazolipwa ziwe halali za kieletroniki badala ya kuwaandikia faini kwa risiti za mkono na kutowaonea wavuvi kwa namna yoyote.

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki yuko katika ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani Lindi ambapo anatarajia pia kukutana na wakulima na wafugaji katika kuhakikisha serikali inaondoa kero za kutoelewana kati ya watu wanaojishulisha katika sekta hizo mbili.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza katika mkutano wa hadhara na wakazi wa Kijiji cha Mchinga Namba Mbili, kilichopo Wilaya ya Mchinga Mkoani Lindi wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani humo na kubainisha kuwa wizara itaandaa mfumo shirikishi wa kupambana na uvuvi haramu siku zote badala ya kuwa na operesheni za vipindi maalum. (21.12.2020) 

 


Mkuu wa Wilaya ya Lindi Bw. Shaibu Ndemanga ambaye amemwakilisha mkuu wa mkoa wa Lindi Bw. Godfrey Zambi katika ziara ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki, akitoa taarifa ya mkoa na namna walivyofanikiwa kutokomeza uvuvi haramu wa kutumia mabomu kwa asilimia mia moja. (21.12.2020) 


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (aliyekaa katikati) amepata fursa ya kusikiliza maoni, maswali na kero mbalimbali za wavuvi alipofanya ziara ya kikazi katika Kijiji cha Mchinga namba Mbili kilichopo Wilaya ya Mchinga Mkoani Lindi na kuahidi kero zinazohusu wizara atahakikisha anazifanyia kazi ili wavuvi waweze kufanya shughuli zao bila bughudha na kuwatahadharisha wasijiingize katika uvuvi haramu. (21.12.2020) 


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) akishika zao la mwani wakati alipotembelea mashamba ya zao hilo yaliyopo kwenye Bahari ya Hindi, katika kijiji cha Mchinga Namba Moja mara baada ya kufanya mkutano wa hadhara katika kijiji cha Mchinga Namba Mbili, vilivyopo Wilaya ya Mchinga Mkoani Lindi na kuwataka wakulima wa zao hilo waliongezee thamani kwa kutengeneza bidhaa mbalimbali zikiwemo sabuni. (21.12.2020) 


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki akiwa ameshika jongoo bahari ambapo ni moja ya mazao yaliyopo baharini ambayo yana soko kubwa nje ya nchi wakati alipokuwa anatembelea mashamba ya zao la mwani yaliyopo kwenye Bahari ya Hindi, katika kijiji cha Mchinga Namba Moja kiilichopo Wilaya ya Mchinga Mkoani Lindi. (21.12.2020) 


Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Nazael Madalla akifafanua namna wizara inavyochukua hatua mbalimbali kuhamasisha wananchi kufuga samaki, upatikanaji wa vifaranga bora pamoja na vyakula bora vya samaki, wakati wa kikao cha uongozi wa Mkoa wa Lindi na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki aliyefika mkoani hapo kwa ziara ya kikazi ya siku mbili. (21.12.2020)


GEKUL AONYA WANAOJIHUSISHA UVUVI HARAMU, UKWEPAJI KODI

 

Na Mbaraka Kambona, Manyara

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul amewataka wale wote wanaojihusisha na uvuvi usiozingatia sheria na taratibu kuacha mara moja kwani Serikali haitakuwa na huruma kwa watakaokamatwa.

 

Gekul alitoa onyo hilo alipokuwa akiongea na Wavuvi wa Mkoa wa Manyara alipofanya ziara mkoani humo Disemba 21, 2020.

 

Kwa mujibu wa Waziri Gekul katika operesheni ya kupambana na uvuvi haramu iliyopita ilitumika karibu bilioni 1. 2 jambo ambalo alisema halivumiliki na hivyo aliwataka wavuvi kutoa ushirikiano kwa serikali ili kukomesha vitendo hivyo.

 

“Hatutavumilia jambo hili liendelee, Sisi kama Wizara tumesema ni lazima tupate muarobaini wa uvuvi haramu lakini na nyinyi wavuvi muwe tayari kutoa ushirikiano kwa serikali ili uvuvi haramu ukomeshwe mara moja,” alisema Gekul

 

Aliongeza kwa kusema kuwa uvuvi haramu ukikomeshwa itasaidia kuokoa mazalia ya samaki na kuongeza idadi ya samaki katika maziwa na maeneo mengine.

 

“Kwa kuwa mmeonesha nia ya kutoa ushirikiano katika hili, shirikianeni na viongozi wenu kuanzia leo hizo nyavu haramu zikatupwe, tusisikie tena kuhusu nyavu haramu iwe mwanzo na mwisho ,” aliongeza Gekul

 

Aidha, Waziri Gekul alisema kuwa kipaumbele cha serikali kwa sasa ni kuimarisha ufugaji wa viumbe maji kwa kutumia Vizimba na Mabwawa jambo ambalo anasema likisimamiwa vizuri litaongeza ajira kwa wananchi na kupunguza umasikini na kuchochea uchumi wa taifa letu. 

 

“Niwaombe Wakurugenzi na Viongozi wengine wa Halmashauri waangalie uwezekano kwenye zile asilimia kumi zinazotolewa na Serikali kwa Vijana, Wanawake na Walemavu badala ya kuwapa mkononi wafanye utafiti ili kujua ujenzi wa mabwawa unagharimu kiasi gani ili wawajengee mabwawa ya kufugia samaki na tukiweza kufanya hivyo tutakuwa tumepunguza tatizo la ajira,” alisisitiza Gekul

 

Katika hatua nyingine, Gekul aliwaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri na Maafisa uvuvi kuwafikia wavuvi wote na kuhakikisha wanalipia leseni za uvuvi ili kuzuia upotevu wa mapato na kukuza pato la Serikali.

 

“Hili litekelezwe haraka, kila mtu ajisikie vizuri kulipa kodi ya serikali, lipeni kodi na mpatiwe risiti za mashine za elekroniki kwa kufanya hivyo kutazuia upotevu wa mapato ya serikali,” alifafanua

 

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Babati, Lazaro Twange alisema kuwa maelekezo yote yaliyotolewa na Naibu Waziri wameyapokea na watayafanyia kazi kama ilivyoelekezwa ili sekta ya uvuvi mkoani humo iweze kupiga hatua inayotarajiwa.

 

“Tutahakikisha wavuvi wote tunawafikia kwa lengo la kutatua kero zinazowakabili lakini vile vile wale ambao hawana leseni waweze kukata leseni ili serikali iweze kuwatambua na kupata mapato kupitia shughuli za uvuvi,” alisema Twange

 

Mwenyekiti wa Wavuvi, Halmashauri ya Babati, Iddi Hassani alisema kuwa watafanyia kazi maelekezo na watahakikisha wanashirikiana na serikali ili wavuvi wote wawe na leseni za uvuvi na wataendelea kupambana na uvuvi haramu ili kunusuru viumbe maji na kuendelea kufanya uvuvi endelevu.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul akisisitiza jambo kwa Muwakilishi wa Kampuni ya XIN SI LU, Suvi Zeng (hayupo pichani) alipotembelea eneo la ufugaji wa Samaki kwa kutumia Mabwawa la Kampuni hiyo lililopo Mkoani Manyara Disemba 21, 2020. Nyuma yake ni Viongozi wa Serikali pamoja na Wananchi waliojitokeza kumpokea Naibu Waziri huyo. 


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (kulia) akipokea samaki aina Sato kutoka kwa Mkurugenzi, Idara ya Uvuvi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Magese Bulayi alipotembelea  eneo la  Kampuni ya XIN SI LU kutoka China iliyowekeza katika ufugaji wa Samaki kwenye Mabwawa Mkoani Manyara Disemba 21, 2020. 


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (kushoto) akimsikiliza Kaimu Mkurugenzi Msaidizi, Ukuzaji Viumbe Maji, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Imani Kapinga alipokuwa akimpa maelekezo Mwakilishi wa Kampuni ya XIN SI LU,  Suvi Zeng (katikati) alipotembelea eneo la ufugaji wa Samaki katika Mabwawa la Kampuni hiyo Disemba 21, 2020.