Nav bar

Alhamisi, 4 Desemba 2025

DKT. BASHIRU AKABIDHI PIKIPIKI 381 KWA MAAFISA UGANI NCHINI

◼️Asisitiza Wafugaji ndio kipimo cha utendaji wao

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amewataka Maafisa ugani nchini kujenga ushirikiano madhubuti baina yao na wafugaji utakaolenga kutoa taarifa sahihi, kuelimisha, kutoa ushauri wa kitaalam, kusambaza teknolojia na kupata mrejesho wa matumizi ya teknolojia hizo.

Mhe. Balozi Dkt. Bashiru ametoa maelekezo hayo wakati wa Hafla fupi ya kukabidhi pikipiki 381 kwa Maafisa ugani wote waliopo kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa iliyofanyika Disemba 04,2025 jijini Dar-es-Salaam ambapo amewataka kutanguliza dhana ya majadiliano zaidi badala ya kufundisha pindi wanapokuwa uwandani.

“Huduma za Ugani ni muhimu na ni kiungo kati ya watafiti na wafugaji ili kupata ufugaji wenye tija hivyo ni vema mkaimarisha mahusiano hayo kwa hiyo niwaombe na nirejee tena kama alivyoelekeza Mhe. Rais twendeni kuwahudumia watu sio kama tunawafundisha kama hawana taaluma au uelewa bali tukajadiliane nao na kuwasikiliza” Amesisitiza Mhe. Balozi Dkt. Bashiru.

Aidha Mhe. Balozi Dkt. Bashiru amewataka maafisa ugani hao kuhakikisha wanatatua changamoto zote zinazowakabili wafugaji huku akiwataka kutoa taarifa kwa upande wa changamoto zinazopaswa kutatuliwa katika ngazi ya Wizara.

Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa pikipiki hizo kwa niaba ya Maafisa ugani nchini Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemhakikishia Mhe. Balozi Dkt. Bashiru kuwa pikipiki hizo zitatunzwa na kufanya kazi iliyokusudiwa.

“Nikuhakikishie Mhe. Waziri hutaziona pikipiki hizi zikitumika kama bodaboda na tutahakikisha kwamba vitendea kazi hivi vinaendelea kutumika kwenye zoezi la Chanjo za Mifugo na Utambuzi linaloendelea nchi nzima” Ameongeza Mhe. Prof. Shemdoe.

Akizungumza kwa Niaba ya Wakuu wa Mikoa Mkuu wa Mkoa wa Dar-es-Salaam Mhe. Albert Chalamila amesema kuwa pikipiki hizo zitasaidia kuchochea ufugaji wa kisasa na kuwafanya wafugaji kukopesheka hatua ambayo itaboresha maisha yao na kuakisi dhana ya “Tabasamu” kupitia Wizara za Mifugo na Uvuvi na ile ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI.

Nao wawakilishi wa Maafisa ugani Bw. Peter Shirima kutoka Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma na Odetha Muchukuzi kutoka mkoani Dar-es-Salaam wameishukuru Serikali kwa kuwapatia nyenzo hizo ambazo wamesema kuwa zitawasaidia kuwahudumia wafugaji kwa urahisi zaidi.

Pikipiki hizo zinaifanya Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuwa imeshagawa jumla ya pikipiki 2581 hadi sasa ambazo zote zimelenga kuwarahisishia maafisa ugani hao kuwafikia wafugaji.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kushoto) akimkabidhi moja ya  pikipiki 381 za Maafisa Ugani nchi nzima (wawakilishi waliokaa kwenye pikipiki) Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Prof. Riziki Shemdoe kwenye hafla fupi iliyofanyika Disemba 04,2025 jijini Dar-es-Salaam. Anayeshuhudia (nyuma) ni Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Prof. Riziki Shemdoe (kushoto) akimkabidhi pikipiki za Maafisa Ugani kwa niaba ya wakuu wa mikoa yote, Mkuu wa Mkoa wa Dar-es-Salaam Mhe. Albert Chalamila ikiwa ni muda mfupi baada ya kukabidhiwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kwenye hafla fupi  iliyofanyika Disemba 04,2025 jijini Dar-es-Salaam.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (wa tatu kutoka kushoto) Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Prof. Riziki Shemdoe (wa nne kutoka kulia), Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani (katikati), Mkuu wa Mkoa wa Dar-es-Salaam Mhe. Albert Chalamila (wa tatu kutoka kulia) na watendaji wengine wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na huo wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa hafla fupi ya kukabidhi pikipiki 381 za Maafisa Ugani iliyofanyika Disemba 04,2025 jijini Dar-es-Salaam.

Sehemu ya pikipiki 381 zilizotolewa na Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa Maafisa Ugani nchini kwenye hafla fupi iliyofanyika Disemba 04,2025 jijini Dar-es-Salaam.






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni