Nav bar

Jumanne, 20 Aprili 2021

MKANDARASI BWAWA LA CHAMAKWEZA ATAKIWA KUKAMILISHA MRADI KWA WAKATI NA KUZINGATIA UBORA

Na. Edward Kondela

 

Serikali imemtaka mkandarasi anayejenga bwawa la Kijiji cha Chamakweza kilichopo Wilaya ya Chalinze Mkoani Pwani, kukamilisha bwawa hilo kwa wakati pamoja na kuzingatia ubora ili liweze kuwa na tija kwa jamii ya wafugaji.

 

Akizungumza (16.04.2021) mara baada ya kufanya ziara ya kikazi ya siku moja kujionea ujenzi wa bwawa hilo, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel amesema endapo kukitokea dosari yoyote katika bwawa hilo wakati wa kipindi cha mwakwa mmoja wa uangalizi mkandarasi atapaswa kugharamia hasara zote pamoja na kuchukuliwa hatua za kisheria.

 

“Tungetamani hili jambo lifike ukomo ili tupokee huu mradi, na umalize haraka kwa wakati na kingine ubora kwa kuwa usipofanya hivyo kile kipindi cha uangalizi cha mwaka mmoja kama kuna kilichoharibika kwanza utalipa fidia, nitakutoza na riba ya kuharibu.” Amesema Prof. Gabriel

 

Ameongeza kuwa bwawa hilo ambalo lipo katika Jimbo la Chalinze ambapo anaisha Rais mstaafu wa awamu ya nne Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete linajengwa kwa heshima kubwa kwa kuwa rais mstaafu amekuwa na mapenzi makubwa na wafugaji hivyo ni vyema kuenzi mchango wake katika uongozi wa nchi hii na kuwataka viongozi wa Kijiji cha Chamakweza kujenga utaratibu wa kuthamini mchango wa viongozi na kuwashukuru wakati bado wakiwa hai.

 

Kwa upande wake mkandarasi anayejenga bwawa la Chamakweza Bw. Peter Kasera kutoka Kampuni ya Westmont Tanzania Limited, amesema ujenzi wa bwawa hilo ambao unagharimu Shilingi Milioni 670 umefikia zaidi ya asilimia 90 na kwamba kazi wanayoendelea nayo ni kuweka mawe, kumalizia kuta na upande wa uzio tayari vifaa vyote vimekamilika kwa ajili ya ujenzi.

 

Amebainisha kuwa mradi huo umeshindwa kukamilika kwa wakati kutokana na changamoto za kifedha, mvua na mambo ya kitaifa hivyo kuhitaji muda kidogo ili kukamlisha sehemu ya kazi iliyobaki kabla ya kuukabidhi mradi huo.

 

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Chamakweza Bw. Mika Ole Kashimba ametaka kufanyika kwa baadhi ya maboresho katika ujenzi wa bwawa hilo hususan kwa kuliongezea kina ili liweze kukusanya maji mengi ambayo yataweza kukaa kwa muda mrefu.

 

Ameongeza kuwa kuna nyakatia kuta za bwawa zimekuwa zikivunjika kutokana na wingi wa maji yanayoingia kwenye bwawa hali inayolifanya bwawa kushindwa kuhimili kutunza kiasi cha maji kinachoingia. 


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa na mmoja wa wafugaji wakati akikagua sehemu ambayo jamii ya wafugaji inayoishi katika Kijiji cha Chamakweza itakuwa ikitumia maji hayo kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kibinadamu, mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa bwawa la kijiji hicho. (16.04.2021)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akikagua ubora wa maji na mmoja wa wafugaji wakati alipotembelea kujionea maendeleo ya ujenzi wa bwawa la Kijiji cha Chamakweza kilichopo Wilaya ya Chalinze Mkoani Pwani na kumtaka mkandarasi Westmont Tanzania limited kukamilisha mradi huo kwa wakati na kuzingatia ubora. (16.04.2021)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akifafanua jambo kwa mmoja wa wafugaji katika Kijiji cha Chamakweza kilichopo Wilaya ya Chalinze Mkoani Pwani, alipotembelea ujenzi wa bwawa la kijiji hicho kwa ajili ya matumizi ya mifugo na shughuli nyingine za kibinadamu. (16.04.2021)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akiendesha ‘excavator’ wakati alipotembelea ujenzi wa bwawa la Kijiji cha Chamakweza kilichopo Wilaya ya Chalinze Mkoani Pwani na kukuta mkandarasi Westmont Tanzania Limited akiendelea na ujenzi huo ambao umefikia zaidi ya asilimia 90. (16.04.2021)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akikagua sehemu ambayo itakuwa inatumiwa na jamii ya wafugaji inayoishi katika Kijiji cha Chamakweza kwa ajili ya kunyweshea mifugo yao maji mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa bwawa la kijiji hicho. (16.04.2021)


Muonekano wa sehemu ya bwawa la Kijiji cha Chamakweza lililopo Wilaya ya Chalinze Mkoani Pwani, ambalo mara baada ya ujenzi wa bwawa na miundombinu yake kukamilika, maji yatatumiwa na jamii ya wafugaji kwa ajili ya shughuli za kibinadamu na kunyweshea mifugo yao maji. (16.04.2021)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wanaojenga bwawa la Kijiji cha Chamakweza kilichopo Wilaya ya Chalinze Mkoani Pwani pamoja na baadhi ya wafugaji wanaoishi katika kijiji hicho. (16.04.2021)







Hakuna maoni:

Chapisha Maoni