Nav bar

Ijumaa, 29 Novemba 2019

HABARI PICHA NA MATUKIO

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akifanya tathmini ya ubora wa samaki aina ya jodari katika Soko la Samaki la Msasani jijini Dar es Salaam wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mvuvi Duniani inayoaadhimisha Novemba 21 kila mwaka.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) akikagua mwalo wa Soko la Samaki la Msasani jijini Dar es Salaam mara baada ya kuwasili katika soko hilo kama mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya Siku ya Mvuvi Duniani inayoadhimishwa Novemba 21 kila mwaka.

Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Viumbe Maji Dkt. Nazael Madala akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Rashid Tamatamah wakati akizungumza na baadhi ya washiriki wakiwemo wavuvi kwenye maadhimisho ya Siku ya Mvuvi Duniani yaliyofanyika katika Soko la Samaki Msasani jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Mvuvi Duniani yaliyofanyika katika Soko la Samaki la Msasani jijini Dar es Salaam akizungumza na washiriki kwenye maadhimisho hayo ambapo pamoja na mambo mengine amesisitiza ufugaji samaki katika Ukanda wa Pwani, pamoja na kutoa zawadi kwa wavuvi walioshinda katika zoezi la uvuaji wa samaki aina ya jodari.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi pamoja na baadhi ya washiriki wakiwemo wavuvi kwenye maadhimisho ya Siku ya Mvuvi Duniani yaliyofanyika katika Soko la Samaki la Msasani jijini Dar es Salaam. Maadhimisho hayo yanafanyika Novemba 21 kila mwaka.


Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kinondoni Mhe. Benjamin Sitta (Kulia) na Katibu Mtendaji wa Muungano wa Taifa wa Uvuvi wa Jodari Tanzania Bw. Winfried Haule wakizungumza na washiriki wa maadhimisho ya Siku ya Mvuvi Duniani (hawapo pichani) yanayoadhimishwa Novema 21 kila mwaka, ambapo mwaka huu kitaifa yamefanyika katika Soko la Samaki la Msasani jijini Dar es Salaam.

WAFUGAJI WAFURAHIA KUPATA MAENEO YA MALISHO



Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega ametatua changamoto ya wafugaji na wananchi wa Kata ya Mabuki katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza kwa kusimamia upatikanaji wa shamba la hekta 450 kwa ajili ya kunenepeshea mifugo.


Mhe. Ulega amesema shughuli za unenepeshaji wa ngombe unatakiwa kuanza mapema ili kuwasaidia wafugaji ambapo ametoa muda wa wiki moja kwa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA) kampasi ya Mabuki, Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Kituo cha Mabuki na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo wawe wameshaanza mchakato wa kuwapatia wafugaji maeneo hayo.


Akizungumza na wafugaji na wananchi wa Kata ya Mabuki katika ziara ya siku moja wilayani Misungwi, Mhe. Ulega amesema wafugaji wengi nchini wanapata shida ya malisho kwa mifugo yao wakati wa kiangazi, hivyo ili kuongeza thamani na kufanya ufugaji kuwa na tija wizara imekuja na njia ya kisasa ya kunenepesha mifugo wakiwemo ngombe ambapo watakuwa wanauza kwa kumpima ng’ombe uzito kwa mzani badala ya kuuza kwa makisio.


Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumetoa eneo la hekta 450 kwa ajili ya wafugaji wa Mabuki kunenepeshea mifugo yao kama ngombe kupitia kituo cha TALIRI Mabuki ambacho kimetoa hekta 150 huku shamba la L.M.U hekta 300, ambapo mashamba hayo yatakodishwa kwa utaratibu wa kuingiza mifugo, hivyo wananchi mzingatie kuwa maeneo hayo ni maalum kwa ajili ya kunenepeshea na atakayebainika ametoa rushwa ili kupatiwa eneo hatopata nafasi hiyo. Amesema Mhe.Ulega.


Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa kituo cha TALIRI Mabuki Dkt. Hemel Massawe akizungumzia utaratibu wa kuingiza ngombe katika mashamba ya kunenepeshea mifugo amesema, kwa hekta moja ngombe watano ndio wanapaswa kuingizwa ambapo gharama za kukodi ni shilingi 30,000 kwa miezi 6.


Naye Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Bw. Juma Sweda amesema, shamba hilo ni mali ya serikali hivyo maeneo hayo yanaweza yasitoshe kwani kuna vijiji 12 katika kata hiyo na wafugaji ni wengi na ngombe ni wengi hivyo wanahitaji kuvumiliana pia kupitia shamba hilo vijana wanapata ajira kwa kupata maziwa ya kutosha kuchakata na kuuza.


Hata hivyo baadhi ya wananchi na wafugaji wa kata hiyo akiwemo Bw. Bernard Bukumbi na Bw. Severine Masele wameishukuru ierikali kupitia wizara hiyo kwa kuwapatia shamba ambalo litawapa nafasi ya kupeleka ngombe wao kunenepeshwa.




Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (Mb), akiongea kwenye mkutano wa hadhara na wanakijiji wa Mabuki Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza. (17/11/2019)

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akitoa maelekezo kwa viongozi mbalimbali wa kata, vijiji na Wilaya juu ya namna ya kuwasaidia wafugaji kupata haki zao bila kuonewa , kusikiliza changamoto zinazowakabili na kutafuta suluhu kabla la tatizo kubwa kutokea, wakati wa mkutano wa hadhara kwenye  kijiji cha mabuki, Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza. (17/11/2019)

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akipokelewa kwa furaha na wanakijiji wa Mabuki, Wilayani Misungwi alipowatembelea, kusikiliza na kutatua changamoto ya upatikanaji wa maeneo ya kufugia Mifugo yao mkoani Mwanza. (17/11/2019)

Alhamisi, 28 Novemba 2019

SERIKALI YAAHIDI KUENDELEA KUSIMAMIA MASLAHI YA WAFUGAJI NA KUWATAKA KUFUATA SHERIA ZA NCHI.



Serikali imewataka wafugaji katika Wilaya za Chunya na Mbarali Mkoani Mbeya kufanya shughuli zao kwa kufuata sheria na taratibu za nchi ikiwemo ya kutoingiza mifugo katika maeneo ya Hifadhi za Taifa ya Ruaha na Pori la Akiba la Ruangwa, hali ambayo imekuwa ikisababisha migogoro kati ya wafugaji na askari wa Hifadhi za Taifa (TANAPA), wanaolinda hifadhi hizo ambapo baadhi ya migogoro hiyo imesababisha vifo vya wafugaji, askari na mifugo.

Akizungumza Jumanne hii (19.11.2019) wakati wa kuhitimisha ziara ya siku mbili ya makatibu wakuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Wizara ya Sheria na Katiba, waliozuru baadhi ya maeneo yenye migogoro katika wilaya hizo, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka wafugaji kuacha tabia ya kuingiza mifugo katika maeneo ya hifadhi kwa ajili ya malisho kwa kuwa ni kinyume na taratibu za nchi.

“Serikali inawataka wafugaji wote kufanya shughuli zao kwa kufuata sheria na kutoingiza mifugo katika maeneo ya hifadhi za taifa kwa kuwa ni kinyume cha sheria pia serikali itaendelea kuhakikisha wafugaji wanafanya shughuli zao kwa amani bila kubughudhiwa ili mradi wanafuata sheria na taratibu za nchi ikiwemo ya kutoingiza mifugo katika mashamba ya wakulima.” Amesema Prof. Gabriel

Akizungumza kwa niaba ya makatibu wakuu wa wizara hizo, Prof. Gabriel amefafanua kuwa kutokana na Tangazo la Serikali (GN) Na. 28 la Tarehe 14 mwezi Machi mwaka 2008, ambalo liliongeza eneo la Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kutoka Kilometa za Mraba 5,878 hadi kufikia Kilometa za Mraba 20,226 hali hiyo imesababisha eneo la malisho kupungua kutoka hekta 259,000 za awali hadi 154,000 katika Wilaya za Chunya na Mbarali ambapo amewataka wafugaji katika wilaya hizo kuheshimu tangazo hilo wakati serikali ikifanyia kazi maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ya kuainishwa kwa vijiji vilivyopo katika maeneo ya hifadhi ili maboresho yaweze kufanyika kwa maslahi ya vijiji hivyo.

Katika ziara hiyo ya makatibu wakuu kutoka wizara nne Mkoani Mbeya uongozi wa TANAPA umekubali kutengeneza barabara za kuainisha mipaka ya maeneo ya hifadhi na vijiji mara baada ya kuainishwa kwa mipaka mipya kufuatia agizo la Rais Dkt. John Magufuli la kutambuliwa kwa maeneo ya vijiji na hifadhi za taifa ambalo tayari linafanyiwa kazi.

Kufuatia matukio ya mauaji ya askari mmoja wa TANAPA na askari mgambo mmoja mwaka 2018 waliouawa na wafugaji wakati wakiswaga ng’ombe waliokamatwa katika Hifadhi ya Ruaha kuelekea Kambi ya Nyota ya TANAPA iliyopo Wilaya ya Mbarali na tukio la hivi karibuni la Tarehe 11 Mwezi Oktoba 2019 la kuvamiwa kwa kambi hiyo na baadhi ya wafugaji wakiwa na silaha za jadi kwa nia ya kukomboa mifugo iliyokamatwa katika Hifadhi ya Ruaha hali iliyosababisha kijana mmoja wa wafugaji (19) kupigwa risasi na askari wa TANAPA na ng’ombe 14 kuuawa, Katibu Mkuu Prof. Gabriel amewataka wafugaji kutumia njia zisizo halali kukomboa mifugo iliyokamatwa.

Akizungumza na baadhi ya wafugaji katika Kijiji cha Igunda, Kata ya Igava Wilayani Mbarali, katibu mkuu huyo amefafanua kwa wafugaji hao kuwa kutokana na sheria na haki za wanyama duniani ni makosa kuua mnyama bila kuwa na sababu za msingi hali iliyosababisha serikali kuchukua hatua kwa askari wa TANAPA waliohusika kupiga ng’ombe hao risasi na hivyo kuwataka wafugaji hao kuwa watulivu kwa kuwa suala hilo linashughulikiwa na vyombo vya dola.

Aidha ameeleza kuwa kuwa pindi mifugo inapokamatwa na askari wa TANAPA inapobainika kuingia kwenye maeneo ya hifadhi, wamiliki wa mifugo hiyo wanapaswa kufuata taratibu za kisheria za kulipa faini na kukabidhiwa mifugo yao na kusisitiza kuwa ni muhimu kwa wafugaji kujiepusha kuingiza mifugo maeneo wasiyoruhusiwa yakiwemo ya Hifadhi za Taifa.

“Sisi viongozi wa Wizara za Mifugo na Uvuvi, Maliasili na Utalii, Mambo ya Ndani ya Nchi na Sheria na Katiba tunasikitishwa sana na matukio haya ya mauaji kijana mdogo amefariki dunia kwa sababu ambazo zingeweza kuepukika kwa kutaka kumdhuru askari kwa kutumia silaha za jadi akiwa na wenzake takriban 20 ili kukomboa ng’ombe waliokamatwa hifadhini, tunawaomba mjiepushe na matukio ya namna hii fuateni sheria na taratibu za nchi ili mfuge bila bughudha.” Amefafanua Prof. Gabriel

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akiwaongoza viongozi wenzake katika ziara hiyo akiwemo Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bw. Ramadhan Kailima, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Sheria na Katiba Bw. Amon Mpanju na Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori Dkt. Maurus Msuha akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Prof. Adolf Mkenda wamefika pia katika Kijiji cha Lualaje Kata ya Lualaje Wilayani Chunya na kuzungumza na baadhi ya wafugaji kufuatia matukio ya wafugaji hao kuingiza ng’ombe katika Hifadhi ya Ruaha.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bw. Ramadhan Kailima amewataka wafugaji hao kufuata sheria na taratibu za nchi na kwamba jeshi la polisi litazidi kutoa ushirikiano kwa wafugaji hao katika matukio mbalimbali yakiwemo ya kuwabaini baadhi ya wafugaji ambao wamekuwa wakiingiza mifugo katika maeneo ya hifadhi pamoja na kujihusisha na uhalifu.

Naye Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Sheria na Katiba Bw. Amon Mpanju amewataka wafugaji kuwa watulivu na walitambue Tangazo la Serikali Na. 20 la Tarehe 14 mwezi Machi mwaka 2008, ambalo liliongeza eneo la Hifadhi ya Taifa ya Ruaha na kupunguza eneo la malisho katika Wilaya za Chunya na Mbarali hali iliyosabisha baadhi ya maeneo waliyokuwa wakiyamiliki kubadilishwa matumizi na kuwa ya hifadhi, ambapo suala hilo tayari linafanyiwa kazi kwa maelekezo ya Rais Magufuli na kuwataka kutoingiza mifugo yao katika eneo la hifadhi hadi serikali itakapotangaza maamuzi mengine.

Kuhusu kuainishwa kwa mipaka kati ya vijiji na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha pamoja na Pori la Akiba la Ruangwa, akizungumza kwa niaba ya katibu mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori kutoka katika wizara hiyo Dkt. Maurus Msuha amesema serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii itahakikisha inatuma timu ya wataamu katika maeneo hayo ili kuweka alama maeneo ambayo wananchi yanawatatiza kufahamu mipaka ya vijiji na maeneo ya hifadhi ili kuondoa migogoro kati ya maeneo ya wakulima na wafugaji na mipaka ya Hifadhi ya Ruaha na Pori la Akiba la Ruangwa.

Baadhi ya wananchi katika Wilaya za Chunya na Mbarali waliopata fursa ya kuzungumza wakati wa ziara ya makatibu wakuu kutoka Wizara za Mifugo na Uvuvi, Maliasili na Utalii, Mambo ya Ndani ya Nchi na Sheria na Katiba wamesema wamefurahishwa na ziara hiyo na kwamba watazingatia maelekezo waliyopatiwa ili kuhakikisha wanafuga kwa kufuata sheria na kwamba watashirikiana na serikali ili kuwabaini baadhi ya wafugaji wanaokiuka sheria na kuingiza mifugo katika maeneo ya Hifadhi ya Ruaha na Pori la Akiba la Ruangwa.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wamefafanua kuwa wamefurahishwa kwa viongozi hao wa juu kutoka wizarani kufika hadi katika maeneo yao na kujionea changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo ya maji na malisho pamoja na kupata taarifa za matukio ambayo yamejitokeza katika wilaya hizo kutoka mamlaka mbalimbali za serikali wakiwemo viongozi wa serikali, wafugaji pamoja jeshi la polisi.

Awali kabla ya makatibu wakuu hao kutembelea wafugaji katika Wilaya za Chunya na Mbarali, wamefika katika Ofisi ya Mkuu wa Mbeya na kuwa na mazungumzo na mkuu wa mkoa huo Mhe. Albert Chalamila pamoja Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mbeya, ambapo Mhe. Chalamila amewaambia serikali ya mkoa huo itaendelea kufanya kazi kwa kusimamia sheria na kuwaasa viongozi wenzake wanapofika mkoani hapo kupata taarifa sahihi ya mkoa kabla ya kufika katika maeneo mbalimbali kuzungumza na wananchi.

Aidha Mhe. Chalamila amebainisha kuwa migogoro ya wafugaji katika Wilaya za Chunya na Mbarali ambao wamekuwa wakiingiza mifugo kwenye maeneo ya Hifadhi ya Ruaha na Pori la Akiba la Ruangwa katika Mkoa wa Mbeya unatokana na wafugaji kuwa na mifugo mingi tofauti na maeneo ya malisho, hali ambayo imekuwa ikiulazimu uongozi wa mkoa kutoa elimu kwa wafugaji juu ya ufugaji wa kisasa na wenye tija kwa wafugaji kuwa na ng’ombe wachache wanaoweza kuwapatia matokeo mazuri.

Ameongeza kuwa uongozi wa Mkoa wa Mbeya utazidi kusimamia na kutoruhusu mifugo kuingizwa katika maeneo ya hifadhi pamoja na maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira ili kuhakikisha mkoa huo unakuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi.

Katika ziara hiyo ya makatibu wakuu wanne Mkoani Mbeya, ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akiambatana na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bw. Ramadhan Kailima, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Sheria na Katiba Bw.
Amon Mpanju na Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori Dkt. Maurus Msuha akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Prof. Adolf Mkenda, ilikuwa na lengo la kupata taarifa sahihi ya hali ya wafugaji katika Wilaya za Chunya na Mbarali pamoja na kupata hadidu za rejea ambazo wataalam watatumia katika kufanya mapitio na maboresho ya Tangazo la Serikali (GN) Na. 28 la Mwaka 2008 ili iwe shirikishi na kupata suluhu ya migogoro ya wakulima na wafugaji.


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Albert Chalamila akiongea na makatibu wakuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Maliasili na Utalii na Wizara ya Sheria na Katiba, mara baada ya kufika ofisini kwake kwa ajili ya kupata taarifa ya hali ya ufugaji katika Wilaya za Chunya na Mbarali ambapo kumekuwa kukijitokeza migogoro ambayo imesababisha vifo vya askari wa Hifadhi za Taifa (TANAPA), askari mgambo, wafugaji na mifugo kutokana na mifugo kuingia katika Hifadhi ya Ruaha na Pori la Akiba la Ruangwa, kabla ya makatibu hao kutembelea maeneo hayo katika ziara ya siku mbili kuanzia Tarehe 18-19 mwezi Novemba 2019.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel (Picha ya kwanza kushoto), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bw. Ramadhan Kailima (Picha ya kwanza ndogo), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Sheria na Katiba Bw. Amon Mpanju (Picha ya pili ndogo) na Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori Dkt. Maurus Msuha akimwakilisha katibu mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii wakizungumza na wananchi katika Kijiji cha Lualaje, Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya juu ya kutoingiza mifugo katika maeneo ya Hifadhi ya Ruaha na Pori la Akiba la Ruangwa wakiwa kwenye ziara ya kutatua changamoto zinazoikabili wilaya hiyo hususan kwa wananchi wanaojishughulisha na kilimo na ufugaji katika ziara ya siku mbili Mkoani Mbeya kuanzia tarehe 18-19 mwezi Novemba 2019.


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akiangalia moja ya vielelezo pamoja na kuoneshwa ramani ya mipaka iliyowekwa kutenganisha maeneo ya vijiji na Hifadhi ya Ruaha na Pori la Akiba la Ruangwa, katika ziara ya siku mbili Mkoani Mbeya kuanzia tarehe 18-19 mwezi Novemba 2019 akiwa na viongozi wengine kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Sheria na Katiba na Wizara ya Maliasili na Utalii.

 

Jumatano, 27 Novemba 2019

WAZIRI MPINA AZINDUA VITUO VYA UCHUNGUZI WA MAGONJWA YA MIFUGO SUMBAWANGA



WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amezindua kwa pamoja vituo viwili vya Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo (ZVC) na Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Magharibi- Sumbawanga na kutangaza msimamo wa Serikali ya awamu ya tano wa kupambana na magonjwa ya mifugo ili kuongeza uzalishaji wa mifugo na mazao yake nchini.

Hivyo Serikali inawahakikishia wananchi uhakika wa upatikanaji wa chanjo kwa bei nafuu kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanyika ikiwa ni pamoja na Taasisi ya Chanjo (TVI) kuzalisha chanjo za kimkakati 11 ifikapo Juni mwakani na kwamba Serikali iko mbioni kutangaza bei elekezi ya Chanjo ili kuwadhibiti watu wachache waliokuwa wanawaibia wananchi.

Aliongeza kuwa hivi sasa kuna ujenzi mkubwa wa Kiwanda kipya cha kuzalisha chanjo cha Hester Bioscience Africa Limited (HBAL) ambacho kitazalisha chanjo 27 ifikapo Juni na uwekezaji wake una thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 50 na kuwezesha upatikanaji wa chanjo zote kwa wafugaji wa ndani ya nchi, Afrika na Dunia.

Akizungumza mara baada ya kuzindua vituo hivyo vitakachohudumia mikoa ya Songwe, Rukwa na Katavi vyenye makao yake mjini Sumbawanga, Waziri Mpina amesema kamwe Serikali haiwezi kukubali mifugo iendelee kufa kwa magonjwa na kwamba sasa magonjwa hayo hayana nafasi tena nchini.

Hivyo Serikali imeamua kuandaa Kanuni mpya za usimamizi wa uogeshaji na uchanjaji mifugo ili kudhibiti utoaji wa chanjo kwa wananchi na kwamba itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa wote wataokwenda kinyume na kanuni hizo.

Hivyo ameziagiza halmashauri zote nchini kuhakikisha zinashirikiana kwa karibu na vituo vya uchunguzi wa magonjwa na wakala wa maabara ya magonjwa ya mifugo vilivyoko katika kanda zao ili kutoa huduma bora kwa wafugaji na kuongeza uzalishaji wa mifugo na mazao yake.

Waziri Mpina pia amemuagiza Katibu Mkuu Mifugo na Katibu Mkuu Tamisemi kufanya mgawanyo mpya wa maafisa mifugo ili kuweza kupelekwa kwenye maeneo ambayo hayana kabisa maafisa mifugo ukiwemo Mkoa wa Katavi ambao hauna kabisa Madaktari wa Mifugo.

Pia ameagiza ZVC na TVLA Kanda ya Magharibi Sumbawanga kuwa wasimamizi na walezi wazuri wa wafugaji na mifugo na kuhakikisha kuwa chanjo, uogeshaji na haki za mifugo zinasimamiwa kikamilifu.

Waziri Mpina pia ameiagiza Kanda kusimamia kikamilifu uingizaji wa chanjo, madawa, viuatilifu, chakula na mazao ya mifugo yanayoingizwa nchini bila vibali, bila kulipiwa ushuru, bila kukaguliwa na yaliyokwisha muda wa matumizi na feki.

Kufuatia mageuzi ya utoaji huduma za mifugo nchini, Waziri Mpina amemwagiza Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo kufanya ukaguzi wa maafisa wa kanda zote ili kupanga safu mpya itakayokuwa tayari kuendana na kasi ya Serikali ya awamu ya tano.

Waziri Mpina ameonya kuwa siku nyingine ikitokea hatua zikachelewa kuchukuliwa kwa maafisa wanaohujumu mifugo basi Mkurugenzi wa huduma za mifugo ataondolewa kwenye wadhifa wake.

Waziri Mpina alisema wafugaji walikuwa wakipata huduma za uchunguzi wa magonjwa kilichopo Iringa umbali wa zaidi ya kilomita 900 kutoka Sumbawanga hali ilisababisha ugumu kwa wafugaji na kusababisha vifo vingi vya mifugo

Hivyo Waziri Mpina amebanisha kuwa uanzishaji wa kanda hiyo utaongeza ufanisi wa kazi ya udhibiti wa magonjwa ya mifugo katika mikoa ya Songwe, Rukwa na Katavi na kuleta ahueni kubwa kwa wafugaji.

Mpina aliongeza kuwa hadi sasa kuna Kanda 8 za Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo na Kanda 11 za Wakala wa Maabara Tanzania (TVLA) ambapo wizara inakusudia kuanzisha kanda nyingine moja katika mwaka fedha wa 2019/ 2020 itakayohudumia mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga kituo hicho kikikamilika kitasogeza huduma ya udhibiti wa magonjwa katika mikoa hiyo.

Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo nchini, Dk Hezron Nonga amesema tangu kuanzishwa kwa kituo hicho kumewezesha kuongezeka kwa huduma za uchunguzi wa magonjwa ya mifugo na mazao yake, shughuli za uchunguzi kimaabara zimesogezwa karibu na wananchi.

Pia upatikanaji wa chanjo kwa wafugaji kwa bei nafuu umekuwa rahisi, kuongezeka kwa upatikanaji wa taarifa za magonjwa , kuongezeka kwa majosho hamasa ya wafugaji kuongeza mifugo na idadi ya lita za kuogesha mifugo.

Pia ongezeko la maduhuli ya Serikali yatokanayo na usafirishaji wa mifugo na mazao yake ndani na nje ya nchi kutoka makadirio ya sh milioni 120 kwa mikoa miwili Rukwa na Katavi hapo awali na kufikia makadirio ya sh milioni 500 kwa mwaka, kufanikiwa kudhibiti ugonjwa wa homa ya nguruwe.

Dk Nonga amesema pia kumeongezeka mahusiano kati ya wizara na Serikali za mitaa na hivyo kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za mifugo kwa wananchi tofauti na ilivyokuwa awali.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina afungua kituo cha kanda cha ufuatiliaji, utambuzi na kuzuiaiya magonjwa ya mifugo Kanda ya Kusini Magharibi Sumbawanga tarehe 30/10/2019 Mkoani Rukwa.


WAZIRI MPINA AZINDUA AGENDA ZA UTAFITI NA KUIBUA TAFITI ZILIZOFICHWA.



WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amezindua Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Mifugo, Uvuvi na Ukuzaji wa Viumbe Maji ya mwaka 2020-2025 na kutangaza kuzifumua na kuziibua tafiti zote  zilizofanywa na wasomi na kutelekezwa kwenye makabati miaka ya nyuma na kuziingiza kwenye mfumo rasmi wa matumizi ili kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na maendeleo.

Pia agenda hizo zitaleta msisimko mpya wa kufanya utafiti nchini na kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na maendeleo tofauti na ilivyokuwa kipindi cha nyuma ambapo tafiti nyingi zilifanywa na kutelekezwa kwenye makabati na watafiti mbalimbali wakiwemo Wanafunzi wa Shahada ya Uzamili (Masters Degree)  na Shahada ya Uzamivu (PHD) katika vyuo vikuu mbalimbali.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa agenda hizo kitaifa katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Kampasi ya Mazimbu mjini Morogoro, Waziri Mpina aliziagiza Taasisi ya Utafiti wa Mifugo(TALIRI) na Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi(TAFIRI) kubadilika ili kufanya tafiti kwa vigezo vilivyowekwa na kuleta mabadiliko chanya katika sekta za mifugo na uvuvi nchini.

Waziri Mpina alisema chimbuko la kuandaliwa kwa ajenda hizo za utafiti ni baada ya kubaini kuwa ajenda zilizokuwepo awali za Mifugo na Uvuvi zilishindwa kuibua na kuzitumia tafiti zilizofanywa kuchochea mabadiliko kwenye sekta hiyo muhimu ya uzalishaji.

Pia ajenda za utafiti zilizokuwepo za Mifugo na Uvuvi hazikuwa na utaratibu wa kuzitambua, kuziorodhesha na kuzitumia tafiti zinazofanywa na Wanafunzi wa Shahada ya Uzamili (Masters Degree) na Uzamivu (PHD) lakini sasa ajenda za utafiti zilizozinduliwa zimeweka utaratibu wa namna ya kuzitambua, kuziorodhesha na kuzitumia tafiti za wasomi hao.

“Haiwezekani tafiti za wasomi wa kiwango cha juu kiasi hicho wanazozifanya wakati wa kukamilisha masomo yao ziishie kupata alama za ufaulu na kutupwa kwenye makabati, Leo kila mhitimu atalazimika kuandaa policy brief ambayo itawezesha watumiaji na Serikali kurekebisha au kuandaa Sera na Sheria” alisema Waziri Mpina.

Aliongeza kuwa Ajenda za Utafiti zilizokuwepo za Mifugo na Uvuvi hazikuwa na utaratibu wa kuweka Kanuni ambazo zitahakikisha kuwa utekelezaji  wa ajenda za utafiti unafanyika, lakini ajenda za utafiti iliyotangazwa inaweka Kanuni zitakazotoa mwongozo na usimamizi wa utekelezaji na wajibu wa kila mhusika.

Aidha Waziri Mpina alibainisha kuwa ajenda za utafiti zilizokuwepo za Mifugo na Uvuvi hazikuwa na utaratibu wa kuwaunganisha Watafiti wa Mifugo na Uvuvi nchini, na hivyo kupelekea kila mmoja kufanya utafiti kivyake hali iliyosababisha jambo moja kufanyiwa utafiti na mtafiti zaidi ya mmoja na kukosa jukwaa la kuratibu na kuchambua tafiti zinazofanywa nchini.

“Agenda ninayoizindua leo inakwenda kujumuisha watafiti na wataalam mbalimbali waliobobea katika fani za mifugo, uvuvi na ukuzaji wa viumbe maji ili kuyapitia matokeo ya utafiti, teknolojia zilizoibuliwa
na utafiti na kuzisambaza kwa watumiaji kwa manufaa ya Taifa” alisema Waziri Mpina
Pia Waziri Mpina alibainisha mapungufu mengine yaliyomo kwenye ajenda za utafiti zilizokuwepo za Mifugo na Uvuvi ni pamoja na kutoweka msingi mzuri wa kusimamia Watafiti na kufanya tafiti kulingana na mahitaji ya soko badala yake  Taasisi za Utafiti na Watafiti kufanya tafiti nyingi za nje na mambo muhimu ya wananchi yanayohitaji kufanyiwa utafiti kutelekezwa.

“Leo hii agenda ninazozizindua zimeweka utaratibu wa kuzingatia vipaumbele vya kitaifa, kupanua mtandao wa utafiti  na kufanya tafiti zote kulingana na mahitaji ya wananchi.  Mfano katika maeneo ya nyama, maziwa, samaki, ngozi, chakula cha samaki na mifugo, magonjwa, malisho na migogoro” alisema Mpina.

Aidha dosari nyingine zilizokuwepo kwenye ajenda za utafiti zilizokuwepo za Mifugo na Uvuvi ni kutojumuisha katika vipaumbele masuala mengi muhimu yenye changamoto nyingi ikiwemo  Mitaala na hali ya ajira.

Mpina alisema mitaala inapoanzishwa haifanyiwi utafiti wa mara kwa mara matokeo yake mafunzo yanayotolewa sio yale yanayohitajika katika soko la ajira huku Wanafunzi wanaohitimu mafunzo hawajulikani wanakwenda wapi baada ya kuhitimu na hakuna mfumo wowote wa uratibu.

“Ukienda kwa wafugaji wanaofuga na kuchunga sio hao waliosomea mifugo, ukienda kwa Wavuvi na Ukuzaji viumbe maji wanaovua na kufuga si hao waliosomea taaluma hizo, ukienda viwandani vilevile”alisema Mpina.

Pia Masoko na Biashara, Uongezaji wa mnyororo wa thamani wa mazao ya mifugo na uvuvi (Livestock and Fisheries value chain value addition), agenda iliyopita ilizingatia uzalishaji pekee bila kuangalia upande wa soko wakati vitu hivi vinakwenda kwa pamoja kwani hakuna uzalishaji bila soko.

Waziri Mpina pia alisema licha ya kushamiri kwa migogoro ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi na eneo hilo kugubikwa na changamoto nyingi  ikiwemo  mifugo kutaifishwa, kupigwa risasi, kufilisiwa, kuuwawa kwa watu na mifugo  na kupigwa faini kubwa kiasi cha kutishia uendelevu wa sekta lakini eneo hili halikujumuishwa katika Agenda ya utafiti iliyopita.

Pia masuala mtambuka, afya ya wanyama na magonjwa ya afya ya jamii (Zoonotic Diseases) ambapo hivi sasa asilimia 60 ya magonjwa yasiyoambukiza yanatokana na mazao ya mifugo, malisho, nyanda za malisho na vyakula vya mifugo na samaki, uvuvi endelevu katika maji ya asili (Uvuvi Haramu na utoroshaji wa mazao ya uvuvi)  ambayo nayo hayakuzingatiwa katika agenda za utafiti zilizopita .

Hivyo Waziri Mpina aliwahakikishia watanzania kuwa Wizara yake itaendelea kushirikiana na wadau wote kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti zinazofanywa zinawafikia walengwa kwa wakati ili tafiti hizo ziongeze tija na kipato kwa watuamiaji na Taifa kwa ujumla.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Profesa Raphael Chibunda alimhakikishia Waziri Mpina kuwa kwa niaba ya watafiti wa Chuo kikuu hicho watatakwenda kuwa sehemu ya utekelezaji wa agenda hizo.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mh. Luhaga Mpina azindua Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Mifugo, Uvuvi na Ukuzaji viumbe kwenye maji 2020 - 2025 katika viwanja vya Freedom Square Kampasi ya Mazimbu, Chuo kikuu  cha Sokoine cha Kilimo (SUA).

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mh. Abdallah Ulega akizungumza umuhimu wa tafiti katika Sekta ya Mifugo na Uvuvi kabla ya  Uzinduzi wa Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Mifugo, Uvuvi na Ukuzaji viumbe kwenye maji 2020 - 2025 uliofanyika leo katika viwanja vya Freedom Square Kampasi ya Mazimbu, Chuo kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA).

Makatibu Wakuu Sekta ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) na Dkt. Rashid Tamatamah (kushoto) wakieleza namna ya tafiti zinavyoweza kusaidia kutatua changamoto zinazokabili Mifugo na Uvuvi, kabla ya Uzinduzi wa Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Mifugo, Uvuvi na Ukuzaji viumbe kwenye maji 2020 - 2025 uliofanyika leo katika viwanja vya Freedom Square Kampasi ya Mazimbu, Chuo kikuu cha Sokoine ch Kilimo (SUA).