Nav bar

Jumanne, 25 Septemba 2018

ULEGA AWATAKA WAFUGAJI KUFUGA KIBIASHARA




Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amewataka Wafugaji kuachana na tabia ya kufuga kuku kwa mazoea badala yake wafuge kibiashara ili kujikwamua kiuchumi.

Naibu waziri amesema hayo Septemba 21 leo, wakati akifungua mafunzo ya siku  moja ya wafugaji wa kuku Mkoa wa Dar es Salaam. Wafugaji hao wametoka wilaya za Ilala, Kinondoni, Kigamboni, Temeke na Ubungo.

Alieleza Ulega ni watu wachache wanaofuga kuku kibiashara, lakini  waliobaki wanafanya shughuli kama sehemu ya maisha yao, hali inayosababisha kutofanikisha  malengo ya  kukuza uchumi.

 “Nataka mfuge kibiashara, hatutaki mfuge kuku kimazoea. Watu watambue  ufugaji kuku ni biashara kama zingine na ni fursa ya kujikwamua kimaisha,”amesema Ulega

Amesema ufugaji wa kuku sehemu mojawapo itakayowakomboa wanawake na vijana  kuondokana na changamoto ya ajira ambayo  imekuwa kilio kwa watu mbalimbali.

Ulega amesema nyama ya kuku inapendwa kila mahali  na kila mtu hususani kwenye miradi mikubwa ya maendeleo inatumika kama kitoweo chao .

“Ni vyema wafugaji wakaiona fursa hii,  kwa kuzalisha kwa wingi kuku. Tunataka watu wazalishe kuku wa kutosha ili nyama yake ishuke bei.

“Sasa hivi baadhi ya watu kula kwao nyama ya kuku hadi kuwe na shughuli fulani au sherehe jambo ambalo halileti picha nzuri hasa kwa karne hii ya uchumi wa viwanda unaosimamiwa na  Rais John Magufuli,”amesema.

Aliendelea kueleza Ulega kuwa, ifikapo 2020 nataka ugonjwa wa mdondo uwe wa kihistoria, na ifike mahala tusiagize chanjo kutoka nje bali tuzalisha wenyewe.

"Dozi moja ya mdondo kwa sasa inauzwa Tshs elfu 20 ambayo ni sawasawa na wastani wa kuku zaidi ya 300", alisema Mhe. Ulega

Ulega amewataka washiriki wa mafunzo hayo, kujiskia kuwa huru kupata ufafanuzi au kuuliza maswali yoyote kwa Wataalamu kuhusu Sekta ya ufugaji na  changamoto zake na njia za  kukabiliana nazo.

Awali ya yote Naibu Waziri alisema, ni muhimu wataalamu wangu Washirikiane na Halmashauri ili kuona ni namna gani wafugaji wetu wanaojiunga na Vyama vya Ushirika iwe njia rahisi ya kujipatia  mikopo.

"Nia yetu sisi tunataka benki ziwe rafiki kwa wafugaji wadogo wadogo na vileville mfugaji aweze kukopesha kirahisi kupitia Ushirika. Alisema

" Nataka mtumie muda huu kujadiliana na kupata mafunzo, watu wapewe vipeperushi vya ratiba ya uchanjaji wa dawa, " alielekeza Ulega

"Ni matarajio ya Serikali kuwa, baada ya mafunzo haya, maarifa ya wafugaji wetu wa kuku yataongezeka, idadi ya vijana na wanawake wanaoingia kwenye tasnia hii itaongezeka, hivyo kupanua soko la uhakika la kuku na mazao yake, alimalizia kusema.

Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti Mafunzo na Ugani Dkt Angelo Mwilawa amesema mafunzo hayo yameshirikisha wafugaji wa wilaya hizo na lengo ni  kuwajengea uwezo.

Mmoja wafugaji akizungumza kwa niaba ya wenzake, Eva Nyella, amesema “ Tulikuwa tunafuga tu, bila kujua nini cha kufanya, fursa zilizopo lakini mafunzo haya yatatusaidia. Hili ni jambo kubwa tunaahidi tutakuwa wafugaji bora.



DKT. ANGELO MWILAWA MKURUGENZI WA UTAFITI, MAFUNZO NA UGANI AKIONGEA MACHACHE NA KUMKARIBISHA MGENI RASMI

 MGENI RASMI MHE. NAIBU WAZIRI AKISOMA HOTUBA FUPI WAKATI WA UFUNGUZI WA MAFUNZO YA KUKU  JIJINI DAR ES SALAAM



WAFUGAJI NA WATAALAMU WAKIMSIKILIZA MGENI RASMI HAYUPO PICHANI


PICHA YA PAMOJA MGENI RASMI AKIWA NA WAFUGAJI NA WATAALAMU KUTOKA WIZARANI