Nav bar

Jumatano, 16 Desemba 2020

NARCO YAANZA KUTEKELEZA MAAGIZO YA WAZIRI, YACHANJA NG’OMBE ZAIDI YA 9000

Katika hatua za kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki Disemba 11, 2020, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) imeshaanza kutekeleza sehemu ya maagizo kwa kuwapatia chanjo ya homa ya mapafu (CBPP) ng’ombe wote 9, 237 waliopo katika Ranchi ya Kongwa iliyopo jijini Dodoma.

 

Kaimu Meneja Mkuu, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO), Masele Shilagi alitoa taarifa hiyo leo Disemba 12, 2020 baada ya zoezi hilo lililochukua takriban masaa 10 mpaka kukamilika kwake.

 

Kwa Mujibu wa Shilagi baada ya kukamilika kwa zoezi hilo hatua inayofuata ni kutoa chanjo kwa ng’ombe wengine wa wawekezaji katika Ranchi za NARCO na tayari wameshawasiliana na Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania ili kupata dozi ya chanjo  kwa ng’ombe  6800 waliobaki katika Ranchi 13 nchini na uchanjaji utaanza mapema wiki ijayo.

 

Aidha, Shilagi amewaomba wafugaji na wananchi wote waliokaribu na maeneo ya Ranchi ya Kongwa kutokuwa na wasiwasi kwa sababu wameshaanza kuchukua hatua stahiki za kukabiliana na tatizo hilo ambalo kimsingi wamewahi kukabiliana nalo katika hatua za awali.

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki alipofanya ziara ya kushtukiza katika Ranchi ya NARCO Kongwa baada ya kupata taarifa ya mlipuko wa ugonjwa wa homa ya mapafu ulioanza kuikumba Ranchi hiyo alimuagiza Kaimu Meneja Mkuu wa NARCO kuhakikisha wanawapa chanjo ng’ombe wote katika Ranchi hiyo na Ranchi nyingine zote za taifa.

Mmoja wa Maafisa Mifugo akishiriki katika zoezi la kuwapa chanjo ya homa ya mapafu ng'ombe waliopo katika Ranchi ya NARCO Kongwa iliyopo jijini Dodoma Disemba 12, 2020.

Kaimu Meneja Mkuu, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO), Masele Shilagi akiwaongoza ng'ombe kuingia katika kibanio cha kuchanjia katika zoezi la kuwapa ng'ombe chanjo ya homa ya mapafu katika Ranchi ya NARCO Kongwa iliyopo jijini Dodoma Disemba 12, 2020.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni