Nav bar

Jumatatu, 26 Januari 2026

TAWFA YAJIVUNIA MAFANIKIO WALIYOYAFIKIA, WAISHUKURU SERIKALI

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake wanaojishughulisha na Uvuvi Tanzania (TAWFA), Bi. Beatrice Mmbaga amekutana na Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agness Meena, Jijini Dodoma Januari 22, 2026 kwa lengo la kuishukuru serikali na kueleza mafanikio waliyoyapata  tangu kuanzishwa kwake mwaka 2019. 

Mwenyekiti huyo  wa TAWFA, Bi. Mmbaga akiwasilisha taarifa yake ya mafanikio alisema  kuwa TAWFA imefanikiwa kuanzisha kanda mbalimbali ikiwemo  Kanda ya Maji ya Bahari na Pwani, Kanda ya Ziwa Tanganyika, Kanda ya Ziwa Victoria pamoja , Kanda ya Ziwa Nyasa na Maji Madogo huku akifafanua kuwa hatua hiyo imeongeza ushiriki wa wanawake, upatikanaji wa mitaji elimu na vitendea kazi. 

“Zaidi ya wanawake 2000 wa TAWFA wamefaidika na VICOBA kwa kupata mikopo yenye riba nafuu yenye thamani ya Tshs. zaidi ya 160,000,000, huku TAWFA ikiendelea  kuimarika kwa kitambulika kikanda na Kimataifa ambapo sasa ni mwanachama wa World FisherFolks na African Women FishWorkers Association (AWFISHNET)”, alibainisha Bi. Mmbaga

Akiwasilisha taarifa yake hiyo, Bi. Mmbaga alisema vipaumbele vyao mbalimbali ikiwemo kupata ithibati ya ubora ya TBS ili waweze kusafirisha bidhaa zao nje ya nchi, upatikanaji  wa vitambulisho, kuwaunganisha  wanachama wao na taasisi za kifedha pamoja na Masoko ya Nje na kuwawezesha Wanachama mafunzo ya uongozi na elimu ya namna ya kuendesha vikundi vyao huku wakiiomba wizara kuwasaidia vitendea kazi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness Meena baada ya kusilikiliza taarifa yao hiyo aliwaeleza kuwa Wizara kama mlezi wao itaendelea kushirikiana na TAWFA kwa kuwaunganisha na taasisi mbalimbali za kifedha  pamoja na benki, hatua itakayowasaidia wanachama wa chama hicho kupata mikopo na mitaji kwa ajili ya kuendeleza shughuli za uvuvi.

Aidha, Bi. Meena aliwahimiza  viongozi hao wa TAWFA kuendelea kujiimarisha zaidi kwa lengo la kuweka misingi mizuri ya kujitegemea zaidi kiuchumi na kukuza shughuli zao ili kuimarisha mchango wa wanawake katika sekta ya uvuvi nchini huku akiwahimiza  kuanzisha vyama vya ushirika vya  kifedha (SACCOS) ili kuwawezesha wanachama kupata mitaji.  

Awali,  Mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) Bi. Prisca  Issangya alieleza kuwa  lengo la FAO ni kuinua wanawake kiuchumi kwa kuwawezesha kupata elimu na uwezo huku akiendelea kubainisha kuwa FAO iko tayari kushirikiana na TAWFA katika kuwaunganisha wanawake na mashirika ya fedha ili kuwasaidia kupata rasilimali zitakazowawezesha kukuza shughuli zao.

Picha ya pamoja ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, watendaji wa Wizara na viongozi wa TAWFA baada ya kikao cha kujadili maendeleo ya wanawake katika sekta ya mifugo na uvuvi  Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness Meena, akizungumza na viongozi wa TAWFA kuhusu umuhimu wakujiimsrisha zaidi Ili kuweza kujijengea uwezo wa kujitegemea kiuchumi, upatikanaji wa mitaji na kukuza ushiriki wa wanawake katika sekta ya mifugo na uvuvi Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Mwenyekiti wa TAWFA Bi. Beatrice Mmbaga akiwasilisha taarifa ya mafanikio, changamoto na vipaumbele vya chama wakati wa kikao na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Mwakilishi wa FAO, Bi. Prisca John, akitoa maelezo kuhusu mchango wa FAO katika kuinua wanawake katika sekta ya  uvuvi wakati wa kikao cha TAWFA kilichofanyika Januari 22, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Mkurugenzi Msaidizi wa Uvuvi Dkt. Baraka Sekadende akizungumza wakati wa kikao kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na viongozi wa TAWFA kilichofanyika Januari 22, 2026 Makao Makuu ya Wizara, Mtumba Jijini Dodoma


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni