Nav bar

Ijumaa, 22 Desemba 2017

TANZANIA NA UGANDA ZASAINI MAKUBALIANO YA KUBORESHA SEKTA YA MIFUGO
Na John Mapepele
Tanzania  na Uganda leo zimesaini  makubaliano ya kuboresha sekta ya mifugo baina ya nchi mbili kwa kuimarisha ushirikiano katika nyanja za kuthibiti magonjwa hatari ya mlipuko na kuanzisha minada ya  pamoja ya kimataifa kwa maslahi ya nchi zote mbili.
Makubaliano hayo yamesainiwa  kwa upande wa Uganda na Balozi wa Uganda nchini bwana Richard Tumusiime  Kabonero na kwa upande wa Tanzania na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo anayeshughulikia sekta ya Mifugo, Dkt. Mary  Mashingo mjini Bukoba.
 Akizungumza mara baada ya utiaji wa saini makubaliano hayo Balozi Kabonero amesema magonjwa ya mlipuko kwa wanyama hayana mipaka hivyo makubaliano yaliyofanyika yatasaidia kudhibiti magonjwa ya wanyama  hatimaye kuboresha  mifugo.
Aidha, amesema  hatua  ya udhibiti wa magonjwa ya mifugo itasaidia kupata mifugo bora itakayokuwa na thamani kubwa katika masoko ya kimataifa na kuingizia  nchi zote  mbili mapato zaidi tofauti na ilivyo sasa ambapo nchi zinapata  hasara kwa kuuza mifugo ikiwa katika kiwango   cha chini.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo anayeshughulikia sekta ya Mifugo, Dkt. Mary  Mashingo amesisitiza kwamba ushirikiano wa kitaalam katika kuratibu,kufuatilia hali ya mifugo na kufanya tathmini ya kila wakati utaleta mafanikio makubwa  baina ya nchi ya Tanzania na Uganda  utaleta mapinduzi  katika sekta badala ya utaratibu wa sasa wa kila nchi kushughulikia  masuala ya peke yake.
“Magonjwa ya mlipuko kwa  wanyama  ni suala mtambuka duniani kote, hivyo ni muhimu kulishughulikia  kwa pamoja ili kuwa na tija” alisisitiza Dkt. Mashingo.

Kwa upande wa himasheria, Dkt. Mashingo amesema kuwa serikali zote zimeangalia namna bora ya kushirikiana utekelezaji wa sheria ili kuwabana wafugaji wasiozingatia sheria  kwenye sekta hiyo.
“Tumeamua kwa pamoja kuanzia sasa  kudhibiti tatizo la utoroshaji wa mifugo kwenye mipaka ya nchi zetu. Hatua kali  zitachukuliwa  ili kutoa fundisho kwa yeyote atakayefanya makosa”
Amesema ili kuboresha masoko  ya mifugo baina ya Uganda na Tanzania wamekubaliana kuwa na minada ya kimataifa katika maeneo ya Mutukula kwa upande wa Tanzania na  Kamwema kwa upande wa Uganda.
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji Mifugo na Masoko  kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, bwana Victor Mwita anasema kuwa kuimarika kwa minada itakayosimamiwa kisheria katika mipaka ya nchi ya Tanzania na Uganda itasaidia kuongeza tija katika sekta ya mifugo  hapa nchini.
Aidha, Dkt. Mashingo alisisitiza kwamba wafugaji wenyewe ndiyo wanaoweza kuifanya sekta kupiga hatua kwa kuzingatia  na kusimamia sheria mbalimbali za mifugo nchini. Alizitaja  baadhi ya sheria ambazo ni kipaombele  kwa wafugaji kuzingatia kwa sasa kuwa ni pamoja na Sheria ya Magonjwa ya Mifugo namba 17 ya mwaka 2003 na  Sheria za Nyanda za Malisho na Vyakula vya Mifugo namba 13 ya mwaka 2010.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia  Sekta ya Mifugo,  Dkt. Mary Mashingo (kulia) wakibadilishana nyaraka za makubaliano ya ushirikiano wa kuboresha sekta ya mifugo baina ya Tanzania na Uganda na Mheshimiwa Balozi wa Uganda nchini Tanzania, bwana Richard  Tumusiime Kabonero leo mjini Bukoba. (Picha na John Mapepele)


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia  Sekta ya Mifugo,  Dkt. Mary Mashingo (kulia) akitia saini nyaraka za makubaliano ya ushirikiano wa kuboresha sekta ya mifugo baina ya Tanzania na Uganda na Mheshimiwa Balozi wa Uganda nchini Tanzania, Bw Richard  Tumusiime Kabonero leo mjini Bukoba. (Picha na John Mapepele)


Alhamisi, 21 Desemba 2017

ZIARA YA KATIBU MKUU SEKTA YA MIFUGO DKT. MARIA MASHINGO ALIPOTEMBELEA MKOA WA KAGERA

Katibu Mkuu waWizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo, Dkt. Mary Mashingo akiongea na wafugaji wa nchini Uganda katika eneo la Omwaarogwamabaare akiwa na balozi wa Uganda nchini Tanzania Mhe. Richard Tumusiime Kabonero waliomzunguka ni wataalam mbalimbali kutoka Wizarani.

Katibu Mkuu waWizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo, Dkt. Mary Mashingo(aliyeshikafimbo) akipima kina cha Kisima kilitengenezwa kienyeji kwaajili ya kunyweshea mifugo katika eneo la Kafunjo Wilaya ya Missenyi Mkoani Kagera. Waliomzunguka ni wataalam mbalimbali kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizaraya Mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa na Halmashauri ya Missenyi.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo, Dkt. Mary Mashingo (aliyenyanyuamkono) akimweleza jambo Balozi wa Uganda nchini Tanzania Mhe. Richard Tumusiime Kabonero walipokuwa katika ziara ya kikazileo kwenye Mto Kagera katikakijiji cha Kakunyu Wengine kushoto kwa Katibu Mkuu ni Dkt. Martin  Ruheta Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kulia kwa Balozi ni Suleiman Ahmed saleh, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Afrika, Wizara ya Mambo ya nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Jumatano, 20 Desemba 2017


Tanzania na Uganda yapiga hatua katika kudhibiti magonjwa ya milipuko


Na John Mapepele
Balozi wa Uganda nchini Bw Richard Tumusiime Kabonero amesema ushirikiano wa karibu baina ya Tanzania na Uganda kwenye sekta ya mifugo unahitajika ili kukabiliana na magonjwa ya milipuko ambayo ni hatari kwa mifugo ya pande zote mbili.
Akizungumza leo mjini Bukoba kwenye mkutano wa wataalam wa mifugo wa Tanzania na Uganda ulioandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi nchini, Balozi Kabonero amesema njia bora ya kudhibiti magonjwa ya wanyama ni kuwa na timu ya pamoja ya wataalam watakaokuwa wakifuatilia hali ya mifugo na kufanya tathmini kila wakati badala ya utaratibu wa sasa wa kila nchi kushughulikia peke yake.
“Uganda kama ndugu wa karibu wa Tanzania tuna kila sababu ya kushirikiana ili kuboresha sekta hii” alisisitiza balozi Kabonero
Akizungumzia kwa upande wa Tanzania, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo anayeshughulikia sekta ya Mifugo, Dkt. Mary Mashingo amewataka wafugaji wa asili kote nchini wabadili mitazamo ya kutegemea serikali katika kukuza sekta badala yake washirikiane nayo ili kuharakisha mapinduzi ya sekta ya mifugo.
“Bado kuna kazi ya kubwa ya kufanya ili kuikwamua sekta, lakini pia tukiamua kwa pamoja baina ya serikali na wafugaji nadhani tutakuwa na kipindi kifupi tu cha kufanya mabadiliko makubwa kwenye sekta hii” aliongeza Dkt. Mashingo
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji Mifugo na Masoko kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, bwana Victor Mwita anasema kuwa kuimarika kwa minada itakayosimamiwa kisheria katika mipaka ya nchi ya Tanzania na Uganda itasaidia kuongeza tija katika sekta ya mifugo hapa nchini.
Aidha, Dkt. Mashingo alisisitiza kwamba wafugaji wenyewe ndiyo wanaoweza kuifanya sekta kupiga hatua kwa kuzingatia na kusimamia sheria mbalimbali za mifugo nchini. Alizitaja baadhi ya sheria ambazo ni kipaombele kwa wafugaji kuzingatia kwa sasa kuwa ni pamoja na Sheria ya Magonjwa ya Mifugo namba 17 ya mwaka 2003 na Sheria za Nyanda za Malisho na Vyakula vya Mifugo namba 13 ya mwaka 2010.
Akitolea mfano wa mafanikio yaliyoletwa na wafugaji wenyewe nchini , Dkt. Mashingo alisema wafugaji wa Mkoa wa Morogoro kwa kushirikiana na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa wakati huo marehemu Joel Bendera waliweza kupunguza kwa kiasi kikubwa migogoro iliyokuwepo baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.
Aidha alisema magonjwa kama Ndigana kali (ECF ) kama ikitokomezwa kabisa yasaidia kuongeza idadi ya mifugo nchini kwa kuwa ugonjwa huo ukiingia unachangia kuua 80% ya ndama wanaozaliwa.
Akichangia katika kikao hicho Mtendaji Mkuu wa Ranchi za Mifugo nchini(NARCO) Profesa Philemoni Wambura alisema bado kuna mahitaji makubwa ya mifugo katika viwanda vya nyama.
“Mahitaji halisi ya ng’ombe wa kuchinjwa katika viwanda vyetu nchini ni 800 kwa siku lakini bado hatujaweza kufikia lengo hilo. Tuna kazi ya kufanya “ alisisitiza Profesa Wambura
Kaimu Mkurugenzi Idara za Huduma za Mifugo katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Martin Ruheta amesema ili sekta ya mifugo ifanikiwe lazima uzalishaji wa malisho uboreshwe malisho yanachangia kwa asilimia 70 hadi 80 kwa ng’ombe wa maziwa na kwa ng’ombe wa nyama inakwenda mpaka asilmia 90 Katika uzalishaji wa mifugo, hakuna miujiza mingine na ndo maana nchi za wenzetu kama vile Brazil wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika sekta hii.

Jumanne, 19 Desemba 2017


NAIBU WAZIRI ULEGA AKAMATA TANI 11 ZA SAMAKI WALIOKUWA WAKITOROSHWA BILA KULIPIWA USHURU WA TSH. 99,000,000/=

Na Kumbuka Ndatta

Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdalla Ulega amekamata tani 11 za Samaki aina ya Sangara katika soko la kimataifa la Mwaloni jijini Mwanza waliokuwa wakitoroshwa bila kuliopiwa wa ushuru wa Tsh.99,000,000 kwenda nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo hivi karibuni

Samaki hao walikuwa wakitoroshwa na wafanyabishara kutoka nchini Kongo waliokuwa na kibali kinachoonyesha  wanaenda kuuzwa Tunduru Mkoani Ruvuma.

 “Jamani naomba msimamie sheria ili kulinda rasilimali zetu zisitoroshwe kwenda nje bila kulipiwa kodi. Lazima tumuunge mkono Rais wetu John Pombe Magufuli katika kuhakikisha Rasilimali hizi ziwanufaishe wananchi na sio watu wachache”alisisitiza wakati akiongea na uongozi wa Manispaa ya Ilemela.

Ulega amesema kuwa ni kinyume cha sheria kuvua samaki wachanga na wazazi, na ameuagiza uongozi wa Manispaa ya Ilemela kupitia Mkurugenzi wake Bw.John Wanga kusimamia sheria ipasavyo ili kudhibiti kuvuliwa kwa samaki wasioruhusiwa kisheria.

“Ikitokea wakati wa ukaguzi wenu mmekamata Samaki wachanga au wazazi taifisheni na sheria ichukue mkondo wake mara moja kwa yeyote anayehusika au anayevunja sheria kwa kujua au kutokujua”alisema Ulega.

Akihutubia wafanyabiashara katika soko la Mwaloni jijini Mwanza, Waziri Ulega alielezwa changamoto wanazokumbana nazo ikiwa ni pamoja na ukosefu wa maji safi na salama na ubovu wa miundombinu ya vyoo katika soko hilo.

Mhe.Ulega amempa siku tatu Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilemele Bw.John Wanga kuhakikisha maji na Miundombinu ya vyoo sokoni hapo inashughulikiwa ndani ya siku tatu, hadi ifikapo Disemba 18, 2017.


Mhe. Naibu Waziri Abdallah Ulega ashika Tani 11 ya samaki waliokuwa wakitoroshwa bila kulipwa ushuru

Jumatatu, 11 Desemba 2017


WAZIRI MPINA AFUTA TOZO ZOTE ZA MIFUGO ZISIZOZINGATIA SHERIA.

Na John Mapepele

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amefuta tozo ya faini ya shilingi elfu hamsini kwa kila Ng’ombe mmoja na ameuagiza Uongozi wa Wilaya ya Singida kuwarudishia mara moja fedha wafugaji wote  walizotozwa faini kinyume cha Sheria  katika zoezi  la kukamata mifugo linaloendelea katika Hifadhi ya Msitu wa Jamii wa Mgori.

Waziri Mpina ametoa maelekezo hayo leo alipotembelea eneo la Hifadhi ya Msitu wa Jamii wa Mgori, kwenye Kijiji cha Handa na kuwaagiza Wakuu wa Mikoa ya Singida na Dodoma kupitia kwa Wakuu wa Wilaya ya Singida na Chemba kushirikiana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo anayeshughulikia Sekta ya Mifugo, Dkt. Mary Mashingo kufika katika eneo hilo kabla ya tarehe15/12/2017 kushughulikia mipaka baina eneo la Singida na Handa kwa upande wa Wilaya ya Chemba  na migogoro ya wafugaji inayoendelea.

“Kama Waziri mwenye dhamana ya kushughulikia Sekta ya Mifugo na Uvuvi nchini sipo tayari kuvunja Sheria kwa kuwakumbatia wahalifu wanaokiuka Sheria za nchi kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi, lakini pia wahalifu wanatakiwa kutozwa faini kulingana  na Sheria na taratibu zilizowekwa. Utozaji wa faini ambao hauzingatii hili ni uvunjaji wa Sheria “ alisisitiza Mpina.

Waziri Mpina alisema utozaji wa faini wa shilingi 50,000/= toka shilingi 20,000/= za awali kwa kila Ng’ombe aliyekamatwa na shilingi 25,000/= kwa Mbuzi toka shilingi 5,000/= za awali haukubaliki na kumuagiza Mkuu wa Wilaya ya Singida, Elias Tarimo kurudisha shilingi 30,000/= kwa kila Ng’ombe ambazo zimetozwa  bila kufuata Sheria yoyote.

Baadhi ya wafugaji waliofika katika kijiji cha Handa kulalamikia tozo  ya shilingi 50,000 kwa kila Ng’ombe  mmoja  walizotozwa  na Halimashauri ya Wilaya ya Singida ni  pamoja na Jerumani Waline aliyetozwa jumla ya shilingi 2,500,000/=, kwa idadi ya mifugo 66, Mabula Mwala aliyetozwa shilingi 1,950,000/= kwa idadi ya mifugo 45, Joel Tahan aliyetozwa jumla ya shilingi 1,000,000/= kwa idadi ya mifugo 31, Elizabeth Hamisi aliyetozwa shilingi 1,050,000/= kwa idadi ya mifugo 34,na Elizabethi Nyambi aliyetozwa jumla ya shilingi 350,000 kwa idadi ya mifugo 8.

Akizungumza kwa niaba ya wafugaji bwana Jerumani Waline, amesema changamoto kubwa kwa sasa ni kuainishwa kwa mipaka ya Kijiji cha Handa na Hifadhi ya Msitu wa jamii wa Mgori na eneo la kunyeshea maji mifugo  ambapo alimuomba Waziri kulishughulikia suala hilo.

Waziri Mpina ameiagiza Halmashauri ya Singida kupitia mara moja tozo hizo na kuzipeleka kwenye Mamlaka husika ili zipitishwe na kuanza kutumika kwa taratibu zinazokubalika kisheria.

Pia amezitaka Halimashauri zote nchini kutojiingiza katika mtego wa kutoza faini ambazo hazipo kisheria kwa kuwa  kufanya hivyo ni kuvunja sheria na kuagiza kuwa kuanzia sasa Halimashauri zote zinatakiwa kutoa  taarifa kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi pindi zinapotaka kuendesha operesheni za  mifugo ili kuwa na ufahamu wa pamoja baina ya Wizara na wadau wengine  hali ambayo itasaidia kuboresha operesheni hizo na kuondoa migongano isiyo ya lazima.

Aidha amewataka Watendaji  kuwa makini wanaposhughulikia masuala  ya mifugo kwa kuhusisha  Sheria  mbalimbali za Sekta ya Mifugo ili kuondokana na migogoro isiyo  ya lazima kwa vyombo vya Serikali na kutolea mfano wa Uongozi wa Pori la Akiba  la Swaga Swaga ulivyowazuia Wakaguzi wa  Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuangalia afya za mifugo iliyokamatwa  katika pori hilo, akasisitiza kuwa ni ukiukwaji wa sheria kwa kuwa sharia namba 17 ya Magonjwa ya Wanyama ya mwaka 2003, kipengele 26 (a)1 kinawapa uwezo Wakaguzi kuingia na kuchunguza  hali ya mifugo  mahali popote ili kuona afya za mifugo.

Alizitaja baadhi ya Sheria za Mifugo ambazo ni muhimu kuzizingatia wakati wa operesheni za mifugo kuwa ni pamoja na Sheria ya  Veternari Namba 16 ya Mwaka 2003, Sheria ya Tasnia ya Maziwa Namba  8 ya Mwaka 2004, Sheria ya Tasnia ya Nyama Namba 10 ya Mwaka 2006, Sheria ya Biashara ya Ngozi (The Hides, Skin and Leather trade Act) Namba 18 ya Mwaka 2008, Sheria ya Ustawi wa Wanyama  Namba 19 ya Mwaka 2008 na Sheria ya Utambuzi, Usajili  na Ufuatiliaji Mifugo Namba 12  ya Mwaka 2010.

Sheria nyingine ni Sheria ya Nyanda za Malisho na Vyakula vya Mifugo Namba 13 ya Mwaka 2010, na Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo namba 4 ya Mwaka 2012.

Akizungumzia ugomvi wa wafugaji kuingiza   mifugo katika Pori la Akiba la Swaga Swaga na Msitu wa Jamii wa Mgori, Waziri Mpina amesema  Viongozi wa Wilaya wanajukumu la kuyalinda maeneo hayo na wafugaji kuheshimu sheria za nchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi , Dkt. Mary Mashingo amesema wataalamu wanatakiwa kushirikiana na kupanga mamna bora ya matumizi ya maeneo hayo ili kuleta tija kwa Sekta zote badala ya kuendelea na migogoro isiyoisha kila uchao.

“Wenzetu wa Ethiopia wamefanya vizuri katika kupanga na kutumia maeneo kama haya,sisi kama Wizara tutahakikisha Sheria na Kanuni zinaboreshwa ili kuinua sekta ya Mifugo” alisisitiza Dkt. Mashingo

Akitoa taarifa kwa Waziri kuhusu zoezi la kuondoa Mifugo na makazi katika eneo hilo, Mkuu wa Wilaya ya Singida Elias Tarimo amesema kwamba wameamua kufanya operesheni hiyo maalum baada ya  wafugaji hao kukataa kuondoka  katika eneo hilo  kuanzia mwaka 2010 ambapo walianza kuvamia na kufanya makazi,kulima mazao na kuchunga mifugo kinyume cha taratibu.

Alisema Wilaya iliamua kutoza faini kubwa  kutokana na  hali ya wafugaji hao kuendelea na uvamizi na  kuendesha shughuli mbalimbali za ujenzi, ufugaji na kulima, hata hivyo alikiri kutofuata taratibu ya kuendesha zoezi hilo na kwamba watafuata taratibu za kisheria ili tozo hizo zipitishwe katika Mamlaka husika.

Aidha alisema operesheni hiyo imekuwa ikishirikisha  Kamati ya Ulinzi na Usalama kwa kuwa wananchi wamekuwa wakitumia silaha kukataa kuondoka na kuchukuliwa mifugo yao hali ambayo imewafanya waendeshe operesheni hiyo kwa tahadhali  kubwa.

Amesema hadi sasa watu 32 wanashikiliwa na Polisi katika kituo cha Singida kutokana na zoezi la kuondoa mifugo linaloendelea, ambapo jumla ya nyumba 138 zimevunjwa na tozo za jumla shilingi 19,750,000/= zimekusanywa.

Mkuu wa Wilaya Tarimo amesema  jumla ya ng’ombe 386 walikamatwa na Halmashauri  lakini hadi sasa wameachiwa  baada ya wafugaji hao kulipa faini. Eneo la Pori la Mgori lina julma ya hekta 40000.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe Luhaga Mpina akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Handa Wilaya ya Chemba Mkoani Dodoma na kuamuru wafugaji waliokamatiwa mifugo yao na kutozwa faini ya sh 50,000 kila ng’ombe warudishiwe kiasi cha sh. 30,000 kutokana na faini hiyo kutozwa kinyume cha sheria.



Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe Luhaga Mpina akimuuliza maswali Mwanasheria wa Halmashauri ya Singida, Fortunata Matinde juu ya sheria gani iliyotumika kutoza faini ya Sh. 50,000 kwa kila ng’ombe ambapo Waziri Mpina alifuta maamuzi hayo (kushoto) ni Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi(Mifugo) Dk Maria Mashingo.





Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe Luhaga Mpina akimsikiliza kwa makini Mkazi wa Kijiji cha Handa wilayani Chemba, Jumanne Sadick kuhusu tatizo la mpaka kati ya Pori la Hifadhi ya Swagaswaga na Mgori ambapo Waziri Mpina aliagiza ifikapo Disemba 15 mwaka huu Katibu Mkuu Mifugo na viongozi wa Mkoa wa Singida na Dodoma kufika eneo hilo ili kuupatia ufumbuzi mgogoro huo.



Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe Luhaga Mpina akisoma stakabadhi ya malipo ya sh 50,000 kwa kila ng’ombe kinyume cha sheria aliyotozwa mfugaji wa Kijiji cha Handa, Tulway Bombo ambapo Waziri Mpina alitangaza kufuta maamuzi hayo na kuamuru wafugaji hao kurudishiwa fedha zao.








Mkuu wa Wilaya ya Singida, Elias Tarimo aliyenyoosha mkono akimweleza  Mhe Luhaga Mpina sehemu ya nyumba (hazipo pichani)walizobomoa wakati wa operesheni ya kufukuza wavamizi wakiwemo wafugaji ndani ya Pori la Akiba la Hifadhi ya Jamii Swagaswaga na Mgori yaliyoko katika Mikoa ya Singida na Dodoma kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi(Mifugo) Dk Maria Mashingo.

Alhamisi, 7 Desemba 2017


 MPINA AMSIMAMISHA KAZI MTUMISHI ALIYESHIRIKI UTOROSHAJI WA KILO 2500 ZA SAMAKI KWENDA BURUNDI ZENYE THAMANI YA SHILINGI 20,850,000.00

Na  John Mapepele

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mh. Luhaga Mpina amemuagiza  Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Yohana  Budeba kumsimamisha  kazi mara moja Afisa wa Kitengo cha Doria na Udhibiti wa Uvuvi wa mpakani katika Mkoa wa Kagera bwana  Ayoub Ngoma kwa tuhuma za  kushiriki  katika utoroshaji wa samaki wenye kilo 2530 kwenda nchini Burundi zenye thamani ya shilingi 20,850,000/= hapo jana.

Akizungumza katika Ofisi ya Kitengo hicho iliyopo mjini Kagera, Mpina  alisema  mnamo tarehe 03/12/2017 majira ya Saa 03:00  asubuhi, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Ngara ilikamata gari lenye namba za uasajili T 614 CLQ aina ya Mitsubishi Canter likiwa limepakia samaki zenye uzito wa kilo 2,000 aina ya Sangara na kilo 530 wa aina ya Sato kwenye mpaka wa Murusagamba wilayani Ngara.

“Katika kipindi cha uongozi wangu, tayari nimesha waagiza Makatibu Wakuu waliopo katika Wizara yangu kutembea na  barua zilizozosainiwa za kusimamisha kazi watumishi wote wanaohujumu jitihada za Serikali ibaki kujaza jina tu. Kwa sasa hatuna hata nusu dakika ya uvumilivu kwa watu kama hawa, tutawaondoa mara moja.” Alisisitiza Mpina

Aidha, Waziri Mpina alisema Afisa huyo na Dereva wa gari hilo bwana Ayuob Sanga wanashikiliwa na polisi kwa hatua za kisheria kwa kuhusika na tukio hilo,  na kuongeza kwamba samaki hawa walikuwa wakitoroshwa kwenda nje ya nchi bila ya kufuata Sheria ya Uvuvi Na 22 ya 2003 na taratibu mbalimbali za usafirishaji wa samaki na mazao yake nje ya nchi.

Afisa Mfawidhi wa Kanda wa Kitengo cha Doria na Udhibiti wa Uvuvi wa mpakani katika Mkoa wa Kagera bwana Gabrieli Mageni alimweleza Waziri Mpina baadhi ya taratibu zilizokiukwa kuwa ni pamoja na samaki hao kutopaswa kuvuliwa kwa kuwa  walikuwa wakubwa zaidi ya sentimeta 85 na wadogo chini ya sentimeta 50, msafirishaji kutokuwa na kibali cha kusafirisha mazao ya uvuvi, kutolipia ushuru na mrabaha wa Serikali, kutokuwa na cheti cha afya pamoja na leseni ya kuuza mazao ya uvuvi nje ya nchi.

Waziri Mpina  alisema samaki hao walitaifishwa na kugawanywa kwa wananchi wa Murusagamba, Kiteule cha Jeshi la Wananchi la Tanzania Murusagamba, Kituo cha Polisi Murusagamba pamoja na Shule ya Sekondari Murusagamba baada ya kupata kibali cha Mahakama.

Alisema  kazi hiyo ilifanyika chini ya usimamizi wa Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Ngara. Luteni kanali,Michael Mtenjele. Aliongeza kuwa uchunguzi wa awali ilibaini kuwa samaki hao walitokea kwenye kijiji cha Izigo wilayani Muleba.

Ametaja baadhi ya matukio yaliyotokea hivi karibuni kuwa ni pamoja na  kukamatwa kwa furu kilo 9100 zilizokuwa zinatoroshwa kwenda nchini Uganda ambapo zilitaifishwa na kuuzwa kwa amri ya mahakama na watuhumiwa wawili kufikishwa mahakamani.

Kukamatwa  kwa uduvi kilo 5000 ambazo zililipiwa mrabaha na mtuhumiwa kulipa faini ya shilingi 100,000/=,kukamatwa  kwa mafurushi 6 ya Samaki aina ya Migebuka yenye kilo 240 katika kituo cha basi cha Kagera zilizotoka mkoani Kigoma kwenda Uganda ambapo mtuhumiwa alikimbia na samaki hao kutaifishwa.

Katika tukio jingine jumla ya kilo 100 za mabondo mabichi ya samaki yamekamatwa kwenye doria mpakani Mtukula na mtuhumiwa  amefikishwa polisi kwa hatua za kisheria.

Waziri Mpina amewaomba wavuvi kuzingatia Sheria na taratibu mbalimbali za uvuvi nchini ili sekta hiyo iwe na tija na kuchangia  katika  uchumi wa kati wa viwanda ifikapo 2025.

Wakichangia kwa nyakati tofauti watumishi wa kituo hicho waliiomba Serikali kupitia kwa Waziri Mpina kuangalia namna ya kuongeza nguvu kazi na vitendea kazi mbalimbali vitakavyosaidia kudhibiti uvuvi haramu.

Nahodha Mkuu wa kituo hicho, bwana Ernest Maguzu alisema kazi ya doria katika Ziwa Viktoria imekuwa ngumu kutokana na  maendeleo  makubwa  ya teknolojia ya mawasiliano kwa kuwa wavuvi wamekuwa wakiwasiliana mara moja kutumia simu za mikononi pindi wanapoziona boti za doria zinaingia ziwani na kufanikiwa kukimbia.

Naye Kaimu Afisa Mfawidhi wa Kitengo cha Udhibiti wa Ubora na Masoko bi, Theresia Temu aliomba kuongeza udhibiti wa usafirishaji wa bidhaa zitokanazo na mazao ya uvuvi nje ya nchi kwa kuwa hivi sasa Serikali imekuwa ikipoteza fedha nyingi kutokana na wafanyabiashara kutorosha mazao hayo mipakani bila kulipa ushuru.

Bi Temu alisema kuwa inakadiriwa kuwa zaidi ya tani mia moja ya  mazao ya uvuvi yanatoroshwa kila mwezi katika mipaka ya nchi jirani hivyo jitihada za pamoja baina ya wadau mbalimbali zinahitajika ili kupambana na tatizo hili

“Mheshimiwa Waziri hili ni tatizo kubwa tunaomba Serikali kuliangalia kwa jicho la tatu namna nyingine tutaendelea kuibiwa” alisisitiza bi Temu

Waziri Mpina  alisema Halimashauri zote nchini zinatakiwa kushiriki kikamilifu katika kulinza raslimali za majini  na baharini kwa kuwa  licha ya  raslimali hizo kutoa mchango  mkubwa wa uchumi kwa taifa pia manufaa yake ni kwa faida ya vizazi vya sasa na baadaye.

“Nataka suala la uvuvi wa mabomu na nyavu za kukokota liwe historia katika nchi yetu. Tutaendelea kuchukua hatua kali kwa yeyote  atakaje tuhujumu” alisisitiza Mpina


 Waziri wa Mifugo na Uvuvi  Mhe.Luhaga Mpina  akiangalia  maboksi ya samaki aina ya Migebuka yenye kilo 240 yaliyokamatwa katika kituo kikuu cha basi cha  mjini Kagera hapo jana
Waziri wa Mifugo na Uvuvi  Mhe.Luhaga Mpina akitoa  tamko la kumsimamisha  kazi mara moja Afisa wa Kitengo cha Doria na Udhibiti wa Uvuvi wa mpakani katika Mkoa wa Kagera bwana  Ayoub Ngoma kwa tuhuma za  kushiriki  katika utoroshaji wa samaki wenye kilo 2530 kwenda nchini Burundi zenye thamani ya shilingi 20,850,000/=

Moja ya boti inayotumika kwenye doria katika ziwa Viktoria na  Kitengo cha Doria na Udhibiti wa Uvuvi wa mpakani katika Mkoa wa Kagera

MPINA ABARIKI NARCO KUVUNJA MKATABA WA MWEKEZAJI MZEMBE KATIKA RANCHI YA KAGOMA

Na John Mapepele

Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi  Luhaga Mpina  ameridhia  maamuzi ya Kampuni ya Ranchi za NARCO kuvunja mkataba baina ya mwekezaji Agri Vision Global Ltd katika  Ranchi ya Kagoma  mkoani Kagera na kuamuru aondoka mara moja baada ya mwekezaji huyo kushindwa kutekeleza mkataba huo katika kipindi cha miaka mitano.

Waziri Mpina ametoa maelekezo  hayo jana  alipotembelea Ranchi ya Kagoma kuangalia shughuli mbalimbali  katika Ranchi hiyo ambapo ametoa siku saba kwa mwekezaji huyo kuondoka katika eneo hilo na badala yake Serikali kupitia NARCO kuendelea kusimamia shughuli za mifugo katika Ranchi hiyo.

“Ninakuagiza  Mkuu wa Wilaya  kuanzia sasa  hakikisha unaimarisha ulinzi katika ranchi hii katika kipindi cha kukabidhi Ranchi baina ya Serikali na Mwekezaji  ili kusitokee hujuma zozote” alisisitiza Mpina

Alitaja baadhi ya mambo ambayo hayakutekelezwa na mwekezaji huyo kuwa ni pamoja na  kujenga  machinjio ya nyama,  kujenga kiwanda, kutoa gawio la shilingi bilioni tatu kila mwaka katika kipindi cha miaka mitano, kutoa shilingi 2672 kwa hekta moja kama tozo la ardhi na kushindwa kuendeleza miundombinu ya NARCO waliyoikuta wakati  wanaingia mikataba hiyo miaka mitano iliyopita.

Waziri Mpina  amemuagiza Meneja Mkuu wa NARCO, Profesa  Philemoni Wambura  kuhakikisha kwamba ndani ya siku saba anamleta Meneja katika Ranchi hiyo kwa ajili ya usimamizi wa shughuli za ranchi hiyo na kuhakikisha kuwa inafanya kazi zake kisasa.

Aidha Mpina ametoa siku saba  kwa   Uongozi wa NARCO kuhakikisha kuwa imefanya tathmini  ya hasara zilizosababishwa na mwekezaji huyo ili taratibu za kisheria zichukuliwe dhidi yake  ili aweze kuilipa Serikali ikiwa ni pamoja na shilingi bilioni kumi na tano kama  gawio la miaka mitano iliyokaa ambalo amesema halijawahi kulipwa hata shilingi moja.

“Sasa tumeamua kuchukua hatua na tutaendelea kuchukua hatua kali dhidi ya wawekezaji wasiowaaminifu wanaotaka kuihujumu serikali katika sekta hizi za mifugo na Uvuvi” alihoji Mpina

Alionya wawekezaji kuacha tabia ya kuidanganya serikali kwamba wanauwezo wa kuwekeza katika vitalu  ili wapewe lakini wanabadili matumizi baada ya kupewa. Aliongeza kwamba  Serikali imegundua  baadhi ya wawekezaji wanaopewa vitalu wanawakodisha wafugaji kutoka nchi jirani  na kujipatia faida wakati  Serikali haipati chochote.

Awali,  akipewa ripoti ya maendeleo ya mifugo na uvuvi na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kagera Deodatus Kinawiro mbaye ni Mkuu wa Wilaya ya Bukoba . alisema kutokana na oparesheni za uvuvi haramu zinazoendelea wilaya ya ngara imekamata tani 6 za samaki zilizokuwa zikipelekwa katika nchi ya burundi .
Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Mhe. Luhaga Mpina  akipima urefu wa bwawa la maji ya kunyeshea mifugo katika Ranchi ya Kagoma Mkoani Bukoba ambapo aliamuru mwekezaji  Agri Vision Global Ltd katika  Ranchi ya Kagoma  Mkoani Kagera kuondoka mara moja baada ya mwekezaji huyo kushindwa kutekeleza mkataba huo katika kipindi cha miaka mitano.

Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi  Mhe. Luhaga Mpina (mwenye Kofia )akitoa maelezo  ya kwa mkuu wa Wilaya ya Richard Lugango kuboresha ulinzi katika Ranchi ya Kagoma baada ya kumuamuru mwekezaji  katika Ranchi hiyo kuondoka mara moja baada ya kushindwa kutekeleza mkataba baina yake ya Serikali.

Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi  Luhaga Mpina  akiwa na viongozi wa Mkoa wa Kagera wa Serikali mara baada ya kuwasili jana kukagua shughuli za mifugo katika Ranchi za Mifugo zilizopo Mkoani.

Jumanne, 5 Desemba 2017


WAZIRI MPINA AUNDA TUME KUCHUNGUZA MKATABA WA KIWANDA CHA NYAMA DODOMA NA SERIKALI.
  • Aagiza Rachi za mifugo kuanza kuchinja mifugo katika kiwanda hicho ifikapo Machi mwakani.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mh. Luhaga Mpina ameunda tume ya watu watano  kufanya tathmini ya utekelezaji wa mkataba  wa kiwanda cha nyama cha Dodoma baina ya  Serikali na Kampuni ya nyama Tanzania(TMC) baada ya muda wa mkataba wa miaka mitano kuisha huku uzalishaji wake ukiwa unasuasua.
Mh. Mpina alitoa maelekezo hayo hivi karibuni  kwa Meneja Mkuu wa Kiwanda hicho, bwana Nashon Kalinga  katika ofisi za kiwanda hicho wakati alipokuwa kwenye ziara ya kukagua shughuli mbalimbali za sekta ya mifugo akitokea katika ranchi ya Kongwa.

“Mimi kama Waziri mwenye dhamana ya Mifugo naelekeza kwamba Tume ipitie Mkataba  huu  ambao ushaisha muda wake na ikibainika kuwa wameshindwa kutekeleza nitaamuru kuvunjwa mara moja ili  kiwanda kifanye kazi kama ilivyokusudiwa” alisisitiza Mpina

Alisema Tume hiyo itawashirikisha wataalam kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Msajili wa Hazina na Ranchi za Taifa za Mifugo.

Katika hatua nyingine, Mh. Waziri amesitisha mkutano wa Bodi ya Kiwanda hicho uliotakiwa kufanyika tarehe 8 Disemba mwaka huu hadi Tume hiyo itakapowasilisha ripoti ya tathmini ya utekelezaji wa mkataba ulioisha wa miaka mitano.

Hata hivyo Mpina amesema  Serikali haiwezi kuruhusu kiwanda kufanya kazi  chini ya kiwango wakati kuna wawekezaji wengi ambao wana nia ya dhati ya kufanya kazi na kwamba Tanzania  bado ina soko kubwa  katika mazao ya mifugo duniani kote.

“Ni bahati mbaya sana tunaona kiwanda kinageuka  machinga badala ya kufanya kazi na kuleta tija katikakuelekea uchumi wa kati wa viwanda hapa nchini. Sisi kama Serikali hatukubaliani na hili” aliongeza Mh.Waziri.

Aidha amesema imefika wakati mwafaka sasa kwa Serikali  kwa Ranchi zote za mifugo kuzalisha  katika kiwango cha juu ili kiwanda hicho cha nyama (TMC) kiwe kinachinja mifugo kutoka Ranchi hizo na  kwa kuanzia amesema  ranchi ya Ruvu na Kongwa  lazima ziendelezwe  mara moja ili kutoa mifugo ya kutosha  na kuchinjwa katika kiwanda hicho. Katika uwekezaji huo Serikali ina hisa ya asilimia 41 wakati muwekezaji ana hisa ya asilimia 51.

“Nasema kuanziamwezi Machi mwakani nataka  tuwe tunachinja mifugo kutoka katika ranchi zetu. Naamini hili linawezekana kabisa, ni lazima tuanze sasa” amesisitiza Mh.Mpina.

Akiwa  katika ranchi ya Kongwa ametoa mwaka mmoja kwa uongozi wa ranchi hiyo kuongeza idadi ya mifugo kutoka 8647 ya sasa hadi kufika 20000 ifikapo Disemba 2018. Eneo la malisho kuwa limesafishwa  kutoka hekta 3000 za sasa hadi kufikia hekta 6000 katika kipindi hicho hicho.

Alisema Wizara itafanya tathmini ya utekelezaji wa maagizo hayo baada ya kipindi cha miezi sita ili kuona utekelezaji wake.Eneo la ranchi ya Kongwa linaukumbwa wa hekta 38000 ambapo ametaka  nusu ya hekta hizo kutumika katika uzalishaji wa malisho na nusu nyingine kwa ajili ya kuhifadhia mifugo hiyo.

Meneja Mkuu wa Ranchi za Mifugo nchini, Profesa Philemoni Wambura amesema Rachi ya Kongwa  uongozi wa rachi hiyo unamalengo ya kuzifanya ranchi zote nchini kuwa  mashamba darasa ya kuwafundishia wananchi namna bora ya uzalishaji wa malisho na mbegu bora  za mifugo.

Aidha amesema  kwa sasa Ranchi ya Kongwa   inayozalisha nyama bora duniani kinachotakiwa ni kuongeza uzalishaji wa nyama hiyo kwa kuwa mahitaji yake ni makubwa.

“Mh. Waziri tumepokea maelekezo yako tunaahidi kuzalisha kwa kiwango cha juu ili tujenge uchumi wetu wa viwanda” ameongeza Profesa.

Profesa amesema  kwa sasa kipaombele cha kwanza ni kuhakikisha kuwa rachi zinazalisha idadi kubwa ya majike  ya mbegu bora na kusambaza kwa wafugaji wote nchini ili kubadili ufugaji asilia na kwenda katika ufugaji wa kisasa wenye tija.

“Kwa kufanya hivyo tutapata mbegu  bora za mifugo wanaokuwa haraka, wanaotoa maziwa mengi na wenye kuhimili magonjwa na hiyo yatakuwa mapinduzi makubwa katika sekta hii nchini”amesisitiza Profesa.

Hata hivyo amesema mpango wa ranchi ni kuangalia namna  bora ya kuziingiza aina nyingine za ng’ombe kutoa kataika mikoa ya singida(Singida White), Sumbawanga(Fipa Type) na Iringa(Iringa Red) ili kuboresha zaidi badala ya kutegemea mbegu kutoka nje ya nchi ambazozina kufa  kwa kiasi kikubwa baada zinashindwa kuhimili hali ya hapa nchini.

Katika hatua nyingine, Mh. Waziri meuagiza uongozi wa rachi kuangalia namna ambavyo wanaweza kupunguza gharama ya kuuza mbegu bora za mifugo, ambapo kwa sasa dume la ngombe aina ya Borani linauzwa kwa milioni mbili hali ambayo inawafanya wafugaji wengi kushindwa kumudu.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu aneyesimamia Sekta ya Mifugo katika ziara hiyo, bwana Victor Mwita, amesema kwa sasa Wizara imejipanga kuhakikisha uzalishaji wa malisho bora  unasimamiwa kikamilifu ili mifugo inayozalishwa kuwa  na tija.







WAZIRI MPINA AAGIZA MIKATABA YA VITALU VYA RANCHI YA TAIFA VYENYE JUMLA YA HEKTA Waziri MPINA 68238 KUVUNJWA MARA MOJA.
Waziri wa  Mifugo na Uvuvi Mh. Luhaga Mpina ameagiza Mtendaji Mkuu wa Ranchi za  Mifugo za Taifa, Profesa Philemoni Wambura kuvunja  mikataba ya wawekezaji wa vitalu vyenye jumla ya hekta 68,238 kwenye ranchi ya Mkata na Dakawa ndani ya mwezi  mmoja baada kushindwa kuviendeleza vitalu  vya ranchi na kushindwa kulipia kwa muda mrefu.

Mpina ameyasema hayo jana wakati alipotembelea katika ranchi ya Mkata na Dakawa kwa lengo la kukagua shughuli mbalimbali zinazofanyika  katika ranchi hizo.

Amezitaja kampuni za wawekezaji  ambazo zilizomilikishwa  vitalu zinatakiwa kuvunja mkataba kwa kushindwa kuendeleza upande wa ranchi ya Mkata katika Wilaya ya Kilosa kuwa ni pamoja na Kadolo Farm Company Ltd  kitalu namba 418 yenye hekta 4005,Bagamoyo Farm kitalu namba 419 yenye hekta 3672.96, A to Z Animal Feeds Company Ltd kitalu namba 420 yenye hekta 3692.97 na Ereto Livestock Keepers kitalu namba 422 yenye hekta 4020.54.

Katika Wilaya ya Mvomero kampuni zilizoshindwa  kuendeleza vitalu ni pamoja na kampuni ya  Overland kitalu namba 415 yenye hekta19446.28, Katenda yenye hekta 2500, Mollel yenye  hekta 2500 na Kiwanda cha Sukari cha Mtibwa (Mtibwa Sugar) chenye hekta 20000 walizomilikishwa toka mwaka 1999 na kushindwa  kukiendeleza na kukilipia kwa miaka 18.

Mpina amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Kilosa kumaliza  mara moja migogoro inayoendelea baina ya wakulima na wafugaji. Aidha Waziri Mpina amemtaka Diwani wa kata yaTwatwatwa, Katibu Tawala  wa Halimashauri ya Wilaya ya Kilosa pamoja na jamii ya wafugaji kumaliza migogoro inayowasumbua kwa muda mrefu kwa njia ya mazungumzo kabla ya kukimbilia muhimili wa mahakama bila sababu yoyote.

Mpina amesema kama  vyombo  vya Serikali vingetumika vizuri kuanzia ngazi ya kijiji kungepunguza  migogoro ya wakulima na wafugaji  katika wilaya  hiyo. Wilaya ya Kilosa ni miongoni mwa Wilaya zinaongoza kwa  kuwa na migogoro mingi baina ya wakulima na wafugaji hapa nchini.

Kwa upande  mwingine, Waziri Mpina amezitaka Halimashauri zote nchini kutotunga sheria kandamizi  dhidi ya wafugaji. Akitolea mfano, wa sheria ndogo ya Halimashauri ya Mvomero ya kutoza faini ya shilingi 25, 000/=kwa kila mfugo kuingia  katika Wilaya hiyo bila kufuata taratibu  badala ya shilingi elfu kumi iliyoelekezwa katika Sheria ya Magonjwa ya  Wanyama namba 17 ya Mwaka 2003.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Chama cha Wafugaji Tanzania (CCWT)  Magembe Makoye amesema upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya wafugaji kutasaidia kuondoa migogoro  baina ya pande hizo na kuendelezwa kwa ranchi hizo za taifa  kutawasaidia wafugaji kupata shamba darasa litakalo wasaidia kufuga kwa kisasa  na kupata mbegu bora  za mifugo.

Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mh. Luhaga Mpina (aliyejishika kiuno)  akiangalia kundi la Mbuzi wapatao 100 walioletwa katika ranchi ya Mkata.

Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mh. Luhaga Mpina akiwa kwenye picha pamoja  na Viongozi wa Wilaya ya Mvomero na Viongozi wa Chama cha Wafugaji Tanzania  alipotembelea ranchi ya Dakawa.

Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mh. Luhaga Mpina (mwenye Kofia) akimsikiliza Mkuu wa Wilaya  ya Mvomero, Muhamed Utaly  kulia  akitoa maelezo ya kuhusu eneo la hekta 20000 zilizoshindwa kuendelezwa na mwekezaji Mtibwa Sugar kwa lengo  la ufugaji. Kushoto ni Meneja Mkuu  wa Kampuni hiyo bwana Stan Rau



MHE WAZIRI AMEAGIZA MACHINJIO YA KISASA YA RUVU YALIYOTEKELEZWA KWA MUDA MREFU KUJENGWA NA KUKAMILIKA IFIKAPO DESEMBA, 2018


Machinjio ya kisasa ya Ruvu lazima yakamilike ifikapo 2018 - Mpina

Waziri  wa Mifugo na Uvuvi Mh. Luhaga  J. Mpina ameagiza machinjio ya kisasa ya Ruvu yaliyotelekezwa kwa muda mrefu kujengwa na  kukamillika  ifikapo Desemba, 2018.

Maagizo hayo ameyatoa jana katika ranchi ya Ruvu, alipokuwa katika ziara ya kutembelea baadhi ranchi za mifugo nchini, ambapo amesema ni muhimu machinjio hayo ya ya kisasa yakamilike ili Tanzania ianze kuuza mazao yatokanayo na mifugo katika masoko ya kimataifa.

Ametoa siku tatu kwa Watendaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kumpelekea mpango kazi unaoainisha  namna ya kukamilisha ujenzi wa machinjio hiyo ya kisasa ambayo  baada ya kukamilika itakuwa machinjio kubwa kuliko zote nchini.

Amesema kuwa Tanzania ni nchi ya tatu katika bara la Afrika kwa kuwa na uwingi wa mifugo hivyo hakuna sababu ya kushindwa kuongoza katika  soko la mazao ya mifugo katika masoko ya duniani.

Aidha, Waziri Mpina  amesema  kukamilika kwa machinjio hayo kutasaidia kupunguza  usumbufu kwa wafanyabiashara wa mifugo ambao wote nawapeleka mifugo yao Dar es Salaam   hali ambayo inaongeza uharibifu wa mazingira  kwa ujumla.

Katika hatua nyingine Waziri Mpina amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Ranchi  za taifa kuhakikisha kuwa  kunatafutwa fedha kwa ajili ya kuzalisha  mbegu bora za mifugo na kuongeza idadi ya mifugo kulingana na uwezo wa eneo la ranchi ya Ruvu lenye ukubwa wa hekta 44,000 ambapo hivi sasa eneo hilo la ranchi ya Ruvu lina mifugo ipatayo 1530 wakati uwezo wa ni kuwa na mifugo kuanzia 12000 hadi 22000.

Alisisitiza kwamba maboresho hayo lazima yafanyike ifikapo Desemba , 2018  ambapo ifikapo Juni 2018 tathimini ya awali itafanyika kuona ni kwa namna gani agizo hilo limetekelezwa.

“Tunataka wananchi wapate sehemu ya kujifunza,ranchi ya Ruvu iwe sehemu ya kupata mbegu bora. Siwezi kuwa Waziri wa Mifugo wakati shamba langu halina mifugo” alisisitiza  Mpina.

Waziri aliongeza kuwa na mfumo wa kisasa wa kufuga  mifugo kitaalamu  badala ya mfumo wa sasa ambapo mifugo  inafugwa  kwa muda mrefu.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina akijaribu kukata nyama kwa kutumia mashine ya kisasa alipotembelea ranchi ya Ruv

Jengo la machinjio ya kisasa lililopo katika eneo la ranchi ya Ruvu ambalo Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mh. Luhaga Mpina amewaagiza Watendaji kuhakikisha linakamilika ifikapo Desemba 2018.

Waziri wa Mifugo na  Uvuvi, Mh. Luhaga Mpina (mwenye miwani) akiwa na  viongozi wa ranchi ya mifugo nchini akionyeshwa mbuzi wanaofugwa katika ranchi ya Ruvu

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina (mwenye miwani) akihakiki taarifa za ununuzi wa dawa za mifugo alipotembelea ranchi ya mifugo ya Ruvu hivi karibuni.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina (mwenye miwani katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa ranchi ya Ruvu na watumishi wa Wizara  ya Mifugo na Uvuvi alipotembelea ranchi.