Nav bar

Jumatatu, 27 Oktoba 2025

SERIKALI KUSHIRIKIANA NA WADAU KUBORESHA LISHE

Na. Martha Mbena, Dodoma. 

Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imesema itaendelea kushirikiana na wadau wa kitaifa na kimataifa kutekeleza mikakati inayolenga kuboresha sekta ya lishe kwa kuifanya kuwa na mifumo endelevu nchini.

Hayo yameelezwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi,  Dkt. Edwin Mhede wakati akifungua kikao cha kujadili  mradi wa Initiative on Climate Action and Nutrition (I-CAN) kilichofanyika  leo Oktoba 16, 2025 katika Hoteli ya Rafiki Jijini Dodoma. 

Dkt.  Mhede amesema serikali inafanya kazi na wadau na mashirika mbalimbali kwa kufanya majadiliano ya  jinsi ya kuoanisha masuala ya kisera katika mabadiliko ya tabianchi na lishe bora.

"Yaliyojadiliwa kwenye kikao cha leo yawe chachu ya kuifanya sekta hii ya lishe isogee mbele zaidi lakini mkakati wa mapitio ya sera kuhusu masuala ya lishe ni jambo la muhimu ", amesema Dkt. Mhede.

Amesema wananchi wanategemea kupata afua za serikali zinazohimiza  matumizi ya nishati safi ya  kupikia ambayo ni rafiki kwa mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

Naye, Mkuu wa miradi  kutoka Shirika la Global Alliance for Improved Nutrition (GAIN) Dkt. Winfrida Mayilla amesema kikao hicho kimelenga  kuyatambua masuala ya hali ya hewa na uhusiano wake kwenye lishe na kwa kuzingatia sera za nchi.

"Tuko hapa na wadau mbalimbali kuhakikisha kwamba sera zetu za Nchi hasahasa sera ya chakula na lishe inaingiza mikakati ya kuboresha mabadiliko haya ya tabianchi na tuje na mbinu mbalimbali ili  tukifanya kazi kwa pamoja ilenge kuboresha afya na lishe za watanzania" amesema Dkt. Mayilla.

Kikao cha mradi wa Initiative on Climate Action and Nutrition (I-CAN) kimejadili mabadiliko ya tabianchi, lishe bora pamoja na sera za kitaifa na uhusiano wake katika kuwekeza kwenye kilimo, ufugaji na uvuvi unaostahimili mabadiliko ya hali ya hewa.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede akiongea kwenye kikao cha kujadili mradi wa Initiative on Climate Action Nutrition (I-CAN) ambao umelenga kuboresha utekelezaji wa sera za lishe katika sekta za kilimo, Mifugo na Uvuvi, kikao hicho kimefanyika katika Hoteli ya Rafiki, jijini Dodoma Oktoba 16, 2025.

Mkuu wa Miradi Shirika la GLOBAL ALLIANC FOR IMPROVED NUTRITION, (GAIN) Dkt. Winfrida Mayilla akiwasilisha namna ya  mradi wa (I-CAN) Initiative on Climate Action and Nutrition utakavyotekelezwa na  tathmini ya utekelezaji wa sera Tanzania katika sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa  wadau wa Lishe kwenye kikao  kilichofanyika  hoteli ya Rafiki Jijini Dodoma Oktoba 16,2025.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Edwin Mhede (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa Lishe kutoka Wizarani na taasisi mbalimbali waliohudhuria kikao cha kujadili mradi wa Initiative on Climate Action and Nutrition (I-CAN) mara baada ya kumaliza kikao hicho kilichofanyika katika  hoteli ya Rafiki Jijini Dodoma,Oktoba 16,2025.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni