Nav bar

Ijumaa, 2 Januari 2026

SERIKALI KUFANYA MAGEUZI UFUGAJI SAMAKI KWENYE VIZIMBA

 Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng'wasi Kamani amesema serikali kupitia wataalam wake sekta ya uvuvi  imeanza kufanya tathmini itakayoongeza uzalishaji wa mazao ya uvuvi pamoja na mnyororo wa thamani ili fedha zinazotolewa na  serikali zitumike kutoa manufaa chanya katika jamii.

Akizungumza na wanufaika wa vizimba vya  kufugia samaki eneo la Kisoko Mkoani Mwanza,  wakati wa ziara yake iliyofanyika Desemba 30, 2025 Mhe. Kamani amesema wizara inaendelea kutekeleza maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa fedha zote zinazopelekwa kwenye miradi zizalishe manufaa chanya kwa wanufaika.

"Lengo la Dkt  Samia Suluhu Hassan na maelekezo mahususi aliyotupa ni kwamba sehemu yeyote tunakoweka fedha ni lazima hiyo fedha iwe na manufaa chanya kwa jamii" alisema  Mhe. Kamani.

Aidha, Mhe. Kamani alisema Wizara imeanza mazungumzo na sekta binafsi kwa ajili ya kufanya uzalishaji wa vifaranga vya samaki, vyakula vya samaki na teknolojia inayohitajika ili kuwapunguzia gharama  za uendeshaji kwa wanufaika wa mradi huo wa vizimba vya kufugia samaki ambao lengo lake ni kuwainua kiuchumi.

Kuhusu uwezeshwaji wa mikopo kwa wanufaika wa ufugaji samaki kwenye vizimba Mhe. Kamani amesema Wizara imeanza mazungumzo na taasisi zingine za fedha ili kupanua wigo wa kuwakopesha wavuvi  mikopo yenye masharti nafuu.

"Kama Wizara tumeanza mazungumzo na kufanya tathmini ya kuzikaribisha taasisi za fedha ili kuwa na wigo mpana na wa uashindani katika kuwakopesha wavuvi wetu , lengo kuwawezesha mikopo yenye masharti nafuu" alisema.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani (wapili, kulia)akilisha chakula samaki waliofungwa kwenye moja ya kizimba cha wanufaika eneo la Kisoko, Mwanza  Desemba 30, 2025, jijini Mwanza.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani  akizungumza na wanufaika wa Vizimba vya Kufugia samaki eneo la Kisoko wakati wa Ziara yake ya kukagua utekelezaji wa shughuli zinazofanywa na wizara Desemba 30, 2025, jijini Mwanza.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng'wasi Kamani (wakwanza, kulia) akiwa ameshika samaki aliyevunwa kwenye moja ya Kizimba eneo la Kisoko, mkoani Mwanza Desemba 30, 2025

Wajasiriamali wanajihusisha na biashara ya samaki kupitia mradi wa Vizimba vya kufugia samaki eneo la Kisoko Mwanza wakimwelezea  Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Kamani changamoto wanazokabiliana nazo katika shughuli zao za kila siku Desemba 30, 2025, jijini Mwanza.

Mnufaika wa Vizimba vya Kufugia Samaki Bw. Pius Mtenya akitoa mapendekezo ya maboresho ya mikopo ya vizimba kwa vijana, wakati wa Ziara ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi mkoani Mwanza, Desemba 30, 2025.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni