Nav bar

Alhamisi, 4 Aprili 2019


MIGOGORO MIKUBWA 14 KATI YA 29 YATATULIWA NA WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amesema wizara kupitia timu yake maalum ya kushughulikia migogoro, hadi sasa imetatua migogoro mikubwa 14 kati ya 29 inayohusisha wakulima na wafugaji pamoja na hifadhi na wawekezaji.

Naibu Waziri Ulega amebainisha hayo alipokuwa akizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Hai Mkoani Kilimanjaro Bw. Lengai Ole Sabaya pamoja na viongozi wengine wa wilaya hiyo, mara baada ya kuarifiwa kuwepo kwa mgogoro wa wakulima na wafugaji katika Wilaya ya Hai na kubainisha kuwa ni hatari kwa jamii inayoishi pamoja kuwa na mgogoro wa aina hiyo.

“Nitamsisitiza katibu mkuu mifugo aliangalie kwa karibu sana hili kwa sababu ni hatari sana kwa jamii inayoishi pamoja kutokuwa na maelewano ya kuachiana maeneo kwa ajili ya shughuli zao za kiuchumi.” Alisema Mhe. Ulega

Mhe. Ulega ametoa kauli hiyo baada ya Mkuu wa Wilaya ya Hai Bw. Lengai Ole Sabaya kumuarifu kuwa baadhi ya maeneo yenye migogoro ni Kata ya KIA ambapo wafugaji wamekuwa wakiingiza mifugo yao katika maeneo ya uwanja wa ndege wa KIA, pamoja na wakulima wilayani humo kutotaka kuwaachia wafugaji maeneo wasiyoyatumia kwa kilimo hususan yenye magadi kwa ajili ya malisho kwa wafugaji hivyo kutengeneza chuki dhidi yao.

Naibu Waziri Ulega amemshauri pia mkuu huyo wa wilaya kutumia Chuo cha Mifugo Tengeru na Kituo cha Uhimilishaji cha Taifa (NAIC) vilivyopo Mkoani Arusha ili kuleta mabadiliko kwa wafugaji katika Wilaya ya Hai Mkoani Kilimanjaro kwa kuwa na ng’ombe wachache na wenye tija ukizingatia ukanda huo kuna kiwanda cha maziwa cha Tanga Fresh ambacho kinahitaji maziwa kwa wingi katika uzalishaji wao.

“Ukanda huu kuna kiwanda cha maziwa cha Tanga Fresh ambacho kinahitaji lita laki moja ya maziwa kwa siku na bado hayatoshelezi hadi inawalazimu kuchukua maziwa kutoka mikoa ya Iringa na Njombe ni vyema mkashirikiana na wizara kutoa elimu ili wafugaji wa wilaya hii wabadilike kwa kufuga kisasa hususan ng’ombe wa maziwa badala ya kuwa na ng’ombe wengi wasio na tija kiuchumi.” Alisema Mhe. Ulega

Naibu Waziri Ulega amemshauri pia mkuu wa wilaya Bw. Sabaya kuwa na kampeni maalum ya kutoa elimu kwa wafugaji pamoja na kushirikiana na wataalam ili wilaya hiyo iwe ya mfano katika kubadilisha fikra za wafugaji.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya Hai Bw. Lengai Ole Sabaya amesema changamoto kubwa zilizopo wilayani hapo ni mgogoro kati ya wakulima na wafugaji ambao tayari upo katika hatua mbalimbali za kutatuliwa pamoja na wafugaji kutokuwa tayari kubadilika kutoka kwenye ufugaji wa zamani wa kuwa na makundi makubwa ya mifugo isiyo na tija.

Kufuatia mazungumzo baina yake na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ulega, mkuu huyo wa wilaya amesema atazidi kushirikiana na wizara hiyo ili kuhakikisha changamoto hizo zinatatulika na kuifanya wilaya hiyo kuzidi kunufaika na mifugo iliyopo.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akifafanua jambo kwa viongozi wa Wilaya ya Hai (hawapo pichani) namna ya kuiboresha sekta ya mifugo wilayani humo




Baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Hai, wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Hai Bw. Lengai Ole Sabaya wakiwasilisha hoja mbalimbali kwa Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni