Nav bar

Jumatano, 6 Machi 2024

BBT-LIFE (UVUVI) AWAMU YA PILI YANG'OA NANGA


Wanufaika waanza kupigwa msasa

Serikali kupitia wizara ya Mifugo na uvuvi imeanza kutekeleza programu ya "Jenga kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na vijana upande wa sekta ya Uvuvi kupitia mafunzo yanayotolewa kwa vijana na wanawake 300 kutoka pande  mbalimbali za nchi yaliyoanza kutolewa februari 19, 2024 kwenye chuo cha mafunzo ya uvuvi (FETA) kampasi ya Mbegani Bagamoyo mkoani Pwani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa wizara hiyo Bi. Imelda Adam amewataka washiriki wa programu hiyo kuzingatia yale yote watayoelekezwa wakati wote wa mafunzo hayo ya nadharia yatakayofanyika kwa siku 5 ili waweze kufanya vizuri watakapoenda vituoni kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo.

"Programu hii inalenga kuwageuza wahitimu wa ngazi mbalimbali kwenye kada ya Uvuvi kuweza kujiajiri badala ya kusubiri kuajiriwa na lengo la Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha vijana na wanawake wengi zaidi wanawezeshwa kupitia programu hii" Amesema Bi Imelda.

Aidha Bi. Imelda amewataka washiriki hao kutobweteka na kiasi cha fedha wanachopewa na Serikali kwa ajili ya kujikimu wakati wote wa mafunzo na badala yake wajikite kwenye mtazamo wa kuandaa kesho yao iliyo bora baada ya kuhitimu mafunzo hayo.

Kwa upande wake Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizarani hapo Bw. Clemence Katunzi amewataka wanufaika hao kuhakikisha elimu watakayoipata mara baada ya kuhitimu mafunzo huo wanaipeleka kwenye jamii zinazowazunguka katika maeneo yao.

"Tutawapanga kwenye vituo mbalimbali ambavyo vitakuwa jumuishi na awamu hii tutakuwa na vituo 17 ambapo kimoja upande wa Zanzibar na 16 vipo Tanzania bara" Ameongeza Bw. Katunzi.

Utekelezaji wa programu ya Jenga kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na vijana awamu ya pili unatarajiwa kuchukua miezi 3 mara baada ya kukamilika kwa mafunzo kwa nadharia yanayofanyika kuanzia Februari 19-23, 2024.


Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Imelda Adam (kulia) akizungumza na wanufaika wa programu ya BBT-LIFE (Uvuvi) awamu ya pili wakati wa ufunguzi wa programu hiyo uliofanyika leo Februari 19, 2024 kwenye Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya Mbegani wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.

 

Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Clemence Katunzi (kulia) akifafanua namna programu ya BBT-LIFE (Uvuvi) awamu ya pili itakavyotekelezwa  wakati wa ufunguzi wa programu hiyo uliofanyika leo Februari 19, 2024 kwenye Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya Mbegani wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni